Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunapaswa Kuwatendea Wengine Jinsi Gani?

Tunapaswa Kuwatendea Wengine Jinsi Gani?

Tunapaswa Kuwatendea Wengine Jinsi Gani?

“Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo.”—LUKA 6:31.

1, 2. (a) Mahubiri ya Mlimani ni nini? (b) Tutazungumzia nini katika habari hii na ile inayofuata?

KWA kweli, Yesu Kristo alikuwa Mwalimu Mkuu. Maadui wake wa kidini walipowatuma watu ili wamkamate, maofisa hao walirudi mikono mitupu na kusema: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” (Yoh. 7:32, 45, 46) Mahubiri ya Mlimani ni kati ya hotuba zenye kuchochea sana za Yesu. Hotuba hiyo inapatikana katika sura ya 5 mpaka sura ya 7 ya Injili ya Mathayo, na pia katika Luka 6:20-49. *

2 Labda maneno yanayojulikana sana katika mahubiri hayo ni yale yanayoitwa Kanuni Bora. Yanaonyesha jinsi tunavyopaswa kuwatendea wengine. Yesu alisema hivi: “Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo.” (Luka 6:31) Na ni kweli aliwatendea watu mambo mengi mazuri sana! Yesu aliwaponya wagonjwa na hata aliwafufua wafu. Hata hivyo, watu walibarikiwa hasa walipokubali habari njema aliyowafundisha. (Soma Luka 7:20-22.) Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunafurahi kushiriki katika kazi kama hiyo ya kuhubiri Ufalme. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Katika habari hii na ile inayofuata, tutazungumzia maneno ya Yesu kuhusu kazi hiyo na pia mambo mengine katika Mahubiri ya Mlimani ambayo yanaonyesha jinsi tunavyopaswa kuwatendea wengine.

Uwe Mwenye Tabia-Pole

3. Tabia-pole ni nini?

3 Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mt. 5:5) Maandiko hayaonyeshi kwamba kuwa na tabia-pole ni udhaifu. Ni upole ambao tunaonyesha tunapotimiza matakwa ya Mungu. Tunaonyesha mtazamo huo katika mwenendo wetu kuelekea wanadamu wenzetu. Kwa mfano, ‘hatumlipi yeyote uovu kwa uovu.’—Rom. 12:17-19.

4. Kwa nini watu walio na tabia-pole ni wenye furaha?

4 Watu walio na tabia-pole ni wenye furaha kwa sababu “watairithi dunia.” Yesu, ambaye alikuwa “mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni,” ndiye ‘aliyewekwa rasmi kuwa mrithi wa vitu vyote’ na kwa hiyo yeye ndiye Mrithi mkuu wa dunia. (Mt. 11:29; Ebr. 1:2; Zab. 2:8) Ilitabiriwa kwamba “mwana wa binadamu” wa Kimasihi angekuwa na watawala washiriki katika Ufalme wa kimbingu. (Dan. 7:13, 14, 21, 22, 27) Wakiwa “warithi pamoja na Kristo,” watiwa-mafuta 144,000 walio na tabia-pole wangeshiriki na Yesu katika kuirithi dunia. (Rom. 8:16, 17; Ufu. 14:1) Watu wengine walio na tabia-pole watabarikiwa kupata uzima wa milele duniani chini ya Ufalme.—Zab. 37:11.

5. Kuwa wapole kama Kristo kuna matokeo gani kwetu?

5 Tukiwa wakali, inaelekea wengine hawatapenda kushirikiana nasi na hivyo tutawafanya watuepuke. Hata hivyo, tukiwa wapole kama Kristo tutakuwa wenye kupendeza na tutawajenga kiroho washiriki wa kutaniko. Upole ni sehemu ya matunda ya roho ambayo nguvu ya utendaji ya Mungu inatokeza ndani yetu ‘tukiishi na kutembea kwa roho.’ (Soma Wagalatia 5:22-25.) Bila shaka, tunataka tuhesabiwe kati ya watu wenye tabia-pole ambao wanaongozwa na roho takatifu ya Yehova!

Walio na Rehema Ni Wenye Furaha Kama Nini!

6. “Walio na rehema” wana sifa gani bora?

6 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema hivi pia: “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” (Mt. 5:7) “Walio na rehema” wana huruma nyororo na wanaonyesha fadhili, hata wanawasikitikia wale walio na matatizo. Yesu aliwasaidia kimuujiza watu walioteseka kwa sababu ‘aliwasikitikia.’ (Mt. 14:14; 20:34) Kwa hiyo, kuwasikitikia na kuwahurumia watu kunapaswa kutuchochea kuwa wenye rehema.—Yak. 2:13.

7. Kuwasikitikia watu kulimchochea Yesu kufanya nini?

7 Umati wa watu ulipomfikia Yesu alipokuwa akitaka kupumzika kidogo, “akawasikitikia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji.” Kwa hiyo, “akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:34) Pia, tunakuwa wenye shangwe kama nini tunapowahubiria wengine ujumbe wa Ufalme na kuwaambia kuhusu rehema kuu ya Mungu!

8. Kwa nini walio na rehema ni wenye furaha?

8 Walio na rehema ni wenye furaha kwa sababu ‘wanaonyeshwa rehema.’ Tunapowatendea watu kwa rehema, kwa kawaida wanatenda kwa njia hiyohiyo. (Luka 6:38) Zaidi ya hayo, Yesu alisema: “Ikiwa mnawasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi pia.” (Mt. 6:14) Wale walio na rehema ndio tu wanaojua furaha inayotokana na msamaha wa dhambi na kupata kibali cha Mungu.

Kwa Nini “Wanaofanya Amani” Ni Wenye Furaha

9. Tutatenda jinsi gani ikiwa sisi ni watu wanaofanya amani?

9 Akitaja sababu nyingine inayoleta furaha, Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani, kwa kuwa wataitwa ‘wana wa Mungu.’” (Mt. 5:9) Ikiwa sisi ni watu wanaofanya amani, hatutakubali au kushiriki katika jambo lolote, kama vile mazungumzo ya uchongezi, ambayo yanaweza ‘kuwatenganisha wale wanaofahamiana.’ (Met. 16:28) Kwa maneno na kwa matendo, tutajitahidi kufanya amani na watu walio ndani na nje ya kutaniko la Kikristo. (Ebr. 12:14) Na tutafanya yote tunayoweza ili tupatikane tukiwa wenye amani hasa pamoja na Yehova Mungu.—Soma 1 Petro 3:10-12.

10. Kwa nini watu “wanaofanya amani” ni wenye furaha?

10 Yesu alisema kwamba wale “wanaofanya amani” ni wenye furaha, “kwa kuwa wataitwa ‘wana wa Mungu.’” Kwa sababu ya kuwa na imani katika Yesu akiwa Masihi, Wakristo watiwa-mafuta wanapewa “mamlaka ya kuwa watoto wa Mungu.” (Yoh. 1:12; 1 Pet. 2:24) Namna gani kuhusu “kondoo wengine” wa Yesu wanaofanya amani? Yesu atakuwa ‘Baba yao wa Milele’ wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu pamoja na warithi wenzake wa kimbingu. (Yoh. 10:14, 16; Isa. 9:6; Ufu. 20:6) Kufikia mwisho wa Utawala wake wa Miaka Elfu, hao “kondoo wengine” wanaofanya amani watakuwa watoto wa kidunia wa Mungu katika maana kamili.—1 Kor. 15:27, 28.

11. Tutawatendea wengine jinsi gani ikiwa tunaongozwa na “hekima inayotoka juu”?

11 Ili kuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova, “Mungu wa amani,” tunapaswa kuiga sifa zake, kutia ndani sifa ya kuwa wenye amani. (Flp. 4:9) Tukikubali kuongozwa na “hekima inayotoka juu,” tutawatendea wengine kwa njia ya amani. (Yak. 3:17) Ndiyo, tutakuwa watu wenye furaha wanaofanya amani.

“Acheni Nuru Yenu Iangaze”

12. (a) Yesu alisema nini kuhusu nuru ya kiroho? (b) Tunaweza kuacha nuru yetu iangaze jinsi gani?

12 Tunawatendea watu kwa njia bora zaidi tunapowasaidia kupata nuru ya kiroho kutoka kwa Mungu. (Zab. 43:3) Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba walikuwa “nuru ya ulimwengu” naye aliwahimiza waache nuru yao iangaze ili watu waweze kuona ‘matendo yao mazuri’ kuelekea wengine. Kwa kufanya hivyo, wangeangaza nuru ya kiroho “mbele ya watu,” au kwa faida ya wanadamu. (Soma Mathayo 5:14-16.) Leo, tunaacha nuru yetu iangaze kwa kuwatendea mema majirani wetu na kushiriki katika kazi ya kuhubiri habari njema “katika ulimwengu wote,” yaani, “katika mataifa yote.” (Mt. 26:13; Marko 13:10) Tuna pendeleo kubwa kama nini!

13. Tunatambuliwa kwa mambo gani?

13 Yesu alisema: “Jiji haliwezi kufichwa likiwa limesimama juu ya mlima.” Ni rahisi kuona jiji lolote lililo juu ya mlima. Vivyo hivyo, tunatambuliwa kwa matendo yetu mazuri tukiwa watangazaji wa Ufalme na kwa sifa kama vile kiasi na usafi wa maadili.—Tito 2:1-14.

14. (a) Eleza jinsi taa za karne ya kwanza zilivyokuwa. (b) Kutoficha nuru ya kiroho chini ya “kikapu cha kupimia” kunamaanisha nini?

14 Yesu alisema kuhusu kuwasha taa na kuiweka, si chini ya kikapu, bali juu ya kinara cha taa ili iwaangazie watu wote walio ndani ya nyumba. Katika karne ya kwanza, kwa kawaida taa ilikuwa chombo cha udongo chenye utambi ambao ulivuta mafuta (kwa kawaida mafuta ya zeituni) ili taa hiyo iendelee kuwaka. Mara nyingi iliwekwa juu ya kinara cha mbao au cha chuma ili ‘iwaangazie watu wote waliomo ndani ya nyumba.’ Watu hawangewasha taa na kuiweka chini ya “kikapu cha kupimia,” chombo kikubwa ambacho kingeweza kuchukua lita tisa hivi. Yesu hakutaka wanafunzi wake wafiche nuru yao ya kiroho chini ya kikapu cha kupimia cha mfano. Kwa hiyo, tunapaswa kuacha nuru yetu iangaze, na tusiruhusu kamwe upinzani au mateso yatufanye tufiche kweli ya Kimaandiko au kuwanyima wengine kweli hiyo.

15. ‘Matendo yetu mazuri’ yanakuwa na uvutano gani juu ya watu fulani?

15 Baada ya kusema kuhusu taa inayowaka, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Vivyo hivyo acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumpa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.” Kwa sababu ya ‘matendo yetu mazuri,’ watu fulani ‘wanampa Mungu utukufu’ kwa kuwa watumishi wake. Tunachochewa kama nini kuendelea ‘kuangaza kama mianga katika ulimwengu’!—Flp. 2:15.

16. Kwa kuwa sisi ni “nuru ya ulimwengu,” tunapaswa kufanya nini?

16 Kwa kuwa sisi ni “nuru ya ulimwengu,” tunapaswa kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Lakini tunahitaji kufanya jambo lingine. Mtume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kutembea kama watoto wa nuru, kwa maana matunda ya nuru yana kila namna ya wema na uadilifu na kweli.” (Efe. 5:8, 9) Sikuzote tunapaswa kuweka mfano mzuri kupitia mwenendo wetu unaompendeza Mungu. Kwa kweli, tunapaswa kutii shauri hili la mtume Petro: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa, ili, katika jambo ambalo wanasema juu yenu ya kuwa ninyi ni watenda-maovu, waweze, likiwa tokeo la matendo yenu mazuri ambayo wameshuhudia kwa macho, kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.” (1 Pet. 2:12) Lakini ni hatua gani tunayopaswa kuchukua ikiwa uhusiano wetu na mwamini mwenzetu si mzuri?

“Fanya Amani Yako Pamoja na Ndugu Yako”

17-19. (a) “Zawadi” inayotajwa katika Mathayo 5:23, 24 ilikuwa nini? (b) Kwa nini ni jambo la maana kupatana na ndugu, na Yesu alionyesha hilo jinsi gani?

17 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu aliwaonya wanafunzi wake juu ya kuendelea kumkasirikia na kumdharau ndugu. Badala yake, walipaswa kufanya haraka kufuatia amani na ndugu aliyekosewa. (Soma Mathayo 5:21-25.) Fikiria kwa uangalifu shauri la Yesu. Endapo ulikuwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na ukakumbuka kwamba ndugu yako alikuwa na jambo fulani juu yako, ulipaswa kufanya nini? Ulipaswa kuacha zawadi yako mbele ya madhabahu na kwenda kufanya amani pamoja na ndugu yako. Baada ya kufanya hivyo, ungerudi na kutoa zawadi yako.

18 Kwa kawaida, “zawadi” hiyo ilikuwa toleo la dhabihu ambalo mtu alitoa kwenye hekalu la Yehova. Dhabihu za wanyama zilikuwa za maana sana, kwa sababu Mungu aliamuru ziwe sehemu ya ibada ya Waisraeli chini ya Sheria ya Musa. Lakini ikiwa ungekumbuka kwamba ndugu yako alikuwa na jambo fulani juu yako, kutatua tatizo hilo kulikuwa jambo la maana zaidi kuliko kutoa zawadi yako. Yesu alisema: “Acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, itoe zawadi yako.” Lilikuwa jambo la maana sana kupatana tena na ndugu yako kabla ya kutoa dhabihu iliyoamuriwa na Sheria.

19 Maneno ya Yesu hayakuhusu tu matoleo fulani au makosa hususa. Kwa hiyo, mtu hakupaswa kutoa toleo lolote ikiwa alikumbuka kwamba ndugu yake ana jambo fulani juu yake. Ikiwa toleo hilo lilikuwa mnyama aliye hai, mnyama huyo alipaswa kuachwa “mbele ya madhabahu” ya toleo la kuteketezwa katika ua wa makuhani kwenye hekalu. Baada ya tatizo kutatuliwa, mkosaji angerudi na kutoa toleo lake.

20. Kwa nini tunapaswa kufanya haraka kusuluhisha mambo ikiwa tumekasirishwa na ndugu?

20 Kwa maoni ya Mungu, uhusiano wetu pamoja na ndugu zetu ni sehemu ya maana ya ibada ya kweli. Dhabihu za wanyama hazikuwa na maana machoni pa Yehova ikiwa wale waliozitoa waliwatendea wanadamu wenzao kwa njia isiyofaa. (Mika 6:6-8) Hivyo, Yesu aliwahimiza wanafunzi wake ‘wawe tayari kusuluhisha mambo upesi.’ (Mt. 5:25) Vivyo hivyo, Paulo aliandika hivi: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.” (Efe. 4:26, 27) Ikiwa tuna sababu ya kukasirika, tunapaswa kufanya haraka kusuluhisha mambo ili tusibaki katika hali ya kuchokozeka na hivyo kumpa Ibilisi nafasi ya kutushinda.—Luka 17:3, 4.

Sikuzote Watendee Wengine kwa Heshima

21, 22. (a) Tunaweza kufuata jinsi gani mashauri ya Yesu ambayo tumezungumzia? (b) Tutachunguza nini katika habari inayofuata?

21 Kujikumbusha mambo fulani yaliyosemwa na Yesu katika Mahubiri yake ya Mlimani kunapaswa kutusaidia kuwatendea wengine kwa fadhili na heshima. Ingawa sisi sote si wakamilifu, tunaweza kufuata mashauri ya Yesu kwa sababu Yesu na Baba yetu wa mbinguni hawatutazamii tutimize mambo ambayo hatuwezi kufanya. Kupitia sala, bidii, na msaada wa Yehova Mungu, tunaweza kuwa wenye tabia-pole, wenye rehema, na wanaofanya amani. Tunaweza kuangaza nuru ya kiroho ambayo inamletea Yehova utukufu. Zaidi ya hayo, tunaweza kufanya amani na ndugu zetu tunapohitaji kufanya hivyo.

22 Ibada inayokubalika machoni pa Yehova inatia ndani kuwatendea majirani wetu kwa njia inayofaa. (Marko 12:31) Katika habari inayofuata, tutachunguza mambo mengine katika Mahubiri ya Mlimani ambayo yatatusaidia kuendelea kuwatendea wengine mema. Hata hivyo, baada ya kutafakari mambo hayo yaliyotajwa katika hotuba hiyo ya Yesu isiyo na kifani, tunaweza kujiuliza, ‘Ninawatendea wengine jinsi gani?’

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Katika funzo lako la kibinafsi, inaelekea utafaidika sana ukisoma maandiko hayo kabla ya kuchunguza makala hii na ile inayofuata.

Ungetoa Jibu Gani?

• Kuwa mwenye tabia-pole kunamaanisha nini?

• Kwa nini “walio na rehema” ni wenye furaha?

• Tunaweza kuacha nuru yetu iangaze jinsi gani?

• Kwa nini tunapaswa ‘kufanya amani pamoja na ndugu yetu’ haraka?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 4]

Kutangaza ujumbe wa Ufalme ni njia ya maana sana ya kuangaza nuru yetu

[Picha katika ukurasa wa 5]

Wakristo wanapaswa kuweka mfano mzuri kupitia mwenendo unaompendeza Mungu

[Picha katika ukurasa wa 6]

Fanya yote unayoweza ili kufanya amani pamoja na ndugu yako