Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Matendo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Matendo

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Matendo

KITABU cha Biblia cha Matendo kinaeleza kwa undani historia ya kuanzishwa na kupanuka kwa kutaniko la Kikristo. Kiliandikwa na tabibu Luka, na kina masimulizi yenye kusisimua ya utendaji wa Wakristo katika kipindi cha miaka 28, kuanzia 33 W.K. mpaka 61 W.K.

Sehemu ya kwanza ya kitabu cha Matendo inazungumzia hasa utendaji wa mtume Petro, na sehemu ya mwisho inahusu mtume Paulo. Luka anatumia maneno yanayoonyesha kwamba alikuwapo matukio fulani yalipotukia. Tukikazia fikira ujumbe wa kitabu cha Matendo tutathamini hata zaidi nguvu za Neno la Mungu lililoandikwa kwa roho yake takatifu. (Ebr. 4:12) Kufanya hivyo kutatuchochea pia kujidhabihu na kutajenga imani yetu katika tumaini la Ufalme.

PETRO ANATUMIA “FUNGUO ZA UFALME”

(Matendo 1:1–11:18)

Baada ya kupokea roho takatifu, mitume wanatoa ushahidi kwa ujasiri. Petro anatumia ufunguo wa kwanza kati ya “funguo za ufalme wa mbinguni” ili kuwafungulia mlango wa ujuzi na kuwapa Wayahudi na watu waliogeuzwa imani “waliokubali neno lake” nafasi ya kuingia katika Ufalme. (Mt. 16:19; Mdo. 2:5, 41) Mateso yanaongezeka na kuwatawanya wanafunzi, lakini hilo linafanya kazi ya kuhubiri ipanuke.

Mitume katika Yerusalemu wanaposikia kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, wanawatuma Petro na Yohana huko. Petro anatumia ufunguo wa pili anapowapa Wasamaria nafasi ya kuingia katika Ufalme. (Mdo. 8:14-17) Sauli wa Tarso anafanya mabadiliko ya kustaajabisha sana labda mwaka mmoja hivi baada ya Yesu kufufuliwa. Katika mwaka wa 36 W.K., Petro anatumia ufunguo wa tatu, na zawadi ya bure ya roho takatifu inamwagwa juu ya watu wasiotahiriwa wa mataifa.—Mdo. 10:45.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:44-47; 4:34, 35—Kwa nini waamini waliuza mali zao na kugawa mapato waliyopata? Watu wengi waliopata kuwa waamini walikuwa wametoka katika maeneo ya mbali sana nao hawakuwa na vyakula vya kutosha ili kuendelea kukaa Yerusalemu. Hata hivyo, walitamani kuendelea kukaa huko kwa muda mrefu zaidi ili wajifunze mengi kuhusu imani yao mpya na kuwatolea wengine ushahidi. Ili kuwasaidia watu hao, Wakristo fulani waliuza mali zao, na wenye uhitaji wakagawiwa pesa zilizokusanywa.

4:13—Je, Petro na Yohana hawakujua kusoma na kuandika au hawakuwa na elimu? Hapana, walikuwa na elimu. Waliitwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu” kwa sababu hawakuhudhuria shule za marabi ili kupata elimu ya kidini.

5:34-39—Luka alijua jinsi gani mambo ambayo Gamalieli alisema katika kikao cha Sanhedrini ambacho hakikuhudhuriwa na watu wote? Inawezekana kwamba alipata habari hizo angalau kwa njia tatu: (1) Labda Paulo, mwanafunzi wa zamani wa Gamalieli, alimjulisha Luka; (2) Labda Luka alizungumza na mshiriki wa Sanhedrini ambaye hakuwa na chuki, kama vile Nikodemo; (3) Huenda Luka alipata habari hizo kupitia mwongozo wa roho ya Mungu.

7:59—Je, Stefano alikuwa akisali kwa Yesu? Hapana, hakusali kwa Yesu. Ibada na pia sala zinapaswa kuelekezwa kwa Yehova Mungu peke yake. (Luka 4:8; 6:12) Chini ya hali za kawaida, Stefano angesali kwa Yehova katika jina la Yesu. (Yoh. 15:16) Hata hivyo, wakati huo, Stefano alipata maono ya “Mwana wa binadamu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.” (Mdo. 7:56) Huku akitambua vizuri kwamba Yesu alikuwa amepewa nguvu za kufufua wafu, Stefano alizungumza na Yesu moja kwa moja akimwomba ailinde roho yake, lakini hakusali kwake.—Yoh. 5:27-29.

Mambo Tunayojifunza:

1:8. Kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote inayofanywa na waabudu wa Yehova haiwezi kutimizwa bila msaada wa roho takatifu.

4:36–5:11. Yosefu wa Kipro alipewa jina Barnaba, ambalo linamaanisha “Mwana wa Faraja.” Labda mitume walimpa jina Barnaba kwa sababu alikuwa mchangamfu, mwenye fadhili, na aliwasaidia wengine. Tunapaswa kuwa kama yeye bali si kama Anania na Safira, ambao walikuwa wadanganyifu, wanafiki, na wenye hila.

9:23-25. Kuwaepa maadui ili kuendelea kuhubiri si tendo la woga.

9:28-30. Ikiwa kuhubiri katika maeneo fulani au kuwahubiria watu fulani kunahatarisha hali yetu ya kimwili, ya kiadili, au ya kiroho, tunahitaji kuchagua kwa busara mahali pa kuhubiri na wakati wa kuhubiri.

9:31. Katika pindi zenye amani ya kadiri, tunapaswa kujitahidi kuijenga imani yetu kwa kujifunza na kutafakari. Kufanya hivyo kutatusaidia kutembea katika kumwogopa Yehova kwa kutumia mambo tunayojifunza na kuwa na bidii katika huduma.

HUDUMA YENYE BIDII YA PAULO

(Matendo 11:19–28:31)

Katika mwaka wa 44 W.K., Agabo anakuja Antiokia, ambako Barnaba na Sauli wamekuwa wakifundisha “kwa mwaka mzima.” Agabo anatabiri “njaa kali,” ambayo inakuja miaka miwili baadaye. (Mdo. 11:26-28) Barnaba na Sauli wanarudi Antiokia “baada ya kutimiza kikamili ile huduma ya misaada katika Yerusalemu.” (Mdo. 12:25) Katika mwaka wa 47 W.K., miaka 12 hivi baada ya Sauli kuwa Mkristo, Barnaba na Sauli wanatumwa na roho takatifu kwa safari ya umishonari. (Mdo. 13:1-4) Katika mwaka wa 48 W.K., wanarudi Antiokia, “walikokuwa wamekabidhiwa kwenye fadhili zisizostahiliwa za Mungu.”—Mdo. 14:26.

Baada ya miezi tisa kupita, Paulo (ambaye pia anaitwa Sauli) anamchagua Sila kuwa mwandamani wake na wanaenda kwenye safari yake ya pili ya umishonari. (Mdo. 15:40) Timotheo na Luka wanajiunga na Paulo njiani. Luka anabaki Filipi naye Paulo anaendelea na safari mpaka Athene kisha Korintho, ambako anakutana na Akila na Prisila na kukaa huko kwa mwaka mmoja na miezi sita. (Mdo. 18:11) Paulo anawaacha Timotheo na Sila huko Korintho, naye anawachukua Akila na Prisila na kusafiri kwenda Siria mwanzoni mwa mwaka wa 52 W.K. (Mdo. 18:18) Akila na Prisila walienda naye mpaka Efeso, wakabaki huko.

Baada ya kukaa Antiokia ya Siria kwa muda fulani, Paulo anaanza safari yake ya tatu mwaka wa 52 W.K. (Mdo. 18:23) “Neno la Yehova [linazidi] kukua na kusitawi” huko Efeso. (Mdo. 19:20) Paulo anakaa huko kwa miaka mitatu hivi. (Mdo. 20:31) Pentekoste ya mwaka wa 56 W.K., inampata Paulo Yerusalemu. Baada ya kukamatwa, anatoa ushahidi bila kuogopa mbele ya wenye mamlaka. Huko Roma, mtume huyo anawekwa chini ya kifungo cha nyumbani kwa miaka miwili (karibu mwaka wa 59-61 W.K.), na akiwa huko anatafuta njia za kuhubiri kuhusu Ufalme na kufundisha “mambo yanayohusu Bwana Yesu Kristo.”—Mdo. 28:30, 31.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

14:8-13—Kwa nini watu wa Listra walimwita ‘Barnaba Zeu, lakini Paulo wakamwita Herme’? Zeu alikuwa mtawala wa miungu katika hadithi za Wagiriki, na mwana wake Herme alijulikana kwa sababu ya ufasaha wake wa kusema. Kwa kuwa Paulo ndiye aliyekuwa akiongoza katika mazungumzo, watu wa Listra walimwita Herme na Barnaba wakamwita Zeu.

16:6, 7—Kwa nini roho takatifu iliwakataza Paulo na washiriki wake wasihubiri katika wilaya ya Asia na Bithinia? Kulikuwa na wafanyakazi wachache tu. Hivyo, roho takatifu iliwaelekeza kwenye maeneo yenye matokeo zaidi.

18:12-17—Kwa nini Liwali Galio hakuwazuia watu walipoanza kumpiga Sosthene? Huenda Galio alifikiri kwamba mtu huyo aliyeongoza umati uliomshambulia Paulo alikuwa akipata alichostahili. Hata hivyo, inaonekana kwamba tukio hilo lilikuwa na matokeo mazuri kwa sababu lilimfanya Sosthene awe Mkristo. Baadaye, Paulo anamwita Sosthene “ndugu yetu.”—1 Kor. 1:1.

18:18—Ni nadhiri gani ambayo Paulo aliweka? Wasomi fulani wanadokeza kwamba Paulo aliweka nadhiri ya Wanadhiri. (Hes. 6:1-21) Hata hivyo, Biblia haisemi Paulo aliweka nadhiri gani. Zaidi ya hilo, Maandiko hayasemi ikiwa nadhiri hiyo iliwekwa kabla au baada ya Paulo kuwa Mkristo au ikiwa alikuwa anaanza kuitimiza au kuimaliza nadhiri hiyo. Kwa vyovyote vile, haikuwa dhambi kuweka nadhiri kama hiyo.

Mambo Tunayojifunza:

12:5-11. Tunaweza na tunapaswa kusali kwa ajili ya ndugu zetu.

12:21-23; 14:14-18. Herode alikubali utukufu ambao ni Mungu peke yake anayepaswa kupewa. Alikuwa tofauti kama nini na Paulo na Barnaba ambao bila kukawia walikataa kabisa sifa au heshima ambayo hawakustahili! Hatupaswi kutamani kupata utukufu kwa sababu ya mambo yoyote ambayo huenda tunatimiza katika utumishi wa Yehova.

14:5-7. Busara inaweza kutusaidia kuendelea na utumishi.—Mt. 10:23.

14:22. Wakristo wanatarajia kupata dhiki. Hawajaribu kuepuka dhiki kwa kulegeza msimamo wao wa imani.—2 Tim. 3:12.

16:1, 2Vijana Wakristo wanapaswa kuwa na bidii kabisa katika mambo ya kiroho na kutafuta msaada wa Yehova ili wawe na sifa nzuri.

16:3. Tunapaswa kufanya yote tunayoweza kupatana na Maandiko ili kufanya habari njema ikubaliwe na wengine.—1 Kor. 9:19-23.

20:20, 21. Kuhubiri nyumba kwa nyumba ni sehemu ya maana ya huduma yetu.

20:24; 21:13. Kudumisha utimilifu kwa Mungu ni jambo la maana zaidi kuliko kuokoa uhai wetu.

21:21-26. Tunapaswa kuwa tayari kukubali mashauri mazuri.

25:8-12. Wakristo leo wanaweza na wanapaswa kutumia mipango ya kisheria iliyopo “katika kutetea na kuithibitisha kisheria habari njema.”—Flp. 1:7.

26:24, 25. Tunapaswa kutangaza “maneno ya kweli na ya utimamu wa akili” hata ingawa ni upumbavu kwa “mtu wa kimwili.”—1 Kor. 2:14.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Petro alitumia “funguo za ufalme” wakati gani?

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote haingeweza kutimizwa bila msaada wa roho takatifu