Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ni Nani Aliye na Hekima na Mwenye Uelewaji Kati Yenu?”

“Ni Nani Aliye na Hekima na Mwenye Uelewaji Kati Yenu?”

“Ni Nani Aliye na Hekima na Mwenye Uelewaji Kati Yenu?”

“Ni nani aliye na hekima na mwenye uelewaji kati yenu? Na aonyeshe kutokana na mwenendo wake mzuri matendo yake kwa upole ulio wa hekima.”—YAK. 3:13.

1, 2. Tunaweza kusema nini kuhusu watu wengi wanaoonwa kuwa wenye hekima?

UNAFIKIRI ni nani aliye na hekima ya kweli? Je, ni wazazi wako, mtu fulani aliyezeeka, au labda profesa wa chuo fulani? Huenda maoni yako kuhusu mtu mwenye hekima yakategemea malezi au hali zako. Hata hivyo, watumishi wa Mungu wanapendezwa hasa na maoni yake.

2 Si watu wote ambao ulimwengu unawaona kuwa wenye hekima walio na hekima ya kweli machoni pa Mungu. Kwa mfano, Ayubu alizungumza na watu waliofikiri kwamba walikuwa wakisema maneno ya hekima, lakini akakata kauli hivi: “Sioni yeyote mwenye hekima kati yenu.” (Ayu. 17:10) Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu watu fulani waliokataa ujuzi wa Mungu: “Ijapokuwa walisisitiza kuwa ni wenye hekima, wakawa wapumbavu.” (Rom. 1:22) Na kupitia nabii Isaya, Yehova alisema hivi waziwazi: “Ole wao walio na hekima machoni pao wenyewe.”—Isa. 5:21.

3, 4. Ni nini kinachohitajiwa ili mtu awe na hekima ya kweli?

3 Kwa wazi, tunahitaji kutambua kinachomfanya mtu awe na hekima ya kweli na kumwezesha kupata kibali cha Mungu. Methali 9:10 inatufahamisha hivi: “Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa hekima, na kumjua aliye Mtakatifu Zaidi ni uelewaji.” Wenye hekima wanapaswa kumwogopa Mungu ifaavyo na kuheshimu viwango vyake. Hata hivyo, mengi yanahitajiwa zaidi ya kukubali tu akilini kwamba kuna Mungu na kwamba ana viwango. Mwanafunzi Yakobo anatuchochea kufikiria jambo hilo. (Soma Yakobo 3:13.) Ona maneno: “Na aonyeshe kutokana na mwenendo wake mzuri matendo yake.” Hekima ya kweli inapaswa kuonekana kutokana na yale unayofanya na kusema kila siku.

4 Hekima ya kweli inatia ndani kutumia kwa mafanikio busara, ujuzi, na uelewaji. Ni matendo gani yatakayoonyesha kwamba tuna hekima ya aina hiyo? Yakobo anaorodhesha mambo fulani yatakayoonekana katika matendo ya wale walio na hekima. * Yakobo alisema nini kinachoweza kutusaidia tuwe na uhusiano mzuri pamoja na waamini wenzetu, na pia wale walio nje ya kutaniko la Kikristo?

Matendo Yanawatambulisha Wale Walio na Hekima ya Kweli

5. Mtu aliye na hekima ya kweli atatenda namna gani?

5 Inafaa tutaje tena kwamba Yakobo alihusianisha hekima na mwenendo mzuri. Kwa sababu kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa hekima, mtu mwenye hekima anajitahidi kujiendesha kupatana na njia na viwango vya Mungu. Hatuzaliwi tukiwa na hekima ya kimungu. Hata hivyo, tunaweza kuipata kwa kujifunza Biblia na kutafakari kila siku. Hilo litatusaidia kufuata himizo la Waefeso 5:1: “Iweni waigaji wa Mungu.” Kadiri tunavyotenda kama Yehova, ndivyo tutakavyoonyesha hekima katika matendo yetu. Njia za Yehova ni za juu sana kuliko njia za wanadamu. (Isa. 55:8, 9) Hivyo, kadiri tunavyoiga njia za Yehova za kufanya mambo, ndivyo wale walio nje ya kutaniko la Kikristo watakavyoona kwamba sisi ni watu tofauti.

6. Kwa nini upole unaonyesha kwamba mtu anamwiga Mungu, na sifa hiyo inatia ndani nini?

6 Yakobo anaonyesha kwamba njia moja ya kuwa kama Yehova ni kuwa na “upole ulio wa hekima.” Ingawa upole unatia ndani hisia nyororo, bado Mkristo anaweza kuwa imara, na hivyo kutenda kwa usawaziko. Ingawa Mungu ana nguvu zisizo na mipaka, yeye ni mpole, nasi hatuogopi kumfikia. Mwana wa Mungu aliiga kikamili sifa ya upole ya Baba yake hivi kwamba angeweza kusema hivi: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.”—Mt. 11:28, 29; Flp. 2:5-8.

7. Kwa nini tunaweza kumwona Musa kuwa mfano mzuri wa upole?

7 Biblia inazungumza kuhusu watu fulani ambao walionyesha upole au unyenyekevu kwa njia ya pekee. Musa alikuwa mmoja wao. Alikuwa na daraka kubwa sana, lakini inasemwa kwamba alikuwa “mpole zaidi kuliko watu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hes. 11:29; 12:3) Na kumbuka nguvu ambazo Yehova alimpa Musa ili afanye mapenzi Yake. Yehova alipendezwa kuwatumia watu wapole kutimiza kusudi lake.

8. Wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kuonyesha jinsi gani “upole ulio wa hekima”?

8 Ni wazi kwamba wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kuonyesha “upole ulio wa hekima.” Namna gani sisi? Tunaweza jinsi gani kufanya maendeleo katika kuonyesha sifa hiyo? Upole ni sehemu ya matunda ya roho takatifu ya Yehova. (Gal. 5:22, 23) Tunaweza kumwomba Mungu atupe roho yake na kufanya kila tunaloweza ili kuonyesha matunda ya roho hiyo huku tukimtegemea atusaidie kuonyesha upole kwa njia bora zaidi. Uhakikisho huu wa mtunga-zaburi unatuchochea sana kufanya hivyo: “[Mungu] atawafundisha wapole njia yake.”—Zab. 25:9.

9, 10. Tunahitaji kujitahidi kadiri gani ili tuonyeshe upole wa kimungu, na kwa nini?

9 Hata hivyo, huenda jitihada nyingi zikahitajiwa ili kufanya maendeleo katika kuonyesha upole. Kwa sababu ya malezi yetu, huenda wengine wetu tusiwe na mwelekeo wa kuwa wapole. Zaidi ya hilo, watu wanaotuzunguka wanaweza kutuchochea tuwe na maoni tofauti, wakisema kwamba “dawa ya moto ni moto.” Lakini, je, hilo ni jambo la hekima? Ikiwa moto mdogo ungeshika nyumba yako, je, ungeumwagilia mafuta au ungeumwagilia maji baridi? Kumwagilia moto mafuta kungeharibu mambo zaidi, lakini kuumwagilia maji baridi kungetimiza kusudi linalofaa. Vivyo hivyo, Biblia inatushauri hivi: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu, lakini neno linaloumiza hufanya hasira ipande.” (Met. 15:1, 18) Wakati ujao matatizo yakitokea, ndani au nje ya kutaniko, tunaweza kuonyesha kwamba tuna hekima ya kweli kwa kutenda kwa upole.—2 Tim. 2:24.

10 Kama ilivyoonyeshwa, wengi ambao wanaongozwa na roho ya ulimwengu hawana sifa ya upole, amani, na utulivu. Badala yake, watu wengi ni wakali na wenye kiburi. Yakobo alijua jambo hilo, naye alitoa maonyo ili watu mmoja-mmoja kutanikoni wasipotoshwe na roho hiyo. Tunaweza kujifunza nini kingine kutokana na shauri alilotoa?

Sifa za Watu Wasio na Hekima

11. Ni sifa gani zinazopingana na hekima ya kimungu?

11 Yakobo aliandika waziwazi kuhusu sifa zinazopingana moja kwa moja na hekima ya kimungu. (Soma Yakobo 3:14.) Wivu na ugomvi ni sifa za kimwili, wala si za kiroho. Ona yale yanayotukia watu wanapofikiri kupatana na mwili. Vikundi sita vya “Kikristo” vinasimamia sehemu mbalimbali za Kanisa la Kaburi Takatifu huko Yerusalemu, ambalo inasemekana kwamba lilijengwa mahali ambapo Yesu aliuawa na kuzikwa. Vikundi hivyo vimekuwa na ugomvi daima. Mwaka wa 2006, gazeti moja (Time) liliripoti kwamba wakati fulani watawa waliokuwa katika kanisa hilo “walipigana kwa saa nyingi, . . . wakitwangana kwa vishikio vikubwa vya mishumaa.” Watawa hao hawaaminiani hata kidogo hivi kwamba wamemkabidhi Mwislamu ufunguo wa kanisa hilo.

12. Ni nini kinachoweza kutokea hekima inapokosekana?

12 Bila shaka, kutaniko la kweli la Kikristo halipaswi kamwe kuwa na ugomvi mkali kama huo. Hata hivyo, nyakati nyingine kutokamilika kumefanya wengine washikilie kwa ukaidi maoni yao. Hilo linaweza kusababisha mashindano na ugomvi kwa kadiri fulani. Mtume Paulo aliona hali hiyo katika kutaniko la Korintho, hivyo akaandika: “Kwa kuwa kuna wivu na mizozo kati yenu, je, ninyi si wa kimwili na je, hamtembei kama wanadamu wanavyotembea?” (1 Kor. 3:3) Hali hiyo yenye kusikitisha iliendelea kwa muda katika kutaniko hilo la karne ya kwanza. Kwa hiyo, tunapaswa kuwa waangalifu ili roho hiyo isiingie katika kutaniko leo.

13, 14. Toa mifano inayoonyesha jinsi roho ya kimwili inavyoweza kuonyeshwa.

13 Roho kama hiyo inaweza kupenya jinsi gani katika kutaniko? Inaweza kuanza kwa mambo madogo. Kwa mfano, Jumba la Ufalme linapojengwa, kunaweza kuwa na maoni tofauti kuhusu ujenzi huo. Ndugu mmoja anaweza kuanzisha ugomvi kwa sababu pendekezo lake halikubaliwi, huenda akachambua vikali maamuzi yanayofanywa. Anaweza hata kukataa kufanya kazi nyingine yoyote inayohusu ujenzi huo! Mtu anayetenda hivyo anasahau kwamba kwa kawaida kutimiza mradi fulani wa kutaniko kunategemea hasa roho ya amani ya kutaniko wala si ufundi hususa unaotumiwa. Yehova atabariki roho ya upole wala si ugomvi.—1 Tim. 6:4, 5.

14 Mfano mwingine unaweza kuwa wakati wazee wa kutaniko wanapoona wazi kwamba mzee mwenzao sasa hana sifa za kustahili za Kimaandiko ingawa ametumikia kwa miaka mingi. Mwangalizi wa mzunguko anayewatembelea anatambua kwamba ndugu huyo amepokea mashauri hususa lakini hayafuati, hivyo anakubali na kuunga mkono pendekezo la kumwondoa mzee huyo. Mzee huyo atafanya nini? Je, atakubaliana na uamuzi uliofanywa na wale wazee wengine na kufuata mashauri ya Kimaandiko kwa roho ya unyenyekevu na upole, na kuazimia kuonyesha tena sifa za kustahili za Kimaandiko ili aweze kutumika tena akiwa mzee? Au atakuwa na kinyongo na wivu kwa sababu hana tena pendeleo alilokuwa nalo? Kwa nini ndugu ajiendeshe kana kwamba alistahili kuwa mwanamume mzee na kumbe kwa kweli hakustahili? Lingekuwa jambo la hekima zaidi kuonyesha unyenyekevu na uelewaji.

15. Kwa nini unaona kwamba shauri lililoongozwa na roho katika Yakobo 3:15, 16 ni la maana sana?

15 Ni kweli kwamba kuna hali nyingine zinazoweza kumfanya mtu awe na mtazamo kama huo. Lakini hata hali gani zitokee, tunapaswa kujitahidi kuepuka sifa kama hizo. (Soma Yakobo 3:15, 16.) Mwanafunzi Yakobo alisema sifa hizo ni za “kidunia” kwa sababu ni za kimwili, wala si za kiroho hata kidogo. Ni za “kinyama” kwa kuwa zinatokana na mielekeo ya kimwili, sawa na sifa za wanyama wasio na akili. Mitazamo kama hiyo ni ya “roho waovu,” kwa kuwa inaonyesha mwelekeo wa viumbe wa roho ambao ni maadui wa Mungu. Ni jambo lisilofaa kama nini kwa Mkristo kuonyesha mitazamo hiyo!

16. Huenda tukahitaji kufanya marekebisho gani, na tunaweza kufanikiwa tukifanya nini?

16 Kila mshiriki wa kutaniko anapaswa kujichunguza mwenyewe na kujitahidi kushinda sifa hizo mbaya. Wakiwa walimu katika kutaniko, waangalizi pia wanapaswa kujitahidi kushinda mitazamo hiyo isiyofaa. Si rahisi kufanya hivyo kwa sababu sisi si wakamilifu na tunakabili uvutano wa ulimwengu huu. Kujaribu kushinda sifa hizo ni kama kujaribu kupanda kilima chenye matope na utelezi. Ikiwa hatuna kitu cha kujishikilia, tutateleza na kurudi nyuma. Hata hivyo, tukishikilia kwa nguvu shauri la Biblia, na kwa msaada wa kutaniko la Mungu la duniani pote, tunaweza kusonga mbele.—Zab. 73:23, 24.

Sifa Ambazo Wenye Hekima Wanajitahidi Kuonyesha

17. Kwa kawaida, watu wenye hekima wanaitikia jinsi gani wanaposhawishiwa watende maovu?

17 Soma Yakobo 3:17. Tunaweza kufaidika tukichunguza sifa fulani za “hekima inayotoka juu.” Kuwa safi kiadili kunatia ndani kutakata na kutokuwa najisi katika matendo na nia yetu. Tunapaswa kukataa mambo maovu bila kukawia. Hilo ndilo linalopaswa kuwa itikio letu la kawaida. Tuseme mtu fulani angejaribu kugusa jicho lako. Ungeondoa kichwa chako haraka au ungeuzuia mkono wake. Hilo ni itikio la kawaida; huhitaji kufikiria utakachofanya. Tunapaswa kuitikia vivyo hivyo tunaposhawishiwa tutende maovu. Usafi wetu wa kiadili na dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia inapaswa kwa kawaida kutuchochea tukatae maovu. (Rom. 12:9) Biblia ina mifano ya watu waliofanya hivyo, kama vile Yosefu na Yesu.—Mwa. 39:7-9; Mt. 4:8-10.

18. Inamaanisha nini (a) kuwa mwenye amani? (b) kuwa mwenye kufanya amani?

18 Pia, hekima ya kimungu inataka tuwe wenye amani. Hilo linatia ndani kuepuka kuwachokoza wengine, mtazamo wa kutaka vita, au matendo yanayoweza kuvuruga amani. Yakobo anaeleza zaidi jambo hilo anaposema hivi: “Mbegu ya tunda la uadilifu hupandwa chini ya hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.” (Yak. 3:18) Ona usemi “wanaofanya amani.” Je, tunajulikana kuwa watu wanaofanya amani, au wanaovuruga amani katika kutaniko? Je, mara nyingi sisi tunakosana na wengine, tunaudhika kwa urahisi au kuwaudhi wengine? Je, tunasisitiza wengine watukubali jinsi tulivyo, au tunajitahidi kwa unyenyekevu kushinda sifa ambazo kwa kweli zinawaudhi wengine? Je, wengine wanatuona kuwa watu walio tayari kufanya juu chini ili kuendeleza amani, kusamehe, na kusahau makosa upesi? Kujichunguza kwa unyoofu kunaweza kutusaidia kuona ikiwa tunahitaji kufanya maendeleo katika kuonyesha hekima ya kimungu kuhusiana na jambo hilo.

19. Mtu anaweza kujulikana jinsi gani kuwa mwenye usawaziko?

19 Yakobo alionyesha kwamba usawaziko ni moja ya sifa zinazoonyesha kwamba mtu ana hekima inayotoka juu. Je, tunajulikana kuwa watu wanaokubali maoni ya wengine bila kusisitiza kwamba viwango vyetu vifuatwe ikiwa kanuni za Kimaandiko hazivunjwi? Je, tunajulikana kuwa wapole na wengine wanajihisi huru kuongea nasi? Kufanya hivyo kunaonyesha kwamba tumejifunza kuwa na usawaziko.

20. Kutakuwa na matokeo gani tukionyesha sifa za kimungu ambazo tumezungumzia?

20 Ndugu na dada wakijitahidi kuonyesha zaidi sifa za kimungu ambazo Yakobo aliandika kuzihusu, kutakuwa na hali zenye kupendeza sana katika kutaniko. (Zab. 133:1-3) Bila shaka, kuwa wapole, wenye kufanya amani, na wenye usawaziko kutaboresha mahusiano yetu na kutaonyesha kwamba tuna “hekima inayotoka juu.” Katika habari inayofuata, tutachunguza jinsi kuwaona wengine kama Yehova anavyowaona kunavyoweza kutusaidia kuonyesha sifa hizo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Mistari mingine katika sura hiyo inaonyesha kwamba Yakobo alizungumza kwanza kuhusu wanaume wazee, au “walimu” wa kutaniko. (Yak. 3:1) Bila shaka, wanaume hao wanapaswa kuweka mfano mzuri katika kuonyesha hekima ya kimungu, lakini sisi sote tunaweza kujifunza kutokana na shauri lake.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni nini kinachomfanya Mkristo awe na hekima ya kweli?

• Tunaweza kufanya maendeleo jinsi gani katika kuonyesha hekima ya kimungu?

• Watu ambao hawana “hekima inayotoka juu” wanaonyesha sifa gani?

• Umeazimia kusitawisha sifa gani hata zaidi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ugomvi unaweza kutokea jinsi gani leo?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, kukataa uovu bila kukawia ndilo itikio lako la kawaida?