Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ndoa na Kuwa Mzazi Katika Wakati Huu wa Mwisho

Ndoa na Kuwa Mzazi Katika Wakati Huu wa Mwisho

Ndoa na Kuwa Mzazi Katika Wakati Huu wa Mwisho

“Wakati uliobaki umepungua.”—1 KOR. 7:29.

1. (a) Ni mabadiliko gani yanayotukia leo yaliyo kati ya mambo ‘magumu kushughulika nayo’? (b) Kwa nini mabadiliko katika viwango vya familia yanatuhusu?

NENO la Mungu lilitabiri kwamba katika “wakati wa mwisho” kungekuwa na vita, matetemeko ya nchi, njaa, na tauni au magonjwa ya kuambukiza. (Dan. 8:17, 19; Luka 21:10, 11) Pia, Biblia ilionya kwamba kipindi hiki kigumu katika historia ya wanadamu kingekuwa kipindi cha mabadiliko makubwa ya kijamii. Misukosuko katika familia ingekuwa kati ya mambo yaliyo ‘magumu kushughulika nayo’ katika ‘siku hizi za mwisho’ zenye hatari. (2 Tim. 3:1-4) Kwa nini mabadiliko hayo yanatuhusu? Ni kwa sababu yameenea sana na yana nguvu sana hivi kwamba yanaweza kubadili maoni ya Wakristo leo kuhusu ndoa na wajibu wa kuwa mzazi. Katika njia gani?

2. Kwa kawaida, ulimwengu una maoni gani kuhusu ndoa na talaka?

2 Leo, talaka zimeenea sana na ni rahisi kutalikiana, na idadi ya talaka inaongezeka katika nchi nyingi. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba maoni ya Yehova Mungu kuhusu ndoa na talaka ni tofauti kabisa na yale yanayokubalika ulimwenguni leo. Kwa hiyo, Yehova ana maoni gani?

3. Yehova na Yesu Kristo wana maoni gani kuhusu ndoa?

3 Yehova Mungu anawatazamia wale waliofunga ndoa wabaki waaminifu kwa nadhiri zao za ndoa. Alipounganisha mwanamume na mwanamke wa kwanza katika ndoa, Yehova alisema kwamba “mwanamume . . . atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.” Baadaye, Yesu Kristo alirudia kutaja maneno hayo na akaongeza hivi: “Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” Zaidi ya hayo, Yesu alisema hivi: “Mtu yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine, ila kwa sababu ya uasherati, anafanya uzinzi.” (Mwa. 2:24; Mt. 19:3-6, 9) Kwa hiyo, Yehova na Yesu wanaiona ndoa kuwa kifungo cha maisha ambacho kinakoma tu mwenzi mmoja anapokufa. (1 Kor. 7:39) Kwa kuwa ndoa ni mpango mtakatifu, watu hawapaswi kutalikiana kimchezo tu. Kwa kweli, Neno la Mungu linasema kwamba Yehova anachukia talaka ambayo haina msingi wa Kimaandiko. *Soma Malaki 2:13-16; 3:6.

Kuichukua Ndoa kwa Uzito

4. Kwa nini vijana fulani Wakristo wanajuta kwamba waliamua kufunga ndoa haraka?

4 Ulimwengu usiomwogopa Mungu ambamo tunaishi leo unapenda sana mambo ya ngono. Kila siku, tunaonyeshwa picha nyingi za ngono. Hatuwezi kupuuza matokeo mabaya ambayo picha hizo zinaweza kuwa nayo juu yetu, hasa juu ya vijana wetu wapendwa katika kutaniko. Vijana Wakristo wanapaswa kutenda jinsi gani kuhusu uvutano huo usiofaa, ambao unaweza kuamsha tamaa ya ngono hata bila wao kupenda? Wengine wamejaribu kukabiliana na tamaa hiyo kwa kufunga ndoa wakiwa na umri mdogo sana. Wanafikiri kwamba kwa kufanya hivyo hawatajiingiza katika mwenendo mchafu kingono. Hata hivyo, muda mfupi baada ya kufunga ndoa, wengi wamejuta kwa sababu ya uamuzi huo. Kwa nini? Kwa sababu baada ya furaha ya kufunga ndoa kupungua, wametambua kwamba wao na wenzi wao hawapatani katika mambo mengi ya kila siku. Inaeleweka kwa nini wenzi wa ndoa kama hao wana matatizo mazito.

5. Ni nini kitakachowasaidia wenzi wa ndoa kubaki waaminifu kwa nadhiri yao ya arusi? (Ona pia maelezo ya chini.)

5 Bila shaka, matatizo yanaweza kutokea ukigundua kwamba umefunga ndoa na mtu ambaye ni tofauti kabisa na vile ulivyotazamia, hata ikiwa ni Mkristo mwenzako. (1 Kor. 7:28) Lakini, hata ndoa iwe na matatizo gani, Wakristo wa kweli wanajua kwamba kutalikiana bila msingi wa Kimaandiko si suluhisho linalokubalika kwa matatizo ya ndoa isiyo na furaha. Hivyo, wale ambao wanaendelea kujitahidi kulinda ndoa yao kwa sababu wanataka kubaki waaminifu kwa nadhiri yao ya arusi, wanastahili kuheshimiwa na kusaidiwa kwa upendo na kutaniko la Kikristo. *

6. Vijana Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kufunga ndoa?

6 Je, wewe ni kijana ambaye hajaoa? Ikiwa ndivyo, unapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kufunga ndoa? Unaweza kuepuka maumivu mengi ya hisia ikiwa utangoja mpaka utakapokuwa tayari kimwili, kiakili, na kiroho kabla ya kuanza uhusiano wa kimapenzi pamoja na Mkristo wa jinsia tofauti. Bila shaka, Maandiko hayataji umri wa kufunga ndoa. * Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba unapaswa kungoja mpaka upite kipindi ambacho hisia za ngono ni zenye nguvu sana. (1 Kor. 7:36) Kwa nini? Kwa sababu tamaa zenye nguvu za ngono zinaweza kufanya utende bila kufikiri na kukuongoza kufanya uamuzi usio wa hekima ambao unaweza kuleta maumivu ya hisia baadaye. Kumbuka kwamba mashauri ya Yehova yaliyo katika Biblia kuhusu ndoa ni yenye hekima na yatakuletea faida na furaha.—Soma Isaya 48:17, 18.

Kuchukua kwa Uzito Wajibu wa Kuwa Mzazi

7. Wenzi fulani wa ndoa ambao ni vijana wanakabili hali gani, na kwa nini hilo linaweza kuleta mvutano katika ndoa?

7 Wenzi fulani wanaofunga ndoa wakiwa vijana wanajikuta wakitazamia kupata mtoto wakiwa wangali vijana sana. Kwa kweli, hawajapata wakati wa kufahamiana vizuri kabla ya kuzaliwa kwa mtoto, ambaye anahitaji kutunzwa kwa saa 24 kila siku. Ni jambo la kawaida kwa mama kumpa uangalifu mwingi mtoto wake mchanga, na mume wake ambaye ni kijana huenda akaona wivu. Zaidi ya hayo, wazazi wanapokosa usingizi kwa sababu ya kumshughulikia mtoto huyo mchanga, hilo linaweza kuleta mvutano katika uhusiano wao. Kwa ghafula, wenzi hao wapya wa ndoa wanatambua kwamba wamepoteza sana uhuru wao. Sasa hawawezi kutembelea sehemu mbalimbali na kufanya mambo waliyofanya kwa uhuru kabla ya kuwa na mtoto. Wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu hali yao ambayo imebadilika?

8. Kuwa mzazi kunapaswa kuonwa jinsi gani, na kwa nini?

8 Kama vile ndoa inavyopaswa kuchukuliwa kwa uzito, ndivyo na kuwa mzazi kunavyopaswa kuonwa kuwa daraka na pendeleo kutoka kwa Mungu. Hata wenzi wa ndoa Wakristo wakilazimika kufanya marekebisho yoyote yale baada ya kuzaa mtoto, wanapaswa kufanya yote wanayoweza ili kuyashughulikia kwa njia nzuri. Kwa kuwa Yehova aliwapa wanadamu uwezo wa kuzaa watoto, wazazi wanahitaji kumwona mtoto aliyezaliwa kuwa “urithi kutoka kwa Yehova.” (Zab. 127:3) Mama na baba Mkristo watajitahidi kutimiza madaraka yao kama ‘wazazi katika muungano na Bwana.’—Efe. 6:1.

9. (a) Kumlea mtoto kunatia ndani nini? (b) Mume anaweza kufanya nini ili kumsaidia mke wake aendelee kuwa mwenye nguvu kiroho?

9 Kumlea mtoto kunatia ndani miaka mingi ya kujidhabihu. Ni kazi inayohitaji wakati na nguvu nyingi. Mume Mkristo anahitaji kuelewa kwamba miaka kadhaa baada ya mtoto kuzaliwa, inaelekea mke wake atakengeushwa wakati wa mikutano na huenda akawa na nafasi chache sana za kujifunza Biblia na kutafakari. Hilo linaweza kudhoofisha hali yake ya kiroho. Mume anayechukua kwa uzito daraka la kuwa mzazi anafanya yote anayoweza ili kusaidia kumtunza mtoto. Anaweza kujaribu kuzungumza na mke wake baadaye nyumbani mambo ambayo amekosa wakati wa mikutano. Pia, mume anaweza kusaidia kumtunza mtoto ili mke wake apate nafasi ya kutosha ya kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme.—Soma Wafilipi 2:3, 4.

10, 11. (a) Watoto wanalelewa jinsi gani katika “mwongozo wa akilini wa Yehova”? (b) Kwa nini wazazi wengi Wakristo wanastahili kupongezwa?

10 Daraka la kuwa mzazi linatia ndani mengi zaidi ya kumpa mtoto chakula, mavazi, makao, na matibabu. Hasa katika wakati huu wa mwisho wenye hatari, watoto wanahitaji kujifunza tangu wakiwa wachanga kanuni za maadili zinazopaswa kuongoza maisha yao. Watoto wanapaswa kulelewa “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Kuwalea katika “mwongozo wa akilini” wa Yehova kunatia ndani kuweka mawazo ya Yehova katika akili ya mtoto tangu akiwa mchanga na kuendelea katika miaka yenye hatari ya utineja.—2 Tim. 3:14, 15.

11 Yesu alipowaambia wafuasi wake kwamba ‘wangefanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ bila shaka alimaanisha kwamba wazazi wangewasaidia watoto wao kuwa wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Hilo si jambo rahisi kwa sababu ya uvutano mbaya wa ulimwengu huu juu ya watoto. Hivyo, wazazi ambao wamefanikiwa kuwalea watoto wao kufikia kuwa Wakristo waliojiweka wakfu, wanastahili kwa kweli kupongezwa kwa uchangamfu na washiriki wote wa kutaniko. ‘Wameushinda’ uvutano wa ulimwengu kwa imani na uaminifu wao kwa kutimiza daraka lao la kuwa wazazi.—1 Yoh. 5:4.

Kubaki Mseja au Kuwa Bila Mtoto kwa Kusudi Linalofaa

12. Kwa nini Wakristo fulani wanaamua kubaki waseja kwa muda fulani?

12 Kwa kuwa “wakati uliobaki umepungua” na “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika,” Neno la Mungu linatuhimiza sote tufikirie faida za useja. (1 Kor. 7:29-31) Hivyo, Wakristo fulani wamechagua kubaki waseja maisha yao yote au wameamua kubaki waseja kwa miaka fulani kabla ya kufunga ndoa. Inapendeza kwamba hawatumii uhuru huo wa useja ili kufuatia mapendezi ya kibinafsi. Wengi wanabaki waseja ili kumtumikia Yehova “bila kukengeushwa fikira.” (Soma 1 Wakorintho 7:32-35.) Wakristo fulani waseja wanatumika wakiwa mapainia au Wanabetheli. Walio wengi wanafanya bidii kustahili kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ili watumiwe zaidi na tengenezo la Yehova. Kwa wazi, wale waliotumika wakiwa wahudumu wa wakati wote kwa muda fulani wakiwa waseja na baadaye wakaamua kufunga ndoa, mara nyingi wanahisi kwamba bado ndoa yao inafaidika kutokana na mambo mazuri waliyojifunza katika miaka hiyo ya useja.

13. Kwa nini wenzi fulani wa ndoa Wakristo wanaamua kujizuia wasipate watoto?

13 Katika sehemu fulani za ulimwengu, kumetokea mabadiliko mengine katika familia, wenzi wengi wa ndoa wameamua kutopata watoto. Wenzi fulani wanaamua hivyo kwa sababu za kiuchumi; wengine wanafanya hivyo kwa sababu wanataka kuwa huru ili kufuatia kazi nzuri ya maisha. Pia, kuna wenzi wa ndoa Wakristo ambao wanajizuia wasipate watoto. Hata hivyo, mara nyingi wanafanya hivyo ili wawe na uhuru wa kumtumikia Yehova. Hilo halimaanishi kwamba wenzi hao hawana maisha ya kawaida ya ndoa. Sivyo. Hata hivyo, wako tayari kujinyima faida fulani za ndoa ili kutanguliza mambo ya Ufalme. (1 Kor. 7:3-5) Baadhi ya Wakristo hao wanamtumikia Yehova na ndugu zao katika kazi ya mzunguko, wilaya, au Betheli. Wengine wao wanatumika wakiwa mapainia au wamishonari. Yehova hatasahau kazi yao na upendo ambao wanaonyesha kwa ajili ya jina lake.—Ebr. 6:10.

“Dhiki Katika Mwili”

14, 15. Wazazi Wakristo wanaweza kupata ‘dhiki gani katika mwili wao’?

14 Mtume Paulo alisema kwamba Wakristo waliofunga ndoa wangekuwa na “dhiki katika mwili wao.” (1 Kor. 7:28) Hilo linaweza kutia ndani matatizo ya kiafya ya wenzi wa ndoa, watoto wao, au ya wazazi wao waliozeeka. Linaweza pia kutia ndani matatizo yanayohusiana na kulea watoto wao. Kama ilivyoonyeshwa mwanzoni mwa habari hii, Biblia ilitabiri kwamba “siku za mwisho” zingekuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Watoto “wasiotii wazazi” wao wangekuwa kati ya mambo hayo magumu kushughulika nayo.—2 Tim. 3:1-3.

15 Kulea watoto si jambo rahisi kwa wazazi Wakristo. Tunapatwa pia na matatizo ya ‘nyakati hizi za hatari.’ Hivyo, wazazi Wakristo wanapaswa kuendelea kupinga uvutano hatari ambao “mfumo wa mambo wa ulimwengu huu” unaweza kuwa nao juu ya watoto wao. (Efe. 2:2, 3) Na bado mapambano yanaendelea! Mwana au binti wa familia ya Kikristo anapoacha kumtumikia Yehova, kwa kweli, hiyo ni “dhiki” kwa wazazi wake ambao walijaribu kumlea katika kweli ya Mungu.—Met. 17:25.

‘Kutakuwa na Dhiki Kuu’

16. Yesu alitabiri kuhusu “dhiki” gani?

16 Hata hivyo, kutakuwa na dhiki iliyo kubwa zaidi kuliko “dhiki” yoyote ile ambayo huenda tukapata katika ndoa au tunapolea watoto. Katika unabii wake kuhusu kuwapo kwake na umalizio wa mfumo wa mambo, Yesu alisema hivi: “Ndipo kutakapokuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.” (Mt. 24:3, 21) Baadaye, Yesu alifunua kwamba umati mkubwa ungeokoka ‘dhiki hiyo kuu.’ Hata hivyo, mfumo wa Shetani utaendelea kuwashambulia mpaka mwisho Mashahidi wa Yehova wenye amani. Bila shaka, huo utakuwa wakati mgumu kwetu sote, yaani, watu wazima na watoto pia.

17. (a) Kwa nini tunaweza kutazamia wakati ujao tukiwa na uhakika? (b) Ni nini kinachopaswa kuongoza maoni yetu kuhusu ndoa na kuwa wazazi?

17 Hata hivyo, hatupaswi kuogopa sana wakati ujao. Wazazi ambao ni waaminifu kwa Yehova wanaweza kutumaini kulindwa pamoja na watoto wao wachanga. (Soma Isaya 26:20, 21; Sef. 2:2, 3; 1 Kor. 7:14) Sasa, kwa kuwa tunajua kwamba tunaishi katika siku zenye hatari, acheni ujuzi huo uongoze maoni yetu kuhusu ndoa na kuwa mzazi katika siku hizi za mwisho. (2 Pet. 3:10-13) Tukifanya hivyo, maisha yetu—iwe sisi ni waseja au tumefunga ndoa, tuna watoto au hatuna watoto—yatamletea heshima na kumtukuza Yehova na kutaniko la Kikristo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ona kitabu Izingatie Siku ya Yehova Maishani chini ya kichwa kidogo “Amechukia Talaka,” kwenye ukurasa wa 125.

^ fu. 5 Wale wanaokabiliana na matatizo ya ndoa watatiwa nguvu kwa kuchunguza tena habari kuhusu ndoa katika Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 2003 (15/9/2003), na Amkeni! la Januari 8, 2001 (8/1/2001).

^ fu. 6 Ona sura ya 30, “Je, Niko Tayari kwa Ajili ya Ndoa?” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi.

Kwa Kupitia

• Kwa nini vijana Wakristo hawapaswi kukimbilia kufunga ndoa?

• Kumlea mtoto kunatia ndani nini?

• Kwa nini Wakristo wengi wanabaki waseja au, ikiwa wamefunga ndoa, hawana watoto?

• Ni “dhiki” gani ambayo huenda wazazi Wakristo wakapata?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kwa nini ni jambo la hekima kwa vijana Wakristo kungoja mpaka wawe watu wazima kabla ya kufunga ndoa?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mume anaweza kumsaidia sana mke wake kushiriki kikamilifu katika utendaji mbalimbali wa kiroho

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kwa nini wenzi fulani wa ndoa Wakristo wanaamua kutopata watoto?