Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pata Shangwe Katika Ndoa Yako

Pata Shangwe Katika Ndoa Yako

Pata Shangwe Katika Ndoa Yako

“Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa utambuzi itasimamishwa imara.”—MET. 24:3.

1. Mungu alionyesha hekima jinsi gani kuhusiana na mwanadamu wa kwanza?

BABA yetu wa mbinguni aliye na hekima anajua kile kinachotufaa. Kwa mfano, Mungu alitambua kwamba ili kusudi Lake litimie, haikuwa “vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake” katika bustani ya Edeni. Sehemu muhimu ya kusudi hilo ilikuwa kwamba watu waliooa wazae watoto na ‘kuijaza dunia.’—Mwa. 1:28; 2:18.

2. Yehova alifanya mpango gani kwa faida ya wanadamu?

2 Yehova alisema: “Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.” Kisha, Mungu akamletea mwanamume wa kwanza usingizi mzito, naye akachukua ubavu kutoka katika mwili mkamilifu wa mwanamume huyo. Alifanya ubavu huo kuwa mwanamke. Yehova alipomletea Adamu mwanamke huyo mkamilifu, Hawa, mwanamume huyo alisema hivi: “Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu. Huyu ataitwa Mwanamke, kwa sababu huyu alitolewa katika mwanamume.” Kwa kweli, Hawa alikuwa kikamilisho cha Adamu. Kila mmoja angeonyesha tabia na sifa za pekee, hata hivyo wote wawili walikuwa wakamilifu na walifanywa kwa mfano wa Mungu. Hivyo, Yehova akaanzisha ndoa ya kwanza. Adamu na Hawa walikubali mpango huo wa Mungu ambao ungewawezesha kusaidiana na kutegemezana.—Mwa. 1:27; 2:21-23.

3. Watu wengi wana maoni gani kuhusu zawadi ya ndoa, na hilo linatokeza maswali gani?

3 Inasikitisha kwamba roho ya uasi imeenea ulimwenguni leo. Mungu hasababishi matatizo yanayotokana na uasi huo. Watu wengi wanadharau zawadi ya Mungu ya ndoa, wakiiona kuwa iliyopitwa na wakati na kwamba ni chanzo cha mfadhaiko au matatizo. Watu wengi wanaofunga ndoa wanatalikiana. Huenda watoto wasionyeshwe upendo wa asili, na matatizo yanapotokea katika ndoa huenda wazazi wakawatumia watoto wao kwa faida yao wenyewe. Wazazi wengi wanakataa kutenda kwa njia yenye usawaziko, hata kwa ajili ya amani na umoja. (2 Tim. 3:3) Hivyo basi, shangwe inaweza kudumishwa jinsi gani katika ndoa nyakati hizi za hatari? Usawaziko unasaidia jinsi gani kuzuia ndoa isivunjike? Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya leo ya wale ambao wamedumisha shangwe katika ndoa zao?

Kukubali Mwongozo wa Yehova

4. (a) Paulo alitoa mwelekezo gani kuhusu ndoa? (b) Wakristo watiifu wanafuata jinsi gani mwelekezo wa Paulo?

4 Mtume Mkristo Paulo alitoa mwelekezo ulioongozwa na roho kwa wajane kwamba ikiwa wangeamua kuolewa tena, wangepaswa kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Hilo halikuwa wazo jipya kwa Wakristo ambao hapo zamani walikuwa katika dini ya Kiyahudi. Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilisema wazi kwamba hawakupaswa ‘kufanya mapatano yoyote ya ndoa’ na mtu yeyote kutoka katika mataifa ya kipagani yaliyowazunguka. Yehova aliongeza maelezo haya ambayo yanaonyesha hatari ya kupuuza kiwango hicho cha kimungu: “Kwa maana [mtu asiye Mwisraeli] atamgeuza mwana wako aache kunifuata, nao watatumikia miungu mingine; na hasira ya Yehova itawaka kwelikweli juu yenu, naye hakika atakuangamiza haraka.” (Kum. 7:3, 4) Yehova anawatazamia watumishi wake leo wawe na msimamo gani kuhusu kuchagua mwenzi wa ndoa? Kwa wazi, mtumishi wa Mungu anapaswa kuchagua mwenzi wa ndoa “katika Bwana tu,” mwabudu mwenzake aliyejiweka wakfu na kubatizwa. Ni jambo la hekima kukubali mwongozo wa Yehova kuhusu kuchagua mwenzi wa ndoa.

5. Yehova na Wakristo waliofunga ndoa wana maoni gani kuhusu nadhiri za ndoa?

5 Nadhiri za ndoa ni takatifu machoni pa Mungu. Akizungumza kuhusu ndoa ya kwanza, Yesu, Mwana wa Mungu, alisema hivi: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mt. 19:6) Mtunga-zaburi anatukumbusha uzito wa nadhiri: “Toa shukrani zikiwa dhabihu yako kwa Mungu, na umtimizie Aliye Juu Zaidi nadhiri zako.” (Zab. 50:14) Ingawa wanaofunga ndoa wanaweza kupata shangwe kubwa, nadhiri zinazotolewa siku ya arusi ni nzito na zinampa mtu wajibu.—Kum. 23:21.

6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yeftha?

6 Fikiria kisa cha Yeftha, ambaye alikuwa mwamuzi wa Israeli katika karne ya 12 K.W.K. Aliweka nadhiri hii kwa Yehova: “Hakika ukiwatia wana wa Amoni mkononi mwangu, itatukia pia kwamba yule atakayetoka nje, atakayetoka nje ya milango ya nyumba yangu kuja kunipokea nitakaporudi kwa amani kutoka kwa wana wa Amoni, lazima atakuwa wa Yehova, nami nitamtoa huyo kuwa toleo la kuteketezwa.” Je, Yeftha alivunja nadhiri yake alipoona kwamba binti yake, mtoto wake pekee, ndiye aliyekuja kukutana naye aliporudi nyumbani kwake Mizpa? Hapana. Alisema hivi: “Nimemfungulia Yehova kinywa changu, nami siwezi kurudi nyuma.” (Amu. 11:30, 31, 35) Yeftha alitimiza ahadi yake kwa Yehova, hata ingawa hilo lilimaanisha kwamba hangekuwa na mzao wa kuendeleza jina lake. Nadhiri ya Yeftha ilikuwa tofauti na nadhiri za arusi, lakini kwa kuitimiza, aliwawekea mfano mzuri waume na wake Wakristo kuhusiana na nadhiri zao.

Ni Nini Kinachofanya Ndoa Ifanikiwe?

7. Wenzi wapya wa ndoa wanahitaji kufanya marekebisho gani?

7 Wenzi wengi wa ndoa wana kumbukumbu nzuri sana za uchumba wao. Walifurahi sana kumfahamu yule ambaye angekuwa mwenzi wao wa ndoa! Kadiri walivyotumia wakati pamoja, ndivyo walivyokuwa na uhusiano wa karibu zaidi. Lakini, iwe walioana baada ya kuchumbiana au walifunga ndoa iliyopangwa, mwishowe wakiwa mume na mke, ilikuwa muhimu wafanye marekebisho fulani. Mume mmoja anasema hivi: “Tatizo kubwa tulilokuwa nalo mwanzoni mwa ndoa yetu lilikuwa kutambua kwamba hatukuwa tena waseja. Kwa muda fulani ilikuwa vigumu kushughulika na marafiki wetu na watu wa familia kwa usawaziko.” Mume mwingine, ambaye amekaa katika ndoa kwa miaka 30 sasa, alitambua mapema katika ndoa yake kwamba ili kuwa mwenye usawaziko, alihitaji kujifunza “kukumbuka kwamba ana mwenzi.” Kabla ya kukubali mwaliko au kufanya mapatano yoyote, anazungumza na mke wake kisha anaamua, huku akifikiria faida zao wawili. Katika hali kama hiyo, usawaziko unasaidia.—Met. 13:10.

8, 9. (a) Kwa nini kuwasiliana vizuri ni muhimu? (b) Kubadilikana kunaweza kusaidia katika mambo gani, na kwa nini?

8 Nyakati nyingine watu wanaofunga ndoa wana malezi na tamaduni mbalimbali. Katika hali hiyo, wanahitaji sana kuwasiliana waziwazi. Njia za kuwasiliana zinatofautiana. Kuchunguza jinsi mwenzi wako wa ndoa anavyozungumza na watu wake wa ukoo kunaweza kukusaidia kumfahamu vizuri zaidi. Nyakati nyingine mawazo ya ndani ya mtu hayafunuliwi na jambo analosema bali jinsi anavyolisema. Na yale yasiyosemwa yanaweza kutufunza mambo mengi sana. (Met. 16:24; Kol. 4:6) Utambuzi ni wa maana sana ili kupata furaha.—Soma Methali 24:3.

9 Kuhusu kuchagua tafrija na burudani, watu wengi wameona umuhimu wa kubadilikana. Kabla ya kufunga ndoa, huenda mwenzi wako alitumia wakati wake katika michezo au burudani fulani. Je, ni muhimu kufanya marekebisho fulani sasa? (1 Tim. 4:8) Swali hilo linahusu pia wakati unaotumiwa pamoja na watu wa ukoo. Inaeleweka kwamba wenzi wa ndoa wanahitaji wakati ili wafanye mambo ya kiroho na shughuli nyingine pamoja.—Mt. 6:33.

10. Kuwa mwenye usawaziko kutachangia jinsi gani uhusiano mzuri kati ya wazazi na watoto wao waliofunga ndoa?

10 Mwanamume anapooa, anaacha baba yake na mama yake, na mwanamke pia anafanya hivyo. (Soma Mwanzo 2:24.) Hata hivyo, mwongozo wa Mungu kuhusu kuwaheshimu baba na mama bado unatumika hata baada ya mtu kufunga ndoa. Hivyo hata baada ya watu kuoana, inaelekea watatumia wakati fulani pamoja na wazazi au wakwe zao. Mume mmoja, ambaye amekaa katika ndoa kwa miaka 25, anasema hivi: “Nyakati nyingine, ni vigumu kusawazisha mapendezi na mahitaji mbalimbali ya mwenzi wa ndoa na yale ya wazazi, ndugu na dada zako, na wakwe zako. Andiko la Mwanzo 2:24 limenisaidia sana kushughulikia hali hiyo. Mtu anapaswa kuwa mshikamanifu na kuwa na wajibu kuelekea washiriki wengine wa familia, hata hivyo, andiko hilo limenionyesha kwamba ninapaswa kwanza kuwa mshikamanifu kwa mwenzi wangu.” Kwa sababu hiyo, wazazi Wakristo wenye usawaziko watatambua kwamba watoto wao waliofunga ndoa wamo katika familia ambamo mume ndiye aliye na wajibu wa kuiongoza.

11, 12. Kwa nini funzo la familia na sala ni muhimu kwa wenzi wa ndoa?

11 Kujifunza Biblia kwa ukawaida katika familia ni jambo la maana sana. Mambo yaliyoonwa katika familia nyingi za Kikristo yanathibitisha jambo hilo. Huenda isiwe rahisi kuwa na funzo kama hilo au kulidumisha. Mume fulani anakiri hivi: “Ikiwa tungerudi nyuma na kubadili kila kitu, tungehakikisha kwamba tunajifunza kwa ukawaida kama familia tangu mwanzo wa ndoa yetu.” Anaongeza hivi: “Ni jambo lenye kupendeza kama nini kuona shangwe ambayo mke wangu anaonyesha anapochochewa na kweli fulani zenye kupendeza za Biblia tunazojifunza pamoja katika funzo letu!”

12 Msaada mwingine ni kusali pamoja. (Rom. 12:12) Mume na mke wanapoungana pamoja katika ibada ya Yehova, uhusiano wao wa karibu pamoja na Mungu unaweza kutia nguvu vifungo vyao vya ndoa. (Yak. 4:8) Mume mmoja Mkristo anasema hivi: “Kuomba msamaha haraka na kutaja makosa mnaposali pamoja ni njia moja ya kuonyesha kwamba mnahuzunikia kikweli hata jambo dogo linaloudhi.”—Efe. 6:18.

Uwe Mwenye Usawaziko Katika Ndoa

13. Ni shauri gani ambalo Paulo alitoa kuhusu uhusiano wa ngono katika ndoa?

13 Wenzi wa ndoa Wakristo wanahitaji kuepuka matendo ambayo yanaharibu uhusiano wa ndoa, kama yale ya watu wengi katika ulimwengu wa leo wenye wazimu wa ngono. Paulo alishauri hivi kuhusu jambo hilo: “Mume na ampe mke wake haki yake; lakini mke pia na amfanyie vivyo hivyo mume wake. Mke hana mamlaka juu ya mwili wake mwenyewe, bali mume wake anayo; vivyo hivyo, pia, mume hana mamlaka juu ya mwili wake mwenyewe, bali mke wake anayo.” Kisha, Paulo akatoa mwelekezo huu ulio wazi: “Msiwe mkinyimana haki hiyo, ila kwa makubaliano kwa wakati uliowekwa.” Kwa nini? “Ili mtenge wakati kwa ajili ya sala na mje pamoja tena, ili Shetani asiendelee kuwajaribu kwa sababu ya ninyi kukosa kujizuia.” (1 Kor. 7:3-5) Kwa kutaja sala, Paulo anaonyesha mambo ambayo Mkristo anapaswa kutanguliza. Lakini anaonyesha pia kwamba kila Mkristo aliyefunga ndoa anapaswa kutambua mahitaji ya kimwili na ya kihisia ya mwenzi wake.

14. Kanuni za Kimaandiko zinatumika jinsi gani inapohusu uhusiano wa ngono katika ndoa?

14 Mume na mke wanahitaji kuzungumza waziwazi na kutambua kwamba kukosa wororo katika uhusiano wa ngono kunaweza kutokeza matatizo. (Soma Wafilipi 2:3, 4; linganisha Mathayo 7:12.) Jambo hilo limethibitika kuwa kweli katika familia fulani zilizogawanyika kidini. Hata ikiwa kuna hali ya kutopatana, kwa kawaida Mkristo anaweza kuboresha mambo kwa kuwa na mwenendo mzuri, kuwa na fadhili, na ushirikiano. (Soma 1 Petro 3:1, 2.) Kumpenda Yehova na mwenzi wa ndoa, na pia kuwa na usawaziko, kutasaidia katika jambo hilo.

15. Heshima inatimiza sehemu gani katika ndoa yenye furaha?

15 Mume mwenye fadhili atamtendea mke wake kwa heshima katika mambo mengine pia. Kwa mfano, atafikiria hisia za mke wake, hata katika mambo madogo. Mume mmoja mwenye umri wa miaka 47 anakubali hivi: “Bado ninaendelea kujifunza kufanya hivyo.” Wake Wakristo wanahimizwa wawaheshimu sana waume zao. (Efe. 5:33) Si jambo la heshima kwa wanawake kuwachambua waume zao na kufunua makosa yao mbele ya wengine. Methali 14:1 inatukumbusha hivi: “Mwanamke mwenye hekima kwelikweli amejenga nyumba yake, lakini aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.”

Usikubaliane na Ibilisi

16. Wenzi wa ndoa wanaweza kutumia jinsi gani Waefeso 4:26, 27 katika ndoa yao?

16 “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.” (Efe. 4:26, 27) Maneno hayo yanapotumiwa yanaweza kutusaidia kusuluhisha matatizo au kuepuka kukosana katika ndoa. Dada mmoja anasema hivi: “Sikumbuki kamwe pindi yoyote tulipokosana na tukashindwa kuzungumzia tatizo na mume wangu hata ikiwa tungetumia saa nyingi kulitatua.” Mwanzoni mwa ndoa yao, yeye na mume wake waliazimia kwamba siku haingeisha bila wao kutatua tofauti zao. “Tuliamua kusameheana na kusahau haidhuru tulikuwa na tatizo gani, na hivyo kuanza kila siku vizuri.” Hivyo, walikataa ‘kumpa Ibilisi nafasi.’

17. Hata ikionekana kwamba wenzi wa ndoa hawafaani sana, ni jambo gani linaloweza kusaidia?

17 Lakini namna gani ikiwa ulifunga ndoa na mtu ambaye hufaani sana naye? Huenda ndoa yako isiwe na upendo kama ndoa za wengine. Hata hivyo, kukumbuka maoni ya Muumba kuhusu kifungo cha ndoa kutakusaidia. Akiongozwa na roho, Paulo aliwashauri hivi Wakristo: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Ebr. 13:4) Na maneno haya hayapaswi kamwe kupuuzwa: “Kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.” (Mhu. 4:12) Wanapohangaikia sana kutakaswa kwa jina la Yehova, mume na mke wanaunganishwa pamoja, na pia wanaunganishwa na Mungu. Wanapaswa kufanya bidii ili ndoa yao ifanikiwe, wakijua kwamba hilo linamletea sifa Yehova, Mwanzilishi wa ndoa.—1 Pet. 3:11.

18. Unaweza kuwa uhakika gani kuhusu ndoa?

18 Bila shaka, Wakristo wanaweza kupata shangwe katika ndoa. Hata hivyo, ili wapate shangwe ni lazima wajitahidi sana na waonyeshe sifa za Kikristo kama vile usawaziko. Leo, katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, kuna wenzi wengi wa ndoa ambao wanathibitisha kwamba hilo linawezekana.

Ungetoa Jibu Gani?

• Kwa nini inawezekana kupata shangwe katika ndoa?

• Ni nini kinachoweza kufanikisha ndoa?

• Ni sifa gani ambazo wenzi wa ndoa wanahitaji kusitawisha?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kwa hekima, wenzi wa ndoa wanawasiliana kabla ya kukubali mwaliko au kufanya mipango fulani

[Picha katika ukurasa wa 10]

Jitahidi kutatua matatizo siku hiyohiyo, na ‘usimpe Ibilisi nafasi’