Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kueneza Habari Njema Juu ya Milima ya Andes

Kueneza Habari Njema Juu ya Milima ya Andes

Kueneza Habari Njema Juu ya Milima ya Andes

TUKIWA watu 18 tulilala kwenye sakafu ya udongo ya kibanda fulani. Tulitetemeka ndani ya mifuko yetu ya kulalia huku mvua kubwa ikipiga paa letu la mabati. Kibanda hicho kilikuwa katika hali mbaya sana hivi kwamba tulijiuliza ikiwa sisi ndio tuliokuwa watu wa kwanza kukaa humo.

Kwa nini kikundi chetu cha watu 18 kilitembelea eneo hilo? Ni kwa sababu tulitamani kutimiza amri ya Yesu ya kuhubiri habari njema “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8; Mt. 24:14) Tulienda kuhubiri eneo la mbali katika Milima ya Andes ya Bolivia.

Kufika Huko

Tatizo la kwanza lilikuwa kufika huko. Tuligundua kwamba magari ya abiria yanayoenda katika maeneo hayo ya mbali hayakuondoka kwa wakati kamili. Basi letu lilipokuja, tuligundua kwamba lilikuwa dogo zaidi kuliko tulivyotarajia, hivyo wengine wetu walisimama ndani ya basi. Lakini mwishowe sote tulifika kwenye eneo.

Kusudi letu lilikuwa kuhubiri katika vijiji vilivyo juu ya Milima ya Andes ya Bolivia. Kwa hiyo, baada ya basi kufika, tulianza kupanda milima hiyo mirefu huku tukifuatana kwa uangalifu tukiwa tumebeba mizigo yetu.

Ingawa vijiji vilionekana vidogo, nyumba hazikuwa karibu-karibu, kwa hiyo tulichukua saa nyingi kutembelea kila kijiji. Hata ingawa tulitembea sana, bado kulikuwa na nyumba nyingine mbali zaidi. Mara nyingi tulipotea katika vijia vilivyojipinda-pinda katika mashamba.

“Kwa Nini Hamkuja Mapema?”

Mwanamke mmoja alivutiwa sana alipojua umbali tuliotembea hivi kwamba alituruhusu tutumie jiko lake na kuni kupikia chakula chetu cha mchana. Mwanamume mmoja alipojifunza yale ambayo Biblia inasema kuhusu hali ya wafu, aliuliza hivi: “Kwa nini hamkuja mapema?” Alipendezwa sana hivi kwamba tulipoondoka katika kijiji chao, alitusindikiza na kuuliza maswali mengine. Mwanamume mwingine hakuwa amepata kusikia kuhusu Mashahidi wa Yehova na alipendezwa sana na vichapo vyetu. Alitushukuru sana kwa sababu ya kuja kisha akatupa ufunguo wa kibanda fulani ili tulale humo.

Usiku mmoja, kulikuwa na giza sana hivi kwamba tulipiga mahema yetu katikati ya chungu wakubwa weusi. Wadudu hao walikasirika na kuanza kutuuma. Hatukutaka kuhamia sehemu nyingine kwa sababu tulikuwa tumechoka sana, tulifurahi kwamba muda si muda wadudu hao walituacha nao wakaendelea na shughuli zao.

Mwanzoni, migongo na mbavu zetu ziliuma kwa sababu ya kulala chini, lakini tulizoea kadiri usiku ulivyoendelea. Asubuhi hatukukumbuka tena maumivu na uchungu wowote tuliokuwa nao tulipotazama kwa mbali mabonde maridadi sana yakifunikwa polepole na mawingu, na pia vilele vyenye theluji vinavyovutia sana. Hakukuwa na sauti yoyote isipokuwa sauti ya kijito kinachotiririka na nyimbo za ndege.

Baada ya kuoga kwenye kijito hicho, tulizungumzia andiko la Biblia pamoja, tukala kiamsha-kinywa, na kuanza kupanda polepole kuelekea kwenye vijiji vingine vya mbali. Jitihada hizo za kupanda milima hazikuwa za bure. Tulikutana na mwanamke mmoja aliyezeeka ambaye alilia alipogundua kwamba jina la Mungu, Yehova, liko katika Biblia. Aliguswa moyo sana. Sasa angeweza kutumia jina la Mungu katika sala zake!

Mwanamume mmoja aliyezeeka alisema kwamba bila shaka Mungu amemkumbuka, kisha akaanza kuimba wimbo uliosema kwamba tulitumwa na malaika. Mwanamume mwingine, ambaye alikuwa mgonjwa sana asiweze kuondoka nyumbani kwake, alituambia kwamba hakuna mtu hata mmoja katika kijiji chao ambaye amewahi kumtembelea. Alishangaa kwamba tulikuwa tumekuja kutoka mbali sana huko La Paz. Mtu mwingine alivutiwa sana kwamba Mashahidi wa Yehova wanawatembelea watu nyumbani kwao, lakini dini nyingine zinawaita tu kwa kengele za kanisa.

Hakuna nyumba yenye umeme katika eneo hilo, kwa hiyo watu wanalala giza linapoingia na kuamka jua linapochomoza. Hivyo, tulilazimika kuanza mahubiri yetu saa 12 asubuhi ili tuwapate watu nyumbani. Kama sivyo, hatungepata watu wengi kwa kuwa walienda kufanya kazi katika mashamba. Baadaye, wengine ambao walikuwa wakifanya kazi katika mashamba walikuwa tayari kuacha kazi zao ili wasikilize ujumbe wetu unaotoka katika Neno la Mungu. Haikosi ng’ombe-dume waliokuwa wakivuta majembe walifurahi kupumzika kidogo. Watu wengi tuliowakuta nyumbani walitutandazia ngozi za kondoo ili tuzikalie nao wakakusanya familia yote ili itusikilize. Wakulima fulani walitupa mahindi mengi kama shukrani kwa ajili ya vichapo vya Biblia ambavyo tuliwaachia.

“Hamkunisahau”

Bila shaka, watu wanahitaji kutembelewa tena na tena ili wapate ujuzi zaidi wa Biblia. Wengi walitusihi turudi na kuwafundisha mengi zaidi. Kwa sababu hiyo, tumerudi mara kwa mara katika eneo hilo la Bolivia.

Pindi moja, mwanamke fulani aliyezeeka alifurahi tuliporudi, naye akasema: “Ninyi ni kama watoto kwangu. Hamkunisahau.” Mtu fulani alitushukuru kwa sababu ya kazi yetu naye akatuomba tukae nyumbani mwake tutakaporudi tena. Labda thawabu kubwa zaidi ya jitihada zetu ni kusikia kwamba mwanamke mmoja tuliyemtembelea wakati uliopita alihamia jijini na sasa anahubiri habari njema.

Siku ya mwisho ya safari yetu ya kwanza, jiko tulilotumia kambini lilikwisha mafuta na chakula chetu kilikuwa karibu kwisha. Tulikusanya kuni za kutosha, tukapika chakula chetu cha mwisho, na kuanza kurudi kwa miguu. Tulikuwa mbali sana kutoka katika mji ambako tungepata basi. Mwishowe, tulifika kukiwa na giza.

Kurudi Nyumbani

Safari ya kurudi ilikuwa na matatizo kwa sababu basi letu liliharibika. Baadaye, tulibebwa na lori fulani lililojaa watu. Hilo lilitupa nafasi ya kuwahubiria wasafiri wenzetu ambao walitaka kujua tulichoenda kufanya huko. Ingawa watu hao ni wanyamavu, kwa ujumla ni wachangamfu na wenye urafiki.

Baada ya kusafiri kwa saa tisa juu ya lori, tulifika nyumbani tukiwa tumenyeshewa na tukihisi baridi kali sana. Hata hivyo, safari hiyo haikuwa ya bure. Njiani, tulifanya mipango ya kujifunza Biblia pamoja na mwanamke ambaye anaishi mjini.

Kwa kweli, kuwahubiria habari njema watu walio katika maeneo kama hayo ya mbali ni pendeleo. Tulihubiri katika vijiji vinne vikubwa na vijiji vingine vingi vidogo. Tulikumbuka maneno haya: “Jinsi inavyopendeza juu ya milima miguu ya yeye anayeleta habari njema, yeye anayetangaza amani, yeye anayeleta habari njema za jambo bora, yeye anayetangaza wokovu.”—Isa. 52:7; Rom. 10:15.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Tukiwa tayari kuhubiri habari njema