Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukombozi Kupitia Ufalme wa Mungu Uko Karibu!

Ukombozi Kupitia Ufalme wa Mungu Uko Karibu!

Ukombozi Kupitia Ufalme wa Mungu Uko Karibu!

“Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—MT. 6:10.

1. Fundisho kuu la Yesu lilikuwa nini?

KATIKA Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu Kristo alitoa sala ya mfano ambayo ilionyesha kwa ufupi fundisho lake kuu. Aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi kwa Mungu: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mt. 6:9-13) Yesu ‘alianza kusafiri kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.’ (Luka 8:1) Kristo aliwasihi wafuasi wake hivi: ‘Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wa Mungu.’ (Mt. 6:33) Unapojifunza habari hii, jitahidi kuona jinsi unavyoweza kuitumia katika huduma yako. Kwa mfano, fikiria jinsi unavyoweza kujibu maswali haya: Ujumbe wa Ufalme ni wa maana kadiri gani? Wanadamu wanahitaji kukombolewa kutokana na nini? Na Ufalme wa Mungu utaleta ukombozi jinsi gani?

2. Ujumbe wa Ufalme ni wa maana kadiri gani?

2 Yesu alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu ni ya maana sana. Ndiyo, huo ndio ujumbe wa maana zaidi ulimwenguni! Katika makutaniko zaidi ya 100,000 ya Mashahidi wa Yehova duniani pote, watumishi wa Mungu milioni saba hivi wanafanya kazi ya kuhubiri isiyo na kifani, wakiwaeleza wengine kwamba Ufalme umeanza kutawala. Hiyo ni habari njema kwa sababu inaonyesha kwamba Mungu ameanzisha serikali mbinguni ambayo itaongoza mambo duniani. Chini ya utawala wa Ufalme, mapenzi ya Yehova yatatendeka duniani kama ilivyo mbinguni.

3, 4. Matokeo yatakuwa nini mapenzi ya Mungu yatakapotendeka duniani?

3 Ni mabadiliko gani ambayo wanadamu wataona wakati mapenzi ya Mungu yatakapotendeka duniani? Yehova “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufu. 21:4) Watu hawatakuwa wagonjwa wala hawatakufa kwa sababu ya dhambi na hali ya kutokamilika waliyorithi. Wafu walio katika kumbukumbu la Mungu watapata pendeleo la kuishi milele, kwa kuwa Biblia inaahidi hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Mdo. 24:15) Hakutakuwa tena na vita, magonjwa, au njaa, na dunia itageuzwa kuwa paradiso. Hata wanyama ambao sasa ni hatari watakuwa na amani pamoja na wanadamu na pamoja na wanyama wengine.—Zab. 46:9; 72:16; Isa. 11:6-9; 33:24; Luka 23:43.

4 Kwa kuwa utawala wa Ufalme utaleta baraka hizo za ajabu, haishangazi kwamba unabii wa Biblia unazungumzia maisha ya wakati huo kwa maneno haya yenye kufariji: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” Lakini namna gani wale wanaosababisha taabu? Maandiko yanatabiri hivi: “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena.” Hata hivyo, “wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia.”—Zab. 37:9-11.

5. Mfumo wa sasa wa mambo utapatwa na nini?

5 Kabla ya mambo yote hayo kutukia, ni lazima mfumo wa sasa wa mambo uondolewe pamoja na mifumo yake yenye kupingana ya kiserikali, kidini, na kibiashara. Hivyo ndivyo serikali hiyo ya kimbingu itakavyofanya. Nabii Danieli alitabiri hivi kwa mwongozo wa roho ya Mungu: “Katika siku za wafalme hao [waliopo sasa], Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [mbinguni] ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [zilizopo], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Dan. 2:44) Ufalme wa Mungu, yaani, serikali mpya ya kimbingu, utatawala wakati huo juu ya jamii mpya ya wanadamu duniani. Kutakuwa na “mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.”—2 Pet. 3:13.

Kuna Uhitaji Mkubwa Zaidi wa Ukombozi Sasa

6. Biblia inasema nini kuhusu ubaya katika ulimwengu huu mbovu?

6 Shetani, Adamu, na Hawa walipomwasi Mungu, wakitaka kujiamulia yaliyo mema na yaliyo mabaya, huo ulikuwa mwanzo wa maisha yenye msiba kwa familia ya wanadamu. Miaka 1,600 baadaye, kabla ya Gharika ya ulimwenguni pote, “ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila mwelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote.” (Mwa. 6:5) Miaka 1,300 hivi baadaye, Sulemani aliona hali zikiwa mbaya sana hivi kwamba aliandika: “Nikawapongeza wafu ambao tayari walikuwa wamekufa badala ya wale wanaoishi waliokuwa wangali hai. Kwa hiyo aliye afadhali kuliko hao wawili ni yule ambaye hajakuwapo bado, ambaye bado hajaona kazi yenye msiba inayofanywa chini ya jua.” (Mhu. 4:2, 3) Leo, baada ya miaka 3,000 hivi kupita, ubaya unazidi kuongezeka.

7. Kwa nini kuna uhitaji mkubwa zaidi sasa wa kukombolewa na Mungu?

7 Ingawa ni kweli kwamba ubaya umekuwapo kwa muda mrefu, ukombozi kupitia Ufalme wa Mungu unahitajiwa zaidi sasa kuliko wakati mwingine wowote. Hali zimekuwa mbaya zaidi katika miaka 100 ambayo imepita kuliko wakati mwingine wowote, na zinaendelea kuzorota. Kwa mfano, ripoti ya shirika moja (Worldwatch Institute) inasema: “Hesabu ya watu waliokufa kwa sababu ya vita katika karne [ya 20] ni zaidi ya mara tatu ya wale waliokufa kutokana na vita vyote tangu karne ya kwanza W.K. mpaka mwaka wa 1899.” Tangu mwaka wa 1914, watu zaidi ya milioni 100 wamekufa kwa sababu ya vita! Kitabu kimoja kinakadiria kwamba hesabu ya watu waliokufa katika Vita vya Pili vya Ulimwengu inafikia milioni 60. Kwa kuwa mataifa fulani sasa hata yana silaha za nyuklia, wanadamu wana uwezo wa kuangamiza hesabu kubwa sana ya wanadamu wenzao. Na ijapokuwa kuna maendeleo ya kisayansi na ya kitiba, kila mwaka watoto milioni tano hivi wanakufa kwa sababu ya njaa.—Ona sura ya 9 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

8. Utawala wa wanadamu ambao umekuwapo kwa maelfu ya miaka umeonyesha wazi ukweli gani?

8 Wanadamu wameshindwa kukomesha ubaya. Mashirika ya kisiasa, kibiashara, na kidini ya ulimwengu huu hayajatimiza uhitaji wa msingi wa wanadamu wa kuwa na amani, ufanisi, na afya. Badala ya kusuluhisha matatizo makubwa ambayo yanawapata wanadamu sasa, mashirika hayo yamezidisha matatizo. Kwa hakika, utawala wa wanadamu ambao umekuwapo kwa maelfu ya miaka umeonyesha wazi ukweli wa maneno haya: “Njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yer. 10:23) Ndiyo, “mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhu. 8:9) Zaidi ya hayo, “uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.”—Rom. 8:22.

9. Wakristo wa kweli wanatazamia kuona hali gani katika ‘siku hizi za mwisho’?

9 Biblia ilitabiri hivi kuhusu nyakati zetu: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Baada ya kueleza hali ambazo zingekuwapo katika siku za mwisho chini ya utawala wa wanadamu, unabii huo unasema: “Watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.” (Soma 2 Timotheo 3:1-5, 13.) Wakristo wanatazamia mambo yawe hivyo kwa kuwa “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” Shetani. (1 Yoh. 5:19) Hata hivyo, habari njema ni kwamba hivi karibuni Mungu atawakomboa wale wanaompenda. Watakombolewa kutoka katika ulimwengu huu, ambao unaendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.

Chanzo Pekee cha Ukombozi Kinachotegemeka

10. Kwa nini Yehova ndiye Chanzo pekee cha ukombozi kinachotegemeka?

10 Unapohubiri habari njema, waambie watu kwamba Yehova ndiye Chanzo pekee cha ukombozi kinachotegemeka. Ni yeye tu aliye na nguvu na nia ya kuwakomboa watumishi wake kutoka katika hali yoyote mbaya. (Mdo. 4:24, 31; Ufu. 4:11) Tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yehova atawakomboa watu wake na kutimiza makusudi yake, kwa maana ameapa hivi: “Hakika kama vile nilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa.” Neno lake “halitarudi [kwake] bila matokeo.”—Soma Isaya 14:24, 25; 55:10, 11.

11, 12. Mungu anawapa watumishi wake uhakikisho gani?

11 Yehova ametoa uhakikisho wa kwamba atawakomboa watumishi wake anapotekeleza hukumu juu ya waovu. Alipokuwa akimtuma nabii Yeremia kuzungumza kwa ujasiri na watu waliotenda dhambi nzito, Mungu alisema hivi: “Usiogope.” Kwa nini? “Mimi niko pamoja nawe ili kukukomboa.” (Yer. 1:8) Vivyo hivyo, Yehova alipokuwa karibu kuharibu majiji yenye uovu ya Sodoma na Gomora, alituma malaika wawili wamwondoe Loti na familia yake katika eneo hilo na kuhakikisha kwamba walikuwa salama. “Ndipo Yehova akanyesha kiberiti na moto . . . juu ya Sodoma na juu ya Gomora.”—Mwa. 19:15, 24, 25.

12 Yehova anaweza pia kuwakomboa wale wanaofanya mapenzi yake hata wakiwa wametapakaa ulimwenguni pote. Alipoharibu ulimwengu mbovu wa kale katika Gharika, “alimlinda Noa, mhubiri wa uadilifu, akiwa salama pamoja na wengine saba.” (2 Pet. 2:5) Kwa mara nyingine tena, Yehova atawakomboa wanyoofu anapoharibu ulimwengu huu mbovu. Hivyo, Neno lake linasema: “Mtafuteni Yehova, ninyi nyote mlio wapole wa dunia . . . Utafuteni uadilifu, utafuteni upole. Huenda mkafichwa katika siku ya hasira ya Yehova.” (Sef. 2:3) Uharibifu huo utakaotukia ulimwenguni pote utawawezesha ‘wanyoofu kukaa duniani, lakini waovu watakatiliwa mbali kutoka ndani yake.’—Met. 2:21, 22.

13. Watumishi wa Yehova waliokufa watakombolewa jinsi gani?

13 Hata hivyo, watumishi wengi wa Mungu tayari wamekufa kwa sababu ya magonjwa, mateso, na mambo mengine. (Mt. 24:9) Basi, wote hao watakombolewa jinsi gani? Kama ilivyotajwa mwanzoni, “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu.” (Mdo. 24:15) Inafariji kabisa kujua kwamba hakuna kitu kinachoweza kumzuia Yehova asiwakomboe watumishi wake!

Serikali Yenye Uadilifu

14. Kwa nini tuna hakika kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali yenye uadilifu?

14 Katika huduma yako, unaweza kueleza kwamba Ufalme wa mbinguni wa Yehova ni serikali yenye uadilifu. Hilo ni kweli kwa sababu Ufalme huo unaonyesha sifa nzuri ajabu za Mungu, kama vile haki, uadilifu, na upendo. (Kum. 32:4; 1 Yoh. 4:8) Mungu amempa Yesu Kristo Ufalme huo kwa kuwa ndiye anayestahili zaidi kuitawala dunia. Pia, Yehova amekusudia Wakristo 144,000 waliotiwa mafuta wachukuliwe kutoka duniani na kufufuliwa kwenye uhai wa mbinguni wakiwa warithi-washirika pamoja na Kristo wakitawala pamoja naye juu ya dunia.—Ufu. 14:1-5.

15. Eleza tofauti iliyopo kati ya utawala wa Ufalme wa Mungu na utawala wa wanadamu.

15 Kutakuwa na tofauti kubwa kama nini kati ya utawala wa Yesu pamoja na wale 144,000 na utawala wa wanadamu wasio wakamilifu! Mara nyingi watawala wa mfumo huu wa mambo wamekuwa wakatili na wamewaongoza raia wao katika vita, na kusababisha mauaji ya mamilioni ya watu. Ndiyo sababu Maandiko yanatushauri tusimtegemee mwanadamu, “ambaye hana wokovu wowote”! (Zab. 146:3) Lakini Kristo atatawala kwa njia nzuri kama nini! Yesu alisema, “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mt. 11:28-30.

Siku za Mwisho Zitakwisha Karibuni!

16. Siku hizi za mwisho zitakwisha jinsi gani?

16 Ulimwengu huu umekuwa katika siku za mwisho, au “umalizio wa mfumo wa mambo,” tangu mwaka wa 1914. (Mt. 24:3) Sasa, hivi karibuni sana, ile ambayo Yesu aliita “dhiki kuu” itatukia. (Soma Mathayo 24:21.) Dhiki hiyo isiyo na kifani itakomesha ulimwengu wote wa Shetani. Lakini dhiki hiyo kuu itaanza jinsi gani? Nayo itakwisha jinsi gani?

17. Biblia inasema nini kuhusu kuanza kwa dhiki kuu?

17 Dhiki kuu itaanza ghafula. Ndiyo, “siku ya Yehova” itakuja bila kutazamiwa “wakati watakapokuwa wakisema: ‘Amani na usalama!’” (Soma 1 Wathesalonike 5:2, 3.) Dhiki hiyo iliyotabiriwa itaanza wakati mataifa yanapofikiri kwamba yako karibu kusuluhisha matatizo fulani makubwa. Uharibifu wa ghafula wa “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo, utaushangaza ulimwengu. Wafalme na watu wengine watashangaa wakati hukumu inapotekelezwa juu ya Babiloni Mkubwa.—Ufu. 17:1-6, 18; 18:9, 10, 15, 16, 19.

18. Yehova atachukua hatua gani Shetani atakapowashambulia watu Wake?

18 Katika wakati unaofaa kabisa, kutakuwa na “ishara katika jua na mwezi na nyota,” na ‘ishara ya Mwana wa binadamu itaonekana mbinguni.’ Hivyo, tunaweza ‘kusimama wima kwa sababu ukombozi wetu unakaribia.’ (Luka 21:25-28; Mt. 24:29, 30) Shetani, au Gogu, ataelekeza majeshi yake yawashambulie watu wa Mungu. Lakini Yehova anasema hivi kuhusu wale wanaowashambulia watumishi wake waaminifu: “Yeye anayewagusa ninyi anaigusa mboni ya jicho langu.” (Zek. 2:8) Hivyo, jaribio la Shetani la kuwaharibu halitafanikiwa. Kwa nini? Kwa sababu Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova atachukua hatua haraka ili kuwakomboa watumishi wake.—Eze. 38:9, 18.

19. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba majeshi ya Mungu ya kutekeleza hukumu yatauharibu mfumo wa Shetani?

19 Mungu atakapochukua hatua juu ya mataifa, ‘yatalazimika kujua kwamba yeye ni Yehova.’ (Eze. 36:23) Atatuma majeshi yake ya kutekeleza hukumu—makumi ya maelfu ya viumbe wa roho wakiongozwa na Kristo Yesu—ili kuharibu sehemu iliyobaki ya mfumo wa Shetani duniani. (Ufu. 19:11-19) Tukikumbuka kwamba katika pindi moja ilimchukua malaika mmoja usiku mmoja tu “kuwaua watu 185,000” ambao walikuwa maadui wa Mungu, tunaweza kuwa na hakika kwamba itakuwa kazi rahisi sana kwa jeshi hilo la mbinguni kuharibu sehemu zilizobaki za mfumo wa Shetani duniani wakati dhiki kuu inapofikia mwisho kwenye Har–Magedoni. (2 Fal. 19:35; Ufu. 16:14, 16) Shetani na roho wake waovu watafungwa katika abiso kwa miaka elfu moja. Mwishowe, wataharibiwa.—Ufu. 20:1-3.

20. Yehova atatimiza nini kupitia Ufalme?

20 Hivyo basi, uovu utakuwa umeondolewa duniani, na wanadamu waadilifu wataishi milele duniani. Yehova atakuwa amethibitika kuwa Mkombozi Mkuu. (Zab. 145:20) Kupitia Ufalme, atatetea enzi yake kuu, atatakasa jina lake takatifu, na kutimiza kusudi lake tukufu kwa ajili ya dunia. Na uwe na shangwe nyingi katika huduma yako unapotangaza hiyo habari njema na kuwasaidia wale ‘wenye mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele’ watambue kwamba ukombozi kupitia Ufalme wa Mungu uko karibu!—Mdo. 13:48.

Je, Unakumbuka?

• Yesu alikazia kwa njia gani kwamba Ufalme ni wa maana?

• Kwa nini ukombozi unahitajiwa zaidi sasa kuliko wakati mwingine wowote?

• Tunaweza kutazamia matukio gani wakati wa dhiki kuu?

• Yehova anathibitika kwa njia gani kuwa Mkombozi Mkuu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Neno la Mungu lilitabiri kwamba kazi isiyo na kifani ya kuhubiri ulimwenguni pote ingefanywa katika siku zetu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yehova anaweza kutukomboa kama vile alivyomkomboa Noa na familia yake

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yehova “atafuta kila chozi . . . , na kifo hakitakuwapo tena.”—Ufu. 21:4