Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Ambavyo Baraza Linaloongoza Limepangwa

Jinsi Ambavyo Baraza Linaloongoza Limepangwa

Jinsi Ambavyo Baraza Linaloongoza Limepangwa

WASHIRIKI wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova ni wanaume waliojiweka wakfu ambao ni watumishi wa Mungu waliotiwa mafuta. Ni wawakilishi wa jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, ambayo ina daraka la kuandaa chakula cha kiroho, kutoa mwongozo, na kuwahimiza Mashahidi wa Yehova washiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme duniani pote.—Mt. 24:14, 45-47.

Mikutano ya Baraza Linaloongoza inafanywa kila juma, kwa kawaida siku ya Jumatano (Siku ya 3). Mikutano hiyo inawawezesha ndugu hao kufanya kazi pamoja kwa umoja. (Zab. 133:1) Washiriki wa Baraza Linaloongoza wanatumika pia katika halmashauri mbalimbali. Ili kushughulikia mambo ya Ufalme, kila halmashauri inasimamia utendaji fulani, kama habari inayofuata inavyoonyesha kwa ufupi.

▪ HALMASHAURI YA MRATIBU: Halmashauri hii ina waratibu wa halmashauri nyingine zote za Baraza Linaloongoza na mwandishi ambaye pia ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Inahakikisha kwamba halmashauri nyingine zote zinaendesha shughuli zake kwa njia nzuri. Halmashauri hiyo pia inashughulikia matatizo makubwa, mateso, misiba, na mambo mengine ya dharura yanayowahusu Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote.

▪ HALMASHAURI YA WAFANYAKAZI: Ndugu walio katika halmashauri hii wamepewa daraka la kusimamia mipango ya kushughulikia hali ya kibinafsi na ya kiroho ya washiriki wa familia ya Betheli duniani pote na kuwasaidia. Halmashauri hii inasimamia kazi ya kuwachagua na kuwaalika washiriki wapya wa familia za Betheli na kushughulikia masuala yanayohusu utumishi wa Betheli.

▪ HALMASHAURI YA UTANGAZAJI: Halmashauri hii inasimamia uchapaji, utangazaji, na usafirishaji wa vichapo vya Biblia ulimwenguni pote. Inasimamia mashini za kuchapia na majengo yanayomilikiwa na kuendeshwa na mashirika mbalimbali yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova. Halmashauri hii inapanga ili michango inayotolewa kwa ajili ya kazi ya Ufalme ya ulimwenguni pote itumiwe kwa njia nzuri zaidi.

▪ HALMASHAURI YA UTUMISHI: Washiriki wa halmashauri hii wanasimamia kazi ya kuhubiri na masuala yanayohusu makutaniko, mapainia, wazee, na waangalizi wanaosafiri. Inasimamia kazi ya kutayarisha Huduma Yetu ya Ufalme na inawaalika wanafunzi wa Shule ya Gileadi na Shule ya Mazoezi ya Kihuduma na kuwapa migawo baada ya kuhitimu.

▪ HALMASHAURI YA UFUNDISHAJI: Halmashauri hii inasimamia programu za ufundishaji katika makusanyiko yote na mikutano ya kutaniko. Inapanga programu za kiroho kwa ajili ya washiriki wa familia ya Betheli na inasimamia shule mbalimbali, kama vile Shule ya Gileadi na Shule ya Utumishi wa Painia, na pia utayarishaji wa programu za video na kaseti.

▪ HALMASHAURI YA UANDIKAJI: Halmashauri hii ina daraka la kusimamia uandikaji wa chakula cha kiroho ili kiweze kuchapishwa na kusambazwa kwa Mashahidi wa Yehova na kwa watu wote. Halmashauri hii inajibu maswali ya Biblia na kuidhinisha vifaa kama vile hati za drama na mihtasari ya hotuba. Pia, inasimamia kazi ya kutafsiri ulimwenguni pote.

Mtume Paulo alilinganisha kutaniko la watiwa-mafuta na mwili wa mwanadamu na kukazia kwamba washiriki wote wanatimiza kazi ya maana sana na pia wanategemeana, wanapendana, na wanashirikiana kufanya kazi waliyopewa na Mungu. (Rom. 12:4, 5; 1 Kor. 12:12-31) Kichwa, Yesu Kristo, anavipa viungo vya mwili kile kinachohitajiwa ili vishirikiane vizuri, vifanye kazi kwa upatano, na kupata chakula cha kiroho. (Efe. 4:15, 16; Kol. 2:19) Baraza Linaloongoza limepangwa kwa njia hiyo ili liongoze kama Yehova anavyolielekeza kwa roho takatifu.