Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana, Mkumbukeni Muumba Wenu Mkuu Sasa

Vijana, Mkumbukeni Muumba Wenu Mkuu Sasa

Vijana, Mkumbukeni Muumba Wenu Mkuu Sasa

“Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.” —MHU. 12:1.

1. Yehova anaonyesha jinsi gani kwamba ana uhakika kuwaelekea vijana wanaomwabudu?

YEHOVA anawaona vijana Wakristo kuwa wenye thamani na wenye kuburudisha kama matone ya umande. Kwa kweli, alitabiri kwamba katika siku ya “jeshi” la Mwana wake, vijana wanaume na wanawake ‘wangejitoa kwa hiari’ katika utumishi wa Kristo. (Zab. 110:3) Unabii huo ungetimizwa wakati ambapo watu kwa ujumla hawangemtii Mungu, wangependa sana pesa na kujifikiria tu, na wangekuwa wasiotii. Hata hivyo, Yehova alijua kwamba vijana wanaomwabudu wangekuwa tofauti. Hilo linaonyesha kwamba Yehova ana uhakika mkubwa sana kuwaelekea ninyi ndugu na dada vijana!

2. Kumkumbuka Yehova kunatia ndani nini?

2 Wazia shangwe ambayo Mungu anapata anapowaona vijana wakimkumbuka akiwa Muumba wao Mkuu. (Mhu. 12:1) Kwa kawaida, kumkumbuka Yehova kunatia ndani mambo mengi zaidi kuliko kumfikiria tu. Kunamaanisha kuchukua hatua ya kufanya yale yanayompendeza, kukubali sheria na kanuni zake zituongoze katika maisha yetu ya kila siku. Kunamaanisha pia kumtegemea Yehova, tukijua kwamba anataka sana kutusaidia. (Zab. 37:3; Isa. 48:17, 18) Je, hivyo ndivyo unavyohisi kuhusu Muumba wako Mkuu?

“Mtegemee Yehova kwa Moyo Wako Wote”

3, 4. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba alimtegemea Yehova, na kwa nini ni jambo la maana kumtegemea Yehova leo?

3 Bila shaka, Yesu Kristo ndiye mfano mzuri kabisa wa mtu aliyemtegemea Mungu. Aliishi kupatana na maneno ya Methali 3:5, 6: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” Muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa, Shetani alimfikia akijaribu kumshawishi akubali mamlaka na utukufu wa ulimwengu. (Luka 4:3-13) Yesu hakupotoshwa. Alijua kwamba “utajiri na utukufu na uzima” wa kweli ni “matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova.”—Met. 22:4.

4 Leo, watu wengi katika ulimwengu wana pupa na uchoyo. Ni jambo la hekima kufuata mfano wa Yesu katika mazingira kama hayo. Kumbuka pia kwamba Shetani ameazimia kutumia njia yoyote ile ili kuwashawishi watumishi wa Yehova watoke kwenye barabara nyembamba inayoongoza kwenye uzima. Anataka kila mtu atembee kwenye barabara pana inayoongoza kwenye uharibifu. Usikubali akudanganye! Badala yake, azimia kumkumbuka Muumba wako Mkuu. Mtegemee kabisa, na ushike imara “uzima ulio wa kweli,” ambao ni hakika na utakuja hivi karibuni.—1 Tim. 6:19.

Vijana, Muwe na Hekima!

5. Una maoni gani kuhusu wakati ujao wa ulimwengu huu?

5 Vijana wanaomkumbuka Muumba wao Mkuu wana hekima kuliko vijana wengine. (Soma Zaburi 119:99, 100.) Kwa sababu wana maoni ya Mungu, wanajua kabisa kwamba hivi karibuni ulimwengu huu utapitilia mbali. Ingawa ninyi vijana hamjaishi miaka mingi, bila shaka mmeona kwamba woga na mahangaiko yanazidi kuongezeka. Ikiwa mngali shuleni, inaelekea mmesikia kuhusu uchafuzi, kuongezeka kwa joto duniani pote, uharibifu wa misitu, na matatizo mengine kama hayo. Watu wanahangaishwa sana na mambo hayo, lakini ni Mashahidi wa Yehova peke yao wanaoelewa kikamili kwamba mambo hayo ni sehemu ya ishara inayoonyesha kwamba ulimwengu wa Shetani unakaribia mwisho wake.—Ufu. 11:18.

6. Vijana fulani wamedanganywa jinsi gani?

6 Inahuzunisha kwamba vijana fulani wanaomtumikia Mungu wameshindwa kukaa macho na hivyo wamepuuza uhakika wa kwamba wakati unaobaki wa ulimwengu huu ni mfupi sana. (2 Pet. 3:3, 4) Mashirika mabaya na ponografia (picha au habari za ngono) zimewatumbukiza vijana wengine katika dhambi nzito. (Met. 13:20) Inahuzunisha kama nini kupoteza kibali cha Mungu sasa tunapokaribia mwisho! Badala yake, jifunze kutokana na mambo yaliyowapata Waisraeli mwaka wa 1473 K.W.K. walipokuwa wamepiga kambi katika Nchi Tambarare za Moabu, wakiwa karibu sana kuingia katika Nchi ya Ahadi. Ni nini kilichotukia?

Walishindwa Wakiwa Karibu Kufika

7, 8. (a) Shetani alitumia mbinu gani katika Nchi Tambarare za Moabu? (b) Shetani anatumia mbinu gani leo?

7 Wakati huo, ni wazi kwamba Shetani alitaka kuwazuia Waisraeli wasipate urithi walioahidiwa. Baada ya Shetani kushindwa kuwalaani kupitia nabii Balaamu, alitumia mbinu ya ujanja zaidi; alijaribu kuwafanya wasistahili kupata baraka za Yehova. Wanawake wa Moabu walitumiwa kuwatongoza na kuwashawishi, na wakati huo Ibilisi alifanikiwa kwa kadiri fulani. Watu walianza kufanya uasherati na binti za Moabu na kumwinamia Baali wa Peori! Ingawa walikuwa karibu kupata urithi wao wenye thamani, yaani, Nchi ya Ahadi, Waisraeli 24,000 walikufa. Ulikuwa msiba mkubwa kama nini!—Hes. 25:1-3, 9.

8 Leo, tunakaribia haraka sana nchi nzuri zaidi ya ahadi, mfumo mpya wa mambo. Kama kawaida, Shetani anatumia upotovu wa maadili kuwachafua watu wa Mungu. Viwango vya maadili katika ulimwengu vimeshuka sana hivi kwamba uasherati unaonwa kuwa zoea la kawaida, na ngono kati ya watu wa jinsia moja inaonwa kuwa jambo la kibinafsi. Dada mmoja Mkristo alisema hivi: “Ni nyumbani tu na katika Jumba la Ufalme ndiko ambako watoto wangu wanajifunza kwamba ngono kati ya watu wa jinsia moja na ngono kati ya watu wasiofunga ndoa ni mwenendo mbaya machoni pa Mungu.”

9. Ni nini kinachoweza kutokea wakati wa “upeo wa ujana,” na vijana wanaweza kushughulikia hali hiyo jinsi gani?

9 Vijana wanaomkumbuka Muumba wao Mkuu wanajua kwamba ngono ni zawadi takatifu ambayo inahusiana na uhai na kuzaa. Hivyo, wanatambua kwamba uhusiano wa ngono unapaswa kupatana na mwongozo wa Mungu, ndani ya mpango wa ndoa. (Ebr. 13:4) Hata hivyo, inaweza kuwa vigumu kudumisha usafi wa kimaadili wakati wa “upeo wa ujana,” wakati ambapo tamaa ya ngono inakuwa yenye nguvu na inaweza kupotosha uwezo wa mtu wa kufanya maamuzi. (1 Kor. 7:36) Unaweza kufanya nini mawazo yasiyofaa yakiingia katika akili yako? Sali kwa bidii kwa Yehova ili akusaidie kukazia fikira mambo yanayofaa. Sikuzote Yehova anawasikiliza wale wanaomwomba kwa unyoofu. (Soma Luka 11:9-13.) Mazungumzo yenye kujenga yanaweza pia kukusaidia kurekebisha mawazo yako.

Chagua Miradi Yako kwa Hekima!

10. Tunapaswa kuepuka mtazamo gani mbaya, na ni maswali gani ambayo tunaweza kujiuliza?

10 Sababu moja inayowafanya vijana ulimwenguni wasijizuie na wafuatie tamaa za kimwili ni kwamba hawana “maono,” yaani, hawana mwongozo wa Mungu au tumaini hakika la wakati ujao. (Met. 29:18) Hali yao ni kama ya Waisraeli waliokataa mwongozo wa Mungu katika siku za Isaya ambao walifuatia tu “furaha na shangwe, . . . kula nyama na kunywa divai.” (Isa. 22:13) Badala ya kuwaonea wivu watu kama hao, kwa nini usitafakari kuhusu tumaini lenye thamani ambalo Yehova ameweka mbele ya watumishi wake washikamanifu? Ikiwa unamtumikia Mungu ukiwa kijana, je, unatazamia sana ulimwengu mpya? Je, unajitahidi kabisa ‘kuishi kwa utimamu wa akili huku ukilingojea tumaini la furaha’ ambalo Yehova ameweka mbele yako? (Tito 2:12, 13) Jibu lako litakusaidia unapojiwekea miradi na mambo ya kutanguliza.

11. Kwa nini vijana Wakristo walio shuleni wanapaswa kusoma kwa bidii?

11 Ulimwengu unataka vijana watumie nguvu zao kufuatia miradi ya kilimwengu. Ninyi vijana mlio shuleni mnapaswa kusoma kwa bidii ili mpate elimu nzuri ya msingi. Mnapaswa kukumbuka kwamba kusudi lenu si kupata tu kazi inayofaa bali pia kulitumikia kutaniko na kuwa wahubiri wa Ufalme wenye mafanikio. Ili kutimiza kusudi hilo, mnahitaji kuwa na uwezo wa kuwasiliana vizuri, busara, na uwezo wa kuwasadikisha wengine kwa utulivu na kwa heshima. Hata hivyo, vijana wanaojifunza Biblia na kujitahidi kufuata kanuni zake katika maisha yao, wanapata elimu bora zaidi nao wanajiwekea msingi mzuri wa maisha ya wakati ujao yenye mafanikio na ya milele.—Soma Zaburi 1:1-3. *

12. Familia za Kikristo zinapaswa kuiga mfano gani?

12 Katika Israeli, wazazi walikuwa na daraka la maana sana la kuwaelimisha watoto wao. Elimu hiyo ilitia ndani sehemu zote za maisha, hasa mambo ya kiroho. (Kum. 6:6, 7) Kwa hivyo, vijana Waisraeli ambao waliwasikiliza wazazi wao na watu wengine wenye umri mkubwa waliomwogopa Mungu hawakupata elimu tu bali pia hekima, ufahamu, uelewaji, na uwezo wa kufikiri, sifa za pekee sana ambazo zinatokana tu na elimu kumhusu Mungu. (Met. 1:2-4; 2:1-5, 11-15) Familia za Kikristo leo zinapaswa kuona elimu kwa njia hiyohiyo.

Wasikilize Wanaokupenda

13. Vijana fulani wanapata mashauri ya aina gani, na kwa nini wanapaswa kuwa waangalifu?

13 Vijana wanapata mashauri kutoka kwa watu wa kila aina, kutia ndani washauri wa shule, ambao mara nyingi wanatoa mashauri kuhusu kufanikiwa katika ulimwengu huu. Tafadhali sali ili Mungu akuongoze kupima mashauri yote kama hayo ukitumia Neno lake pamoja na chakula cha kiroho kinachotayarishwa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Unajua kupitia funzo lako la Biblia kwamba Shetani anawalenga hasa vijana na wale wasio na uzoefu. Kwa mfano, katika bustani ya Edeni, ingawa Hawa asiye na uzoefu hakumjua Shetani, alimsikiliza, na Shetani hakuwa ameonyesha kamwe kwamba anampenda. Matokeo yangekuwa tofauti kama nini ikiwa Hawa angemsikiliza Yehova, ambaye alikuwa amethibitisha katika njia nyingi kwamba alimpenda!—Mwa. 3:1-6.

14. Kwa nini tunapaswa kumsikiliza Yehova na wazazi waamini?

14 Muumba wako Mkuu anakupenda wewe pia, naye anakupenda akiwa na nia nzuri kabisa. Anataka uwe na furaha milele, si wakati huu tu! Kwa hiyo, kama mzazi anayejali, anakuambia hivi kwa fadhili, wewe pamoja na wote wanaomwabudu: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.” (Isa. 30:21) Ikiwa una wazazi waamini ambao wanampenda Yehova kikweli, una baraka nyingine. Sikiliza kwa heshima mashauri yao unapopanga miradi na mambo ya kutanguliza. (Met. 1:8, 9) Kwa kweli, wanataka upate uzima, ambao ni wenye thamani zaidi kuliko utajiri au umashuhuri katika ulimwengu huu.—Mt. 16:26.

15, 16. (a) Tunaweza kuwa na uhakika gani katika Yehova? (b) Ni somo gani la maana tunalojifunza kutokana na kisa cha Baruku?

15 Wale wanaomkumbuka Muumba wao Mkuu wanaishi maisha rahisi, wakiwa na uhakika kwamba Yehova hatawaacha wala kuwatupa “hata kidogo.” (Soma Waebrania 13:5.) Kwa sababu mtazamo huo mzuri unapingana na maoni ya ulimwengu, ni lazima tuwe waangalifu kutoruhusu roho ya ulimwengu ituongoze. (Efe. 2:2) Kuhusiana na hilo, mfikirie Baruku, mwandishi wa Yeremia. Baruku aliishi siku za mwisho za Yerusalemu zilizokuwa ngumu sana kabla tu ya jiji hilo kuharibiwa mwaka wa 607 K.W.K.

16 Huenda Baruku alitaka kuishi maisha mazuri zaidi ya kimwili. Yehova aliona hilo, na kwa fadhili akamwonya Baruku asiendelee kujitafutia “makuu.” Baruku alikuwa mnyenyekevu na mwenye hekima, kwa kuwa alimsikiliza Yehova na kuokoka uharibifu wa Yerusalemu. (Yer. 45:2-5) Hata hivyo, muda si muda, watu wengine walioishi siku za Baruku ambao walijitafutia mambo “makuu” ya kimwili na kutotanguliza ibada ya Yehova, walipoteza vitu vyao vyote mikononi mwa Wakaldayo (Wababiloni). Zaidi ya hilo, wengi wao waliuawa. (2 Nya. 36:15-18) Kisa cha Baruku kinatusaidia kuona kwamba uhusiano mzuri pamoja na Mungu ni wa maana zaidi kuliko utajiri na umashuhuri katika ulimwengu huu.

Iga Mifano Bora

17. Kwa nini Yesu, Paulo, na Timotheo ni mifano bora ya kuigwa na watumishi wa Yehova leo?

17 Neno la Mungu linatusaidia kutembea katika barabara ya uzima kwa kutupa mifano mingi mizuri ya kuiga. Kwa mfano, Yesu alikuwa na vipawa vingi kuliko mwanadamu mwingine yeyote aliyepata kuishi, hata hivyo, alikazia fikira ujumbe ambao ungewasaidia watu milele, yaani, “habari njema ya ufalme wa Mungu.” (Luka 4:43) Ili ampe Yehova yaliyo bora, mtume Paulo aliacha kazi nzuri sana, naye akatumia wakati na nguvu zake kuhubiri habari njema. Timotheo, ‘mtoto kwelikweli katika imani,’ aliiga mfano bora wa Paulo. (1 Tim. 1:2) Je, Yesu, Paulo, na Timotheo walijuta kwa sababu ya kufuata njia hiyo ya maisha? Hawakujuta kamwe! Kwa kweli, Paulo alisema kwamba aliona vitu vilivyotolewa na ulimwengu kuwa “takataka nyingi” vikilinganishwa na pendeleo la kumtumikia Mungu.—Flp. 3:8-11.

18. Ndugu mmoja kijana alifanya mabadiliko gani makubwa, na kwa nini hana majuto yoyote?

18 Vijana wengi Wakristo leo wanaiga imani ya Yesu, Paulo, na Timotheo. Kwa mfano, ndugu mmoja kijana ambaye zamani alikuwa na kazi yenye mshahara mnono aliandika hivi: “Nilipandishwa cheo kazini kwa sababu ninaishi kupatana na kanuni za Biblia. Hata ingawa ningepata pesa nyingi, nilihisi kwamba nilikuwa nikifuatilia upepo. Nilipozungumza na wasimamizi wa kampuni na kuwaeleza kwamba nilitaka kufuatia utumishi wa wakati wote, mara moja waliniahidi pesa zaidi huku wakifikiri kwamba ningeendelea na kazi. Lakini nilikuwa nimeazimia kuacha kazi. Watu wengi hawangeweza kuelewa kwa nini niliacha kazi nzuri ili kufuatia utumishi wa wakati wote. Niliwaeleza kwamba ninataka kutimiza kikweli wakfu wangu kwa Mungu. Sasa kwa kuwa ninatumia maisha yangu kumtumikia Yehova, nimepata uradhi na furaha ambayo singeweza kupata nikiwa na pesa nyingi au umashuhuri.”

19. Ni uamuzi gani wenye hekima ambao vijana wanatiwa moyo kufanya?

19 Maelfu ya vijana ulimwenguni pote wamefanya maamuzi kama hayo ya hekima. Kwa hivyo, ninyi vijana mnapofikiria wakati wenu ujao, iwekeni siku ya Yehova karibu akilini. (2 Pet. 3:11, 12) Msiwaonee wivu wale ambao wanautumia ulimwengu huu kikamili. Badala yake, wasikilize wale ambao wanakupenda kikweli. Kujiwekea “hazina mbinguni” ndilo jambo bora zaidi ambalo unaweza kufanya na ndilo jambo pekee linaloweza kukuletea faida za milele. (Mt. 6:19, 20; soma 1 Yohana 2:15-17.) Ndiyo, mkumbuke Muumba wako Mkuu. Yehova atakubariki ukifanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kuhusu elimu ya juu na kazi ya kuajiriwa, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi, Oktoba 1, 2005, ukurasa wa 26-31.

Je, Unakumbuka?

• Tunaonyesha jinsi gani kwamba tunamtegemea Mungu?

• Ni elimu gani iliyo bora zaidi?

• Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na Baruku?

• Ni nani walio mifano bora ya kuigwa, na kwa nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Yehova anatoa elimu bora zaidi

[Picha katika ukurasa wa 15]

Baruku alimsikiliza Yehova akaokoka uharibifu wa Yerusalemu. Unaweza kujifunza nini kutokana na mfano huo?