Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yohana

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yohana

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yohana

YOHANA—“mwanafunzi ambaye Yesu alikuwa akimpenda”—ndiye mtu wa mwisho kuandika simulizi lililoongozwa na roho kuhusu maisha na huduma ya Kristo. (Yoh. 21:20) Injili ya Yohana, ambayo iliandikwa wapata mwaka wa 98 W.K., inarudia mambo machache sana yaliyotajwa katika Injili zile nyingine tatu.

Mtume Yohana aliandika Injili yake akiwa na kusudi hususa akilini. Alisema hivi kuhusu mambo ambayo aliandika: “Haya yameandikwa ili mpate kuamini kwamba Yesu ndiye Kristo Mwana wa Mungu, na kwamba, kwa sababu ya kuamini, mpate kuwa na uzima kupitia jina lake.” (Yoh. 20:31) Ujumbe wake ni wa maana sana kwetu.—Ebr. 4:12.

“ONA, MWANA-KONDOO WA MUNGU”

(Yoh. 1:1–11:54)

Anapomwona Yesu, Yohana Mbatizaji anatangaza hivi kwa uhakika: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu!” (Yoh. 1:29) Yesu anaposafiri kupitia Samaria, Galilaya, Yudea, na nchi iliyo mashariki mwa Yordani akihubiri, kufundisha, na kufanya kazi nyingi zenye nguvu, ‘watu wengi wanamjia na kumwamini.’—Yoh. 10:41, 42.

Moja ya miujiza ya pekee ambayo Yesu anafanya ni kumfufua Lazaro. Wengi wanamwamini Yesu wanapomwona mtu aliyekufa kwa siku nne akiwa hai tena. Hata hivyo, wakuu wa makuhani na Mafarisayo wanakata shauri kumuua Yesu. Hivyo, Yesu anatoka huko na kwenda kwenye ‘nchi iliyo karibu na nyika, na kuingia katika jiji linaloitwa Efraimu.’—Yoh. 11:53, 54.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:35, 40—Zaidi ya Andrea, ni mwanafunzi gani aliyesimama pamoja na Yohana Mbatizaji? Pindi zote, msimuliaji anamrejelea Yohana Mbatizaji kuwa “Yohana,” naye hatumii kamwe jina hilo katika Injili yake. Hivyo, inaonekana kwamba mwanafunzi huyo asiyetajwa kwa jina ambaye aliandika Injili hiyo ni Yohana.

2:20—Ni hekalu gani ambalo “lilijengwa kwa miaka 46”? Wayahudi walikuwa wakizungumzia kujengwa upya kwa hekalu la Zerubabeli na Mfalme Herode wa Yudea. Kulingana na mwanahistoria Yosefo, kazi hiyo ilianza mwaka wa 18 wa utawala wa Herode, au mwaka wa 18/17 K.W.K. Patakatifu pa hekalu na majengo mengine makuu yalijengwa kwa miaka minane. Hata hivyo, ujenzi wa hekalu uliendelea hata baada ya Pasaka ya 30 W.K., wakati ambapo Wayahudi walisema hekalu lilijengwa kwa miaka 46.

5:14—Je, ugonjwa unasababishwa na kutenda dhambi? Si nyakati zote. Mtu aliyeponywa na Yesu alikuwa mgonjwa kwa miaka 38 kwa sababu ya kurithi hali ya kutokamilika. (Yoh. 5:1-9) Kile ambacho Yesu alimaanisha ni kwamba kwa kuwa sasa mtu huyo alikuwa ameonyeshwa rehema, ilimpasa kufuata njia ya wokovu na kuepuka kutenda dhambi kimakusudi ili asipatwe na madhara makubwa zaidi kuliko ugonjwa. Mtu huyo angekuwa na hatia ya kutenda dhambi isiyoweza kusamehewa, ambayo ingefanya astahili kufa bila tumaini la ufufuo.—Mt. 12:31, 32; Luka 12:10; Ebr. 10:26, 27.

5:24, 25—Ni nani ambao ‘wamevuka kutoka katika kifo na kuingia katika uzima’? Yesu anazungumza kuhusu watu ambao wakati fulani walikuwa wamekufa kiroho lakini ambao baada ya kusikia maneno yake walimwamini na kuacha mazoea ya kutenda dhambi. ‘Wanavuka kutoka katika kifo na kuingia katika uzima’ katika maana ya kwamba wanaondolewa hukumu ya kifo, nao wanapewa tumaini la uzima wa milele kwa sababu ya kumwamini Mungu.—1 Pet. 4:3-6.

5:26; 6:53—Ni nini maana ya mtu kuwa na “uzima ndani yake mwenyewe”? Kwa upande wa Yesu Kristo, hilo linamaanisha kupokea kutoka kwa Mungu uwezo wa aina mbili—uwezo wa kuwapa wanadamu msimamo mzuri mbele za Yehova na uwezo wa kuwapa watu uhai kwa kuwafufua wafu. Kwa upande wa wafuasi wa Yesu, ‘kuwa na uhai ndani yao wenyewe’ kunamaanisha kupata uhai kamili. Wakristo waliotiwa mafuta wanapata uhai huo wanapofufuliwa kuishi mbinguni. Waaminifu wenye tumaini la kuishi duniani watapata uhai kamili baada ya kupita jaribu la mwisho ambalo litatukia punde tu baada ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo.—1 Kor. 15:52, 53; Ufu. 20:5, 7-10.

6:64—Wakati ambapo Yesu alimchagua Yuda Iskariote, je, Yesu alijua kwamba Yuda atamsaliti? Inaonekana hakujua. Hata hivyo, pindi moja katika mwaka wa 32 W.K., Yesu aliwaambia mitume wake: “Mmoja wenu ni mchongezi.” Inawezekana kwamba wakati huo, Yesu alitambua kwamba Yuda Iskariote alikuwa ‘ameanza’ kufuata njia isiyofaa.—Yoh. 6:66-71.

Mambo Tunayojifunza:

2:4. Yesu alikuwa akimdokezea Maria kwamba kwa kuwa yeye ni Mwana wa Mungu aliyebatizwa na kutiwa mafuta, anapaswa kupata maagizo kutoka kwa Baba yake wa mbinguni. Ingawa Yesu alikuwa akianza tu huduma yake, alijua kabisa saa, au wakati, wa huduma aliyopewa, kutia ndani kifo chake cha kujidhabihu. Hakuna mtu yeyote, hata mtu wa karibu wa familia yake kama Maria, ambaye angeruhusiwa kumzuia asitimize mapenzi ya Mungu. Tunapaswa kumtumikia Yehova Mungu tukiwa na azimio kama hilo.

3:1-9. Tunajifunza mambo mawili kupitia mfano wa Nikodemo, mtawala wa Wayahudi. Kwanza, kwa kumwona mwana wa seremala wa hali ya chini kuwa mwalimu aliyetumwa na Mungu, Nikodemo alionyesha unyenyekevu, ufahamu, na alitambua uhitaji wake wa kiroho. Leo, Wakristo wa kweli wanahitaji kuwa wanyenyekevu. Pili, Nikodemo alisita kuwa mwanafunzi wakati Yesu alipokuwa duniani. Huenda ilikuwa kwa sababu aliogopa wanadamu, alipenda sana cheo chake katika Sanhedrini, au alipenda mali. Kutokana na hilo, tunajifunza somo hili la maana: Hatupaswi kuruhusu mambo hayo yatuzuie ‘tusiuchukue mti wetu wa mateso na kumfuata Yesu sikuzote.’—Luka 9:23.

4:23, 24. Ili ibada yetu impendeze Mungu, inapaswa kupatana na kweli inayofunuliwa katika Biblia na inapaswa kuongozwa na roho takatifu.

6:27. Kufanyia kazi “chakula ambacho hudumu kufikia uzima wa milele” kunamaanisha kujitahidi kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho. Tunapofanya hivyo, tunakuwa na furaha.—Mt. 5:3.

6:44. Yehova anatujali kibinafsi. Anatuvuta kwa Mwana wake kwa kutufikia kibinafsi kupitia kazi ya kuhubiri na kwa kutusaidia kuelewa na kutumia kweli za Biblia kupitia roho Yake takatifu.

11:33-36. Kuonyesha hisia zetu si udhaifu.

‘ENDELEA KUMFUATA’

(Yohana 11:55–21:25)

Pasaka ya 33 W.K. inapokaribia, Yesu anarudi Bethania. Nisani 9, anakuja Yerusalemu, akiwa amepanda punda. Nisani 10, Yesu anafika hekaluni tena. Sala yake kwamba jina la Baba yake litukuzwe inajibiwa na sauti inayotoka mbinguni ambayo inasema: “Nimelitukuza na pia nitalitukuza tena.”—Yoh. 12:28.

Mlo wa Pasaka unapoendelea, Yesu anawapa wafuasi wake mashauri ya mwisho-mwisho na kusali kwa ajili yao. Baada ya kukamatwa, kujaribiwa, na kutundikwa mtini, Yesu anafufuliwa.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

14:2—Ni kwa njia gani Yesu ‘angetayarisha mahali’ mbinguni kwa ajili ya wafuasi wake waaminifu? Matayarisho hayo yangetia ndani kuhalalisha agano jipya kwa kufika mbele za Mungu na kumpa thamani ya damu yake. Pia, matayarisho hayo yangetia ndani Kristo kupokea mamlaka ya kifalme, kisha ufufuo wa wafuasi wake watiwa-mafuta watakaoishi mbinguni ungeanza.—1 The. 4:14-17; Ebr. 9:12, 24-28; 1 Pet. 1:19; Ufu. 11:15.

19:11—Je, Yesu alikuwa akizungumza kumhusu Yuda Iskariote alipokuwa akiongea na Pilato kuhusu mtu ambaye Alimtia mikononi mwake? Yesu hakuwa akizungumza kuhusu Yuda au mtu fulani hususa, bali inaonekana kwamba alimaanisha watu wote waliokuwa na hatia ya kushiriki katika dhambi ya kumuua. Hao walitia ndani Yuda, “wakuu wa makuhani na Sanhedrini nzima,” na hata “umati” ulioshawishiwa kuomba Baraba afunguliwe.—Mt. 26:59-65; 27:1, 2, 20-22.

20:17—Kwa nini Yesu alimwambia Maria Magdalene aache kumng’ang’ania? Inaonekana kwamba Maria alimng’ang’ania Yesu kwa sababu alifikiri kwamba Yesu alikuwa karibu kupanda kwenda mbinguni naye hangemwona tena kamwe. Ili kumhakikishia kwamba hangeondoka wakati huo, Yesu alimwambia Maria aache kumng’ang’ania, na badala yake aende kuwapasha habari wanafunzi wake kwamba amefufuliwa.

Mambo Tunayojifunza:

12:36. Ili tuwe “wana wa nuru,” au wachukuaji wa nuru, tunahitaji kupata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu, Biblia. Halafu tunapaswa kutumia ujuzi huo kuwavuta watu kutoka kwenye giza la kiroho na kuingia katika nuru ya Mungu.

14:6. Hatuwezi kupata kibali cha Mungu isipokuwa tu kupitia Yesu Kristo. Ni kwa kumwamini tu Yesu na kufuata mfano wake ndipo tunaweza kumkaribia Yehova.—1 Pet. 2:21.

14:15, 21, 23, 24; 15:10. Kutii mapenzi ya Mungu kutatusaidia kukaa katika upendo wa Mungu na katika upendo wa Mwana wake.—1 Yoh. 5:3.

14:26; 16:13. Roho takatifu ya Yehova inatufundisha na kutukumbusha mambo. Pia inafunua kweli. Hivyo, inaweza kutusaidia kuongeza ujuzi, hekima, ufahamu, utambuzi, na uwezo wa kufikiri. Hivyo, tunapaswa kudumu katika sala, na kusema waziwazi katika sala kwamba tunahitaji roho hiyo.—Luka 11:5-13.

21:15, 19. Petro aliulizwa ikiwa anampenda Yesu kuliko “hawa,” yaani, samaki waliokuwa hapo. Hivyo, Yesu alikazia kwamba Petro anahitaji kuchagua kumfuata nyakati zote badala ya kufuatia kazi ya uvuvi. Baada ya kuchunguza masimulizi ya Injili, acheni tuazimie hata zaidi kumpenda Yesu kuliko vitu vingine vyovyote vinavyoweza kutuvutia. Ndiyo, acheni tuendelee kumfuata kwa moyo wote.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Tunajifunza nini kutokana na Nikodemo?