Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kataa Kabisa “Vitu Visivyo na Thamani”

Kataa Kabisa “Vitu Visivyo na Thamani”

Kataa Kabisa “Vitu Visivyo na Thamani”

“Anayefuatilia vitu visivyo na thamani amepungukiwa moyoni.”—MET. 12:11.

1. Taja vitu fulani vyenye thamani tulivyo navyo, na ni njia gani bora zaidi ya kuvitumia?

TUKIWA Wakristo, sote tuna vitu mbalimbali vyenye thamani. Huenda vitu hivyo vikatia ndani afya nzuri na nguvu za kadiri, uwezo mzuri wa kiakili ambao tumerithi, au pesa. Tunafurahi kutumia vitu hivyo katika utumishi wa Yehova kwa sababu tunampenda, na hivyo tunatii himizo hili lililoandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu: “Mheshimu Yehova kwa vitu vyako vyenye thamani.”—Met. 3:9.

2. Biblia inatoa onyo gani kuhusu vitu visivyo na thamani, na onyo hilo linatumika jinsi gani?

2 Kwa upande mwingine, Biblia pia inazungumzia vitu visivyo na thamani na inatuonya tusipoteze wakati na nguvu zetu kwa kuvifuatilia. Fikiria maneno ya Methali 12:11 kuhusu vitu hivyo: “Anayelima shamba lake yeye mwenyewe atashiba mkate, lakini anayefuatilia vitu visivyo na thamani amepungukiwa moyoni.” Ni rahisi kuona ukweli wa methali hiyo. Mtu akitumia wakati na nguvu zake kuitafutia familia yake riziki, huenda akapata usalama fulani wa kifedha na wa kimwili. (1 Tim. 5:8) Hata hivyo, akipoteza wakati na nguvu zake kufuatilia vitu visivyo na thamani, anaonyesha kwamba “amepungukiwa moyoni,” yaani, amekosa usawaziko na nia nzuri. Inaelekea sana kwamba mtu kama huyo atakuwa na uhitaji.

3. Onyo la Biblia kuhusu vitu visivyo na thamani linahusu ibada yetu jinsi gani?

3 Hata hivyo, namna gani tukitumia kanuni ya methali hiyo kuhusiana na ibada yetu? Tunapofanya hivyo tunaona kwamba Mkristo ambaye anamtumikia Yehova kwa bidii na uaminifu ana usalama wa kweli. Anaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atambariki sasa naye ana tumaini hakika la wakati ujao. (Mt. 6:33; 1 Tim. 4:10) Lakini, Mkristo ambaye anakengeushwa na vitu visivyo na thamani anahatarisha uhusiano wake pamoja na Yehova na tumaini lake la uzima wa milele. Tunaweza kuepuka hatari hiyo jinsi gani? Ni lazima tutambue vitu “visivyo na thamani” katika maisha yetu na kusitawisha azimio la kuvikataa kabisa.—Soma Tito 2:11, 12.

4. Kwa ujumla, ni vitu gani visivyo na thamani?

4 Basi, ni vitu gani visivyo na thamani? Kwa ujumla, vinaweza kuwa vitu vyovyote vinavyotuzuia tusimtumikie Yehova kwa nafsi yote. Kwa mfano, vinaweza kutia ndani aina mbalimbali za burudani. Bila shaka, tunaweza kufaidika tunapofurahia burudani kwa kiasi. Lakini tukitumia wakati mwingi sana kuponda raha na kupuuza utendaji unaohusiana na ibada yetu, burudani inakuwa kitu kisicho na thamani, na inaweza kuharibu uhusiano wetu pamoja na Mungu. (Mhu. 2:24; 4:6) Ili kuepuka jambo hilo, Mkristo anakuwa na usawaziko kwa kuwa mwangalifu kuhusu jinsi anavyotumia wakati wake wenye thamani. (Soma Wakolosai 4:5.) Hata hivyo, kuna vitu visivyo na thamani ambavyo ni hatari zaidi kuliko burudani. Vinatia ndani miungu ya uwongo.

Kataa Kabisa Miungu Isiyo na Thamani

5. Mara nyingi Biblia inatumia maneno “isiyo na thamani” kuhusiana na nini?

5 Inastaajabisha kwamba mistari mingi ya Biblia ambayo ina maneno “isiyo na thamani,” inahusu miungu ya uwongo. Kwa mfano, Yehova aliwaambia Waisraeli hivi: “Msijifanyie miungu isiyo na thamani, wala msijisimamishie sanamu ya kuchongwa au nguzo takatifu, wala msiweke jiwe kuwa sanamu katika nchi yenu ili kuliinamia.” (Law. 26:1) Mfalme Daudi aliandika hivi: “Yehova ni mkuu na wa kusifiwa sana, naye ni wa kuogopwa kuliko miungu mingine yote. Kwa maana miungu yote ya vikundi vya watu ni miungu isiyo na thamani. Lakini Yehova, alizifanya mbingu.”—1 Nya. 16:25, 26.

6. Kwa nini miungu ya uwongo haina thamani?

6 Kama Daudi alivyoonyesha, tumezungukwa na vitu vingi vinavyothibitisha kwamba Yehova ni mkuu. (Zab. 139:14; 148:1-10) Waisraeli walikuwa na pendeleo kubwa kama nini la kuwa na uhusiano wa agano pamoja na Yehova! Walikuwa wapumbavu kama nini kwa kumpa mgongo na kuinamia sanamu za kuchongwa na nguzo takatifu! Nyakati za taabu, miungu yao ya uwongo ilithibitika kuwa isiyo na thamani yoyote. Haikuwa na nguvu za kuwaokoa wale walioiabudu wala haikuwa na nguvu za kujiokoa yenyewe.—Amu. 10:14, 15; Isa. 46:5-7.

7, 8. “Utajiri” unaweza kuwa kama mungu jinsi gani?

7 Katika nchi nyingi leo, bado watu wanainamia sanamu zilizotengenezwa na watu, na miungu kama hiyo ni ya bure tu kama ilivyokuwa zamani. (1 Yoh. 5:21) Hata hivyo, zaidi ya miungu, Biblia inataja vitu vingine pia kuwa sanamu. Kwa mfano, fikiria maneno haya ya Yesu: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.”—Mt. 6:24.

8 “Utajiri” unaweza kuwa kama mungu jinsi gani? Kwa mfano, fikiria jiwe likiwa kwenye uwanja fulani katika Israeli la kale. Jiwe kama hilo lingeweza kutumiwa kujenga nyumba au ukuta. Kwa upande mwingine, ikiwa lingewekwa kama “nguzo takatifu” au ‘jiwe ambalo ni sanamu,’ lingewakwaza watu wa Yehova. (Law. 26:1) Vivyo hivyo, pesa zina faida zake. Tunazihitaji ili kuishi, na tunaweza kuzitumia vizuri katika utumishi wa Yehova. (Mhu. 7:12; Luka 16:9) Lakini tukitanguliza pesa badala ya utumishi wetu wa Kikristo, pesa zinakuwa kama mungu kwetu. (Soma 1 Timotheo 6:9, 10.) Katika ulimwengu huu, ambamo watu wanathamini sana utajiri, ni lazima tuhakikishe kwamba tunadumisha maoni yenye usawaziko kuhusu pesa.—1 Tim. 6:17-19.

9, 10. (a) Mkristo ana maoni gani kuhusu elimu? (b) Elimu ya juu ina hatari gani?

9 Mfano mwingine wa kitu chenye faida ambacho kinaweza kuwa kisicho na thamani ni elimu ya ulimwengu. Tunataka watoto wetu wapate elimu nzuri ili wafanikiwe katika maisha. Jambo la maana hata zaidi ni kwamba Mkristo mwenye elimu anaweza kusoma Biblia na kuielewa, kuchanganua matatizo na kufanya maamuzi mazuri, na kufundisha kweli za Biblia kwa njia iliyo wazi na yenye kusadikisha. Kupata elimu nzuri kunachukua wakati, lakini faida ni nyingi.

10 Lakini namna gani kuhusu kupata elimu ya juu katika chuo kikuu au chuo kingine? Watu wengi wanaona kupata elimu ya juu kuwa jambo la maana sana ili mtu afanikiwe. Hata hivyo, mwishowe akili za watu wengi wanaofuatia elimu kama hiyo zinajaa hekima ya ulimwengu yenye kudhuru. Elimu kama hiyo inapoteza miaka yenye thamani ya ujana ambayo ingeweza kutumiwa vizuri katika utumishi wa Yehova. (Mhu. 12:1) Haishangazi kwamba katika nchi ambako wengi wamepata elimu hiyo, watu wengi sana hawamwamini Mungu. Badala ya kutegemea elimu ya juu ya ulimwengu huu ilete usalama, Mkristo anamtegemea Yehova.—Met. 3:5.

Msiache Tamaa ya Mwili Iwe Kama Mungu

11, 12. Kwa nini Paulo alisema hivi kuhusu watu fulani: “Mungu wao ni tumbo lao”?

11 Katika barua yake kwa Wafilipi, mtume Paulo anataja jambo lingine ambalo linaweza kuwa mungu. Anasema hivi kuhusu watu fulani ambao walikuwa waabudu wenzake zamani: “Kuna wengi, nilikuwa nikiwataja mara nyingi lakini sasa nawataja pia nikilia, wanaotembea kama adui za mti wa mateso wa Kristo, na mwisho wao ni uharibifu, na mungu wao ni tumbo lao, . . . nao wamekaza akili zao juu ya vitu vilivyo duniani.” (Flp. 3:18, 19) Tumbo la mtu linaweza kuwa mungu jinsi gani?

12 Inaonekana kwamba watu hao ambao Paulo alifahamiana nao waliona tamaa ya mwili kuwa ya maana sana kuliko kumtumikia Yehova kama Paulo. Huenda wengine wao walikula na kunywa mpaka wakawa walafi au walevi. (Met. 23:20, 21; linganisha na Kumbukumbu la Torati 21:18-21.) Labda wengine waliamua kutumia kikamili nafasi zilizokuwapo katika ulimwengu wa karne ya kwanza na hivyo wakakengeushwa na kuacha kumtumikia Yehova. Na tusiruhusu kamwe tamaa ya kupata yale yanayoitwa eti maisha mazuri ituzuie tusimtumikie Yehova kwa nafsi yote.—Kol. 3:23, 24.

13. (a) Ni nini maana ya kutamani, na Paulo alifafanua sifa hiyo jinsi gani? (b) Tunaweza kufanya nini ili kuepuka kutamani?

13 Paulo alitaja jambo lingine linalohusiana na ibada ya uwongo. Aliandika hivi: “Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.” (Kol. 3:5) Kutamani kunamaanisha kutaka sana kitu fulani ambacho hatuna. Tamaa hiyo inaweza kutia ndani tamaa ya vitu vya kimwili au hata tamaa ya ngono haramu. (Kut. 20:17) Kwa kuwa kutamani mambo hayo ni sawa na ibada ya sanamu au ibada ya mungu wa uwongo, je, hatuoni kwamba kuyatamani ni jambo zito? Yesu alitumia mfano ulio wazi kuonyesha umuhimu wa kujitahidi kabisa kuzuia tamaa hizo mbaya.—Soma Marko 9:47; 1 Yohana 2:16.

Jihadhari na Maneno Yasiyo na Thamani

14, 15. (a) Watu wengi katika siku za Yeremia walikwazwa na ‘kitu gani kisicho na thamani’? (b) Kwa nini maneno ya Musa yalikuwa na thamani?

14 Vitu visivyo na thamani vinaweza kutia ndani maneno. Kwa mfano, Yehova alimwambia Yeremia hivi: “Manabii wanatoa unabii wa uwongo katika jina langu. Mimi sikuwatuma, wala sikuwaamuru wala kusema nao. Maono ya uwongo na uaguzi na kitu kisicho na thamani na udanganyifu wa moyo wao ndiyo mambo wanayowaambia ninyi kwa njia ya unabii.” (Yer. 14:14) Manabii hao wa uwongo walidai kwamba wanasema kwa jina la Yehova, lakini walikuwa wakifundisha mawazo yao, hekima yao wenyewe. Kwa hiyo, maneno yao yalikuwa “kitu kisicho na thamani.” Hayakuwa na faida yoyote na yalikuwa hatari sana kiroho. Katika mwaka wa 607 K.W.K., watu wengi waliosikiliza maneno hayo yasiyo na thamani walikufa kifo cha mapema mikononi mwa askari-jeshi Wababiloni.

15 Kwa upande mwingine, Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “Tieni mioyo yenu katika maneno yote ninayosema kwa kuwaonya ninyi leo . . . Kwa maana hilo si neno lisilo na thamani kwenu, bali linamaanisha uhai wenu, na kwa neno hili mnaweza kurefusha siku zenu juu ya udongo ambao mnavuka Yordani ili kuumiliki.” (Kum. 32:46, 47) Ndiyo, maneno ya Musa yaliongozwa na roho ya Mungu. Hivyo, yalikuwa na thamani, ndiyo, yalikuwa ya maana sana ili taifa hilo liwe na hali nzuri. Wale ambao waliyatii waliishi kwa muda mrefu, nao walifanikiwa. Na tukatae sikuzote maneno yasiyo na thamani na kushikamana na maneno yenye thamani ya kweli.

16. Tuna maoni gani kuhusu maneno ya wanasayansi yanayopingana na Neno la Mungu?

16 Je, tunasikia mambo yasiyo na thamani yakisemwa leo? Ndiyo. Kwa mfano, wanasayansi fulani wanasema kwamba fundisho la mageuzi na mambo mengine ambayo yamegunduliwa na sayansi yanaonyesha kwamba hakuna haja ya kumwamini Mungu, na kwamba kila kitu kilitokana na utendaji wa kiasili. Je, tunapaswa kuhangaishwa na maneno hayo yanayochochewa na kiburi? Hapana! Hekima ya wanadamu inatofautiana na hekima ya Mungu. (1 Kor. 2:6, 7) Hata hivyo, tunajua kwamba mafundisho ya wanadamu yanapopingana na yale ambayo Mungu amefunua, sikuzote ni mafundisho ya wanadamu yanayoonekana kuwa na kasoro. (Soma Waroma 3:4.) Hata ingawa sayansi imeleta maendeleo katika sehemu mbalimbali za maisha, maneno ya Biblia kuhusu hekima ya wanadamu bado ni ya kweli: “Hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu.” Hekima ya wanadamu ni ubatili ikilinganishwa na hekima ya Mungu isiyo na mipaka.—1 Kor. 3:18-20.

17. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu maneno ya waasi-imani na ya viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo?

17 Mfano mwingine wa maneno yasiyo na thamani ni yale yanayosemwa na viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo. Viongozi hao wanadai kwamba wanasema kwa jina la Mungu, lakini maneno mengi wanayosema hayategemei Maandiko, na kwa kweli hayana faida yoyote. Pia, waasi-imani wanasema maneno yasiyo na thamani, wakidai kwamba wana hekima nyingi zaidi kuliko yule “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye amewekwa rasmi. (Mt. 24:45-47) Hata hivyo, waasi-imani wanasema hekima yao wenyewe, na maneno yao hayana thamani, yanamkwaza mtu yeyote anayeyasikiliza. (Luka 17:1, 2) Tunaweza kufanya nini ili tusidanganywe nao?

Jinsi ya Kukataa Kabisa Maneno Yasiyo na Thamani

18. Tunaweza kutumia shauri la 1 Yohana 4:1 katika njia gani?

18 Mtume Yohana aliyezeeka alitoa shauri zuri kuhusu jambo hilo. (Soma 1 Yohana 4:1.) Kulingana na shauri la Yohana, sikuzote tunawatia moyo wale ambao tunawahubiria wajaribu mambo ambayo wamefundishwa kwa kuyalinganisha na Biblia. Hiyo ni kanuni nzuri ambayo sisi pia tunapaswa kufuata. Tukisikia maneno yoyote yanayopinga ile kweli au yanayochafua jina la kutaniko, wazee, au ndugu yetu yeyote, hatupaswi kuyaamini tu bila kuyachunguza. Badala yake, tunapaswa kujiuliza hivi: “Je, yule anayesambaza habari hizi anatenda kupatana na yale ambayo Biblia inasema? Je, habari hizi au madai haya yanaendeleza kusudi la Yehova? Je, yanadumisha amani ya kutaniko?” Jambo lolote tunalosikia ambalo linabomoa undugu wetu badala ya kuujenga ni kitu kisicho na thamani.—2 Kor. 13:10, 11.

19. Wazee wanahakikisha namna gani kwamba maneno yao ni yenye thamani?

19 Wazee pia wanajifunza somo la maana kuhusu maneno yasiyo na thamani. Wakati wowote wanapohitaji kutoa mashauri, wanakumbuka udhaifu wao, nao wanaepuka kabisa kutoa mashauri yanayotegemea ujuzi wao maishani. Sikuzote wanapaswa kuonyesha yale ambayo Biblia inasema. Maneno haya ya mtume Paulo yanaonyesha kanuni nzuri inayopaswa kufuatwa: “Msipite mambo yaliyoandikwa.” (1 Kor. 4:6) Wazee hawapiti mambo yaliyoandikwa katika Biblia. Na kwa kuongezea, hawapiti mashauri yanayotegemea Biblia yaliyoandikwa katika vichapo vya mtumwa mwaminifu na mwenye busara.

20. Ni mambo gani yanayotusaidia kukataa kabisa vitu visivyo na thamani?

20 Vitu visivyo na thamani ni hatari sana, iwe ni “miungu,” maneno, au kitu kingine chochote. Kwa sababu hiyo, tunasali sikuzote ili Yehova atusaidie kutambua vitu vyote visivyo na thamani, na tunamwomba atuongoze ili tujue jinsi ya kuvikataa kabisa. Tunapofanya hivyo, tunamwiga mtunga-zaburi aliyesema hivi: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa; unihifadhi hai katika njia yako mwenyewe.” (Zab. 119:37) Katika habari inayofuata, tutazungumza zaidi kuhusu faida za kukubali mwongozo wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa ujumla, ni ‘vitu gani visivyo na thamani’ tunavyopaswa kukataa kabisa?

• Tunaweza kufanya nini ili pesa zisiwe kama mungu kwetu?

• Tamaa za mwili zinaweza kuwa ibada ya sanamu kwa njia gani?

• Tunaweza kufanya nini ili kukataa kabisa maneno yasiyo na thamani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 3]

Waisraeli walitiwa moyo ‘walime shamba lao,’ badala ya kufuatilia vitu visivyo na thamani

[Picha katika ukurasa wa 5]

Usiruhusu kamwe tamaa ya vitu vya kimwili ipunguze bidii yako ya kumtumikia Yehova

[Picha katika ukurasa wa 6]

Maneno ya wazee yanaweza kuwa na thamani kubwa