Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Barua kwa Waroma

Mambo Makuu Katika Barua kwa Waroma

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Barua kwa Waroma

AKIWA katika safari yake ya tatu ya umishonari mwaka wa 56 hivi W.K., mtume Paulo anafika katika jiji la Korintho. Amepata habari kwamba Wakristo Wayahudi na wasio Wayahudi huko Roma wana maoni yanayotofautiana. Akitamani kuwaunganisha kabisa katika Kristo, Paulo anachukua hatua ya kuwaandikia barua.

Katika barua hiyo kwa Waroma, Paulo anaeleza jinsi wanadamu wanavyotangazwa kuwa waadilifu na jinsi wanavyopaswa kujiendesha maishani. Barua hiyo inaongeza ujuzi wetu kumhusu Mungu na Neno lake, inakazia fadhili zisizostahiliwa za Mungu, nayo inaonyesha jinsi Kristo alivyo na daraka la maana sana kuhusiana na wokovu wetu.—Ebr. 4:12.

WANATANGAZWA KUWA WAADILIFU—JINSI GANI?

(Rom. 1:1–11:36)

Paulo anaandika hivi: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu, nayo ni zawadi ya bure kwamba wanatangazwa [na Mungu] kuwa waadilifu kwa fadhili zake zisizostahiliwa kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa.” Pia, Paulo anasema hivi: “Mtu hutangazwa kuwa mwadilifu kwa imani bila matendo ya sheria.” (Rom. 3:23, 24, 28) Kupitia imani katika “tendo moja la kutetewa kuwa haki,” Wakristo watiwa-mafuta na washiriki wa “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” wanaweza ‘kutangazwa kuwa waadilifu,’ yaani, watiwa-mafuta kwa ajili ya uzima wa mbinguni wakiwa warithi pamoja na Kristo huku washiriki wa umati mkubwa wakiwa marafiki wa Mungu, wakitarajia kuokoka “ile dhiki kuu.”—Rom. 5:18; Ufu. 7:9, 14; Yoh. 10:16; Yak. 2:21-24; Mt. 25:46.

Paulo anauliza hivi: “Je, tufanye dhambi kwa sababu hatuko chini ya sheria bali chini ya fadhili zisizostahiliwa?” Anajibu hivi: “Hilo lisitendeke kamwe!” Paulo anaeleza hivi: “Ninyi ni watumwa . . . , ama watumwa wa dhambi kwa kutazamia kifo ama wa utii kwa kutazamia uadilifu.” (Rom. 6:15, 16) “Mkiyaua mazoea ya mwili kwa roho, mtaishi,” anasema.—Rom. 8:13.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:24-32—Je, mwenendo mpotovu kiadili ambao unaelezwa hapa unawahusu Wayahudi au watu wasio Wayahudi? Ingawa ufafanuzi huo ungeweza kufaa vikundi vyote viwili, Paulo alikuwa hasa akizungumza kuhusu Waisraeli wa zamani waasi-imani. Hata ingawa walijua amri ya uadilifu ya Mungu, “hawakukubali kumjua Mungu katika ujuzi sahihi.” Hivyo, walipaswa kulaumiwa.

3:24, 25—“Fidia ambayo Kristo Yesu alilipa” ingefunika jinsi gani “dhambi zilizotokea wakati uliopita” kabla ya fidia kulipwa? Unabii wa kwanza wa Kimasihi ulioandikwa katika Mwanzo 3:15, ulitimia mwaka wa 33 W.K., Yesu alipouawa kwenye mti wa mateso. (Gal. 3:13, 16) Hata hivyo, Yehova alipotoa unabii huo, kwa maoni yake ni kana kwamba bei ya fidia ilikuwa tayari imelipwa, kwa kuwa hakuna kitu kinachoweza kumzuia Mungu asitimize makusudi yake. Hivyo, kwa msingi wa dhabihu ambayo Yesu Kristo angetoa wakati ujao, Yehova angesamehe dhambi za wazao wa Adamu ambao walionyesha kwamba wana imani katika ahadi hiyo. Pia, fidia itawawezesha wale ambao walikufa kabla ya nyakati za Ukristo kufufuliwa.—Mdo. 24:15.

6:3-5—Inamaanisha nini kubatizwa katika Kristo Yesu na kubatizwa katika kifo chake? Yehova anapowatia mafuta kwa roho takatifu wafuasi wa Kristo, wanaunganishwa na Yesu na wanakuwa washiriki wa kutaniko ambalo ni mwili wa Kristo, yeye akiwa Kichwa. (1 Kor. 12:12, 13, 27; Kol. 1:18) Hiyo ndiyo maana ya kubatizwa katika Kristo Yesu. Pia, Wakristo watiwa-mafuta ‘wanabatizwa katika kifo cha Kristo’ katika maana ya kwamba wanaishi maisha ya kujidhabihu na wanaachana na tumaini lolote la kuishi milele duniani. Kwa hiyo, kifo chao, ni cha kidhabihu, kama ilivyokuwa na kifo cha Yesu. Hata hivyo, kifo chao hakina thamani ya fidia. Ubatizo wao katika kifo cha Kristo unakamilishwa wanapokufa na kufufuliwa kwenye uzima wa mbinguni.

7:8-11—‘Dhambi ilichochewa na amri’ jinsi gani? Sheria iliwasaidia watu kuelewa kwa ukamili kile ambacho dhambi ilimaanisha, na hivyo ikawafanya watambue zaidi hali yao ya kuwa watenda-dhambi. Kwa sababu hiyo, watu wengi walitambua au kuthibitishwa waziwazi kuwa watenda-dhambi. Hivyo, inaweza kusemwa kwamba dhambi ilichochewa na Sheria.

Mambo Tunayojifunza:

1:14, 15. Tuna sababu nyingi za kutangaza habari njema kwa bidii. Sababu moja ni kwamba tuna wajibu kuelekea watu ambao walinunuliwa kwa damu ya Yesu na tuna wajibu wa kuwasaidia kiroho.

1:18-20. Watu wasiomwogopa Mungu na ambao si waadilifu “hawana sababu ya kujitetea,” kwa kuwa sifa zisizoonekana za Mungu zinaonekana wazi katika uumbaji.

2:28; 3:1, 2; 7:6, 7Baada ya kusema mambo ambayo huenda yakaonekana kuwa ya kuwadharau Wayahudi, Paulo sasa anatumia maneno yenye kutuliza. Anatuwekea kielelezo kuhusu jinsi ya kushughulikia kwa busara na kwa akili habari zenye kutatanisha.

3:4. Maneno ya wanadamu yanapotofautiana na yale ambayo Mungu anasema katika Neno lake, tunaacha ‘Mungu aonekane kuwa wa kweli’ kwa kuamini ujumbe wa Biblia na kutenda kulingana na mapenzi ya Mungu. Kwa kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi, tunaweza kuwasaidia wengine wamwone Mungu kuwa wa kweli.

4:9-12. Imani ya Abrahamu ilimfanya ahesabiwe kuwa mwadilifu hata kabla hajatahiriwa akiwa na umri wa miaka 99. (Mwa. 12:4; 15:6; 16:3; 17:1, 9, 10) Katika njia hiyo nzuri sana, Mungu alionyesha kile kinachomwezesha mtu kuwa na msimamo wa uadilifu mbele zake.

4:18. Tumaini ni sehemu ya maana sana ya imani. Imani yetu inategemea tumaini.—Ebr. 11:1.

5:18, 19. Paulo anaeleza kwa njia yenye kusadikisha jinsi Yesu anavyolingana na Adamu. Anaeleza kwa njia rahisi jinsi mtu mmoja anavyoweza “kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” (Mt. 20:28) Kufundisha kwa njia rahisi na kwa njia yenye kusadikisha ni njia bora za kufundisha tunazopaswa kuiga.—1 Kor. 4:17.

7:23. Viungo vya mwili kama vile mikono, miguu, na ulimi vinaweza ‘kutuchukua mateka kwa sheria ya dhambi,’ hivyo tunapaswa kujihadhari ili tusivitumie vibaya.

8:26, 27. Tunapokabili hali zenye kutatanisha hivi kwamba hatujui mambo ya kusema tunaposali, “roho yenyewe hutuombea.” Basi Yehova, yule “Msikiaji wa sala,” anakubali sala ambazo zimeandikwa katika Neno lake zinazopatana na hali yetu, naye anaona ni kama zimetoka kwetu.—Zab. 65:2.

8:38, 39. Misiba, roho waovu, na serikali za wanadamu haziwezi kumfanya Yehova aache kutupenda, wala hatupaswi kuruhusu zitufanye tuache kumpenda.

9:22-28; 11:1, 5, 17-26. Unabii mbalimbali kuhusu kurudishwa kwa Waisraeli unatimizwa na kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta, ambalo washiriki wake ‘wanaitwa si kutoka kati ya Wayahudi peke yao bali pia kutoka kati ya mataifa.’

10:10, 13, 14. Zaidi ya kumpenda Mungu na wanadamu wenzetu, imani yenye nguvu katika Yehova na ahadi zake inaweza kutuchochea tushiriki kwa bidii katika huduma ya Kikristo.

11:16-24, 33. “Fadhili na ukali wa Mungu” zimesawazika kwa njia nzuri kama nini! Ndiyo, ‘yeye ni Mwamba, kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki.’—Kum. 32:4.

KUONYESHA MAISHANI KWAMBA TUMETANGAZWA KUWA WAADILIFU

(Rom. 12:1–16:27)

Paulo anasema hivi: “Kwa sababu hiyo nawasihi ninyi kwa huruma za Mungu, akina ndugu, mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu.” (Rom. 12:1) “Kwa sababu hiyo,” au kwa kuwa Wakristo wanatangazwa kuwa waadilifu kwa sababu ya imani yao, yale ambayo Paulo anasema sasa yanapaswa kubadili mtazamo wao kujielekea, kuelekea wengine, na kuelekea mamlaka za serikali.

Paulo anaandika hivi: “Namwambia kila mtu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.” Kisha anatoa himizo hili: “Upendo wenu na uwe bila unafiki.” (Rom. 12:3, 9) “Kila nafsi na ijitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa.” (Rom. 13:1) Kuhusu mambo ya dhamiri, Paulo anawatia moyo Wakristo ‘wasiwe wakihukumiana.’—Rom. 14:13.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

12:20—Tunakusanya “makaa yenye moto” juu ya kichwa cha adui jinsi gani? Katika nyakati za Biblia, mawe yenye chuma yalitiwa katika tanuru ya moto na makaa ya moto yakawekwa juu na chini ya mawe hayo. Kuongeza joto juu ya mawe hayo kulisaidia kuyeyusha vyuma na kuvitenganisha na uchafu uliokuwa ndani yake. Vivyo hivyo, tunaweka makaa ya moto juu ya kichwa cha adui tunapomtendea kwa fadhili, na hivyo kuyeyusha ugumu wake na kumfanya aonyeshe sifa nzuri.

12:21—‘Tunaendelea kuushinda uovu kwa wema’ jinsi gani? Njia moja ya kuushinda uovu kwa wema ni kuendelea kufanya bila woga kazi ambayo tumepewa na Mungu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme mpaka Yehova aridhike.—Marko 13:10.

13:1—Ni katika njia gani mamlaka zilizo kubwa “zimesimamishwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri”? Mamlaka za serikali “zimesimamishwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri” katika maana ya kwamba Mungu anaziruhusu zitawale, na utawala wa serikali fulani ulitabiriwa na Mungu. Hilo linaonyeshwa wazi na yale ambayo Biblia ilitabiri kuhusu watawala fulani.

Mambo Tunayojifunza:

12:17, 19. Kujilipizia kisasi ni kujichukulia daraka ambalo ni la Yehova peke yake. Tungetenda kwa kimbelembele kama nini ikiwa ‘tungemlipa yeyote uovu kwa uovu’!

14:14, 15. Hatupaswi kumhuzunisha au kumkwaza ndugu yetu kwa chakula au kinywaji ambacho tunampa.

14:17. Kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu hakutegemei hasa kile tunachokula au kunywa wala kile tusichokula au kunywa. Badala yake, kunategemea uadilifu, amani, na shangwe.

15:7. Tunapaswa kuwakaribisha bila ubaguzi katika kutaniko watu wote ambao wanatafuta kweli kwa unyoofu na tunapaswa kuwatangazia ujumbe wa Ufalme watu wote tunaokutana nao.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Je, fidia inaweza kuondoa dhambi ambazo zilifanywa kabla ya fidia kulipwa?