Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafuta Mwongozo wa Mungu Katika Kila Jambo

Tafuta Mwongozo wa Mungu Katika Kila Jambo

Tafuta Mwongozo wa Mungu Katika Kila Jambo

“Huyu ni Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele. Yeye mwenyewe atatuongoza mpaka tufe.”—ZAB. 48:14.

1, 2. Kwa nini tunapaswa kufuata mwongozo wa Yehova badala ya kutegemea hekima yetu wenyewe, na ni maswali gani yanayotokea?

NI RAHISI kujidanganya kwa kufikiri kwamba vitu visivyo na thamani au vyenye kudhuru vinavutia. (Met. 12:11) Ikiwa kweli tunataka kutenda jambo ambalo Mkristo hapaswi kufanya, mara nyingi moyo wetu unatushawishi tulifanye. (Yer. 17:5, 9) Kwa hiyo, mtunga-zaburi alionyesha hekima aliposali hivi kwa Yehova: “Tuma nuru yako na kweli yako. Na hivyo vyenyewe viniongoze.” (Zab. 43:3) Badala ya kutegemea hekima yake yenye mipaka, alimtegemea Yehova ambaye anatoa mwongozo bora kabisa. Kama mtunga-zaburi, tunapaswa kumtegemea Mungu ili atuongoze.

2 Hata hivyo, kwa nini tunapaswa kutegemea mwongozo wa Yehova badala ya mwongozo mwingine wowote? Tunapaswa kuutafuta wakati gani? Tunapaswa kusitawisha mitazamo gani ili tufaidike na mwongozo huo, na Yehova anatuongoza jinsi gani leo? Maswali hayo ya maana yatazungumziwa katika habari hii.

Kwa Nini Tutegemee Mwongozo wa Yehova?

3-5. Tuna sababu gani za kutegemea kabisa mwongozo wa Yehova?

3 Yehova ni Baba yetu wa mbinguni. (1 Kor. 8:6) Anamjua kila mmoja wetu vizuri sana naye anaweza kusoma mioyo yetu. (1 Sam. 16:7; Met. 21:2) Mfalme Daudi alimwambia Mungu hivi: “Wewe mwenyewe umepata kujua kuketi kwangu na kusimama kwangu. Umeichunguza fikira yangu tokea mbali. Kwa maana hamna neno hata moja katika ulimi wangu, lakini, tazama! Ee Yehova, tayari unajua yote.” (Zab. 139:2, 4) Kwa kuwa Yehova anatujua vizuri sana, hatupaswi kamwe kuwa na shaka kwamba anajua kile kinachotufaa zaidi. Zaidi ya hilo, Yehova ana hekima isiyo na kifani. Anaona kila kitu, anachunguza ndani zaidi kuliko wanadamu, naye anajua matokeo ya mambo tangu mwanzo. (Isa. 46:9-11; Rom. 11:33) Yeye ni “Mungu, mwenye hekima peke yake.”—Rom. 16:27.

4 Kwa kuongezea, Yehova anatupenda na sikuzote anataka tuwe na maisha bora kabisa. (Yoh. 3:16; 1 Yoh. 4:8) Anatuonyesha ukarimu akiwa Mungu mwenye upendo. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu, kwa maana hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni.” (Yak. 1:17) Wale wanaokubali Mungu awaongoze wanafaidika sana kutokana na ukarimu wake.

5 Mwishowe, Yehova ni mweza-yote. Mtunga-zaburi alisema hivi kuhusu hilo: “Yeyote anayekaa mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi atajipatia makao katika kivuli cha Mweza-Yote. Nitamwambia Yehova: ‘Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ambaye nitamtegemea.’” (Zab. 91:1, 2) Tunapofuata mwongozo wa Yehova, tunamkimbilia Mungu ambaye hawezi kushindwa. Yehova anatutegemeza hata tunapopata upinzani. Hawezi kutukatisha tamaa. (Zab. 71:4, 5; Soma Methali 3:19-26.) Ndiyo, Yehova anajua kile kinachotufaa zaidi, anataka tupate kilicho bora kabisa, naye ana nguvu za kutupa kilicho bora kabisa. Ni jambo la upumbavu kama nini kupuuza mwongozo wake! Lakini ni wakati gani tunapohitaji mwongozo wake?

Ni Wakati Gani Tunapohitaji Mwongozo?

6, 7. Ni wakati gani tunapohitaji mwongozo wa Yehova?

6 Kwa kweli, tunahitaji mwongozo wa Mungu katika maisha yetu yote, tangu ujana mpaka uzee. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Mungu huyu ni Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele. Yeye mwenyewe atatuongoza mpaka tufe.” (Zab. 48:14) Kama mtunga-zaburi, Wakristo wenye hekima hawaachi kamwe kutafuta mwongozo wa Mungu.

7 Bila shaka, kuna nyakati ambazo tunahisi kwamba tunahitaji sana msaada wa haraka. Nyakati nyingine tunakuwa katika “dhiki kali,” labda tunakabili mateso, ugonjwa mbaya sana, au tunapoteza kazi ghafula. (Zab. 69:16, 17) Nyakati kama hizo, tunapata faraja kwa kumfikia Yehova, tukiwa na uhakika kwamba atatupa nguvu za kuvumilia naye atatuongoza ili tufanye maamuzi mazuri. (Soma Zaburi 102:17.) Hata hivyo, tunahitaji msaada wake katika pindi nyingine pia. Kwa mfano, tunapoenda kuwahubiria majirani wetu habari njema ya Ufalme, tunahitaji mwongozo wa Yehova ili tufanikiwe katika kazi yetu ya kuhubiri. Na wakati wowote tunapofanya uamuzi kuhusiana na tafrija, kuvaa na kujipamba, marafiki, kazi, elimu, au kitu kingine chochote, ni jambo la hekima kufuata miongozo ya Yehova. Kwa kweli, tunahitaji mwongozo katika kila hali tunayokabili maishani.

Hatari za Kutotafuta Mwongozo wa Mungu

8. Uamuzi wa Hawa wa kula tunda lililokatazwa ulionyesha nini?

8 Ingawa hivyo, kumbuka kwamba tunapaswa kufuata mwongozo wa Yehova kwa kupenda. Mungu hatatulazimisha kufuata mwongozo wake ikiwa hatutaki. Mwanadamu wa kwanza aliyechagua kutofuata mwongozo wa Yehova ni Hawa, na mfano wake unaonyesha hatari ya kufanya uamuzi mbaya kama huo. Pia, fikiria uamuzi wa Hawa ulionyesha nini. Hawa alikula tunda lililokatazwa kwa sababu alitaka ‘kuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya.’ (Mwa. 3:5) Kwa kufanya hivyo, alijichukulia daraka la Mungu, akajiamulia mwenyewe yaliyo mema na maovu badala ya kufuata miongozo ya Yehova. Hivyo, alikataa enzi kuu ya Yehova. Alitaka kujiongoza. Mume wake, Adamu, alifuata njia hiyohiyo ya uasi.—Rom. 5:12.

9. Tukikataa mwongozo wa Yehova, ni kana kwamba tunafanya nini, na kwa nini si jambo la hekima hata kidogo kufanya hivyo?

9 Leo, ikiwa hatufuati mwongozo wa Yehova, tunakataa pia kukubali enzi yake kuu. Kwa mfano, fikiria mtu ambaye amekuwa na zoea la kutazama ponografia (picha au habari za ngono). Ikiwa anashirikiana na kutaniko la Kikristo, anajua miongozo ya Yehova kuhusu jambo hilo. Hatupaswi kufurahia kutazama mambo machafu wala hayapaswi kutajwa hata kidogo. (Efe. 5:3) Mtu anayetazama mambo hayo anakataa miongozo ya Yehova na hivyo anapinga enzi kuu ya Yehova, anakataa ukichwa wa Yehova. (1 Kor. 11:3) Kufanya hivyo si jambo la hekima hata kidogo, kwa kuwa Yeremia alisema kwamba “mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yer. 10:23.

10. Kwa nini tunapaswa kutumia uhuru wetu wa kuchagua kwa njia inayofaa?

10 Huenda watu fulani wakatilia shaka maneno ya Yeremia, wakifikiri kwamba kwa kuwa Yehova alitupa uhuru wa kuchagua, hapaswi kutushutumu tunapoutumia. Hata hivyo, usisahau kwamba uhuru wa kuchagua ni wajibu na vilevile ni zawadi. Tuna wajibu mbele za Mungu kwa sababu ya mambo tunayosema na kufanya. (Rom. 14:10) Yesu alisema hivi: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” Pia alisema: “Mawazo mabaya hutoka moyoni, mauaji, uzinzi, uasherati, wizi, ushuhuda wa uwongo, makufuru.” (Mt. 12:34; 15:19) Kwa hivyo, maneno na matendo yetu yanafunua hali ya moyo wetu. Yanaonyesha waziwazi sisi ni watu wa aina gani. Ndiyo sababu Mkristo mwenye hekima anatafuta mwongozo wa Yehova katika kila jambo. Anapofanya hivyo, Yehova anamwona kuwa ‘mnyoofu moyoni’ na ‘atamtendea mema.’—Zab. 125:4.

11. Tunajifunza nini kutokana na historia ya Waisraeli?

11 Kumbuka historia ya Waisraeli. Walipofanya maamuzi mazuri na kutii amri za Yehova, aliwalinda. (Yos. 24:15, 21, 31) Hata hivyo, mara nyingi walitumia vibaya uhuru wao wa kuchagua. Yehova aliwaambia hivi katika siku za Yeremia: “Hawakusikiliza, wala hawakutega sikio lao, bali wakatembea katika mashauri kwa ukaidi wa moyo wao mbaya, hivi kwamba wakawa watu wa kuelekea nyuma wala si mbele.” (Yer. 7:24-26) Inahuzunisha kama nini! Tusikatae kamwe mwongozo wa Yehova na kutembea katika mashauri yetu wenyewe kwa sababu ya ukaidi au tamaa. Tukikataa mwongozo wake tutakuwa “watu wa kuelekea nyuma wala si mbele”!

Tunahitaji Nini Ili Kufuata Mashauri ya Mungu?

12, 13. (a) Ni sifa gani inayotuchochea kufuata mwongozo wa Yehova? (b) Kwa nini imani ni muhimu?

12 Kumpenda Yehova kunatuchochea kufuata mwongozo wake. (1 Yoh. 5:3) Hata hivyo, Paulo alitaja jambo lingine tunalohitaji aliposema hivi: “Tunatembea kwa imani, si kwa kuona.” (2 Kor. 5:6, 7) Kwa nini imani ni muhimu? Yehova anatuongoza katika “mapito ya uadilifu,” lakini mapito hayo hayatuongozi kupata utajiri au cheo katika ulimwengu huu. (Zab. 23:3) Kwa hivyo, jicho letu la imani linahitaji kukazia thawabu za kiroho zisizo na kifani tunazopata tunapomtumikia Yehova. (Soma 2 Wakorintho 4:17, 18.) Na imani inatusaidia kutosheka na vitu vichache vya kimwili.—1 Tim. 6:8.

13 Yesu alionyesha kwamba ibada ya kweli inahusisha kujidhabihu, na imani inahitajiwa ili kujidhabihu. (Luka 9:23, 24) Waabudu fulani waaminifu wamejidhabihu sana kwa kuvumilia umaskini, uonevu, ubaguzi, hata mateso makali. (2 Kor. 11:23-27; Ufu. 3:8-10) Wameweza kujidhabihu kwa shangwe kwa sababu tu ya kuwa na imani yenye nguvu. (Yak. 1:2, 3) Imani yenye nguvu inatufanya tuwe na hakika kabisa kwamba sikuzote kufuata mwongozo wa Yehova ni jambo bora. Sikuzote, mwongozo wake unatuletea faida ya kudumu. Hatuna shaka yoyote kwamba wale wanaovumilia kwa ushikamanifu watapata thawabu kubwa ambayo haiwezi kulinganishwa na mateso yoyote ya muda wanayovumilia.—Ebr. 11:6.

14. Kwa nini Hagari alihitaji kuonyesha unyenyekevu?

14 Fikiria pia jinsi unyenyekevu unavyotusaidia kufuata mwongozo wa Yehova. Mfano wa Hagari, mjakazi wa Sara, unaonyesha jambo hilo. Sara alipoendelea kuwa tasa, alimruhusu Abrahamu alale na Hagari, naye Hagari akapata mimba. Kisha, Hagari akawa na kiburi kuelekea bimkubwa wake aliyekuwa tasa. Hivyo, Sara “akaanza kumfedhehesha,” na Hagari akakimbia. Malaika wa Yehova alikutana na Hagari akamwambia: “Rudi kwa bimkubwa wako ujinyenyekeze chini ya mkono wake.” (Mwa. 16:2, 6, 8, 9) Labda Hagari angependelea mwongozo mwingine. Ili atende kupatana na mwongozo wa malaika, angehitaji kuacha mtazamo wake wa kiburi. Hata hivyo, kwa unyenyekevu Hagari alifanya kama malaika huyo alivyosema, na mwana wake, Ishmaeli, akazaliwa katika kambi ya baba yake yenye usalama.

15. Eleza hali fulani ambazo zinaweza kutulazimu kuonyesha unyenyekevu leo ili tufuate mwongozo wa Yehova.

15 Huenda sisi pia tukahitaji kujinyenyekeza ili tufuate mwongozo wa Yehova. Huenda wengine wakahitaji kukubali wanapoambiwa kwamba tafrija fulani wanayopenda haimpendezi Yehova. Huenda Mkristo amemkosea mwingine na hivyo anahitaji kuomba msamaha. Au huenda amefanya kosa na anahitaji kukubali kosa lake. Namna gani ikiwa mtu ametenda dhambi nzito? Anahitaji kujinyenyekeza na kuungama dhambi hiyo mbele ya wazee. Huenda mtu hata akatengwa na ushirika. Ili arudishwe katika kutaniko, ni lazima atubu kwa unyenyekevu na kugeuka. Katika hali hizo na hali nyinginezo, maneno ya Methali 29:23 yanafariji: “Majivuno ya mtu wa udongo yatamshusha, lakini yeye aliye na roho ya unyenyekevu atapata utukufu.”

Yehova Anatuongoza Jinsi Gani Leo?

16, 17. Tunaweza kufaidika kabisa jinsi gani kutokana na Biblia ikiwa chanzo cha mwongozo wa kimungu?

16 Chanzo kikuu cha mwongozo wa kimungu ni Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (Soma 2 Timotheo 3:16, 17.) Ili tufaidike kabisa kutokana na Neno hilo, si jambo la hekima kungoja hali ngumu itokee ndipo tutafute mashauri katika Maandiko. Badala yake, tunapaswa kuwa na zoea la kusoma Biblia kila siku. (Zab. 1:1-3) Tukifanya hivyo, tunapata kujua mambo yaliyo katika Neno la Mungu. Mawazo ya Mungu yanakuwa mawazo yetu, na tunakuwa tayari kupambana na matatizo, hata yale tusiyotazamia.

17 Kwa kuongezea, ni jambo la maana kutafakari kuhusu yale tunayosoma katika Maandiko na kusali kuhusiana nayo. Tunapotafakari kuhusu mistari ya Biblia, tunaona jinsi tunavyoweza kutumia habari hizo katika hali fulani hususa. (1 Tim. 4:15) Tunapopatwa na matatizo mazito, tunasali kwa Yehova na kumwomba atusaidie kupata mwongozo tunaohitaji. Roho ya Yehova itatusaidia kukumbuka kanuni muhimu sana za Kimaandiko tulizosoma katika Biblia au katika vichapo vinavyotegemea Biblia.—Soma Zaburi 25:4, 5.

18. Yehova anatuongoza katika njia gani akitumia undugu wetu wa Kikristo?

18 Undugu wetu wa Kikristo ni chanzo kingine chenye thamani sana cha mwongozo wa Yehova. Sehemu ya maana sana ya undugu huo ni yule “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” pamoja na Baraza Linaloongoza ambalo linamwakilisha. Baraza hilo linaendelea kutoa chakula cha kiroho kupitia vichapo na programu za mikutano na makusanyiko. (Mt. 24:45-47; linganisha na Matendo 15:6, 22-31.) Kwa kuongezea, undugu wetu wa Kikristo una Wakristo wakomavu, hasa wazee, ambao wana sifa za kustahili kutusaidia kibinafsi na kutupa mashauri ya Kimaandiko. (Isa. 32:1) Vijana walio katika familia za Kikristo wana chanzo kingine chenye thamani cha mwongozo. Wazazi wao ambao ni waamini wana mamlaka ambayo wamepewa na Mungu na sikuzote vijana wanatiwa moyo kuomba mwongozo kutoka kwao.—Efe. 6:1-3.

19. Tunapata baraka gani kwa sababu ya kuendelea kutafuta mwongozo wa Yehova?

19 Ndiyo, Yehova anatuongoza kwa njia mbalimbali, na tunapaswa kujitahidi kufaidika kabisa kutokana na mwongozo huo. Mfalme Daudi alisema hivi kuhusu wakati ambapo Waisraeli walikosa uaminifu: “Baba zetu walikutegemea wewe; walikutegemea, nawe ukaendelea kuwaokoa. Walikulilia, nao wakawa salama; walikutegemea, nao hawakuona aibu.” (Zab. 22:3-5) Tukitegemea na kufuata mwongozo wa Yehova, sisi pia ‘hatutaona aibu.’ Tumaini letu halitatukatisha tamaa. ‘Tukimkabidhi Yehova njia yetu,’ badala ya kutegemea hekima yetu wenyewe, tutapata baraka nyingi sana hata sasa. (Zab. 37:5) Na tukivumilia kwa ushikamanifu katika njia hiyo, tutafurahia baraka hizo milele. Mfalme Daudi aliandika hivi: “Yehova ni mpenda-haki, naye hatawaacha washikamanifu wake. Hakika watalindwa mpaka wakati usio na kipimo . . . Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zab. 37:28, 29.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini tunategemea mwongozo wa Yehova?

• Tunaonyesha nini tunapokataa mwongozo wa Yehova?

• Mkristo anahitaji unyenyekevu katika hali gani?

• Yehova anatuongoza jinsi gani leo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Je, unamtegemea Yehova katika kila jambo maishani mwako?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Hawa alikataa enzi kuu ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 10]

Hagari alihitaji sifa gani ili afuate mwongozo wa malaika?