Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fanya Maendeleo ya Kiroho kwa Kufuata Mfano wa Paulo

Fanya Maendeleo ya Kiroho kwa Kufuata Mfano wa Paulo

Fanya Maendeleo ya Kiroho kwa Kufuata Mfano wa Paulo

“Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani.”—2 TIM. 4:7.

1, 2. Sauli wa Tarso alifanya mabadiliko gani katika maisha yake, naye alianza kufanya kazi gani ya maana?

ALIKUWA mtu mwenye akili na mwenye msimamo imara. Hata hivyo, ‘alijiendesha kupatana na tamaa za mwili wake.’ (Efe. 2:3) Baadaye, alisema kwamba alikuwa “mkufuru na mtesaji na mtu mwenye dharau.” (1 Tim. 1:13) Mtu huyo alikuwa Sauli wa Tarso.

2 Baada ya muda, Sauli alifanya mabadiliko makubwa katika maisha yake. Aliacha kabisa njia zake za zamani na akajitahidi sana ‘kutafuta faida ya walio wengi badala ya faida yake mwenyewe.’ (1 Kor. 10:33) Akawa mpole na akawaonyesha upendo mwororo wale ambao aliwatesa zamani. (Soma 1 Wathesalonike 2:7, 8.) Aliandika hivi, “Mimi nilikuja kuwa mhudumu,” kisha akaongezea, “Mimi, niliye mtu mdogo kuliko aliye mdogo zaidi kati ya watakatifu wote, nilipewa fadhili hizi zisizostahiliwa, ili niwatangazie mataifa habari njema juu ya utajiri usiopimika wa Kristo.”—Efe. 3:7, 8.

3. Kujifunza barua za Paulo na masimulizi ya huduma yake kutatusaidia jinsi gani?

3 Sauli, ambaye pia aliitwa Paulo, alifanya maendeleo makubwa sana ya kiroho. (Mdo. 13:9) Njia moja nzuri kabisa ya kufanya maendeleo ya haraka katika kweli ni kujifunza barua za Paulo na masimulizi ya huduma yake na kuiga mfano wake wa imani. (Soma 1 Wakorintho 11:1; Waebrania 13:7.) Acheni tuone jinsi kufanya hivyo kutakavyotuchochea kusitawisha mazoea mazuri ya kujifunza kibinafsi, kusitawisha upendo wa kweli kuelekea watu, na kuwa na maoni yanayofaa kujihusu.

Mazoea ya Paulo ya Kujifunza

4, 5. Funzo la kibinafsi lilimsaidia Paulo jinsi gani?

4 Akiwa Farisayo ambaye alielimishwa ‘miguuni pa Gamalieli, na kufundishwa kwa usahihi kabisa Sheria ya mababu,’ tayari Paulo alijua Maandiko kwa kadiri fulani. (Mdo. 22:1-3; Flp. 3:4-6) Mara tu baada ya kubatizwa, ‘alienda akaingia Arabia,’ labda katika Jangwa la Siria au mahali fulani penye utulivu katika Rasi ya Arabia ambapo palikuwa pazuri sana kwa ajili ya kutafakari. (Gal. 1:17) Inaonekana kwamba Paulo alitaka kutafakari kuhusu maandiko yaliyothibitisha kwamba Yesu ndiye Masihi. Zaidi ya hayo, Paulo alitaka kujitayarisha kwa ajili ya kazi iliyokuwa mbele yake. (Soma Matendo 9:15, 16, 20, 22.) Paulo alitenga wakati wa kutafakari kuhusu mambo ya kiroho.

5 Ujuzi na ufahamu wa Maandiko ambao Paulo alipata kupitia funzo lake la kibinafsi ulimwezesha kufundisha kweli kwa njia bora. Kwa mfano, kwenye sinagogi huko Antiokia katika Pisidia, Paulo alitumia angalau manukuu matano ya moja kwa moja kutoka katika Maandiko ya Kiebrania ili kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Masihi. Mara nyingi, Paulo alitaja pia maandiko matakatifu. Hoja zake za Kibiblia zilikuwa zenye kusadikisha sana hivi kwamba “wengi kati ya Wayahudi na kati ya wageuzwa-imani waliomwabudu Mungu wakawafuata Paulo na Barnaba” ili kujifunza mengi. (Mdo. 13:14-44) Wakati kikundi cha Wayahudi Waroma kilipomtembelea katika makao yake miaka mingi baadaye, Paulo aliwaeleza mambo “kwa kutoa ushahidi kamili kuhusiana na ufalme wa Mungu na kwa kutumia ushawishi kwao kuhusu Yesu kutoka katika sheria ya Musa na pia Manabii.”—Mdo. 28:17, 22, 23.

6. Ni nini kilichomsaidia Paulo kuendelea kuwa na nguvu za kiroho alipopata majaribu?

6 Alipopata majaribu, Paulo aliendelea kuchunguza Maandiko na kupata nguvu kutokana na ujumbe wake ulioandikwa kwa mwongozo wa Mungu. (Ebr. 4:12) Paulo alipokuwa amefungwa gerezani huko Roma kabla ya kuuawa, alimwomba Timotheo amletee “vitabu vya kukunjwa” na “vya ngozi.” (2 Tim. 4:13) Inaelekea kwamba vitabu hivyo vilikuwa sehemu ya Maandiko ya Kiebrania ambayo Paulo alitumia kujifunza kwa undani. Paulo alihitaji sana kujifunza Biblia kwa ukawaida na kupata ujuzi wa Maandiko ili aweze kusimama imara.

7. Taja faida unazoweza kupata ukijifunza Biblia kwa ukawaida.

7 Kujifunza Biblia kwa ukawaida, na vilevile kutafakari tukiwa na kusudi fulani, kutatusaidia kufanya maendeleo ya kiroho. (Ebr. 5:12-14) Mtunga-zaburi aliimba hivi kuhusu umuhimu wa Neno la Mungu: “Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu, kuliko maelfu ya vipande vya dhahabu na fedha. Amri yako hunifanya kuwa na hekima kuliko adui zangu, kwa sababu ni yangu mpaka wakati usio na kipimo. Nimeizuilia mbali miguu yangu kutoka katika kila pito baya, kusudi nipate kulishika neno lako.” (Zab. 119:72, 98, 101) Je, una zoea la kujifunza Biblia kibinafsi? Je, unajitayarisha kwa ajili ya migawo ya wakati ujao katika utumishi wa Mungu kwa kusoma Biblia kila siku na kutafakari kuhusu yale unayosoma?

Sauli Alijifunza Kuwapenda Watu

8. Sauli aliwatendea jinsi gani wale ambao hawakufuata dini ya Kiyahudi?

8 Kabla ya kuwa Mkristo, Sauli alikuwa na bidii katika dini yake, lakini hakuwajali sana watu ambao hawakufuata dini ya Kiyahudi. (Mdo. 26:4, 5) Alitazama na kuwaunga mkono Wayahudi fulani waliokuwa wakimpiga mawe Stefano. Huenda Sauli alipotazama tukio hilo alipata ujasiri zaidi wa kuwatesa Wakristo, na labda alifikiri kwamba Stefano alistahili adhabu ya kifo. (Mdo. 6:8-14; 7:54–8:1) Masimulizi hayo yaliyoongozwa na roho takatifu yanasema hivi: “Sauli akaanza kushughulikia kutaniko kwa njia mbaya kabisa. Akawa akivamia nyumba moja baada ya nyingine, akiwakokota nje wanaume na wanawake, na kuwatia gerezani.” (Mdo. 8:3) Alifikia “hatua ya kuwatesa hata katika majiji ya nje.”—Mdo. 26:11.

9. Ni tukio gani lililomfanya Sauli achunguze jinsi alivyowatendea watu?

9 Sauli alikuwa njiani kwenda Damasko ili kuwatesa wanafunzi wa Kristo wakati Bwana Yesu alipomtokea. Nuru isiyo ya kawaida ya Mwana wa Mungu ilimpofusha macho Sauli, naye akalazimika kuwategemea wengine ili wamwongoze. Kufikia wakati ambapo Yehova alimtumia Anania kurudisha uwezo wa Sauli wa kuona, mtazamo wa Sauli kuelekea watu ulikuwa umebadilika kabisa. (Mdo. 9:1-30) Baada ya kuwa mfuasi wa Kristo, alijitahidi sana kuwatendea watu wote kama Yesu alivyowatendea. Kwa hiyo, alihitaji kuacha kabisa jeuri na “kufanya amani na watu wote.”—Soma Waroma 12:17-21.

10, 11. Ni kwa njia gani Paulo alionyesha upendo wa kweli kuelekea watu?

10 Paulo hakutosheka tu kufanya amani na wengine. Alitaka kuwaonyesha upendo wa kweli, na huduma ya Kikristo ilimpa nafasi ya kufanya hivyo. Katika safari yake ya kwanza ya umishonari, alihubiri habari njema katika Asia Ndogo. Ingawa walipata upinzani mkali, Paulo na waandamani wake walijitahidi sana kuwasaidia wapole wawe Wakristo. Walirudi tena Listra na Ikoniamu, hata ingawa wapinzani walikuwa wamejaribu kumuua Paulo katika majiji hayo.—Mdo. 13:1-3; 14:1-7, 19-23.

11 Baadaye, Paulo na kikundi chake waliwatafuta watu wenye mwelekeo unaofaa katika jiji la Filipi, huko Makedonia. Lidia, Myahudi aliyegeuzwa imani alisikiliza habari njema na kuwa Mkristo. Wenye mamlaka waliwapiga Paulo na Sila kwa fimbo na kuwatupa gerezani. Hata hivyo, Paulo alimhubiria mlinzi wa jela, na mlinzi huyo pamoja na familia yake wakabatizwa na kuwa waabudu wa Yehova.—Mdo. 16:11-34.

12. Ni nini kilichomchochea Sauli mwenye dharau awe mtume mwenye upendo wa Yesu Kristo?

12 Kwa nini Sauli ambaye zamani alikuwa akiwatesa Wakristo aligeuka na kuwa Mkristo? Ni nini kilichomchochea mtu huyo mwenye dharau ageuke na kuwa mtume Paulo ambaye alikuwa mwenye fadhili na mwenye upendo, mtu aliyekuwa tayari kuhatarisha uhai wake ili awafundishe wengine kweli kumhusu Mungu na Kristo? Paulo mwenyewe anaeleza hivi: ‘Mungu, aliniita kupitia fadhili zake zisizostahiliwa, alipoona vema kumfunua Mwana wake kuhusiana nami.’ (Gal. 1:15, 16) Paulo alimwandikia hivi Timotheo: ‘Nilionyeshwa rehema ili kwamba kupitia mimi nikiwa ndiye wa kwanza kabisa Kristo Yesu aonyeshe ustahimilivu wake wote kuwa mfano wa wale watakaokuwa na imani yao kwake kwa ajili ya uzima wa milele.’ (1 Tim. 1:16) Yehova alimsamehe Paulo, na rehema na fadhili zisizostahiliwa ambazo alionyeshwa zilimchochea kuwaonyesha wengine upendo kwa kuwahubiria habari njema.

13. Ni nini kinachopaswa kutuchochea kuwaonyesha wengine upendo, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

13 Vivyo hivyo, Yehova anasamehe dhambi na makosa yetu. (Zab. 103:8-14) Mtunga-zaburi aliuliza hivi: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zab. 130:3) Bila rehema za Mungu, sisi sote hatungepata shangwe ya kutoa utumishi mtakatifu, wala hatungekuwa na tumaini la kupata uzima wa milele. Mungu ametuonyesha sisi sote fadhili nyingi zisizostahiliwa. Kwa hivyo, kama Paulo, tunapaswa kuwa na tamaa ya kuwaonyesha wengine upendo kwa kuwahubiria na kuwafundisha kweli na kuwatia nguvu waamini wenzetu.—Soma Matendo 14:21-23.

14. Tunaweza kupanua huduma yetu jinsi gani?

14 Paulo alitaka kufanya maendeleo akiwa mhudumu wa habari njema, na mfano wa Yesu uligusa moyo wake. Njia moja ambayo Mwana wa Mungu aliwaonyesha watu upendo usio na kifani ni kupitia kazi yake ya kuhubiri. Yesu alisema hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:35-38) Kwa kuwa mfanyakazi mwenye bidii, Paulo alitenda kupatana na sala yoyote ambayo huenda alitoa ya kuomba wafanyakazi zaidi. Namna gani wewe? Je, unaweza kuboresha huduma yako? Au unaweza kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme, labda hata kupanga kufanya utumishi wa upainia? Acheni tuwaonyeshe wengine upendo wa kweli kwa kuwasaidia wapate “kulishika sana neno la uzima.”—Flp. 2:16.

Maoni ya Paulo Kujihusu

15. Paulo alikuwa na maoni gani kujihusu akijilinganisha na Wakristo wenzake?

15 Akiwa mhudumu Mkristo, Paulo alituwekea mfano mzuri katika njia nyingine. Ingawa alipata mapendeleo mengi katika kutaniko la Kikristo, Paulo alijua vizuri kwamba hakustahili baraka hizo na kwamba hakupewa baraka hizo kwa sababu ya uwezo wake. Alitambua kwamba alipata baraka hizo kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu. Paulo alitambua kwamba Wakristo wengine pia walikuwa wahudumu wenye mafanikio wa habari njema. Paulo aliendelea kuwa mnyenyekevu hata ingawa alikuwa na mapendeleo kati ya watu wa Mungu.—Soma 1 Wakorintho 15:9-11.

16. Paulo alionyesha kwa njia gani unyenyekevu na kiasi kuhusiana na suala la kutahiriwa?

16 Fikiria jinsi Paulo alivyoshughulikia tatizo ambalo lilitokea katika jiji la Antiokia huko Siria. Kutaniko la Kikristo lililokuwa huko liligawanyika kwa sababu ya suala la kutahiriwa. (Mdo. 14:26–15:2) Kwa kuwa Paulo alikuwa amewekwa rasmi aongoze katika kazi ya kuwahubiria Watu wa Mataifa ambao hawakuwa wametahiriwa, huenda angejiona kuwa mtaalamu wa kushughulika na watu wasio Wayahudi na hivyo angejiona anastahili kabisa kusuluhisha tatizo hilo. (Soma Wagalatia 2:8, 9.) Hata hivyo, alipoona kwamba jitihada zake hazikufaulu kusuluhisha tatizo hilo, kwa unyenyekevu na kiasi aliunga mkono mipango ya kupeleka suala hilo kwa baraza linaloongoza huko Yerusalemu ili lizungumziwe. Paulo alishirikiana kikamili na washiriki wa baraza linaloongoza waliposikiliza suala hilo, wakafanya uamuzi, na kumchagua yeye kuwa mmoja wa wajumbe ambao wangetumwa kwenye makutaniko. (Mdo. 15:22-31) Hivyo, Paulo ‘alikuwa wa kwanza katika kuwaonyesha heshima’ watumishi wenzake.—Rom. 12:10b.

17, 18. (a) Paulo alikuza hisia gani kuelekea washiriki wa makutaniko? (b) Tunajifunza nini kumhusu Paulo kutokana na itikio la wazee wa Efeso alipokuwa akiwaacha?

17 Paulo aliyekuwa mnyenyekevu hakujitenga na ndugu na dada zake katika makutaniko. Badala yake, aliwapenda sana. Mwishoni mwa barua yake kwa Waroma, aliwasalimu watu zaidi ya 20 kwa kutaja majina yao. Wengi wao hawatajwi tena katika Maandiko, na ni wachache tu waliokuwa na mapendeleo ya pekee. Lakini walikuwa watumishi washikamanifu wa Yehova, na Paulo aliwapenda sana.—Rom. 16:1-16.

18 Urafiki na unyenyekevu wa Paulo ulijenga makutaniko. Baada ya kukutana na wazee wa Efeso kwa mara ya mwisho, ‘walimwangukia Paulo shingoni na kumbusu kwa wororo, kwa sababu waliumizwa hasa na neno alilosema kwamba hawangemwona uso wake tena.’ Hawangetenda hivyo ikiwa angekuwa mtu mwenye kiburi anayejitenga na watu.—Mdo. 20:37, 38.

19. Tunaweza kuonyesha jinsi gani “unyenyekevu wa akili” tunaposhughulika na Wakristo wenzetu?

19 Ni lazima watu wote wanaotaka kufanya maendeleo ya kiroho waonyeshe roho ya unyenyekevu kama Paulo alivyofanya. Aliwahimiza Wakristo wenzake ‘wasifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili wakiwaona wengine kuwa ni bora kuliko wao.’ (Flp. 2:3) Tunaweza kufuata shauri hilo jinsi gani? Njia moja ni kushirikiana na wazee wa kutaniko letu, kufuata mwongozo wao, na kuunga mkono maamuzi ya kihukumu wanayofanya. (Soma Waebrania 13:17.) Njia nyingine ni kuwaheshimu sana ndugu na dada zetu wote katika imani. Mara nyingi makutaniko ya watu wa Yehova yana watu kutoka katika mataifa, tamaduni, jamii, na makabila mbalimbali. Lakini je, hatupaswi kujifunza kuwatendea wote kwa upendo na bila ubaguzi kama Paulo? (Mdo. 17:26; Rom. 12:10a) Tunatiwa moyo ‘tukaribishane, kama vile Kristo pia alivyotukaribisha sisi, kwa kusudi la kumpa Mungu utukufu.’—Rom. 15:7.

‘Kimbia kwa Uvumilivu’ Shindano la Uzima

20, 21. Ni nini kitakachotusaidia kukimbia shindano la uzima kwa mafanikio?

20 Maisha ya Mkristo yanaweza kulinganishwa na mbio za masafa marefu. Paulo aliandika hivi: “Nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani. Tangu wakati huu na kuendelea nimewekewa akiba ya taji la uadilifu, ambalo Bwana, aliye mwamuzi mwadilifu, atanipa kuwa thawabu katika siku ile, lakini si mimi tu, bali pia na wale wote ambao wamependa kufunuliwa kwake.”—2 Tim. 4:7, 8.

21 Kufuata mfano wa Paulo kutatusaidia kukimbia shindano la uzima wa milele kwa mafanikio. (Ebr. 12:1) Hivyo basi, kwa vyovyote vile, acheni tuendelee kufanya maendeleo ya kiroho kwa kuwa na mazoea mazuri ya kujifunza kibinafsi, kwa kusitawisha upendo mwingi kuelekea watu, na kwa kudumisha mtazamo wa unyenyekevu.

Ungetoa Jibu Gani?

• Paulo alifaidika jinsi gani kwa kujifunza Maandiko kibinafsi kwa ukawaida?

• Kwa nini kuwapenda sana watu ni jambo la maana kwa Wakristo wa kweli?

• Ni sifa gani zitakazokusaidia kuwatendea wengine bila ubaguzi?

• Mfano wa Paulo unaweza kukusaidia jinsi gani kushirikiana na wazee wa kutaniko lenu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Pata nguvu kutokana na Maandiko, kama Paulo alivyofanya

[Picha katika ukurasa wa 24]

Waonyeshe wengine upendo kwa kuwahubiria habari njema

[Picha katika ukurasa wa 25]

Je, unajua kwa nini ndugu walimpenda sana Paulo?