Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fuatia “Utakatifu Katika Kumwogopa Mungu”

Fuatia “Utakatifu Katika Kumwogopa Mungu”

Fuatia “Utakatifu Katika Kumwogopa Mungu”

BIBLIA inaonyesha kwamba Yehova Mungu ana utakatifu usio na kifani inaposema hivi: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova.” (Isa. 6:3; Ufu. 4:8) Maneno ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa “utakatifu” yanamaanisha utakato au usafi wa kidini, kutokuwa na uchafu. Utakatifu wa Mungu unarejelea ukamilifu wake wa kimaadili katika mambo yote.

Je, Mungu mtakatifu, Yehova, hatazamii wale wanaomwabudu wawe watakatifu, yaani, wawe safi kimwili, kimaadili, na pia kiroho? Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Yehova anataka watu wake wawe watakatifu. Tunasoma hivi katika 1 Petro 1:16: “Muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.” Je, kweli wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kuiga utakatifu wa Yehova? Ndiyo, wanaweza, hata ingawa hawawezi kumwiga kikamilifu. Mungu anaweza kutuona kuwa watakatifu tukimwabudu tukiwa safi kiroho na tukiwa na uhusiano wa karibu pamoja naye.

Basi tunaweza kufanya nini ili kuwa safi katika ulimwengu wenye maadili machafu? Ni mazoea gani tunayopaswa kuepuka? Huenda tukahitaji kufanya mabadiliko gani katika usemi na mwenendo wetu? Acheni tuone yale tunayoweza kujifunza kutokana na maagizo ambayo Mungu aliwapa Wayahudi waliokuwa wakirudi katika nchi yao kutoka Babiloni mwaka wa 537 K.W.K.

‘Kutakuwa na Njia ya Utakatifu’

Yehova alitabiri kwamba watu wake ambao walikuwa utekwani Babiloni wangerudishwa katika nchi yao. Unabii huo wa kurudishwa uliwahakikishia hivi: “Hakika kutakuwa na njia kuu hapo, ndiyo, njia; nayo itaitwa Njia ya Utakatifu.” (Isa. 35:8a) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Yehova hakuwawezesha tu Wayahudi kurudi nyumbani bali pia aliwahakikishia kwamba angewalinda njiani.

Yehova aliwafungulia watumishi wake walio duniani leo “Njia ya Utakatifu” kutoka katika Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo. Katika mwaka wa 1919, aliwaweka huru Wakristo watiwa-mafuta kutoka katika utumwa wa kiroho wa dini ya uwongo, nao wakasafisha ibada yao hatua kwa hatua na kuondoa mafundisho yote ya uwongo. Tukiwa waabudu wa Yehova leo, tunafurahia mazingira ya kiroho yaliyo safi na yenye utulivu ambamo tunaweza kumwabudu Yehova na kuwa na uhusiano wenye amani pamoja naye na pamoja na wanadamu wenzetu.

Washiriki wa “kundi dogo” la Wakristo watiwa-mafuta na “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” ambao unaongezeka wamechagua kutembea katika njia ambayo ni takatifu nao wanawaalika wengine wajiunge nao. (Luka 12:32; Ufu. 7:9; Yoh. 10:16) “Njia ya Utakatifu” iko wazi kwa ajili ya watu wote ambao wako tayari ‘kutoa miili yao ikiwa dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu.’—Rom. 12:1.

“Asiye Safi Hatapita Juu Yake”

Katika mwaka wa 537 K.W.K., Wayahudi waliokuwa wakirudi walihitaji kutimiza takwa moja la maana. Andiko la Isaya 35:8b linasema hivi kuhusu wale wanaostahili kutembea kwenye “Njia ya Utakatifu”: “Asiye safi hatapita juu yake. Nayo itakuwa kwa ajili ya yule anayetembea katika njia hiyo, wala hakuna wapumbavu watakaotembea huku na huku juu yake.” Kwa kuwa Wayahudi walikuwa wanarudi Yerusalemu ili kuanzisha tena ibada safi, hakuna mtu yeyote mwenye nia ya ubinafsi, asiyeheshimu mambo matakatifu, au asiye safi kiroho angekubaliwa. Wale waliorudi walihitaji kufuata viwango vya juu vya Yehova vya maadili. Wale wanaotamani kupata kibali cha Mungu leo wanahitaji kutimiza takwa hilohilo. Ni lazima wafuatie “utakatifu katika kumwogopa Mungu.” (2 Kor. 7:1) Hivyo basi, ni mazoea gani tunayopaswa kuepuka?

Mtume Paulo aliandika hivi: “Matendo ya mwili ni wazi, nayo ni uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu.” (Gal. 5:19) Uasherati unatia ndani matendo yote ya kingono yanayohusisha matumizi ya viungo vya uzazi yanayofanywa nje ya kifungo cha ndoa. Mwenendo mpotovu unahusisha “ufisadi; ufasiki; mwenendo usio wa aibu; mwenendo mchafu.” Bila shaka, uasherati na mwenendo mpotovu ni mazoea ambayo hayapatani kabisa na utakatifu wa Yehova. Hivyo, wale ambao wanaendelea kuzoea mambo kama hayo hawaruhusiwi kuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo au wanatengwa na ushirika wa kutaniko. Ndivyo ilivyo na wale ambao wanazoea mwenendo mchafu sana, yaani, “ukosefu wa usafi wa kila namna kwa pupa.”—Efe. 4:19.

“Uchafu” unatia ndani dhambi mbalimbali. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa uchafu linamaanisha ukosefu wa usafi au uchafu wa kila aina, katika mwenendo, katika usemi, na kushirikiana kidini na watu wasioamini. Linatia ndani mazoea fulani machafu ambayo hayastahili hatua ya kihukumu. * Lakini je, wale wanaozoea kutenda mambo hayo machafu wanafuatia maisha ya utakatifu?

Tuseme kwamba Mkristo anaanza kutazama kwa siri ponografia (picha au habari za ngono). Hatua kwa hatua, tamaa chafu zinaamshwa na azimio lake la kuendelea kuwa safi machoni pa Yehova linadhoofika. Huenda mwenendo wake usiwe umefikia hatua ya kuwa mwenendo mchafu sana, lakini haendelei kufikiria tu ‘mambo yoyote yaliyo safi kiadili, yanayosemwa vema, ya wema wa adili, na yanayostahili sifa.’ (Flp. 4:8) Ponografia ni chafu na bila shaka inaharibu uhusiano wa mtu pamoja na Mungu. Ukosefu wa usafi wa aina yoyote haupaswi hata kutajwa katikati yetu.—Efe. 5:3.

Fikiria mfano mwingine. Tuseme Mkristo ana zoea la kupiga punyeto, yaani, kusisimua viungo vyake vya uzazi kimakusudi, iwe anafanya hivyo akitazama ponografia au bila kutazama ponografia. Ingawa usemi “kupiga punyeto” haupatikani katika Biblia, je, kuna shaka yoyote kwamba zoea hilo linachafua akili na hisia? Je, si kweli kwamba mtu anayeendelea kujichafua kwa njia hiyo ataharibu kabisa uhusiano wake pamoja na Yehova naye atakuwa mchafu machoni pa Mungu? Acheni tuchukue kwa uzito shauri la mtume Paulo na “tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho” na ‘kuviua viungo vya mwili wetu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani.’—2 Kor. 7:1; Kol. 3:5.

Ulimwengu huu unaotawaliwa na Shetani unakubali na hata kuwahimiza watu wafuatie mwenendo mchafu. Inaweza kuwa vigumu sana kushinda kishawishi cha kushiriki katika mwenendo mchafu. Lakini Wakristo wa kweli hawapaswi “kutembea kama vile mataifa wanavyotembea pia katika ubatili wa akili zao.” (Efe. 4:17) Yehova ataturuhusu tuendelee kutembea katika “Njia ya Utakatifu” ikiwa tu tutaepuka mwenendo mchafu, iwe ni katika siri au mbele ya watu.

“Hakuna Simba Atakayekuwa Hapo”

Ili kupata kibali cha Mungu mtakatifu, Yehova, huenda watu fulani wakahitaji kufanya mabadiliko fulani makubwa katika mwenendo na usemi. Andiko la Isaya 35:9 linasema hivi: “Hakuna simba atakayekuwa hapo, na wanyama-mwitu wenye kunyafua hawatakuja juu yake,” yaani, “Njia ya Utakatifu.” Kwa njia ya mfano, watu ambao ni wajeuri na wakali katika usemi na matendo wanalinganishwa na wanyama-mwitu. Bila shaka, hawataruhusiwa kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu. (Isa. 11:6; 65:25) Kwa hivyo, ni jambo la maana kwamba wote wanaotamani kupata kibali cha Mungu waache kabisa tabia hizo za kinyama na kufuatia maisha ya utakatifu.

Maandiko yanatushauri hivi: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.” (Efe. 4:31) Tunasoma hivi katika Wakolosai 3:8: “Yaondoleeni mbali mambo haya yote kutoka kwenu, ghadhabu, hasira, ubaya, matukano, na maneno machafu kutoka kinywani mwenu.” Neno “matukano” linalotumiwa katika maandiko hayo mawili linamaanisha maneno yenye kuumiza, kuaibisha, au ya kukufuru.

Leo, watu wengi wanatumia maneno yenye kuumiza na machafu, hata nyumbani. Wenzi wa ndoa wanarushiana maneno yenye kuumiza, maovu, au ya dharau na kuwatukana pia watoto wao. Wakristo hawapaswi kutumia maneno kama hayo katika nyumba zao.—1 Kor. 5:11.

Kufuatia “Utakatifu Katika Kumwogopa Mungu” Ni Baraka!

Ni pendeleo kubwa kama nini kumtumikia Mungu mtakatifu, Yehova! (Yos. 24:19) Yehova ametuingiza katika paradiso ya kiroho yenye thamani sana. Bila shaka, kudumisha mwenendo wetu ukiwa mtakatifu machoni pa Yehova ndiyo njia bora ya maisha.

Hivi karibuni dunia itakuwa Paradiso kama Mungu alivyoahidi. (Isa. 35:1, 2, 5-7) Wale wanaotamani Paradiso hiyo na kuendelea kufuatia maisha yanayompendeza Mungu watapata baraka ya kuishi humo. (Isa. 65:17, 21) Acheni basi tufanye yote tunayoweza kuendelea kumwabudu Mungu katika hali safi kiroho na kudumisha uhusiano wa karibu pamoja naye.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Kwa mazungumzo kuhusu tofauti ya kutenda “ukosefu wa usafi . . . kwa pupa” na “uchafu,” ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2006 (15/7/2006), ukurasa wa 29-31.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wayahudi walihitaji kutimiza matakwa gani ili watembee katika “Njia ya Utakatifu”?

[Picha katika ukurasa wa 27]

Ponografia inaharibu uhusiano wa mtu pamoja na Yehova

[Picha katika ukurasa wa 28]

“Kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu”