Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kinachofanya Maisha Yawe Yenye Kusudi?

Ni Nini Kinachofanya Maisha Yawe Yenye Kusudi?

Ni Nini Kinachofanya Maisha Yawe Yenye Kusudi?

“Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake.”—MHU. 12:13.

1, 2. Tunaweza kufaidika jinsi gani kwa kuchunguza kitabu cha Mhubiri?

FIKIRIA mtu ambaye anaonekana kuwa ana kila kitu. Ni kiongozi mashuhuri, mmoja wa watu matajiri zaidi duniani, na mwenye hekima zaidi katika kizazi chake. Hata hivyo, ingawa ametimiza mambo mengi, bado anajiuliza, ‘Ni nini kinachofanya maisha yawe yenye kusudi?’

2 Kwa kweli, mtu huyo aliishi miaka elfu tatu hivi iliyopita. Aliitwa Sulemani, na katika kitabu cha Mhubiri anaeleza jinsi alivyojaribu kupata maisha yenye kuridhisha. (Mhu. 1:13) Tunaweza kujifunza mambo mengi kutokana na maisha ya Sulemani. Kwa kweli, hekima inayopatikana katika kitabu cha Mhubiri inaweza kutusaidia kujiwekea miradi ambayo itafanya maisha yetu yawe yenye kusudi la kweli.

“Kufuatilia Upepo”

3. Ni jambo gani la hakika kuhusu maisha ya wanadamu ambalo linatuhusu sisi sote?

3 Sulemani anaeleza kwamba Mungu aliumba vitu vingi vyenye kuvutia sana duniani, vitu vyenye kustaajabisha ambavyo tunaendelea kufurahia. Hata hivyo, kwa sababu maisha yetu ni mafupi sana, hatuwezi kwa kweli kuvumbua mambo mengi kuhusu uumbaji wa Mungu. (Mhu. 3:11; 8:17) Kama Biblia inavyosema, siku zetu ni chache na zinapita haraka. (Ayu. 14:1, 2; Mhu. 6:12) Jambo hilo la hakika linapaswa kutuchochea kutumia maisha yetu kwa hekima. Hilo si jambo rahisi, kwa kuwa ulimwengu wa Shetani unaweza kutupotosha.

4. (a) Neno “ubatili” linamaanisha nini? (b) Tutachunguza mambo gani ambayo watu wanafuatia maishani?

4 Ili kuonyesha hatari ya kutumia maisha yetu kwa njia isiyo ya hekima, Sulemani anatumia neno “ubatili” mara 30 hivi katika kitabu cha Mhubiri. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “ubatili” linamaanisha kitu ambacho ni kitupu, bure kabisa, kisicho na maana, au kisicho na thamani ya kudumu. (Mhu. 1:2, 3) Nyakati nyingine Sulemani anatumia neno “ubatili” badala ya maneno “kufuatilia upepo.” (Mhu. 1:14; 2:11) Kwa wazi, kujaribu kushika upepo ni ubatili. Mtu yeyote anayejaribu kufanya hivyo anaambulia patupu. Kufuatia miradi isiyo ya hekima ni jambo lenye kukatisha tamaa. Maisha katika mfumo huu ni mafupi sana hivi kwamba hatupaswi kuyapoteza kwenye shughuli zitakazotuacha mikono mitupu. Kwa hiyo, ili kutusaidia kuepuka kufanya kosa hilo, acheni tuchunguze mambo fulani ambayo Sulemani anaonyesha kwamba watu wanafuatia kwa ukawaida maishani. Kwanza, tutachunguza kufuatia raha na mali. Baadaye, tutazungumzia thamani ya kazi ambayo inampendeza Mungu.

Je, Kufuatia Raha Kunatuletea Furaha?

5. Sulemani alitafuta maisha yenye kuridhisha kwa kufanya mambo gani?

5 Kama watu wengi leo, Sulemani alijaribu kupata maisha yenye kuridhisha kwa kufuatia raha. Anasema hivi: “Sikuunyima moyo wangu shangwe ya aina yoyote.” (Mhu. 2:10) Alitafuta raha katika mambo gani? Kulingana na Mhubiri sura ya 2, ‘aliuchangamsha mwili wake kwa divai,’ na wakati huohuo akiwa mwenye kujizuia, alifanya kazi kama vile kutengeneza mabustani, kuchora ramani za majumba ya kifalme, kusikiliza muziki, na kufurahia chakula kizuri.

6. (a) Kwa nini si vibaya kufurahia vitu fulani vizuri maishani? (b) Ni usawaziko gani ambao unahitajiwa katika kujiburudisha?

6 Je, Biblia inashutumu kujifurahisha pamoja na marafiki? Hapana. Kwa mfano, Sulemani anasema kwamba kufurahia chakula katika mazingira yenye kustarehesha baada ya kazi ngumu ni zawadi ya Mungu. (Soma Mhubiri 2:24; 3:12, 13.) Zaidi ya hayo, Yehova mwenyewe anawaambia vijana ‘washangilie na moyo wao uwafanyie mema’ kwa njia inayofaa. (Mhu. 11:9) Tunahitaji kupumzika na kujiburudisha kwa njia inayofaa. (Linganisha na Marko 6:31.) Hata hivyo, kujiburudisha hakupaswi kuwa jambo kuu katika maisha yetu. Badala yake, kustarehe ni kama tunda linaloliwa baada ya kula, si chakula chenyewe. Je, hukubali kwamba hata tunda likiwa tamu jinsi gani, utachoshwa nalo ikiwa huli chakula kingine, na halitakupa lishe ya kutosha? Vivyo hivyo, Sulemani alitambua kwamba kufuatia maisha ya raha ni “kufuatilia upepo.”—Mhu. 2:10, 11.

7. Kwa nini tunapaswa kuchagua burudani kwa uangalifu?

7 Zaidi ya hayo, si burudani zote ambazo zinafaa. Burudani nyingi zinadhuru kabisa, kiroho na kiadili. Mamilioni ya watu wamepatwa na madhara maishani kwa sababu tu ‘walitaka kujifurahisha.’ Walitumia vibaya dawa za kulevya, walikunywa pombe kupindukia, au walicheza kamari. Kwa fadhili, Yehova anatuonya kwamba tukiruhusu moyo wetu au macho yetu yatuongoze kwenye mambo yenye kudhuru, tunapaswa kutazamia matokeo mabaya.—Gal. 6:7.

8. Kwa nini ni jambo la hekima kutafakari juu ya maisha yetu?

8 Zaidi ya hayo, kufuatia raha bila usawaziko kutatuzuia tusikazie uangalifu mambo mazito zaidi. Kumbuka kwamba maisha yanapita haraka na hatuna uhakika wowote kwamba sikuzote tutakuwa wenye afya nzuri na hatutapata matatizo katika maisha yetu mafupi. Ndiyo sababu, kama Sulemani alivyosema, tunaweza kupata faida kubwa zaidi kwa kuhudhuria mazishi, hasa ya ndugu au dada Mkristo mshikamanifu, kuliko kwenda kwenye “nyumba ya kushangilia.” (Soma Mhubiri 7:2, 4.) Kwa nini? Tunaposikiliza hotuba ya mazishi na kutafakari juu ya maisha ya uaminifu ya mtumishi aliyekufa wa Yehova, tunaweza kuchochewa kuchunguza maisha yetu wenyewe. Kwa sababu hiyo, huenda tukakata kauli kwamba tunahitaji kurekebisha miradi yetu ili kutumia kwa hekima muda unaobaki wa maisha yetu.—Mhu. 12:1.

Je, Vitu vya Kimwili Vitatuwezesha Kuwa na Maisha Yenye Kuridhisha?

9. Sulemani aligundua nini kuhusu kuwa na mali?

9 Sulemani alikuwa mmoja wa watu matajiri zaidi duniani alipoandika kitabu cha Mhubiri. (2 Nya. 9:22) Alikuwa na uwezo wa kupata chochote alichotaka. Aliandika hivi: “Sikuyanyima macho yangu chochote ambacho yaliomba.” (Mhu. 2:10) Hata hivyo, aligundua kwamba mali peke yake hazimfanyi mtu kuwa na maisha yenye kuridhisha. Alimalizia hivi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.”—Mhu. 5:10.

10. Ni nini kinachoweza kumfanya mtu aridhike kikweli na kupata utajiri wa kweli?

10 Ingawa vitu vya kimwili vina thamani ya muda tu, bado utajiri unaweza kuwa na uvutano wenye nguvu. Kulingana na uchunguzi fulani uliofanywa hivi karibuni huko Marekani, asilimia 75 ya wanafunzi wote wa mwaka wa kwanza kwenye chuo kikuu walisema mradi wao mkuu maishani ni kuwa na “pesa nyingi.” Hata wakifikia mradi wao, je, kweli watakuwa wenye furaha? Si lazima. Wachunguzi wamesema kwamba kufuatia sana vitu vya kimwili, kwa kweli, kunamzuia mtu asipate furaha au kuridhika. Sulemani alikuwa tayari amekata kauli hiyo zamani za kale. Aliandika hivi: “Pia nikajikusanyia fedha na dhahabu, na mali iliyo ya pekee kwa wafalme . . . Na, tazama! kila kitu kilikuwa ubatili na kufuatilia upepo.” * (Mhu. 2:8, 11) Tofauti na hilo, tukitumia maisha yetu kumtumikia Yehova kwa moyo wote na hivyo kupata baraka zake, tutapata utajiri wa kweli.—Soma Methali 10:22.

Ni Kazi ya Aina Gani Inayomfanya Mtu Aridhike Kikweli?

11. Maandiko yanaonyesha nini kuhusu umuhimu wa kazi?

11 Yesu alisema: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa, na mimi ninaendelea kufanya kazi.” (Yoh. 5:17) Hapana shaka kwamba Yehova na Yesu wanaridhika kutokana na kazi. Biblia inaonyesha kwamba Yehova aliridhika na kazi yake ya uumbaji inaposema hivi: “Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.” (Mwa. 1:31) Malaika ‘walianza kupaaza sauti kwa kushangilia’ walipoona yote ambayo Mungu alikuwa amefanya. (Ayu. 38:4-7) Vivyo hivyo, Sulemani alithamini umuhimu wa kazi yenye kusudi.—Mhu. 3:13.

12, 13. (a) José na Miguel wanaonyesha jinsi gani kwamba wanaridhika kwa kufanya kazi kwa unyoofu? (b) Kwa nini kazi ya kimwili inaweza kuvunja moyo nyakati nyingine?

12 Wanadamu wengi wanaelewa umuhimu wa kazi inayofanywa kwa unyoofu. Kwa mfano, José, mchoraji mwenye mafanikio, anasema hivi: “Ukifaulu kuchora kwenye kitambaa picha uliyo nayo akilini, unahisi kana kwamba umefaulu kupanda mlima mrefu.” Miguel, * ambaye ni mfanyabiashara, anasema: “Kazi inakufanya uridhike kwa sababu inakuwezesha kutosheleza mahitaji ya familia yako. Pia, inaweza kukuletea furaha kwa kuwa umetimiza jambo fulani.”

13 Kwa upande mwingine, kazi nyingi ni zenye kuchosha na hazimpi mtu nafasi za kutosha za kuvumbua mambo mapya. Nyakati nyingine, watu wanavunjwa moyo na hata wanatendewa isivyo haki kazini. Kama Sulemani anavyoonyesha, huenda mvivu akapata thawabu ya mfanyakazi mwenye bidii labda kwa sababu watu wenye mamlaka wanamjua. (Mhu. 2:21) Huenda pia kuna mambo mengine yanayoweza kuvunja moyo. Huenda biashara inayoonekana kuwa yenye faida sana ikaporomoka kwa sababu ya matukio yasiyotazamiwa au kuharibika kwa hali ya kiuchumi. (Soma Mhubiri 9:11.) Mara nyingi, mtu anayejitahidi sana kufanikiwa anafadhaika na kuvunjika moyo anapotambua kwamba amekuwa ‘akifanya kazi ngumu kwa ajili ya upepo.’—Mhu. 5:16.

14. Ni kazi gani ambayo sikuzote inaridhisha kikweli?

14 Je, kuna kazi yoyote ambayo haivunji moyo kamwe? José, mchoraji aliyetajwa mwanzoni, anasema hivi: “Kadiri miaka inavyopita, huenda michoro ikapotea au kuharibiwa. Sivyo ilivyo na mambo ya kiroho tunayofanya katika utumishi wa Mungu. Kwa kumtii Yehova kwa kuhubiri habari njema, nimewasaidia wengine kujenga kitu fulani chenye kudumu, yaani, kuwa Wakristo wazuri ambao wanamwogopa Mungu. Hilo ni jambo lenye thamani sana.” (1 Kor. 3:9-11) Vivyo hivyo, Miguel anasema kwamba kuhubiri ujumbe wa Ufalme kunaridhisha zaidi kuliko kazi yake ya kimwili. Anasema hivi: “Hakuna jambo lingine linaloweza kukuletea shangwe kama kuzungumza na mtu kweli za Biblia na kuona kweli hizo zikigusa moyo wake.”

“Tupa Mkate Wako”

15. Ni nini kwa kweli kinachofanya maisha yawe yenye kusudi?

15 Kwa kumalizia, ni nini kwa kweli kinachofanya maisha yawe yenye kusudi? Tunaridhika kikweli tunapotumia maisha yetu mafupi katika mfumo huu wa mambo kutenda mema na kumpendeza Yehova. Tunaweza kujenga uhusiano wa karibu pamoja na Mungu, tunaweza kuwafundisha watoto wetu viwango vya Biblia, tunaweza kuwasaidia wengine wamjue Yehova, na tunaweza kusitawisha urafiki wenye kudumu pamoja na ndugu na dada zetu. (Gal. 6:10) Jitihada hizo zote zina thamani ya kudumu na zinawaletea baraka wale wanaofanya bidii kuzipata. Sulemani alitumia mfano mzuri sana ili kueleza thamani ya kutenda mema. Alisema hivi: “Tupa mkate wako juu ya uso wa maji, kwa maana baada ya siku nyingi utaupata tena.” (Mhu. 11:1) Yesu aliwahimiza hivi wanafunzi wake: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi.” (Luka 6:38) Zaidi ya hayo, Yehova mwenyewe anaahidi kuwapa thawabu wale wanaowatendea wengine mema.—Met. 19:17; soma Waebrania 6:10.

16. Ni wakati gani ulio mzuri kupanga miradi tutakayofuatia maishani?

16 Biblia inatuhimiza tuamue kwa hekima, tukiwa bado vijana, jinsi tutakavyotumia maisha yetu. Tukifanya hivyo, tutaepuka kufadhaika katika miaka ya baadaye. (Mhu. 12:1) Litakuwa jambo lenye kusikitisha kama nini ikiwa tutapoteza miaka bora ya maisha yetu tukifuatia vitu vyenye kuvutia vya ulimwengu, na kugundua baadaye kwamba tulikuwa tukifuatia upepo tu!

17. Ni nini kitakachokusaidia kuchagua njia nzuri zaidi ya maisha?

17 Kama baba yeyote mwenye upendo, Yehova anataka ufurahie maisha, utende mema, na uepuke maumivu ya moyoni yanayoepukika. (Mhu. 11:9, 10) Ni nini kitakachokusaidia kufanya hivyo? Jiwekee miradi ya kiroho na ufanye bidii kuifikia. Karibu miaka 20 iliyopita, Javier alihitaji kuchagua kati ya kazi nzuri ya udaktari na huduma ya wakati wote. Anasema hivi: “Ingawa kazi ya daktari inaweza kuridhisha, hakuna kinachoweza kulinganishwa na shangwe niliyohisi nilipowasaidia watu kadhaa kujua kweli. Utumishi wa wakati wote umenisaidia kufurahia maisha kikamili. Ninasikitika tu kwamba sikuanza mapema zaidi.”

18. Kwa nini maisha ya Yesu duniani yalikuwa yenye kusudi la kweli?

18 Hivyo basi, ni kitu gani chenye thamani zaidi ambacho tunapaswa kujitahidi kupata? Kitabu cha Mhubiri kinasema hivi: “Jina ni bora kuliko mafuta mazuri, na siku ya kufa kuliko siku ya kuzaliwa kwa mtu.” (Mhu. 7:1) Maisha ya Yesu yanathibitisha jambo hilo vizuri zaidi. Hapana shaka kwamba alijifanyia jina bora zaidi pamoja na Yehova. Yesu alipokufa akiwa mwaminifu, alitetea enzi kuu ya Baba yake na kutoa dhabihu ya fidia, ambayo ilitufungulia njia ya kupata wokovu. (Mt. 20:28) Wakati wa maisha yake mafupi duniani, Yesu alituwekea kielelezo kikamilifu cha maisha yenye kusudi la kweli. Tunapaswa kujitahidi kuiga kielelezo hicho.—1 Kor. 11:1; 1 Pet. 2:21.

19. Sulemani alitoa shauri gani lenye hekima?

19 Sisi pia tunaweza kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu. Kuwa na sifa nzuri machoni pa Yehova ni jambo lenye maana zaidi kwetu kuliko kuwa na mali. (Soma Mathayo 6:19-21.) Kila siku, tunaweza kupata njia za kutenda mambo mema machoni pa Yehova na hilo litaboresha maisha yetu. Kwa mfano, tunaweza kuwahubiria wengine habari njema, kutia nguvu ndoa yetu na familia yetu, na kuboresha uhusiano wetu pamoja na Yehova kwa kujifunza kibinafsi na kuhudhuria mikutano. (Mhu. 11:6; Ebr. 13:16) Hivyo basi, je, unataka kufurahia maisha yenye kusudi la kweli? Ikiwa ndivyo, endelea kufuata shauri hili la Sulemani: “Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”—Mhu. 12:13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Sulemani alikuwa na mapato ya msingi ya talanta 666 (zaidi ya kilogramu 22,000) za dhahabu kila mwaka.—2 Nya. 9:13.

^ fu. 12 Jina limebadilishwa.

Ungetoa Jibu Gani?

• Ni nini kinachopaswa kutuchochea kufikiri kwa uzito kuhusu miradi yetu maishani?

• Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kufuatia raha na mali?

• Ni kazi ya aina gani itakayotuletea uradhi unaodumu?

• Ni kitu gani chenye thamani ambacho tunapaswa kujitahidi kupata?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tafrija inapaswa kuwa muhimu kadiri gani katika maisha yetu?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Ni nini kinachofanya kazi ya kuhubiri iwe yenye kuridhisha sana?