Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umefurahia kusoma matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

• Wanajimu walienda kumwona Yesu wakati gani?

Tafsiri moja ya Biblia inasema hivi: “Mamajusi hawakwenda kumwona Yesu kwenye hori usiku aliozaliwa kama walivyofanya wachungaji. Walikuja baada ya miezi kadhaa.” Wakati huo, Yesu alikuwa “mtoto mchanga” na alikuwa anaishi katika nyumba. (Mt. 2:7-11) Ikiwa Yesu alipewa dhahabu na zawadi nyingine zenye thamani usiku aliozaliwa, je, Maria angetoa ndege wawili tu siku 40 baadaye kwenye hekalu?—1/1, ukurasa wa 31.

• Watu wengi wanaweza kufanya nini ili kuboresha maisha yao?

Mtu anaweza kujiuliza, ‘Je, ninaweza kurekebisha hali zangu na kurahisisha mtindo wangu wa maisha?’ Amy alifanya hivyo. Alikuwa tajiri lakini hakuwa na furaha. Alitambua kwamba alikuwa karibu kupotoshwa kutoka kwenye imani kwa sababu ya kufuatia kazi katika ulimwengu huu. Hivyo, aliamua kutanguliza mambo ya Ufalme naye aliweza kufanya upainia kwa muda fulani. Amy anasema hivi: “Sasa ninahisi nimetimiza jambo fulani, hisia ambayo sikuwahi kuwa nayo” nilipokuwa nikifuatia miradi ya ulimwengu.—1/15, ukurasa wa 19.

• Ni nini kinachoweza kuwasaidia akina mama wafanikiwe?

Mama wengi wanafanya kazi inayowaletea riziki. Wengine wanafanya hivyo ili kugharimia mahitaji ya msingi ya familia, na wengine ili wajitegemee kifedha au waishi maisha ya starehe. Mama wengine wanafanya kazi kwa sababu wanaifurahia. Mama Wakristo wanatimiza daraka la maana sana nyumbani hasa mtoto anapokuwa mchanga. Mama fulani wameamua kufanya kazi ya muda au kuacha kazi ili kuitunza familia, jambo ambalo linawafanya waridhike sana.—2/1, ukurasa wa 28-31.

• Ni “kizazi” gani ambacho Yesu alikuwa akizungumzia katika Mathayo 24:34?

Mara nyingi Yesu alitumia neno “kizazi” kiovu alipokuwa akizungumza na watu waovu au kuhusu watu hao. Lakini hakusema hivyo katika andiko hilo alipokuwa akizungumza na wanafunzi wake ambao punde si punde wangetiwa mafuta kwa roho takatifu. Hao ndio wangeweza kuelewa maana ya mambo yanayotajwa katika Mathayo 24:32, 33. Kwa hiyo, inaonekana kwamba Yesu alikuwa akizungumza kuhusu wafuasi wake watiwa-mafuta wa karne ya kwanza na wa leo.—2/15, ukurasa wa 23-24.

• Sheria ilikuwa mtunzaji kwa njia gani, kama andiko la Wagalatia 3:24 linavyosema?

Kwa kawaida, katika nyakati za zamani mtunzaji alikuwa mtumwa aliyetumainiwa ambaye alihakikisha kwamba mtoto yuko salama na kwamba maagizo ya baba kumhusu mtoto huyo yalifuatwa. Vivyo hivyo, Sheria iliwalinda Wayahudi kutokana na uvutano mpotovu, kama vile kuoana na wapagani. Lakini kama vile mtunzaji alivyomtunza mtoto kwa muda tu, ndivyo Sheria ilivyokuwa ya muda tu, na ilitumika mpaka Kristo alipofika.—3/1, ukurasa wa 18-21.

• Kulingana na Yakobo 3:17, tunapaswa kuonyesha sifa gani?

Tukiwa safi kiadili, tunapaswa kukataa kabisa mambo maovu bila kukawia. (Mwa. 39:7-9) Tunapaswa pia kuwa wenye amani, na kuepuka kuwachokoza wengine, au kuepuka matendo yanayoweza kuvuruga amani. Kwa hiyo, kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninajulikana kuwa mtu anayefanya amani au anayevuruga amani? Je, mara nyingi ninakosana na wengine? Je, ninaudhika kwa urahisi au mara nyingi ninawaudhi wengine? Au je, niko tayari kusamehe na ninaepuka kusisitiza wengine wafuate viwango vyangu?’—3/15, ukurasa wa 24-25.

• Kwa nini Yesu alimponya mtu fulani kipofu hatua kwa hatua? (Marko 8:22-26)

Biblia haisemi waziwazi kwa nini alifanya hivyo. Hata hivyo, inawezekana kwamba kwa kumponya mtu huyo kipofu hatua kwa hatua, Yesu alimpa wakati wa kutosha ili azoee hali yake mpya ya kuweza kuona. Hilo linaonyesha kwamba Yesu alimpenda na kumjali mtu huyo kipofu.—4/1, ukurasa wa 30.