Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Yesu Alikuwa Akizungumza Kuhusu Moto wa Mateso?

Je, Yesu Alikuwa Akizungumza Kuhusu Moto wa Mateso?

Je, Yesu Alikuwa Akizungumza Kuhusu Moto wa Mateso?

WATU fulani ambao wanaamini fundisho la moto wa mateso wanataja maneno ya Yesu kwenye Marko 9:48 (au mistari 44, 46). Alitaja wadudu (au funza) ambao hawafi na moto ambao hauzimwi. Ikiwa mtu fulani angekuuliza maana ya maneno hayo, ungemwambia nini?

Ikitegemea tafsiri ya Biblia anayotumia, mtu huyo anaweza kusoma mstari wa 44, 46, au 48 kwa sababu tafsiri fulani za Biblia zinatumia maneno yaleyale katika mistari hiyo. * Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inasema hivi: “Ikiwa jicho lako linakufanya ukwazike, litupe mbali; ni afadhali uingie katika ufalme wa Mungu ukiwa na jicho moja kuliko kutupwa katika Gehena ukiwa na macho mawili, mahali ambapo funza wake hafi na ule moto hauzimwi.”—Marko 9:47, 48.

Vyovyote vile, wengine wanadai kwamba maneno ya Yesu yanaunga mkono maoni ya kwamba baada ya kifo nafsi za waovu zinateswa milele. Kwa mfano, maelezo fulani kuhusu tafsiri ya Biblia ya Kihispania Sagrada Biblia ya Chuo Kikuu cha Navarre yanasema hivi: “Bwana wetu anatumia [maneno hayo] kurejelea moto wa mateso. Mara nyingi imesemekana kwamba ‘funza wasiokufa’ wanamaanisha huzuni ya kudumu ya wale walio katika moto wa milele; na ‘moto usiozimika’ unamaanisha maumivu yao ya kimwili.”

Hata hivyo, linganisha maneno ya Yesu na mstari wa mwisho wa unabii wa Isaya. * Je, si wazi kwamba Yesu alikuwa akirejelea mstari huo katika Isaya sura ya 66? Inaelekea nabii huyo anazungumza kuhusu kwenda nje ya “Yerusalemu mpaka kandokando ya Bonde la Hinomu (Gehena), ambako wakati fulani dhabihu za wanadamu zilitolewa (Yer. 7:31) na mwishowe likawa sehemu ya kutupia takataka za jiji hilo.” (The Jerome Biblical Commentary) Lugha ya mfano inayotumiwa kwenye Isaya 66:24 haionyeshi kamwe kwamba watu wanateswa katika moto; andiko hilo linazungumza kuhusu mizoga. Katika andiko hilo, funza ndio wanaosemwa kuwa hawafi, bali si wanadamu walio hai au nafsi zisizoweza kufa. Hivyo basi, Yesu alimaanisha nini?

Ona maelezo kuhusu Marko 9:48 katika Buku la 2 la kichapo kimoja cha Kikatoliki (El evangelio de Marcos. Análisis lingüístico y comentario exegético): “Maneno hayo yanatoka katika Isaya (66,24). Hapo nabii anataja mambo mawili kuonyesha jinsi miili ya watu waliokufa ilivyoharibika: ilioza na kuteketezwa . . . Kutaja funza pamoja na moto katika maandishi hayo kunakazia wazo la uharibifu. . . . Nguvu hizo mbili za kuharibu zinaelezwa kuwa za kudumu (‘hazizimwi, hazifi’): hakuna njia yoyote ya kuziepuka. Katika maana hii ya mfano, ni funza na moto tu ndivyo haviharibiwi, bali si watu, na vinaharibu kabisa kila kitu kilicho katika uwezo wake. Kwa hiyo, huo si ufafanuzi wa mateso ya milele, lakini wa uharibifu wa milele. Wale wanaopata uharibifu huo hawafufuliwi kamwe, kifo chao ni cha milele. Hivyo basi, moto unafananisha kuharibiwa kabisa.”

Mtu yeyote anayejua kwamba Mungu wa kweli ni mwenye upendo na mwenye haki anapaswa kuona kwamba ni jambo linalopatana na akili kuyaelewa maneno ya Yesu katika njia hiyo. Hakuwa akisema kwamba waovu watateswa milele. Badala yake, wanakabili hatari ya kuharibiwa kabisa bila tumaini la ufufuo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Hati za Biblia zinazotegemeka zaidi hazina mistari ya 44 na 46. Wasomi wanasema kwamba huenda mistari hiyo miwili iliongezwa baadaye. Profesa Archibald T. Robertson anaandika hivi: “Mistari hiyo miwili haipatikani katika hati bora zaidi na za kale zaidi. Ilitokana na vikundi vya hati za Magharibi na Siria (Bizantiamu). Mistari hiyo inarudia tu mstari wa 48. Kwa hiyo, tunaondoa mistari ya 44 na 46 ambayo si sahihi.”

^ fu. 5 “Kwa kweli wataenda na kuitazama mizoga ya wale watu waliokuwa wakinikosea; kwa maana funza walio juu yao hawatakufa na moto wao hautazimwa, nao watakuwa chukizo kwa wanadamu wote.”—Isa. 66:24.