Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Mtume Paulo alisema kwamba Israeli wote wangeokolewa.’ (Rom. 11:26) Je, alimaanisha kwamba Wayahudi wote wangegeuka na kuwa Wakristo?

Hapana, Paulo hakumaanisha hivyo. Wakiwa taifa, wazao wa asili wa Abrahamu walimkataa Yesu akiwa Masihi. Na miaka mingi baada ya kifo cha Yesu, ilikuwa wazi kwamba Wayahudi wote hawangegeuka na kuwa Wakristo. Hata hivyo, maneno ya Paulo kwamba ‘Israeli wote wangeokolewa’ yalikuwa ya kweli. Katika njia gani?

Yesu aliwaambia hivi viongozi wa dini ya Kiyahudi wa siku zake: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” (Mt. 21:43) Kwa sababu taifa la Israeli kwa ujumla lilimkataa Yesu, Yehova aligeuza uangalifu wake kuelekea taifa jipya, taifa la kiroho. Paulo aliliita taifa hilo “Israeli wa Mungu.”—Gal. 6:16.

Mistari mingine katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo inathibitisha kwamba washiriki wa “Israeli wa Mungu” ni Wakristo 144,000 waliotiwa mafuta kwa roho. (Rom. 8:15-17; Ufu. 7:4) Andiko la Ufunuo 5:9, 10, linathibitisha kwamba kikundi hicho kingetia ndani watu wasio Wayahudi kwa kuwa linasema kwamba Wakristo watiwa-mafuta ‘wanatoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa.’ Washiriki wa Israeli la kiroho walichaguliwa hasa ili kuwa “ufalme na makuhani . . . , nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” Ingawa Yehova aliwakataa Waisraeli kuwa taifa lililochaguliwa, watu mmoja-mmoja wangepatanishwa naye. Watu hao walitia ndani mitume na Wakristo wengine wengi wa mapema. Bila shaka, Wayahudi hao, kama wanadamu wengine wote, walipaswa kununuliwa kwa damu ya Yesu Kristo.—1 Tim. 2:5, 6; Ebr. 2:9; 1 Pet. 1:17-19.

Uhakika wa kwamba Wayahudi wengi wa asili katika karne ya kwanza walipoteza nafasi ya kutawala pamoja na Yesu haukuzuia kusudi la Mungu lisitimie. Kusudi hilo halingeweza kuzuiwa, kwa kuwa Yehova alisema hivi kupitia nabii wake: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isa. 55:11.

Hivyo, kusudi la Mungu la kuwaweka wale 144,000 watawale pamoja na Mwana wake mbinguni halingekosa kutimia. Biblia inaonyesha wazi kwamba Mungu angetia mafuta idadi kamili ya watu 144,000. Hakuna mmoja wao angekosekana!—Ufu. 14:1-5.

Hivyo, Paulo alipoandika kwamba ‘Israeli wote wangeokolewa,’ hakuwa akitabiri kwamba Wayahudi wote wangegeuzwa na kuwa Wakristo. Badala yake, alimaanisha kwamba kusudi la Mungu la kuwa na Waisraeli wa kiroho 144,000 ambao wangetawala pamoja na Mwana Wake, Yesu Kristo, huko mbinguni lingetimia. Kwa wakati uliowekwa na Mungu, idadi kamili ya “Israeli wote,” ingeokolewa, na mwishowe wangetawala wakiwa wafalme na makuhani katika Ufalme wa Kimasihi.—Efe. 2:8.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Watiwa-mafuta ‘wanatoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa’