Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sifa Ambazo Ni Lazima Tufuatilie

Sifa Ambazo Ni Lazima Tufuatilie

Sifa Ambazo Ni Lazima Tufuatilie

“Fuatilia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, [na] tabia-pole.”—1 TIM. 6:11.

1. Toa mifano ili kuonyesha maana ya neno “fuatilia.”

UNAFIKIRIA nini unaposikia neno “fuatilia”? Labda unafikiria siku za Musa wakati jeshi la Wamisri ‘lilipoanza kuwafuatilia’ Waisraeli, lakini likaangamizwa katika Bahari Nyekundu. (Kut. 14:23) Au huenda ukakumbuka hatari ambayo ilimkabili mtu aliyemuua mwingine bila kukusudia katika Israeli la kale. Alihitaji kukimbia haraka kwenye jiji moja kati ya majiji sita yaliyochaguliwa kuwa majiji ya makimbilio. Kama hangefanya hivyo, ‘mlipiza-kisasi cha damu, ambaye alimfuatilia muuaji huyo kwa hasira kali, angemfikia na kumuua.’—Kum. 19:6, Tanakh.

2. (a) Mungu amewaalika Wakristo fulani wafuatilie tuzo gani? (b) Yehova anawatolea Wakristo wengi leo tumaini gani?

2 Tofauti na mifano hiyo ya Biblia, fikiria mtazamo huu mzuri ambao mtume Paulo alikuwa nao: “Ninafuatilia kuelekea ule mradi kwa ajili ya tuzo la mwito wa Mungu wa kwenda juu kwa njia ya Kristo Yesu.” (Flp. 3:14) Biblia inaonyesha kwamba jumla ya Wakristo watiwa-mafuta 144,000, Paulo akiwa mmoja wao, wanapokea tuzo au zawadi ya uhai wa kimbingu. Watashiriki pamoja na Yesu Kristo katika Utawala wake wa Miaka Elfu Moja juu ya dunia. Watu hao wamealikwa na Mungu wafuatilie mradi mzuri kama nini! Hata hivyo, hesabu kubwa ya Wakristo wa kweli leo, wana tumaini au mradi tofauti. Kwa upendo, Yehova anawatolea kile ambacho Adamu na Hawa walipoteza, yaani, tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani wakiwa na afya kamilifu.—Ufu. 7:4, 9; 21:1-4.

3. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu?

3 Wanadamu wenye dhambi hawawezi kupata uzima wa milele kwa sababu ya jitihada zao zisizo kamilifu za kufanya yaliyo sawa. (Isa. 64:6) Wanaweza kupata uzima wa milele tu kwa kuwa na imani katika mpango wenye upendo wa Mungu wa kuwaokoa kupitia Yesu Kristo. Tunaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba tunathamini fadhili hizo zisizostahiliwa za Mungu? Jambo la kwanza ambalo tunaweza kufanya ni kutii amri hii: “Fuatilia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, [na] tabia-pole.” (1 Tim. 6:11) Kuchunguza sifa hizo kunaweza kumsaidia kila mmoja wetu aazimie hata zaidi kuendelea kuzifuatilia “kwa ukamili zaidi.”—1 The. 4:1.

“Fuatilia Uadilifu”

4. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba kufuatilia “uadilifu” ni jambo la maana, na ni lazima mtu achukue hatua gani za kwanza?

4 Katika barua zake mbili kwa Timotheo, mtume Paulo alitaja sifa ambazo tunapaswa kufuatilia, na katika kila barua alitaja “uadilifu” kwanza. (1 Tim. 6:11; 2 Tim. 2:22) Zaidi ya hayo, maandiko mengine ya Biblia yanatuhimiza tena na tena tufuatilie uadilifu. (Met. 15:9; 21:21; Isa. 51:1) Hatua ya kwanza ya kufuatilia uadilifu ni ‘kupata ujuzi juu ya Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule aliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yoh. 17:3) Kufuatilia uadilifu kutamchochea mtu achukue hatua ya kutubu dhambi alizotenda zamani na ‘kugeuka’ ili afanye mapenzi ya Mungu.—Mdo. 3:19.

5. Ni lazima tufanye nini ili tupate na kuendelea kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu?

5 Mamilioni ya watu ambao wanajitahidi kikweli kufuatilia uadilifu wamejiweka wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji. Ikiwa wewe ni Mkristo aliyebatizwa, je, umefikiria uhakika wa kwamba njia yako ya maisha inapaswa, na huenda inaonyesha kwamba unaendelea kufuatilia uadilifu? Njia moja ya kufanya hivyo ni kutumia Biblia kutambua “yaliyo sawa na yaliyo makosa” unapofanya maamuzi ya maana maishani. (Soma Waebrania 5:14.) Kwa mfano, ikiwa wewe ni Mkristo mseja aliyefikia umri wa kufunga ndoa, je, umeazimia kabisa kuepuka kuanzisha uhusiano wowote wa kimapenzi na mtu mwingine ambaye si Mkristo aliyebatizwa? Ikiwa unafuatilia uadilifu basi umeazimia kufanya hivyo.—1 Kor. 7:39.

6. Kufuatilia uadilifu kikweli kunahusisha nini?

6 Kuwa mwadilifu ni tofauti na kujiona kuwa mwadilifu au kuwa “mwadilifu kupita kiasi.” (Mhu. 7:16) Yesu alionya kuhusu kuonyesha uadilifu wa aina hiyo ili tuonekane kuwa bora kuliko wengine. (Mt. 6:1) Kufuatilia uadilifu kikweli kunahusisha moyo, kurekebisha mawazo, mitazamo, nia, na tamaa zisizofaa. Tukiendelea kujitahidi kufanya hivyo, inaelekea kwamba hatutatenda dhambi nzito. (Soma Methali 4:23; linganisha na Yakobo 1:14, 15.) Zaidi ya hayo, Yehova atatubariki na kutusaidia tunapofuatilia sifa nyingine muhimu za Kikristo.

“Fuatilia . . . Ujitoaji-Kimungu”

7. “Ujitoaji-kimungu” ni nini?

7 Kujitoa kunatia ndani kuwa mshikamanifu na mwenye bidii kabisa. Kamusi moja ya Biblia inasema kwamba neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa kuwa “ujitoaji-kimungu” linamaanisha “mtazamo unaofaa wa kuwa mwangalifu kutoruhusu jambo lolote lituzuie tusimwogope Mungu.” Mara nyingi Waisraeli walishindwa kuonyesha ujitoaji huo, na matendo yao ya kutotii hata baada ya kuwekwa huru na Mungu kutoka Misri yanaonyesha hivyo.

8. (a) Ni swali gani lililohitaji kujibiwa baada ya Adamu kufanya dhambi? (b) ‘Siri hiyo takatifu’ ilifunuliwa jinsi gani?

8 Maelfu ya miaka baada ya mwanadamu mkamilifu Adamu kutenda dhambi, bado swali hili halikuwa limejibiwa: “Je, mwanadamu yeyote anaweza kuishi maisha makamilifu ya ujitoaji-kimungu?” Katika miaka yote hiyo, hakuna mwanadamu mwenye dhambi aliyeweza kufanya hivyo. Lakini kwa wakati wake, Yehova alifunua ‘siri hiyo takatifu.’ Alihamisha uhai wa Mwana wake mzaliwa-pekee wa kimbingu na kuutia katika tumbo la uzazi la Maria ili azaliwe akiwa mwanadamu mkamilifu. Katika maisha yake yote duniani na wakati wa kifo chake chenye aibu, Yesu alionyesha maana ya kujitoa kikamili na kuwa na ushikamanifu mkamilifu kwa Mungu wa kweli. Sala zake zilionyesha kwamba alimheshimu Baba yake wa mbinguni mwenye upendo. (Mt. 11:25; Yoh. 12:27, 28) Hivyo, Yehova alimwongoza Paulo kwa roho yake ataje “ujitoaji-kimungu” alipokuwa akieleza kuhusu kielelezo bora cha maisha ambacho Yesu aliweka.—Soma 1 Timotheo 3:16.

9. Tunaweza kufuatilia jinsi gani ujitoaji-kimungu?

9 Katika hali yetu ya dhambi, hatuwezi kuonyesha ujitoaji-kimungu kwa ukamilifu. Lakini tunaweza kuufuatilia. Tunahitaji kufanya yote tunayoweza ili kufuata kielelezo cha Kristo kwa ukaribu. (1 Pet. 2:21) Hivyo, hatutakuwa kama wanafiki ambao ‘wana namna ya ujitoaji-kimungu lakini wanazikana nguvu zake.’ (2 Tim. 3:5) Hilo halimaanishi kwamba ujitoaji-kimungu wa kweli hauwezi kuonyeshwa kwa nje. Bila shaka unaweza kuonyeshwa. Kwa mfano, tunapochagua nguo ya arusi au mavazi ya kuvaa tunapoenda matembezi, sura yetu inapaswa sikuzote kuonyesha kwamba tunaishi kupatana na dai letu la kwamba ‘tunamheshimu Mungu.’ (1 Tim. 2:9, 10) Ndiyo, ili kufuatilia ujitoaji-kimungu tunahitaji kutilia maanani viwango vya Mungu vya uadilifu katika maisha yetu ya kila siku.

“Fuatilia . . . Imani”

10. Ni lazima tufanye nini ili imani yetu iendelee kuwa yenye nguvu?

10 Soma Waroma 10:17. Ili Mkristo apate na kuendelea kuwa na imani yenye nguvu, ni lazima atafakari kwa ukawaida kuhusu kweli zenye thamani zilizo katika Neno la Mungu. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametutayarishia vitabu vingi vizuri. Vitabu vitatu vya pekee, yaani, Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, na ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu,’ vimekusudiwa kutusaidia kumfahamu Kristo vizuri zaidi na kumwiga. (Mt. 24:45-47) Jamii ya mtumwa inapanga pia mikutano na makusanyiko ambayo mara nyingi yanakazia “neno kumhusu Kristo.” Je, unaona jambo lolote ambalo unaweza kufanya ili ufaidike zaidi na mipango hiyo unapokazia “uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida” maandalizi ya Mungu?—Ebr. 2:1.

11. Kusali na kutii kunatusaidia jinsi gani kufuatilia imani?

11 Sala inasaidia pia katika kujenga imani yenye nguvu. Pindi moja, wafuasi wa Yesu walimsihi hivi: “Tupe imani zaidi.” Sisi pia tunaweza kumwomba Mungu kwa unyenyekevu atupe imani zaidi. (Luka 17:5) Ili tuwe na imani zaidi, tunapaswa kusali ili roho takatifu ya Mungu itusaidie kwa kuwa imani ni sehemu ya “matunda ya roho.” (Gal. 5:22) Kwa kuongezea, kutii amri za Mungu kunaitia nguvu imani yetu. Kwa mfano, tunaweza kujitahidi kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri. Inaelekea kwamba kufanya hivyo kutatuletea furaha nyingi zaidi. Na tukitafakari kuhusu baraka ambazo tunapata kwa sababu ya “kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu],” imani yetu itakua.—Mt. 6:33.

“Fuatilia . . . Upendo”

12, 13. (a) Yesu alitoa amri gani mpya? (b) Tunapaswa kufuatilia upendo kama wa Kristo katika njia gani muhimu?

12 Soma 1 Timotheo 5:1, 2Paulo alitoa mashauri mazuri kuonyesha jinsi Wakristo wanavyoweza kupendana. Ni lazima ujitoaji-kimungu wetu utie ndani kutii ile amri mpya ya Yesu ya ‘kupendana’ kama vile alivyotupenda sisi. (Yoh. 13:34) Mtume Yohana alisema hivi: “Yeyote aliye na riziki ya ulimwengu huu naye amwone ndugu yake akiwa na uhitaji na bado amfungie mlango wa huruma zake nyororo, ni katika njia gani kumpenda Mungu hukaa ndani yake?” (1 Yoh. 3:17) Je, unaweza kufikiria nyakati ambazo ulionyesha upendo huo kwa kuwasaidia wengine?

13 Njia nyingine ya kufuatilia upendo ni kuwa wenye kusamehe na kuepuka kuwawekea ndugu zetu kinyongo moyoni. (Soma 1 Yohana 4:20.) Badala yake, tunataka kufuata shauri hili lililoongozwa na roho: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.” (Kol. 3:13) Je, kuna mtu yeyote kutanikoni ambaye unaweza kumsamehe kama andiko hilo linavyosema? Je, utamsamehe?

“Fuatilia . . . Uvumilivu”

14. Tunaweza kujifunza nini kutokana na kutaniko la Filadelfia?

14 Ni rahisi kujikaza ili kutimiza mradi fulani wa muda mfupi lakini si rahisi kutimiza mradi ambao ni mgumu au utakaochukua muda mrefu kuliko tulivyotazamia. Ni wazi kwamba kufuatilia mradi wa uzima wa milele kunahitaji uvumilivu. Bwana Yesu aliliambia hivi kutaniko la Filadelfia: “Kwa sababu ulilishika neno juu ya uvumilivu wangu, mimi pia nitakulinda kutokana na ile saa ya jaribu.” (Ufu. 3:10) Kwa kweli, Yesu alifundisha kuhusu uhitaji wa uvumilivu, sifa ambayo inatusaidia kutovunjika moyo tunapopatwa na majaribu na vishawishi. Ni wazi kwamba ndugu wa kutaniko la Filadelfia katika karne ya kwanza walionyesha uvumilivu wa pekee walipopata mateso mengi ya imani. Hivyo, Yesu aliwahakikishia kwamba angewasaidia wakati wa jaribu kubwa ambalo lingekuja.—Luka 16:10.

15. Yesu alifundisha nini kuhusu uvumilivu?

15 Yesu alijua kwamba wafuasi wake wangechukiwa na watu wao wa ukoo ambao si waamini na ulimwengu kwa ujumla, hivyo aliwatia moyo hivi: “Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mt. 10:22; 24:13) Pia, Yesu alionyesha jinsi ambavyo wanafunzi wake wangepata nguvu ambazo wangehitaji ili kuvumilia. Katika mfano mmoja, alisema kwamba watu ambao “hulipokea lile neno [la Mungu] kwa shangwe” na ambao wanaanguka wanapopata majaribu ya imani ni kama udongo ulio kwenye mwamba. Hata hivyo, aliwalinganisha wafuasi wake waaminifu na udongo mzuri kwa sababu ‘wanalihifadhi’ neno la Mungu na “kuzaa matunda kwa uvumilivu.”—Luka 8:13, 15.

16. Ni uandalizi gani wenye upendo ambao umewasaidia mamilioni ya watu kuvumilia?

16 Je, uliona siri ya kuvumilia? Ni lazima ‘tulihifadhi’ Neno la Mungu ili liendelee kuwa hai katika mioyo na akili zetu. Tunaweza kufanya hivyo kwa sababu tuna Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, ambayo ni tafsiri sahihi, rahisi kusoma, na inapatikana katika lugha nyingi zaidi. Kutafakari kuhusu sehemu fulani ya Neno la Mungu kila siku kutatusaidia kupata nguvu tunazohitaji ili kuendelea kuzaa matunda “kwa uvumilivu.”—Zab. 1:1, 2.

“Fuatilia . . . Tabia-Pole” na Amani

17. (a) Kwa nini “tabia-pole” ni sifa ya maana sana? (b) Yesu alionyesha namna gani kwamba alikuwa mwenye tabia-pole?

17 Hakuna mtu anayefurahia kulaumiwa kwa sababu ya jambo ambalo hajasema wala kufanya. Kwa kawaida, wanadamu wanapolaumiwa isivyo haki wanapinga mashtaka hayo kwa hasira. Ni jambo bora zaidi kuonyesha “tabia-pole.” (Soma Methali 15:1.) Mtu anahitaji kuwa na nguvu nyingi ili ashughulikie mashtaka yasiyo ya haki kwa njia ya upole. Yesu Kristo alituwekea mfano mkamilifu katika kufanya hivyo. “Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa matukano. Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho, bali aliendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu.” (1 Pet. 2:23) Hatuwezi kumwiga Yesu kikamili katika jambo hilo, lakini je, tunaweza kujitahidi kufanya maendeleo zaidi katika kuonyesha tabia-pole?

18. (a) Tabia-pole ina faida gani? (b) Ni sifa gani nyingine ambayo tunatiwa moyo tuifuatilie?

18 Acheni tumwige Yesu kwa ‘kuwa tayari sikuzote kutetea’ imani yetu, ‘tukifanya hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.’ (1 Pet. 3:15) Ndiyo, tukiwa na tabia-pole tutaepuka kuchochea mabishano na watu tunaokutana nao katika huduma yetu au na waamini wenzetu wenye maoni tofauti na yetu. (2 Tim. 2:24, 25) Tabia-pole inatusaidia kuwa na amani. Huenda ndiyo sababu Paulo, katika barua yake ya pili kwa Timotheo, alitaja “amani” pamoja na sifa tunazopaswa kufuatilia. (2 Tim. 2:22; linganisha na 1 Timotheo 6:11.) Ndiyo, “amani” ni sifa nyingine ambayo Maandiko yanatutia moyo tuifuatilie.—Zab. 34:14; Ebr. 12:14.

19. Baada ya kuzungumzia sifa saba za Kikristo, umeazimia kufuatilia nini, na kwa nini?

19 Tumezungumzia sifa saba za Kikristo ambazo tunatiwa moyo tufuatilie, yaani, uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, tabia-pole, na amani. Ni baraka kama nini wakati ndugu na dada katika kila kutaniko wanapojitahidi kuonyesha kwa ukamili zaidi sifa hizo zenye thamani! Kufanya hivyo kutamletea Yehova heshima, naye ataweza kutufinyanga ili tumletee sifa.

Mambo ya Kutafakari

• Kufuatilia uadilifu na ujitoaji-kimungu kunatia ndani nini?

• Ni nini kitakachotusaidia kufuatilia imani na uvumilivu?

• Upendo unapaswa kutuongoza jinsi gani tunaposhughulika na wenzetu?

• Kwa nini tunahitaji kufuatilia tabia-pole na amani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Yesu alionya kuhusu kuonyesha uadilifu ili kuwapendeza watu

[Picha katika ukurasa wa 13]

Tunaweza kufuatilia imani kwa kutafakari kuhusu kweli za Neno la Mungu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tunaweza kufuatilia upendo na tabia-pole