Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwenye Nguvu Ingawa Dhaifu

Mwenye Nguvu Ingawa Dhaifu

Mwenye Nguvu Ingawa Dhaifu

UDHAIFU wako unaweza kukulemea. Unashikamana nawe kama kupe. Huenda ukafikiri kwamba hutaweza kamwe kushinda udhaifu huo, au unaweza kuhisi kwamba hufai unapojilinganisha na wengine na kuona kwamba wao ni bora zaidi. Kwa upande mwingine, huenda unakabiliana na ugonjwa wenye kudhoofisha unaokufanya usiwe na furaha maishani. Kwa vyovyote vile, inaonekana kwamba umenaswa. Unaweza kuhisi kama Ayubu, aliyemwambia Mungu hivi: “Laiti ungenificha katika Kaburi, kwamba ungenificha mpaka hasira yako igeuke, kwamba ungeniwekea kikomo cha wakati na kunikumbuka!”—Ayubu 14:13.

Unaweza kushinda jinsi gani hisia hizo za kukata tamaa? Ingawa inaweza kuwa vigumu sana, unahitaji kuepuka kufikiria matatizo yako kila mara. Kwa mfano, unaweza kufikiria maswali ambayo Yehova alimuuliza mtumishi wake mwaminifu Ayubu: “Ulikuwa wapi nilipoweka msingi wa dunia? Niambie, ikiwa unaelewa. Ni nani aliyeweka vipimo vyake, ikiwa unajua, au ni nani aliyenyoosha juu yake kamba ya kupimia?” (Ayubu 38:4, 5) Tukifikiria maana ya maswali hayo, inaelekea tutachochewa kutambua hekima na nguvu za Yehova zisizo na kifani. Ana sababu nzuri za kuruhusu ulimwengu wa sasa uendelee.

“Mwiba Katika Mwili”

Mtumishi mwingine mwaminifu alimwomba Yehova amwondolee “mwiba katika mwili,” yaani, tatizo fulani lenye kudumu. Mtume Paulo alimsihi Mungu mara tatu amwondolee jaribu hilo. Hata iwe alikuwa na tatizo gani ambalo lilimsumbua kama mwiba, lingemfanya Paulo apoteze shangwe yake ya kumtumikia Yehova. Paulo alilinganisha tatizo hilo na kupigwa makofi daima. Yehova alimjibu hivi: “Fadhili zangu zisizostahiliwa zinakutosha wewe; kwa maana nguvu zangu zinakamilishwa katika udhaifu.” Yehova hakuondoa mwiba huo katika mwili. Paulo alipaswa kujitahidi kuishi nao, lakini aliongeza hivi: “Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa mwenye nguvu.” (2 Kor. 12:7-10) Alimaanisha nini?

Tatizo la Paulo halikutoweka kimuujiza. Hata hivyo, halikumzuia asitimize mambo makubwa katika utumishi wa Yehova. Paulo alimtegemea Yehova na sikuzote alimwomba msaada. (Flp. 4:6, 7) Mwishoni mwa maisha yake, Paulo alisema hivi: “Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani.”—2 Tim. 4:7.

Yehova anawatumia wanadamu wasio wakamilifu kutimiza mapenzi yake ingawa wana udhaifu na matatizo, na hivyo sifa zinastahili kumwendea. Anaweza kuwapa mwongozo na hekima ili kushughulikia matatizo yao na kudumisha shangwe yao katika utumishi wake. Ndiyo, anaweza kuwatumia wanadamu wasio wakamilifu kufanya mambo makubwa ingawa wana udhaifu.

Paulo alionyesha kwa nini Mungu hakuondoa mwiba huo katika mwili wake aliposema hivi: “Ili nisijione kuwa nimeinuliwa mno.” (2 Kor. 12:7) “Mwiba” wa Paulo ulimkumbusha udhaifu wake na ulimsaidia kuendelea kuwa mnyenyekevu. Hilo linapatana na yale ambayo Yesu alifundisha: “Yeyote yule anayejiinua atanyenyekezwa, na yeyote yule anayejinyenyekeza atainuliwa.” (Mt. 23:12) Majaribu yanaweza kuwafundisha watumishi wa Mungu unyenyekevu na kuwasaidia kutambua kwamba ili wavumilie kwa uaminifu wanahitaji kumtegemea Yehova. Hivyo, kama mtume huyo, wanaweza ‘kujisifu katika Yehova.’—1 Kor. 1:31.

Udhaifu Usioonekana

Huenda watu fulani wasitambue kwamba wana udhaifu au huenda hata hawataki kukubali kwamba wana udhaifu. Kwa mfano, huenda mtu akajitumaini sana na kutegemea mali yake. (1 Kor. 10:12) Udhaifu mwingine wa kawaida kwa wanadamu wasio wakamilifu ni tamaa ya kupata umaarufu.

Yoabu, ambaye alikuja kuwa jemadari wa jeshi la Mfalme Daudi, alikuwa hodari, asiyeogopa, na mwenye uwezo wa kusuluhisha matatizo. Hata hivyo, Yoabu alikuwa na hatia ya kosa zito sana ambalo lilionyesha roho ya kimbelembele na kiburi. Aliwaua kikatili majemadari wawili wa jeshi. Kwanza, alilipiza kisasi kwa kumuua Abneri. Baadaye, Yoabu alijifanya kuwa anamsalimu binamu yake Amasa, akashika ndevu za Amasa kwa mkono wake wa kuume ili ambusu, kisha akamuua kwa kumchoma upanga kwa mkono wake wa kushoto. (2 Sam. 17:25; 20:8-10) Kwa kuwa Amasa alikuwa amewekwa kuwa jemadari wa jeshi badala ya Yoabu, Yoabu alitumia nafasi hiyo kumuua mpinzani wake, labda akifikiri kwamba angepata tena cheo cha kuwa jemadari. Unaweza kuona kwamba Yoabu hakuzuia mwelekeo wake pamoja na tamaa yake ya kichoyo ya kupata umaarufu. Alitenda kwa ukatili bila kuonyesha majuto yoyote. Mfalme Daudi alipokaribia mwisho wa maisha yake, alimwagiza mwana wake Sulemani ahakikishe kuwa Yoabu ameadhibiwa kwa sababu ya uovu wake.—1 Fal. 2:5, 6, 29-35.

Bila shaka, tunapaswa kujitahidi kushinda tamaa zetu mbaya; tunaweza kushinda udhaifu wetu. Kwanza, tunapaswa kutambua na kukubali udhaifu wetu. Kisha, tunaweza kuchukua hatua ya kuushinda. Tunaweza kusali kwa Yehova kwa ukawaida tukimwomba atusaidie kushinda udhaifu huo na kujifunza Neno lake kwa bidii, huku tukitafuta njia za kupambana na mielekeo hiyo. (Ebr. 4:12) Huenda tukahitaji kuendelea kufanyia kazi udhaifu wetu bila kukata tamaa. Huenda pambano hilo likaendelea maadamu sisi si wakamilifu. Paulo alitambua jambo hilo katika kisa chake mwenyewe, alipoandika hivi: “Lile ninalolitaka, hilo sizoei kulifanya; bali lile ninalochukia ndilo ninalofanya.” Hata hivyo, kama unavyojua, Paulo hakukata tamaa, kana kwamba hangeweza kamwe kujizuia. Badala yake, aliendelea kupambana na udhaifu wake, huku akitegemea msaada wa Mungu kupitia Yesu Kristo. (Rom. 7:15-25) Katika andiko lingine, Paulo alisema hivi: “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa, ili, baada ya mimi kuwahubiria wengine, mimi mwenyewe nisikataliwe kwa njia fulani.”—1 Kor. 9:27.

Wanadamu wana mwelekeo wa kujitetea. Tunaweza kuushinda mwelekeo huo kwa kusitawisha maoni ya Yehova na kufanya kama Paulo alivyowahimiza Wakristo: “Chukieni maovu, shikamaneni na mema.” (Rom. 12:9) Katika pambano letu la kushinda udhaifu wetu, tutahitaji kuwa wanyoofu, wastahimilivu, na kujitia nidhamu. Daudi alimwomba Yehova hivi: “Usafishe figo zangu na moyo wangu.” (Zab. 26:2) Alijua kwamba Mungu anaweza kuchunguza kwa usahihi mielekeo yetu ya ndani kabisa na kutupa msaada tunapouhitaji. Tukifuata mwongozo ambao Yehova anatoa kupitia Neno lake na roho yake takatifu, tunaweza kufanya maendeleo katika kuushinda udhaifu wetu.

Huenda wengine wakafadhaishwa na matatizo ambayo wanahisi kwamba hawawezi kuyashughulikia kwa nguvu zao wenyewe. Bila shaka, wazee wa kutaniko wanaweza kutusaidia kwa upendo na kututia moyo. (Isa. 32:1, 2) Lakini ni jambo la hekima kuwa na usawaziko kuhusiana na matarajio yetu. Kuna matatizo ambayo hayawezi kusuluhishwa kabisa katika mfumo huu wa mambo. Hata hivyo, watu wengi wamejifunza kuvumilia, na hilo limewasaidia kuishi maisha yenye kuridhisha.

Uhakikisho wa Kupata Msaada wa Yehova

Haidhuru tunakabiliana na matatizo gani katika nyakati hizi ngumu, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatuongoza na kututunza. Biblia inatuhimiza hivi: “Kwa hiyo, jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue ninyi katika wakati unaofaa; huku mkitupa mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.”—1 Pet. 5:6, 7.

Kathy ambaye alitumikia Betheli kwa miaka mingi alipotambua kwamba mume wake ana ugonjwa wa Alzheimer, alihisi kwamba hangeweza kuvumilia matatizo yaliyokuwa mbele yake. Alisali kwa Yehova kila siku ili ampe hekima na nguvu. Kadiri hali ya mume wake ilivyozidi kuzorota, ndugu wenye upendo walijitahidi kujua jinsi ya kushughulikia ugonjwa huo na akina dada wanaojali walimtia moyo. Wakristo hao walitumiwa na Yehova kumtegemeza, na Kathy aliweza kumtunza mume wake mpaka alipokufa miaka 11 hivi baadaye. Anasema hivi: “Nililia na kumshukuru Yehova kwa moyo wote kwa ajili ya msaada wake wote ambao uliniwezesha kuvumilia. Kwa sababu nilikuwa nimechoka sana, sikudhani kwamba ningetimiza mambo niliyotimiza kwa muda huo wote!”

Msaada wa Kushinda Udhaifu Usioonekana Wazi

Watu wanapojiona hawafai, huenda wakafikiri kwamba Yehova hatasikiliza wanapomwomba msaada wakati wa shida. Hivyo, ni vizuri hasa kufikiria yale ambayo Daudi alisema alipohuzunika sana kwa sababu ya dhambi yake nzito pamoja na Bath-sheba: “Moyo uliovunjika na kupondwa, Ee Mungu, hutaudharau.” (Zab. 51:17) Daudi alitubu kikweli, na alijua kwamba angeweza kumkaribia Mungu na kupata rehema zake. Yesu pia anajali kama Yehova. Mathayo, mwandikaji wa Injili, alionyesha jinsi Yesu alivyotimiza maneno haya ya Isaya: “Hakuna tete lililovunjika ambalo ataliponda, na hakuna utambi wa kitani unaotoa moshi atakaouzima.” (Mt. 12:20; Isa. 42:3) Alipokuwa duniani, Yesu aliwahurumia watu wa hali ya chini na waliokandamizwa. Kwa njia ya mfano, hakuzima nguvu ya uhai iliyobaki ndani ya mtu aliyekuwa kama utambi wa taa ya mafuta uliokuwa karibu kuzimika. Badala yake, aliwatunza kwa huruma walioteseka na kuwapa tena tumaini la kuishi. Alifanya hivyo alipokuwa duniani. Je, unaamini kwamba Yesu hajabadilika na kwamba anaweza kuusikitikia udhaifu wako? Ona kwamba andiko la Waebrania 4:15 linaonyesha kwamba Yeye ndiye anayeweza “kuusikitikia udhaifu wetu.”

Alipokuwa akiandika kuhusu “mwiba katika mwili,” Paulo alisema kwamba nguvu za Kristo zilikuwa kama “hema” juu yake. (2 Kor. 12:7-9) Alihisi ulinzi wa Mungu kupitia Kristo, kama tu mtu aliye ndani ya hema anavyohisi kwamba analindwa kutokana na hali mbaya ya hewa. Kama Paulo, hatuhitaji kukata tamaa kwa sababu ya udhaifu na matatizo yetu. Ili kuendelea kuwa wenye nguvu kiroho, tunapaswa kutumia maandalizi yote ambayo Yehova anatupa kupitia kutaniko lake la kidunia. Tunaweza kufanya yote tunayoweza na kumtegemea Yehova tukiwa na hakika kabisa kwamba ataongoza hatua zetu. Tunapoona jinsi nguvu za Mungu zinavyotusaidia katika udhaifu wetu, tutaweza kusema kama Paulo alivyosema: “Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa mwenye nguvu.”—2 Kor. 12:10.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Paulo alimwomba Yehova daima amwongoze katika kutimiza huduma yake

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mfalme Daudi alimweka Yoabu kuwa mkuu wa jeshi

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yoabu alimuua mpinzani wake, Amasa

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kwa upendo, wazee wanatupa mwongozo wa Kimaandiko unaoweza kutusaidia kushughulikia matatizo yetu