Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wako Peke Yao Lakini Hawajasahauliwa

Wako Peke Yao Lakini Hawajasahauliwa

Wako Peke Yao Lakini Hawajasahauliwa

MTUME Paulo aliwashauri Wakristo wenzake hivi: “Tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Gal. 6:10) Leo, bado tunafuata shauri hilo lililoandikwa kwa mwongozo wa roho na tunatafuta njia za kuwatendea mema waamini wenzetu. Kati ya wale wanaohitaji na wanaostahili kuonyeshwa upendo na kutaniko la Kikristo ni ndugu na dada zetu wapendwa waliozeeka ambao wanaishi katika makao ya kuwatunzia wazee.

Ni kweli kwamba katika nchi fulani ni jambo la kawaida kwa familia kuwatunza wazazi wazee nyumbani. Hata hivyo, katika nchi nyingine, mara nyingi watu wengi wazee wanakaa katika makao ya kuwatunzia wazee. Namna gani Wakristo waliozeeka wanaoishi katika makao hayo? Wanakabili magumu gani? Wanaweza kufanya nini ikiwa hawategemezwi na washiriki wa familia zao? Kutaniko la Kikristo linaweza kuwasaidia jinsi gani? Nasi tunapata faida gani tunapowatembelea kwa ukawaida?

Magumu ya Kuwa Katika Makao ya Kuwatunzia Wazee

Wakristo waliozeeka wanapohamia katika makao ya kuwatunzia wazee, wanaweza kujikuta katika eneo la kutaniko wasilolijua. Hivyo, huenda Mashahidi wa eneo hilo wasiwatembelee mara nyingi. Kwa kuongezea, katika makao hayo, inaelekea kwamba wataishi na watu walio na imani tofauti na yao. Kwa sababu hiyo huenda Mashahidi wenzetu waliozeeka wakakabili hali ngumu.

Kwa mfano, katika sehemu fulani, makao ya kuwatunzia wazee yanapanga kuwe na ibada ya kidini. Mfanyakazi mmoja katika makao hayo alisema: “Mashahidi fulani waliozeeka ambao hawawezi kuongea waziwazi wamepelekwa kwenye ibada kanisani kwa viti vya magurudumu bila kuombwa maoni yao.” Zaidi ya hilo, mara nyingi wafanyakazi wa makao hayo wanaona karamu za siku za kuzaliwa, Krismasi, au Ista kuwa nafasi nzuri za kuwafurahisha watu wanaotunzwa. Pia, Mashahidi fulani wanaotunzwa katika makao hayo wamepewa chakula ambacho dhamiri zao haziwaruhusu kula. (Mdo. 15:29) Tukiwatembelea kwa ukawaida ndugu na dada zetu wazee, tutaweza kuwasaidia kushughulikia hali hizo ngumu.

Msaada wa Kutaniko

Wakristo wa mapema walitambua kwamba wana daraka la kuwasaidia wenye umri mkubwa ambao hawakuwa na watu wa familia wa kuwategemeza. (1 Tim. 5:9) Vivyo hivyo, waangalizi leo wako macho kuhakikisha kwamba Mashahidi waliozeeka walio katika makao ya kuwatunzia wazee katika eneo lao hawapuuzwi. * Robert, ambaye ni mzee wa kutaniko, anasema hivi: “Inafaa kwa waangalizi Wakristo kuwatembelea kibinafsi watu waliozeeka ili kuona mahali wanapoishi na kusali pamoja nao. Kutaniko linaweza kufanya mengi ili kushughulikia mahitaji yao.” Tukitenga wakati wa kuwatembelea watu waliozeeka, tunaonyesha tunatambua kwamba Yehova anaona kuwatunza wale wenye uhitaji kuwa jambo la maana sana.—Yak. 1:27.

Kunapokuwa na uhitaji, wazee wanajitolea kufanya mipango ya kuwasaidia akina ndugu na dada zao wanaotunzwa kwenye makao yaliyo katika eneo lao. Robert anaeleza uhitaji mmoja: “Tunapaswa kuwatia moyo akina ndugu na dada waliozeeka wahudhurie mikutano ya Kikristo ikiwa wanaweza kufanya hivyo.” Hata hivyo, wazee wanaweza kufanya mipango mingine kwa ajili ya wale wasioweza kufika kwenye Jumba la Ufalme. Jacqueline, ambaye ana umri wa zaidi ya miaka 80 na anaugua ugonjwa wa kuvimba viungo, husikiliza mikutano kupitia simu. Anasema: “Ninafaidika sana ninaposikiliza mikutano inapoendelea. Siwezi kuruhusu kitu chochote kinizuie nisisikilize mikutano!”

Ikiwa Mkristo aliyezeeka hawezi kusikiliza mikutano kwa simu, wazee wanaweza kupanga mikutano irekodiwe. Yule anayepeleka kanda zilizorekodiwa kwa ndugu au dada aliye katika makao ya kuwatunzia wazee, anaweza kutumia nafasi hiyo kuwa na mazungumzo yenye kutia moyo pamoja na mtu huyo. Mwangalizi mmoja alisema hivi: “Kuwapasha habari ndugu na dada hao kuhusu washiriki wa kutaniko kunafanya wahisi kwamba bado wao ni sehemu ya familia yetu ya kiroho.”

Endelea Kuwasiliana Nao

Watu wengi waliozeeka wanafadhaika na kuvurugika sana wanapoanza kuishi katika makao hayo. Kwa sababu hiyo, wengine wanaamua kutochangamana na watu wengine. Hata hivyo, tukiwatembelea ndugu na dada zetu waliozeeka mara tu baada ya wao kuanza kuishi katika makao hayo na kuwaonyesha kwamba tunataka kuendelea kuwategemeza, tutawasaidia sana kupata tena amani ya moyoni na shangwe.—Met. 17:22.

Ndugu au dada waliozeeka wanapopoteza uwezo wa kufahamu mambo au uwezo wa kusikia au wanapokuwa na matatizo mengine yanayozuia mawasiliano, huenda wengine wakakata kauli kwamba hakuna haja ya kuwatembelea. Hata hivyo, tukijitahidi kuendelea kuwatembelea, hata ikiwa ni vigumu sana kuwasiliana nao, tunaonyesha kwamba tunaendelea ‘kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha heshima’ waamini wenzetu. (Rom. 12:10) Ndugu aliyezeeka anapoanza kusahau mambo yaliyotukia karibuni, tunaweza kumtia moyo asimulie mambo ya zamani—hata ya utotoni—au kutueleza jinsi alivyopata kweli ya Biblia. Tunaweza kufanya nini ikiwa anashindwa kupata maneno yanayofaa? Sikiliza kwa subira, na ikiwezekana, taja maneno mawili au matatu ambayo huenda anatafuta, au urudie mambo aliyosema na kumtia moyo aendelee kuzungumza. Akichanganyikiwa au ikiwa ana tatizo la kusema na haeleweki kwa urahisi, tunaweza kujaribu kuelewa anachomaanisha kwa kusikiliza kwa makini sauti yake.

Ikiwa haiwezekani kuwasiliana kwa kuongea, njia nyingine zinaweza kutumiwa. Laurence, ambaye ni painia, anamtembelea kwa ukawaida Madeleine, dada Mkristo mwenye umri wa miaka 80 ambaye hawezi kuzungumza. Laurence anaeleza jinsi dada huyo anavyowasiliana na watu: “Mimi hushika mkono wa Madeleine tunaposali pamoja. Naye huufinya mkono wangu kidogo na kupepesa macho kuonyesha kwamba anathamini pindi hizo.” Kushika mkono wa marafiki wetu waliozeeka au kuwakumbatia kwa shauku kunaweza kuwatia moyo sana.

Kuwapo Kwako Ni Muhimu

Kuwatembelea kwa ukawaida watu waliozeeka kunaweza kufanya watunzwe vizuri zaidi. Danièle, ambaye amekuwa akiwatembelea Mashahidi wenzake katika makao ya kuwatunzia wazee kwa miaka 20 hivi, anasema: “Wafanyakazi wa makao ya kuwatunzia wazee wanapotambua kwamba mtu anatembelewa kwa ukawaida, wanamtunza vizuri zaidi.” Robert, aliyenukuliwa juu, anasema: “Wafanyakazi wa makao ya wazee wanamsikiliza kwa utayari zaidi mtu anayemtembelea kwa ukawaida yule anayetunzwa. Huenda wasimheshimu kwa njia hiyo mgeni anayetembelea makao hayo mara mojamoja tu.” Kwa kuwa mara nyingi wafanyakazi hao wanashughulika na familia zenye kudai mengi mno, wanathamini sana wageni wanapowashukuru. Zaidi ya hayo, tukiwa na uhusiano mzuri pamoja nao, huenda wakawa tayari zaidi kuheshimu kanuni na imani za Shahidi ambaye wanamtunza.

Tunaweza pia kusitawisha uhusiano mzuri pamoja na wafanyakazi wa makao hayo kwa kujitolea kusaidia kazi ndogondogo. Katika maeneo fulani, ukosefu mkubwa wa wafanyakazi wenye ustadi unaweza kupunguza ubora wa huduma ambazo waliozeeka wanaweza kupata. Rébecca, ambaye anawatunza waliozeeka, anapendekeza hivi: “Kuna hekaheka nyingi sana wakati wa chakula. Kwa hiyo, huo unaweza kuwa wakati mzuri wa kumtembelea rafiki na kumsaidia kula.” Hatupaswi kusita kuwauliza wafanyakazi hao jinsi tunavyoweza kuwasaidia.

Tunapotembelea makao yaleyale kwa ukawaida, tutaweza kutambua mahitaji ya ndugu au dada yetu aliyezeeka, na kwa ruhusa ya wafanyakazi wa makao hayo, tunaweza kuyatimiza. Kwa mfano, tunaweza kurembesha chumba chake kwa picha za wapendwa wake au picha zilizochorwa na watoto. Kwa kufikiria mahitaji ya yule anayetunzwa katika makao hayo, tunaweza kumletea vazi la kumpasha joto au mafuta ya kujipaka, sabuni, na vitu vingine kama hivyo. Ikiwa kuna bustani katika makao hayo, tunaweza kumpeleka nje ili apunge hewa. Laurence, aliyenukuliwa mapema, anasema: “Madeleine anatazamia nimtembelee kila juma. Ninapowapeleka watoto, anatabasamu na kuchangamka!” Jitihada kama hizo zinaweza kuwachochea sana wale wanaoishi katika makao ya kuwatunzia wazee.—Met. 3:27.

Wote Wanafaidika

Kumtembelea kwa ukawaida mtu aliyezeeka kunaweza kuujaribu “uhalisi wa upendo” wetu. (2 Kor. 8:8) Kwa njia gani? Huenda tukahuzunika kuona rafiki akidhoofika hatua kwa hatua. Laurence anakubali hivi: “Mwanzoni, kudhoofika kwa Madeleine kuliniumiza sana hivi kwamba nililia kila wakati baada ya kumtembelea. Lakini niligundua kwamba kusali kwa bidii kunaweza kutusaidia kushinda mahangaiko yetu na kuwatia moyo wengine.” Kwa miaka mingi, Robert amekuwa akimtembelea ndugu Mkristo anayeitwa Larry ambaye ana ugonjwa wa kutetemeka (Parkinson). Robert anasema: “Ugonjwa huo umemdhoofisha sana Larry hivi kwamba siwezi tena kuelewa hata neno moja analosema. Lakini tunaposali pamoja, bado ninaweza kuona imani yake.”

Tunapowatembelea waamini wenzetu waliozeeka, si wao tu wanaofaidika, bali hata sisi tunafaidika. Azimio lao la kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova ijapokuwa wanaishi na watu wenye imani tofauti linatufundisha kwamba tunahitaji kuwa na imani na ujasiri. Utayari wao wa kupokea chakula cha kiroho ijapokuwa wana matatizo ya kusikia na kuona unakazia kwamba “mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mt. 4:4) Kwa kufurahia mambo madogo-madogo, kama vile tabasamu ya mtoto au kula pamoja na wengine, watu hao waliozeeka wanatukumbusha tutosheke na vitu tulivyo navyo. Kuthamini kwao mambo ya kiroho kunaweza kutusaidia kutanguliza mambo yanayofaa.

Kwa kweli, kutaniko lote linafaidika kutokana na msaada ambao tunawapa watu waliozeeka. Jinsi gani? Kwa kuwa watu ambao ni dhaifu kimwili wanategemea hasa upendo wa kindugu, hiyo ni nafasi nzuri kwa kutaniko kusitawisha sifa ya rehema. Kwa hiyo, sisi sote tunapaswa kuona kazi ya kuwatunza wale waliozeeka, hata kwa muda mrefu, kuwa sehemu ya kuhudumiana. (1 Pet. 4:10, 11) Wazee wakiongoza katika kazi hiyo, watawasaidia washiriki wengine wa kutaniko kuona kwamba sehemu hiyo ya utendaji wetu wa Kikristo haipaswi kupuuzwa kamwe. (Eze. 34:15, 16) Tukiwategemeza kwa upendo na kwa utayari Wakristo wenzetu waliozeeka, tunawahakikishia kwamba hawajasahauliwa!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Mwandishi wa kutaniko anapojua kwamba ndugu au dada katika kutaniko ameanza kuishi katika makao ya kuwatunzia wazee katika eneo lingine, litakuwa jambo linalofaa na la upendo kuwajulisha bila kukawia wazee wa kutaniko katika eneo hilo.

[Blabu katika ukurasa wa 28]

“Wafanyakazi wa makao ya kuwatunzia wazee wanapotambua kwamba mtu anatembelewa kwa ukawaida, wanamtunza vizuri zaidi”

[Picha katika ukurasa wa 26]

Sala zetu za kutoka moyoni zinaweza kumsaidia Shahidi mwenzetu aliyezeeka kupata tena amani ya moyoni

[Picha katika ukurasa wa 26]

Tutawatia nguvu waamini wenzetu waliozeeka tukiwaonyesha kwamba tunawapenda