Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha “Upendo Uliokuwa Nao Mwanzoni”

Dumisha “Upendo Uliokuwa Nao Mwanzoni”

Dumisha “Upendo Uliokuwa Nao Mwanzoni”

“Endelea kushika sana kile ulicho nacho.”—UFU. 3:11.

1, 2. Ulihisi jinsi gani uliposadiki kwamba yale uliyokuwa ukijifunza kumhusu Yehova ni kweli?

JE, UNAKUMBUKA mara ya kwanza ulipojifunza kuhusu tumaini zuri ambalo Yehova anawapa wanadamu watiifu? Ikiwa ulikuwa mshiriki wa dini nyingine, ulihisi jinsi gani ulipoelezwa makusudi ya Mungu kupitia Maandiko au wakati mafundisho ambayo hukuelewa hapo zamani yalipofafanuliwa? Labda ulitambua kwamba ulikuwa umepotoshwa. Lakini sasa unafurahi kama nini kwamba unajua kweli! Ikiwa ulilelewa na wazazi Wakristo, je, unakumbuka jinsi ulivyohisi uliposadiki kwamba yale uliyokuwa ukijifunza kumhusu Yehova ni kweli na ukaamua kuishi kupatana na kweli hiyo?—Rom. 12:2.

2 Ndugu zako wengi wa kiroho watakuambia kwamba walifurahi sana, walihisi wakiwa karibu na Yehova, na kushukuru kwamba amewavuta kwake. (Yoh. 6:44) Furaha yao iliwachochea kushiriki katika utendaji wa Kikristo. Walikuwa na shangwe nyingi sana hivi kwamba walitaka kumweleza kila mtu jinsi walivyohisi. Je, ulihisi hivyo pia?

3. Ni hali gani iliyokuwa katika kutaniko la Efeso wakati Yesu alipowatumia ujumbe?

3 Katika ujumbe wake kwa kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza huko Efeso, Yesu alizungumza kuhusu ‘upendo waliokuwa nao mwanzoni.’ Waefeso walikuwa na sifa nyingi nzuri, lakini upendo waliokuwa nao mwanzoni kwa Yehova ulikuwa umepoa. Hivyo, Yesu aliwaambia: “Mimi nayajua matendo yako, na kazi yako ya jasho na uvumilivu, na kwamba huwavumilii watu wabaya, na kwamba uliwajaribu wale wanaosema kwamba wao ni mitume, lakini wao sio, nawe uliwaona kuwa waongo. Wewe pia unaonyesha uvumilivu, nawe umestahimili kwa ajili ya jina langu nawe hujachoka. Hata hivyo, nina jambo hili dhidi yako, kwamba umeacha upendo uliokuwa nao mwanzoni.”—Ufu. 2:2-4.

4. Kwa nini ujumbe wa Yesu kwa Waefeso unafaa leo?

4 Mashauri ya Yesu kwa Waefeso na kwa makutaniko mengine aliyoyazungumzia katika kitabu cha Ufunuo yanafaa hasa tunapofikiria hali zilizokuwapo kwa muda fulani kati ya Wakristo watiwa-mafuta kuanzia mwaka wa 1914. (Ufu. 1:10) Hata hivyo, Wakristo fulani hata sasa wanaweza kuacha ‘upendo waliokuwa nao mwanzoni’ kwa Yehova na kweli ya Kikristo. Tukiwa na hilo akilini, acheni tuchunguze jinsi kukumbuka na kutafakari mambo ambayo yametukia katika maisha yako kunavyoweza kukusaidia kudumisha, kuchochea, na kujenga upendo na bidii uliyokuwa nayo mwanzoni kwa ajili ya Mungu na ile kweli.

Ni Nini Kilichokusadikisha Kwamba Umeipata Ile Kweli?

5, 6. (a) Kila Mkristo anapaswa kujihakikishia nini? (b) Ni nini kilichokusadikisha kwamba Mashahidi wa Yehova wanafundisha kweli? (c) Ni nini kinachoweza kumsaidia mtu kuuchochea upendo aliokuwa nao mwanzoni?

5 Kila mtu anayejiweka wakfu kwa Yehova anapaswa kwanza ‘ajihakikishie’ mwenyewe “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Rom. 12:1, 2) Hilo linatia ndani kujifunza kweli ya Biblia. Kile kinachomsadikisha mtu fulani kwamba Mashahidi wa Yehova wanafundisha kweli kinaweza kuwa tofauti na kile kinachomsadikisha mwingine. Wengine wanakumbuka kwamba mtazamo wao ulibadilika waliposoma jina la Mungu katika Biblia au walipojua kweli kuhusu hali ya wafu. (Zab. 83:18; Mhu. 9:5, 10) Wengine walivutiwa na upendo uliopo kati ya watu wa Yehova. (Yoh. 13:34, 35) Na wengine walifikiria kwa uzito maana ya kutokuwa sehemu ya ulimwengu. Walikata kauli kwamba Wakristo wa kweli hawapaswi kujihusisha katika mizozo ya kisiasa au vita vya taifa lolote lile.—Isa. 2:4; Yoh. 6:15; 17:14-16.

6 Mambo hayo na mengine ndiyo yaliyowachochea wengi waanze kumpenda Mungu. Hebu tua kidogo na ukumbuke kile kilichokusadikisha wewe mwenyewe kwamba umeipata ile kweli. Kwa kuwa hali zako na sifa zako ni tofauti na za wengine, huenda sababu zako za msingi za kumpenda Yehova na kuamini ahadi zake ni tofauti na za wengine. Inaelekea sana kwamba bado unaona sababu hizo kuwa za kweli leo kama ulivyoziona ulipojifunza kwa mara ya kwanza. Kweli haibadiliki. Hivyo, kujikumbusha mambo hayo na jinsi ulivyohisi kunaweza kuamsha na kuchochea upendo wako wa kwanza kwa ajili ya ile kweli.—Soma Zaburi 119:151, 152; 143:5.

Jenga Juu ya Msingi Wako

7. Kwa nini tunapaswa kukuza upendo wetu wa kwanza kwa ajili ya ile kweli, nasi tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

7 Huenda maisha yako yamebadilika sana tangu ulipojiweka wakfu kwa Yehova. Upendo wako wa kwanza kwa ajili ya ile kweli ulikuwa wa maana sana, lakini muda ulipopita, ulihitaji kuwa na upendo mwingi zaidi ili kushughulikia matatizo mapya yaliyojaribu imani yako. Hata hivyo, Yehova alikutegemeza. (1 Kor. 10:13) Hivyo, mambo uliyojionea maishani kadiri miaka ilivyopita ni yenye thamani pia kwako. Yamekusaidia kukuza upendo uliokuwa nao mwanzoni, na ni njia nyingine ya kujihakikishia mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika.—Yos. 23:14; Zab. 34:8.

8. Yehova alijitambulisha kwa Musa jinsi gani, na ni kwa njia gani Waisraeli walipata kumjua Mungu kwa ukaribu zaidi?

8 Kwa mfano, fikiria hali ya Waisraeli wakati Yehova alipotangaza kusudi lake la kuwakomboa kutoka utumwani huko Misri. Mungu alijitambulisha kwa Musa aliposema hivi: “Nitakuwa kile nitakachokuwa.” (Kut. 3:7, 8, 13, 14) Ni kana kwamba Yehova alikuwa akisema angekuwa chochote ambacho angehitaji kuwa ili kuwaweka huru watu wake. Katika matukio yaliyofuata na ikitegemea hali zilizokuwapo, Waisraeli waliona Yehova akifunua utu wake kwa njia mbalimbali—akiwa Mweza-Yote, Hakimu, Kiongozi, Mkombozi, Shujaa wa Vita, na Mwandalizi.—Kut. 12:12; 13:21; 14:24-31; 16:4; Neh. 9:9-15.

9, 10. Ni hali gani zinazoweza kumsaidia mtu kumjua Mungu, na kwa nini ni vizuri kukumbuka pindi hizo?

9 Hali yako ni tofauti na ile ya Waisraeli wa kale. Hata hivyo, inaelekea kwamba kuna mambo fulani katika maisha yako ambayo yamekusadikisha kwamba Mungu anakujali, na hivyo yametia nguvu imani yako. Huenda kwa njia fulani Yehova alithibitika kuwa Mwandalizi, Mfariji, au Mwalimu. (Soma Isaya 30:20b, 21.) Au huenda uliona sala yako ikijibiwa waziwazi. Labda ulikuwa ukikabili tatizo fulani, kisha Mkristo mwenzako akakusaidia. Au pengine funzo la kibinafsi lilikusaidia kupata maandiko yanayofaa hali yako.

10 Ukiwaeleza watu mambo hayo, huenda wengine wasishangae sana. Labda ni kwa sababu mambo hayo si ya kimuujiza. Lakini wewe binafsi unayaona kuwa ya maana sana. Ndiyo, Yehova alithibitika kuwa kile alichohitaji kuwa ili kukusaidia wewe binafsi. Hebu fikiria miaka yote ambayo umekuwa katika kweli. Je, unakumbuka pindi zote ambazo ulihisi kwamba Yehova anakujali? Ikiwa ndivyo, kukumbuka mambo yaliyotukia na jinsi ulivyohisi kunaweza kukuchochea umpende Yehova kama ulivyompenda wakati huo. Thamini sana pindi hizo. Tafakari kuhusu mambo hayo. Yanathibitisha kwamba Yehova anakujali wewe binafsi, na hakuna anayeweza kukunyang’anya usadikisho huo.

Jichunguze

11, 12. Ikiwa upendo wa Mkristo kwa ajili ya kweli umepoa, sababu inaweza kuwa nini, na Yesu alitoa shauri gani?

11 Ikiwa upendo uliokuwa nao kuelekea Mungu na ile kweli umepoa, si kwa sababu amebadilika. Yehova habadiliki kamwe. (Mal. 3:6; Yak. 1:17) Alikujali wakati huo, naye anakujali leo pia. Kwa hiyo, ni nini ambacho huenda kimefanya uhusiano wako pamoja na Yehova ubadilike? Je, inawezekana kwamba una mikazo mingi sana au mahangaiko mengi ya maisha? Huenda zamani ulisali na kujifunza kwa bidii zaidi na kutafakari mara nyingi zaidi. Je, ulikuwa na bidii zaidi katika huduma na ulihudhuria mikutano kwa ukawaida kuliko sasa?—2 Kor. 13:5.

12 Huenda usitambue mabadiliko hayo, lakini ikiwa unayatambua, yalisababishwa na nini? Je, mahangaiko yanayofaa, kama vile kuiandalia familia yako vya kutosha, kutunza afya yako, au mambo mengine kama hayo yamefanya ufikiri kwamba siku ya Yehova iko mbali sana? Yesu aliwaambia mitume wake hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego. Kwa maana itakuja juu ya wale wote wanaokaa juu ya uso wa dunia yote. Basi, endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia.”—Luka 21:34-36.

13. Yakobo alilinganisha Neno la Mungu na nini?

13 Mwandikaji wa Biblia, Yakobo, ambaye aliongozwa na roho ya Mungu, aliwahimiza waamini wenzake wajichunguze kwa unyoofu kwa kutumia Neno la Mungu. Yakobo aliandika hivi: “Iweni watendaji wa neno, na si wasikiaji tu, mkijidanganya wenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli. Kwa maana ikiwa yeyote ni msikiaji wa neno, na si mtendaji, huyo ni kama mtu anayeutazama uso wake wa asili katika kioo. Kwa maana yeye hujitazama, naye huenda zake na kusahau mara moja yeye ni mtu wa namna gani. Lakini yeye anayechunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo, mtu huyo, kwa sababu amekuwa, si msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.”—Yak. 1:22-25.

14, 15. (a) Biblia inaweza kukusaidia kwa njia gani kuboresha hali yako ya kiroho? (b) Unaweza kutafakari kuhusu maswali gani?

14 Mtu anaweza kutumia kioo kuhakikisha kwamba yuko safi. Kwa mfano, mwanamume akiona kwamba tai yake iko kombo, anaweza kuinyoosha. Mwanamke akiona kwamba nywele zake ziko ovyoovyo, anaweza kuzitengeneza. Vivyo hivyo, Maandiko yanatusaidia kujichunguza. Tunapojichunguza kwa kutegemea mambo yanayosemwa katika Biblia, basi tunaitumia kama kioo. Lakini kuna haja gani ya kujitazama kwenye kioo ikiwa haturekebishi kasoro tunayoiona? Tunaonyesha kwamba tuna hekima tunapotenda kupatana na mambo tunayoona katika “sheria kamilifu” ya Mungu, na hivyo kuwa “watendaji” wa neno. Hivyo, yeyote anayetambua kwamba upendo wake wa kwanza kuelekea Yehova na ile kweli umepoa, anapaswa kujiuliza hivi: ‘Ni matatizo gani ninayokabili maishani, nami ninayashughulikia kwa njia gani? Nilikuwa nikiyashughulikia kwa njia gani zamani? Je, kuna mabadiliko yoyote?’ Ukigundua kasoro zozote baada ya kujichunguza, usizipuuze. Ikiwa unahitaji kufanya marekebisho, yafanye bila kukawia.—Ebr. 12:12, 13.

15 Kutafakari kunaweza kukusaidia pia kujiwekea miradi yenye usawaziko ili ufanye maendeleo ya kiroho. Mtume Paulo alimpa mfanyakazi mwenzake Timotheo shauri lililoongozwa na roho ili aboreshe huduma yake. Paulo alimhimiza hivi kijana huyo: “Tafakari mambo haya; zama katika hayo, ili maendeleo yako yawe wazi kwa watu wote.” Kwa kutumia Neno la Mungu, sisi pia tunapaswa kutafakari kuhusu maendeleo tunayoweza kufanya.—1 Tim. 4:15.

16. Unahitaji kuwa macho kuhusu hatari gani unapojichunguza kwa kutegemea Maandiko?

16 Unapojichunguza kwa unyoofu utagundua udhaifu fulani. Huenda hilo likakuvunja moyo, lakini usiruhusu hilo litukie. Kusudi la kujichunguza ni kukuwezesha kutambua marekebisho unayohitaji kufanya. Bila shaka, Shetani angependa Mkristo ajione kwamba hafai kwa sababu ya kutokamilika kwake. Kwa hakika, tayari dai limetolewa kwamba Mungu anadharau jitihada zozote zile za kumtumikia. (Ayu. 15:15, 16; 22:3) Huo ni uwongo ambao Yesu aliupinga vikali; Mungu anamwona kila mmoja wetu kuwa mwenye thamani. (Soma Mathayo 10:29-31.) Kutambua kwamba wewe si mkamilifu kunapaswa kukuchochea uazimie kufanya marekebisho kwa unyenyekevu, kwa msaada wa Yehova. (2 Kor. 12:7-10) Ikiwa ugonjwa au uzee unakuzuia usitimize mengi, basi jiwekee miradi unayoweza kutimiza, lakini usikate tamaa wala kuacha upendo wako upoe.

Kuna Mambo Mengi ya Kuthamini

17, 18. Ni faida gani zinazotokana na kujenga juu ya upendo uliokuwa nao mwanzoni?

17 Kuna faida nyingi za kuendelea kujenga juu ya msingi wa upendo uliokuwa nao mwanzoni. Unaweza kuongeza ujuzi wako kumhusu Mungu na uthamini wako kwa mwongozo wake wenye upendo. (Soma Methali 2:1-9; 3:5, 6.) “Katika kuyashika [maamuzi ya hukumu ya Yehova] kuna thawabu kubwa,” alisema mtunga-zaburi. “Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, humfanya asiye na uzoefu awe na hekima.” Zaidi ya hayo, “wenye furaha ni wale wasio na kosa katika njia yao, wale wanaotembea katika sheria ya Yehova.”—Zab. 19:7, 11; 119:1.

18 Bila shaka, utakubali kwamba una mambo mengi mazuri ya kuthamini. Unajua kwa nini mambo mbalimbali yanatukia ulimwenguni. Unafaidika kutokana na utunzaji wa kiroho na maandalizi ambayo Mungu anawapa watu wake leo. Na hakuna shaka kwamba unafurahi kwa kuwa Yehova amekuvuta kwenye kutaniko lake la ulimwenguni pote na kukupa pendeleo la kuwa mmoja wa Mashahidi wake. Thamini baraka ulizo nazo! Ikiwa ungeziandika zote, inaelekea kwamba ungeandika orodha ndefu sana. Kufanya hivyo mara nyingi sana kutakusaidia kutii himizo hili: “Endelea kushika sana kile ulicho nacho.”—Ufu. 3:11.

19. Zaidi ya kutafakari kuhusu uhusiano wako pamoja na Mungu, ni mambo gani mengine ya maana yatakayokusaidia kudumisha hali nzuri ya kiroho?

19 Kutafakari jinsi ambavyo imani yako imekua kadiri ambavyo wakati umepita ni hatua moja tu inayoweza kukusaidia kushika sana kile ulicho nacho. Gazeti hili limerudia mara nyingi mambo mengine ya maana yanayohitajiwa ili kudumisha hali nzuri ya kiroho. Mambo hayo yanatia ndani sala, kuhudhuria na kushiriki katika mikutano ya Kikristo, na kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri. Mambo hayo yanaweza kukusaidia kuendelea kuamsha, kuchochea, na kujenga juu ya upendo uliokuwa nao mwanzoni.—Efe. 5:10; 1 Pet. 3:15; Yuda 20, 21.

Ungetoa Jibu Gani?

• Sababu zilizokufanya umpende Yehova zinaweza kukutia moyo sasa kwa njia gani?

• Kutafakari kuhusu mambo uliyojionea kadiri ambavyo miaka imepita kunaweza kukusadikisha kuhusu nini?

• Kwa nini unapaswa kuchunguza upendo wako kuelekea Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ni jambo gani ambalo lilikusadikisha na kukuvutia katika kweli?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Je, unaona mambo fulani unayohitaji kurekebisha?