Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uko Tayari Kuitetea Imani Yako?

Je, Uko Tayari Kuitetea Imani Yako?

Je, Uko Tayari Kuitetea Imani Yako?

JE, UMEWAHI kuwa katika hali iliyokulazimisha kuitetea imani yako? Fikiria yale yaliyompata Susana, dada mwenye umri wa miaka 16 huko Paraguay. Alipokuwa darasani, mwanafunzi fulani alisema kwamba Mashahidi wa Yehova hawakubali “Agano la Kale,” Yesu Kristo, au Maria. Pia, wanafunzi walidai kwamba Mashahidi wanashikilia sana imani yao na kwamba wako tayari kufa badala ya kukubali matibabu. Ungefanya nini ikiwa ungekuwa katika hali hiyo?

Susana alisali kwa Yehova, kisha akainua mkono. Mwishoni mwa somo hilo, alimwomba mwalimu ruhusa ya kueleza kuhusu imani yake akiwa Shahidi wa Yehova. Mwalimu akakubali. Kwa majuma mawili yaliyofuata, Susana alitayarisha habari yake, huku akitumia broshua yenye kichwa Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini?

Siku ilipofika, Susana alieleza kwa nini tunaitwa Mashahidi wa Yehova. Pia, alieleza tumaini letu la wakati ujao na kwa nini tunakataa kutiwa damu mishipani. Kisha, akawaomba wanafunzi kuuliza maswali. Wanafunzi wengi waliinua mikono ili kuuliza maswali. Mwalimu alishangazwa na jinsi ambavyo msichana huyo alijibu maswali hayo kwa kutumia Maandiko.

Mwanafunzi mmoja alieleza hivi: “Wakati mmoja nilikuwa katika Jumba la Ufalme na sikuona hata sanamu moja.” Mwalimu alitaka kujua kwa nini. Susana alisoma Zaburi 115:4-8 na Kutoka 20:4. Mwalimu alishangaa na kusema hivi: “Basi, kwa nini makanisa yetu yana sanamu nyingi sana ingawa Biblia inashutumu matumizi ya sanamu?”

Mazungumzo ya maswali na majibu yaliendelea kwa dakika 40. Susana alipowauliza wanafunzi ikiwa wangependa kuona video No Blood—Medicine Meets the Challenge (au Pas de sang: la médecine relève le défi), wote walijibu ndiyo. Kwa hiyo, mwalimu akapanga mazungumzo mengine siku iliyofuata. Baada ya wote kutazama video hiyo, Susana alieleza kuhusu matibabu mengine yasiyohusisha damu ambayo Mashahidi wa Yehova wanakubali. Kuhusu hilo, mwalimu akasema: “Sikujua kwamba kuna matibabu mengine mengi hivyo; wala sikujua faida za kutibiwa bila damu. Je, matibabu hayo ni kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova tu?” Aliposikia kwamba matibabu hayo si kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova tu, mwalimu alisema hivi: “Mashahidi wa Yehova watakaponitembelea, nitazungumza nao.”

Susana alikuwa amejitayarisha kwa ajili ya mazungumzo ya dakika 20, lakini yalichukua muda wa saa tatu. Juma moja baadaye, wanafunzi wengine walieleza kuhusu imani yao. Baada ya kueleza kuhusu imani yao, waliulizwa maswali mengi, lakini hawangeweza kuitetea. Mwalimu aliwauliza: “Kwa nini hamwezi kuitetea imani yenu kama alivyofanya mwanafunzi mwenzenu ambaye ni Shahidi wa Yehova?”

Walijibu hivi: “Wanajifunza Biblia kwelikweli. Sisi hatufanyi hivyo.”

Mwalimu akamwambia hivi Susana: “Unajifunza Biblia kwelikweli na unajitahidi kufanya yale inayosema. Unastahili pongezi.”

Ikiwa Susana angetaka, angenyamaza. Hata hivyo, kwa kuwaeleza wengine kuhusu imani yake, Susana alifuata mfano mzuri wa msichana mdogo Mwisraeli ambaye jina lake halitajwi aliyechukuliwa mateka na Wasiria. Msichana huyo aliishi katika nyumba ya Naamani, jemadari Msiria, ambaye alikuwa na ugonjwa wa ukoma. Msichana huyo Mwisraeli alimwambia bimkubwa wake hivi: “Laiti bwana wangu angekuwa mbele ya nabii aliye katika Samaria! Hapo ndipo angemponya ukoma wake.” Msichana huyo hangejizuia kutoa ushahidi kuhusu Mungu wa kweli. Matokeo yalikuwa kwamba bwana wake, Naamani, alikuja kuwa mwabudu wa Yehova.—2 Fal. 5:3, 17.

Vivyo hivyo, Susana hangejizuia kutoa ushahidi kuhusu Yehova na watu wake. Kwa kuchukua hatua ya kuitetea imani yake alipoulizwa kuhusu yale anayoamini, Susana alitii amri hii ya Kimaandiko: “Mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu, sikuzote mkiwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hutaka kutoka kwenu sababu ya tumaini lililo ndani yenu, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.” (1 Pet. 3:15) Je, uko tayari kuitetea imani yako nafasi inapotokea?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Vifaa hivi vinaweza kukusaidia kuitetea imani yako