Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Chagua Kumtumikia Yehova Ukiwa Kijana

Chagua Kumtumikia Yehova Ukiwa Kijana

Chagua Kumtumikia Yehova Ukiwa Kijana

“Endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini.”—2 TIM. 3:14.

1. Yehova ana maoni gani kuhusu utumishi wa Mashahidi wake vijana?

YEHOVA anaona utumishi mtakatifu ambao vijana wanatoa kuwa wa maana sana hivi kwamba aliongoza unabii unaowahusu utolewe. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Watu wako watajitoa kwa hiari katika siku ya jeshi lako. Katika fahari za utakatifu, kutoka tumbo la uzazi la mapambazuko, una kundi lako la vijana kama matone ya umande.” (Zab. 110:3) Ndiyo, Yehova anawathamini sana vijana wanaotaka kumtumikia.

2. Vijana leo wanakabili vishawishi gani kutoka katika ulimwengu wanapofanya maamuzi kuhusu wakati ujao?

2 Enyi vijana katika kutaniko la Kikristo, je, mmejiweka wakfu kwa Yehova? Huenda ikawa vigumu kwa vijana wengi kuamua kumtumikia Mungu wa kweli. Wasimamizi wa biashara, walimu, na nyakati nyingine washiriki wa familia na marafiki wanawatia moyo vijana kufuatia miradi ya kimwili. Vijana wanapofuatia miradi ya kiroho, mara nyingi ulimwengu unawadharau. Lakini, ukweli ni kwamba kumtumikia Mungu wa kweli ndiyo njia bora zaidi ya maisha. (Zab. 27:4) Kuhusiana na jambo hilo, fikiria maswali haya matatu: Kwa nini unapaswa kumtumikia Mungu? Unaweza kufanya nini ili ufanikiwe kuishi kulingana na wakfu wako kwa Mungu bila kujali mambo ambayo huenda watu wakasema au kufanya? Ni nafasi gani nzuri za utumishi mtakatifu zinazoweza kutokea?

Kumtumikia Yehova Ndio Uamuzi Unaofaa

3. Uumbaji wa Yehova unapaswa kutuchochea kufanya nini?

3 Kwa nini unapaswa kumtumikia yule Mungu wa kweli aliye hai? Andiko la Ufunuo 4:11 linataja sababu kuu: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” Yehova ndiye Muumba mkuu wa vitu vyote vilivyopo. Lo! Jinsi dunia ilivyo maridadi! Yehova ameumba vitu vyote—miti, maua, wanyama, bahari, milima, na maporomoko ya maji. Zaburi 104:24 inasema kwamba ‘dunia imejaa vitu ambavyo Mungu alitokeza.’ Tunashukuru kama nini kwamba kwa sababu ya upendo wake, Yehova ametupa mwili na akili inayotuwezesha kufurahia dunia na vitu vizuri vilivyomo! Je, kuthamini kutoka moyoni uumbaji huo wenye kustaajabisha hakupaswi kutuchochea tumtumikie?

4, 5. Ni matendo gani ya Mungu yaliyomfanya Yoshua amkaribie Yehova?

4 Sababu nyingine ya kumtumikia Yehova inaonyeshwa na maneno ya Yoshua, kiongozi wa Waisraeli. Mwishoni mwa maisha yake, Yoshua aliwaambia watu wa Mungu hivi: “Mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu.” Kwa nini Yoshua angeweza kusema hivyo?—Yos. 23:14.

5 Yoshua alipokuwa mtoto huko Misri, inaonekana alisikia kuhusu ahadi ya Yehova ya kuwapa Waisraeli nchi ambayo wangemiliki. (Mwa. 12:7; 50:24, 25; Kut. 3:8) Kisha, Yoshua aliona Yehova akianza kutimiza ahadi hiyo kwa kuleta Mapigo Kumi juu ya Misri na kumlazimisha Farao mkaidi awaruhusu wana wa Israeli waende zao. Yoshua alikuwa kati ya watu waliokombolewa kupitia Bahari Nyekundu, kisha aliona bahari hiyo ikimmeza Farao na jeshi lake. Wakati wa safari ndefu kupitia “ile nyika kubwa na yenye kuogopesha” ya Jangwa la Sinai, Yoshua aliona jinsi Yehova alivyowapa Waisraeli kila kitu walichohitaji. Hakuna hata mmoja wao aliyekufa kwa kiu au njaa. (Kum. 8:3-5, 14-16; Yos. 24:5-7) Wakati ulipofika wa Waisraeli kushinda mataifa yenye nguvu ya Wakanaani na kuimiliki Nchi ya Ahadi, Yoshua aliona jinsi kazi hiyo ilivyotegemezwa na yule Mungu ambaye yeye na Waisraeli wengine waliabudu.—Yos. 10:14, 42.

6. Ni nini kitakachokusaidia kusitawisha tamaa ya kumtumikia Mungu?

6 Yoshua alijua kwamba Yehova alikuwa ametimiza ahadi Zake. Hivyo, Yoshua alitangaza hivi: “Mimi na nyumba yangu, tutamtumikia Yehova.” (Yos. 24:15) Namna gani wewe? Unapofikiria ahadi ambazo Mungu wa kweli tayari ametimiza na zile atakazotimiza, je, unatamani kumtumikia kama Yoshua alivyofanya?

7. Kwa nini kubatizwa katika maji ni hatua ya maana?

7 Kutafakari kazi za uumbaji za Yehova na ahadi zake nzuri ajabu na zenye kutegemeka kabisa, kunapaswa kukuchochea kujiweka wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji. Ubatizo ni hatua ya maana inayopaswa kuchukuliwa na wale wanaotaka kumtumikia Mungu. Hilo linaonyeshwa wazi na Yesu ambaye ni Kielelezo chetu. Kabla tu ya kuanza kazi yake akiwa Masihi, alienda kubatizwa na Yohana Mbatizaji. Kwa nini Yesu alichukua hatua hiyo? Baadaye alisema hivi: “Nimeshuka kutoka mbinguni kufanya, si mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenituma.” (Yoh. 6:38) Yesu alibatizwa ili kuonyesha kwamba anajitoa kufanya mapenzi ya Baba yake.—Mt. 3:13-17.

8. Kwa nini Timotheo aliamua kumwabudu Mungu, na huenda ukahitaji kufanya nini?

8 Pia mfikirie Timotheo, kijana Mkristo ambaye baadaye alipewa kazi nyingi na mapendeleo mengi na Yehova. Kwa nini Timotheo aliamua kumwabudu Mungu wa kweli? Biblia inatuambia kwamba ‘alijifunza mambo na kushawishiwa kuyaamini.’ (2 Tim. 3:14) Ikiwa umejifunza Neno la Mungu na kushawishiwa kuamini kwamba mafundisho yake ni ya kweli, hali yako ni kama ile ya Timotheo. Sasa unahitaji kufanya uamuzi. Kwa nini usizungumze na wazazi wako kuhusu mambo ambayo ungependa kufanya? Wazazi wako pamoja na wazee wanaweza kukusaidia kuelewa matakwa ya Kimaandiko ya ubatizo.—Soma Matendo 8:12.

9. Wengine wanaweza kuhisi jinsi gani ukibatizwa?

9 Ubatizo ni mwanzo mzuri wa kumtumikia Mungu wa kweli. Unapochukua hatua hiyo, unaanza mbio za masafa marefu ambazo thawabu yake ni uzima wa milele na shangwe inayopatikana sasa kwa kufanya mapenzi ya Mungu. (Ebr. 12:2, 3) Pia, washiriki wa familia yako, ambao tayari wameanza kukimbia mbio hizo, na marafiki wako katika kutaniko la Kikristo watashangilia sana. Jambo la maana zaidi ni kwamba utafanya moyo wa Yehova ushangilie. (Soma Methali 23:15.) Ni kweli kwamba huenda wengine wasielewe kwa nini umechagua kumwabudu Yehova, na wanaweza kutilia shaka uamuzi wako. Wanaweza hata kukupinga. Lakini unaweza kukabiliana na matatizo hayo kwa mafanikio.

Wengine Wanapokuuliza Maswali au Kukupinga

10, 11. (a) Ni maswali gani ambayo huenda watu wakakuuliza kuhusu uamuzi wako wa kumtumikia Mungu? (b) Unaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyojibu maswali kuhusu ibada ya kweli?

10 Uamuzi wako wa kumtumikia Yehova unaweza kuwashangaza wanashule, majirani, na watu wa ukoo. Wanaweza kukuuliza kwa nini umefanya uamuzi huo na kukuuliza mambo unayoamini. Unapaswa kuwajibu kwa njia gani? Bila shaka, unahitaji kuchunguza maoni na hisia zako ili uweze kueleza sababu za kufanya uamuzi huo. Na unapojibu maswali kuhusu mambo unayoamini, je, kweli kuna kielelezo kingine bora unachoweza kufuata kuliko kile cha Yesu?

11 Viongozi wa kidini Wayahudi walipomuuliza Yesu maswali kuhusu ufufuo, aliwaelekeza kwenye andiko ambalo hawakuwa wamelifikiria. (Kut. 3:6; Mt. 22:23, 31-33) Mwandishi fulani alipomuuliza Yesu ni amri gani iliyo kubwa zaidi, Yesu alimtajia Maandiko yanayofaa ya Biblia. Mtu huyo alimshukuru Yesu kwa sababu ya jibu lake. (Law. 19:18; Kum. 6:5; Marko 12:28-34) Njia ya Yesu ya kutumia Maandiko na njia yake ya kuzungumza ilisababisha “mgawanyiko juu yake . . . kati ya umati,” na wapinzani wake hawangeweza kumdhuru. (Yoh. 7:32-46) Unapojibu maswali kuhusu imani yako, tumia Biblia na ujibu kwa “tabia-pole na heshima kubwa.” (1 Pet. 3:15) Ikiwa hujui jibu la swali fulani, kubali jambo hilo na uombe kufanya utafiti. Baadaye, chunguza habari hiyo ukitumia Fahirisi au programu ya kompyuta ya Watchtower Library ikiwa inapatikana katika lugha yenu. Ukijitayarisha vizuri, utajua ‘jinsi unavyopaswa kujibu.’—Kol. 4:6.

12. Kwa nini hupaswi kuruhusu mateso yakuvunje moyo?

12 Huenda ukakabili mambo mengi zaidi kuliko maswali kuhusu uamuzi wako na mambo unayoamini. Shetani Ibilisi, adui ya Mungu, anatawala ulimwengu. (Soma 1 Yohana 5:19.) Si jambo la busara kutazamia kupongezwa au kukubaliwa na kila mtu, na huenda ukapingwa. Huenda watu fulani ‘wakakutukana,’ na wanaweza kuendelea kufanya hivyo. (1 Pet. 4:4) Lakini kumbuka kwamba wengine pia waliteswa kama wewe. Yesu Kristo pia aliteswa. Mtume Petro aliteswa pia, naye aliandika hivi: “Wapendwa, msishangazwe juu ya moto unaowaka [mateso] katikati yenu, unaowapata ninyi ili kuwa jaribu, kana kwamba jambo geni linawapata. Kinyume chake, endeleeni kushangilia kwa maana ninyi ni washiriki katika mateso ya Kristo.”—1 Pet. 4:12, 13.

13. Kwa nini Wakristo wanaweza kushangilia wanapoteswa?

13 Kuvumilia mateso au upinzani ukiwa Mkristo ni sababu ya kushangilia. Kwa nini? Kwa sababu kukubaliwa na ulimwengu kunaweza kuonyesha kwamba unaishi kulingana na viwango vya Shetani, si vya Mungu. Yesu alionya hivi: “Ole, wakati wowote ule watu wote wanaposema vema juu yenu, kwa maana mambo kama hayo ndiyo ambayo mababu zao waliwafanyia manabii wa uwongo.” (Luka 6:26) Mateso yanaonyesha kwamba Shetani na ulimwengu wake wamekasirishwa nawe kwa sababu unamtumikia Yehova. (Soma Mathayo 5:11, 12.) Na ‘kushutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo’ ni jambo la kushangilia.—1 Pet. 4:14.

14. Ni mambo gani mazuri yanayoweza kutokea mtu anapoendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova hata anapoteswa?

14 Unapoendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova hata unapoteswa, kunakuwa na angalau matokeo manne mazuri. Unatoa ushahidi kumhusu Mungu na Mwana wake. Uvumilivu na uaminifu wako unawatia moyo ndugu na dada zako Wakristo. Watu fulani ambao hawamjui Yehova wanaweza kuchochewa kumtafuta. (Soma Wafilipi 1:12-14.) Na unapoona jinsi Yehova anavyokupa nguvu za kuvumilia majaribu, unazidi kumpenda.

Umefunguliwa “Mlango Mkubwa”

15. Ni ‘mlango gani mkubwa’ ambao mtume Paulo alifunguliwa?

15 Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu huduma yake huko Efeso: “Nimefunguliwa mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.” (1 Kor. 16:8, 9) Mlango huo uliongoza kwenye utendaji mkubwa wa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi katika jiji hilo. Kwa kutumia nafasi hiyo, Paulo aliwasaidia wengi kujifunza kumhusu Yehova na Kumwabudu.

16. Ni kwa njia gani mabaki ya watiwa-mafuta walipitia “mlango uliofunguliwa” katika mwaka wa 1919?

16 Mwaka wa 1919, Yesu Kristo aliyetukuzwa aliweka “mlango uliofunguliwa” mbele ya mabaki ya watiwa-mafuta. (Ufu. 3:8) Waliingia katika mlango huo na kuanza kuhubiri habari njema na kufundisha kweli ya Biblia kwa bidii zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Huduma yao ilizaa matunda gani? Sasa habari njema imefika katika sehemu za mbali zaidi za dunia, na karibu watu milioni saba wana tumaini la kupata uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu.

17. Ni kwa njia gani unaweza kupitia “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji”?

17 “Mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji” ungali wazi kwa watumishi wote wa Yehova. Wale wanaopitia katika mlango huo wanapata shangwe na wanaridhika wanaposhiriki zaidi katika kuhubiri habari njema. Enyi watumishi vijana wa Yehova, mnathamini kadiri gani pendeleo lisilo na kifani la kuwasaidia wengine ‘wawe na imani katika habari njema’? (Marko 1:14, 15) Je, umefikiria kutumika ukiwa painia wa kawaida au painia msaidizi? Ujenzi wa Majumba ya Ufalme, utumishi wa Betheli, na umishonari ni njia nyingine zinazoweza kufunguliwa kwa wengi wenu. Kwa kuwa wakati uliobaki wa ulimwengu huu mbovu wa Shetani ni mfupi, kuna uhitaji wa haraka wa kushiriki katika sehemu hizo za utumishi wa Ufalme. Je, utapitia “mlango mkubwa” kukiwa bado na wakati?

“Onjeni Mwone ya Kuwa Yehova Ni Mwema”

18, 19. (a) Ni jambo gani lililomsaidia Daudi kutamani sana kumtumikia Yehova? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Daudi hakujuta kamwe kumtumikia Mungu?

18 Mtunga-zaburi aliyeongozwa na roho aliwaalika wengine ‘waonje waone ya kuwa Yehova ni mwema.’ (Zab. 34:8) Mfalme Daudi wa Israeli la kale alipokuwa mvulana mchungaji, Yehova alimwokoa kutoka kwa mashambulizi ya wanyama-mwitu. Mungu alimtegemeza alipopigana na Goliathi na kumwokoa kutoka katika misiba mingine mingi. (1 Sam. 17:32-51; Zab. 18, maandishi ya utangulizi) Kwa sababu ya fadhili nyingi zenye upendo za Mungu, Daudi alichochewa kuandika hivi: “Wewe mwenyewe umefanya mambo mengi, Ee Yehova Mungu wangu, naam, kazi zako za ajabu na mawazo yako kutuelekea; hakuna wa kulinganishwa nawe.”—Zab. 40:5.

19 Daudi alimpenda sana Yehova, naye alitaka kumsifu kwa moyo na akili yake yote. (Soma Zaburi 40:8-10.) Kadiri miaka ilivyopita, Daudi hakujuta kamwe kutumia maisha yake akimwabudu Mungu wa kweli. Alithamini hasa kuishi kwa ujitoaji-kimungu—maisha ambayo yanaleta furaha isiyo na kifani. Alipozeeka, Daudi alisema: “Wewe ni tumaini langu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova, tegemeo langu tangu ujana wangu. Na mpaka wakati wa uzee na wa kuwa na kichwa chenye mvi, Ee Mungu, usiniache.” (Zab. 71:5, 18) Daudi alizidi kumtegemea Yehova na urafiki wao uliimarika, hata ingawa nguvu zake za kimwili zilikuwa zimepungua.

20. Kwa nini kumtumikia Mungu ndiyo njia bora ya kutumia maisha yako?

20 Maisha ya Yoshua, Daudi, na Timotheo yanaonyesha wazi kwamba kumtumikia Yehova ndiyo njia bora ya maisha. Faida za kimwili za muda mfupi zinazotokana na kufanya kazi katika ulimwengu huu haziwezi kufikia faida za muda mrefu unazopata kwa ‘kumtumikia Yehova kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote.’ (Yos. 22:5) Ikiwa hujajiweka wakfu kwa Yehova katika sala, jiulize, ‘Ni jambo gani linalonizuia nisiwe Shahidi wa Yehova?’ Ikiwa tayari wewe ni mwabudu aliyebatizwa wa Yehova, je, ungependa kuongeza furaha yako maishani? Basi, panua huduma yako, na uendelee kufanya maendeleo ya kiroho. Habari inayofuata itaonyesha jinsi unavyoweza kukua kiroho kwa kufuata kielelezo cha mtume Paulo.

Ungetoa Jibu Gani?

• Taja sababu mbili zinazoonyesha kwa nini tunapaswa kumtumikia Mungu.

• Ni mambo gani yaliyomsaidia Timotheo aamue kumtumikia Mungu?

• Kwa nini unapaswa kuendelea kuwa imara unapoteswa?

• Ni nafasi gani za utumishi unazoweza kutumia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kumtumikia Yehova ndiyo njia bora ya maisha

[Picha katika ukurasa wa 19]

Je, unaweza kujibu maswali kuhusu imani yako?