Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vitu Ambavyo Ni Lazima Tuvikimbie

Vitu Ambavyo Ni Lazima Tuvikimbie

Vitu Ambavyo Ni Lazima Tuvikimbie

“Ninyi uzao wa nyoka-vipiri, ni nani ambaye amewaonyesha ninyi kuikimbia ghadhabu inayokuja?”—MT. 3:7.

1. Toa mifano fulani ya Biblia ya watu ambao walikimbia.

UNAFIKIRIA nini unaposikia neno “kimbia”? Huenda wengine wakamfikiria yule kijana mwenye sura nzuri, Yosefu, akimkimbia mke wa Potifa aliyekuwa akimshawishi alale naye. (Mwa. 39:7-12) Huenda wengine wakawafikiria Wakristo ambao walikimbia kutoka Yerusalemu mwaka wa 66 W.K., kwa kutii onyo hili la Yesu: “Mtakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo . . . wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani, na wale walio katikati yake na waondoke.”—Luka 21:20, 21.

2, 3. (a) Yohana Mbatizaji alimaanisha nini alipowashutumu viongozi wa kidini? (b) Yesu alikazia jinsi gani onyo ambalo Yohana alikuwa ametoa?

2 Watu wanaotajwa hapo juu walikimbia kihalisi. Leo, kuna uhitaji wa haraka wa Wakristo wa kweli katika karibu kila nchi duniani pote, kukimbia kwa njia ya mfano. Yohana Mbatizaji alitumia neno “kimbia” kwa njia hiyo ya mfano. Kati ya watu ambao walikuja kumwona Yohana ni viongozi wa dini ya Kiyahudi waliojiona kuwa waadilifu na ambao hawakuona uhitaji wa kutubu. Waliwadharau watu wa kawaida ambao walikuwa wakibatizwa ili kuonyesha kwamba wametubu. Bila woga, Yohana alifunua kwamba viongozi hao walikuwa wanafiki. Alisema hivi: “Ninyi uzao wa nyoka-vipiri, ni nani ambaye amewaonyesha ninyi kuikimbia ghadhabu inayokuja? Kwa hiyo basi zaeni matunda yanayofaa toba.”—Mt. 3:7, 8.

3 Yohana hakuwa akizungumza kuhusu kukimbia kihalisi. Alikuwa akionya kuhusu hukumu iliyokuwa ikija, siku ya ghadhabu; na aliwaonya viongozi hao wa kidini kwamba ikiwa walitaka kuokoka siku hiyo, walihitaji kuzaa matunda yanayoonyesha kwamba wametubu. Baadaye, Yesu aliwashutumu bila woga viongozi hao wa kidini. Mtazamo wao wa kuua ulionyesha kwamba baba yao halisi alikuwa Ibilisi. (Yoh. 8:44) Yesu alikazia onyo ambalo Yohana alikuwa ametoa kwa kuwaita viongozi hao “uzao wa nyoka-vipiri” kisha akawauliza: “Mtaikimbiaje hukumu ya Gehena?” (Mt. 23:33) Yesu alimaanisha nini aliposema “Gehena”?

4. Yesu alimaanisha nini alipotaja “Gehena”?

4 Gehena lilikuwa bonde ambalo lilikuwa nje ya kuta za Yerusalemu ambamo uchafu na mizoga ya wanyama iliteketezwa. Yesu alitumia Gehena kama mfano wa kifo cha milele. (Ona ukurasa wa 27.) Swali lake kuhusu kuikimbia Gehena lilionyesha kwamba jamii hiyo ya viongozi wa kidini ilistahili kuharibiwa milele.—Mt. 5:22, 29.

5. Kulingana na historia, onyo la Yohana na Yesu lilitimizwa jinsi gani?

5 Viongozi wa dini ya Kiyahudi walizidisha dhambi zao kwa kumtesa Yesu na wafuasi wake. Baadaye, kama Yohana na Yesu walivyokuwa wameonya, siku ya Mungu ya ghadhabu ilikuja. Wakati huo ‘ghadhabu iliyokuwa ikija’ ingekumba eneo fulani, yaani, Yerusalemu na Yudea, kwa hiyo watu wangeweza kukimbia kwa njia halisi. Ghadhabu hiyo ilikuja wakati majeshi ya Roma yalipoharibu Yerusalemu na hekalu lake mwaka wa 70 W.K. Yerusalemu halikuwa limekumbwa na “dhiki” kama hiyo kabla ya hapo. Watu wengi waliuawa au kuchukuliwa mateka. Dhiki hiyo ilikuwa ishara ya uharibifu mkubwa zaidi ambao utawapata watu wengi wanaodai kuwa Wakristo na watu wa dini nyingine.—Mt. 24:21.

Ghadhabu Inayokuja Ambayo Tunapaswa Kuikimbia

6. Ni nini kilichoanza kutokea katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza?

6 Wakristo fulani wa karne ya kwanza waliasi imani na kupata wafuasi. (Mdo. 20:29, 30) Mitume wa Yesu walipokuwa hai, walikuwa kama “kizuizi” cha uasi-imani huo, lakini walipokufa, vikundi vingi vya Kikristo vya uwongo vilitokea. Leo, kuna mamia ya dini zinazodai kuwa za Kikristo ambazo zina mafundisho yanayopingana. Biblia ilitabiri kuhusu kutokea kwa makasisi wa dini hizo. Kwa ujumla inawaita “mtu wa uasi-sheria” na “mwana wa maangamizi . . . ambaye Bwana Yesu atamwangamiza . . . na kumfanya kuwa si kitu kwa ufunuo wa kuwapo kwake.”—2 The. 2:3, 6-8.

7. Kwa nini makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wanastahili kuitwa “mtu wa uasi-sheria”?

7 Makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo ni waasi-sheria kwa sababu wamewapotosha mamilioni ya watu kwa kueneza mafundisho, sikukuu, na tabia ambazo hazipatani na Biblia. Kama viongozi wa kidini ambao walishutumiwa na Yesu, waabudu wa leo ambao ni sehemu ya “mwana wa maangamizi” wataharibiwa bila tumaini la ufufuo. (2 The. 1:6-9) Hata hivyo, ni nini kitakachowapata watu ambao wamepotoshwa na makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo na viongozi wa dini nyingine za uwongo? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze mambo ambayo yalitukia baada ya uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K.

“Kimbieni Kutoka Katikati ya Babiloni”

8, 9. (a) Yeremia alikuwa na ujumbe gani wa kinabii kwa Wayahudi waliokuwa utekwani Babiloni? (b) Baada ya Wamedi na Waajemi kushinda Babiloni, ni nafasi gani ya kukimbia iliyotokea?

8 Nabii Yeremia alitabiri kuhusu uharibifu wa Yerusalemu uliotukia mwaka wa 607 K.W.K. Alisema kwamba watu wa Mungu wangepelekwa utekwani lakini wangerudishwa katika nchi yao baada ya “miaka 70.” (Yer. 29:4, 10) Yeremia alikuwa na ujumbe wa maana kwa Wayahudi waliopelekwa utekwani huko Babiloni; walipaswa kuepuka kuchafuliwa na dini ya uwongo ambayo ilifuatwa huko Babiloni. Hivyo, wangekuwa tayari kurudi Yerusalemu na kurudisha ibada safi kwa wakati uliowekwa na Yehova. Hilo lilitukia mara tu baada ya Wamedi na Waajemi kushinda Babiloni mwaka wa 539 K.W.K. Mfalme Koreshi wa Pili wa Uajemi aliwaagiza Wayahudi warudi na kujenga upya hekalu la Yehova huko Yerusalemu.—Ezra 1:1-4.

9 Maelfu ya Wayahudi walitumia nafasi hiyo kurudi. (Ezra 2:64-67) Kwa kufanya hivyo, walitimiza amri ya kinabii iliyotolewa na Yeremia kwa kukimbia kwa njia ya mfano, yaani, kukimbilia sehemu nyingine. (Soma Yeremia 51:6, 45, 50.) Hali hazikuwaruhusu Wayahudi wote wafunge safari hiyo ndefu ya kurudi Yerusalemu na Yuda. Wale waliobaki Babiloni, kama vile nabii Danieli aliyezeeka, wangebarikiwa na Mungu, ikiwa tu wangeunga mkono kwa moyo wote ibada safi huko Yerusalemu na kuendelea kujitenga na ibada ya uwongo ya Babiloni.

10. “Babiloni Mkubwa” amesababisha “machukizo” gani?

10 Leo, mabilioni ya wanadamu wanashiriki katika dini mbalimbali za uwongo ambazo zilianzia Babiloni ya kale. (Mwa. 11:6-9) Kwa ujumla, dini hizo zinaitwa “Babiloni Mkubwa, mama wa makahaba na wa machukizo ya dunia.” (Ufu. 17:5) Kwa muda mrefu, dini za uwongo zimekuwa zikiunga mkono watawala wa kisiasa wa ulimwengu huu. Kati ya “machukizo” ambayo dini hizo zimesababisha ni vita vingi ambamo mamia ya mamilioni ya watu “wameuawa juu ya dunia.” (Ufu. 18:24) “Machukizo” mengine yanatia ndani vitendo vya kufanya ngono na watoto na matendo mengine mapotovu ya kingono yanayofanywa na makasisi na kuruhusiwa na viongozi wa makanisa. Haishangazi kwamba hivi karibuni Yehova Mungu ataondoa kabisa dini za uwongo duniani!—Ufu. 18:8.

11. Kabla ya kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa, Wakristo wa kweli wana daraka gani?

11 Wakristo wa kweli, ambao wanajua jambo hilo, wana daraka la kuwaonya washiriki wa Babiloni Mkubwa. Njia moja wanayotumia kuwaonya ni kusambaza Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia vinavyochapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” ambaye amewekwa rasmi na Yesu ili atoe ‘chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.’ (Mt. 24:45) Watu wanapopendezwa na ujumbe wa Biblia, mipango inafanywa ili kuwasaidia kupitia funzo la Biblia. Tunatumaini kwamba wataona uhitaji wa ‘kukimbia kutoka katikati ya Babiloni’ kabla hawajachelewa mno.—Ufu. 18:4.

Ikimbieni Ibada ya Sanamu

12. Mungu ana maoni gani kuhusu kuabudu mifano na sanamu?

12 Zoea lingine lenye kuchukiza ambalo limeenea sana katika Babiloni Mkubwa ni ibada ya mifano au sanamu. Mungu anasema kwamba hivyo ni ‘vitu vyenye kuchukiza’ na ‘sanamu za mavi.’ (Kum. 29:17) Ni lazima watu wote ambao wanataka kumpendeza Mungu waepuke ibada ya sanamu, kama Mungu anavyosema: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu; nami sitampa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe, wala sitazipa sanamu za kuchongwa sifa yangu.”—Isa. 42:8.

13. Tunahitaji kukimbia ibada gani za sanamu ambazo hazitambuliki waziwazi?

13 Neno la Mungu linafunua pia ibada nyingine za sanamu ambazo hazitambuliki waziwazi. Kwa mfano, linasema kwamba kutamani ni “ibada ya sanamu.” (Kol. 3:5) Neno linalotafsiriwa “kutamani” linamaanisha kuwa na tamaa ya kupata kitu ambacho kimekatazwa, kama vile mali ya mtu mwingine. (Kut. 20:17) Malaika ambaye alikuja kuwa Shetani Ibilisi alisitawisha tamaa ya kuwa kama Mungu Aliye Juu Zaidi na ya kuabudiwa. (Luka 4:5-7) Tamaa hiyo ilimfanya amwasi Yehova na kumshawishi Hawa atamani kitu ambacho Mungu alikataza. Kwa njia fulani, Adamu pia aliabudu sanamu kwa sababu aliruhusu tamaa ya kichoyo ya kushirikiana na mke wake iwe ya maana zaidi kuliko kumtii Baba yake wa mbinguni mwenye upendo. Kinyume chake, wote wanaotaka kuikimbia siku ya ghadhabu ya Mungu ni lazima wajitoe kikamili kwa Mungu na kuepuka kutamani kwa njia yoyote ile.

“Ukimbieni Uasherati”

14-16. (a) Kwa nini Yosefu ni mfano mzuri kuhusiana na maadili? (b) Tunapaswa kufanya nini tunapokuwa na tamaa chafu ya ngono? (c) Tunaweza kufanya nini ili tufaulu kuukimbia uasherati?

14 Soma 1 Wakorintho 6:18. Mke wa Potifa alipojaribu kumshawishi Yosefu, Yosefu alikimbia kihalisi na kumwacha. Yosefu ni mfano mzuri kama nini kwa Wakristo wote, waseja na waliofunga ndoa! Ni wazi kwamba dhamiri ya Yosefu ilikuwa imezoezwa na matukio ya zamani ambayo yalionyesha maoni ya Mungu kuhusu uasherati. Ikiwa tunataka kutii amri ya ‘kuukimbia uasherati,’ tutaepuka mambo ambayo yanaweza kuchochea tamaa ya kufanya ngono na mtu mwingine ambaye si mwenzi wetu wa ndoa. Tunaambiwa hivi: “Viueni viungo vya mwili wenu . . . kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu. Kwa sababu ya mambo hayo ghadhabu ya Mungu inakuja.”—Kol. 3:5, 6.

15 Ona kwamba “ghadhabu ya Mungu inakuja.” Watu wengi katika ulimwengu wanasitawisha na kufuata tamaa zisizofaa za ngono. Hivyo, sisi Wakristo tunahitaji kuomba msaada wa Mungu na roho takatifu ili tamaa chafu za ngono zisituongoze. Kwa kuongezea, kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kuwahubiria majirani wetu habari njema kutatusaidia ‘kuendelea kutembea kwa roho.’ Tukifanya hivyo, ‘hatutatenda tamaa ya kimwili hata kidogo.’—Gal. 5:16.

16 Bila shaka, tukitazama ponografia (picha au habari za ngono), hatutakuwa ‘tukitembea kwa roho.’ Vivyo hivyo, kila Mkristo anahitaji kujilinda ili asisome, asitazame, au kusikiliza mambo yanayochochea tamaa ya ngono. Pia, “watu watakatifu” wa Mungu hawapaswi kufurahia kufanya mizaha au kuzungumza kuhusu mambo hayo. (Efe. 5:3, 4) Tunapofanya hivyo, tunamwonyesha Baba yetu mwenye upendo kwamba kwa kweli tunataka kuikimbia ghadhabu yake inayokuja na kuishi katika ulimwengu mpya wenye uadilifu.

Ukimbieni Mtego wa “Kupenda Pesa”

17, 18. Kwa nini ni lazima tukimbie mtego wa “kupenda pesa”?

17 Katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo, Paulo alikazia kanuni ambazo zinapaswa kuwaongoza watumwa Wakristo, kwa kuwa wengine wao walitazamia kupata faida za kimwili kutokana na mabwana wao Wakristo. Huenda wengine walijaribu kutumia mambo matakatifu ili kupata faida za kichoyo. Paulo alionya kuhusu ‘kufikiri kwamba ujitoaji-kimungu ni njia ya kupata faida’ za kimwili. Huenda tatizo hilo lilisababishwa na “kupenda pesa,” ambako kunaweza kuwa na matokeo mabaya kwa mtu yeyote, awe tajiri au maskini.—1 Tim. 6:1, 2, 5, 9, 10.

18 Je, unakumbuka watu fulani katika Biblia ambao uhusiano wao pamoja na Mungu uliharibika kwa sababu ya “kupenda pesa” au kupenda vitu visivyo na maana vinavyoweza kununuliwa kwa pesa? (Yos. 7:11, 21; 2 Fal. 5:20, 25-27) Paulo alimhimiza hivi Timotheo: “Wewe, Ee mtu wa Mungu, yakimbie mambo hayo. Lakini fuatilia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, tabia-pole.” (1 Tim. 6:11) Ni lazima wote wanaotaka kuokoka siku inayokuja ya ghadhabu watii shauri hilo.

“Zikimbie Tamaa Zinazotukia Ujanani”

19. Vijana wote wanahitaji nini?

19 Soma Methali 22:15. Ujinga ulio katika moyo wa kijana unaweza kumwongoza kwa urahisi katika njia isiyofaa. Nidhamu inayotegemea Biblia inaweza kusaidia kuondoa ujinga huo. Vijana wengi Wakristo ambao wazazi wao si Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kutafuta na kutumia kanuni za Biblia. Vijana wengine wanafaidika kwa kufuata mashauri yenye hekima ya washiriki wa kutaniko ambao wamekomaa kiroho. Kutii mashauri yanayotegemea Biblia kunaweza kuongoza kwenye furaha sasa na wakati ujao, haidhuru ni nani anayetoa mashauri hayo.—Ebr. 12:8-11.

20. Vijana wanaweza kupata wapi msaada wa kukimbia tamaa zisizofaa?

20 Soma 2 Timotheo 2:20-22. Mioyo ya vijana wengi ambao hawajapata nidhamu inayofaa imenaswa na njia za ujinga, kama vile roho ya mashindano, tamaa, uasherati, kupenda pesa, na kufuatia raha. Mambo hayo yanahusiana na “tamaa zinazotukia ujanani,” ambazo tunahimizwa na Biblia tuzikimbie. Ili kijana Mkristo azikimbie tamaa hizo, anapaswa kujilinda kutokana na uvutano wowote ule wenye kudhuru. Vijana wanaweza kulindwa hasa wakitii shauri la Mungu la kufuatilia sifa za Kikristo “pamoja na wale wanaomwitia Bwana kutokana na moyo safi.”

21. Yesu Kristo alitoa ahadi gani nzuri ajabu kuhusu wafuasi wake walio mfano wa kondoo?

21 Tuwe vijana au wazee, tunapokataa kuwasikiliza watu ambao wanajaribu kutupotosha tunaonyesha kwamba tunataka kuwa kati ya wafuasi wa Yesu walio mfano wa kondoo ambao ‘wanakimbia sauti ya wageni.’ (Yoh. 10:5) Hata hivyo, ili tuikimbie siku ya Mungu ya ghadhabu, tunahitaji kufanya mengi zaidi kuliko kukimbia tu mambo yenye kudhuru. Ni lazima pia tufuatie sifa nzuri. Habari inayofuata itazungumzia sifa saba. Tuna sababu nzuri ya kuchunguza zaidi mambo hayo, kwa kuwa Yesu anatoa ahadi hii nzuri ajabu: “Ninawapa [kondoo wangu] uzima wa milele, nao hawataharibiwa kamwe, wala hakuna atakayewanyakua kutoka mkononi mwangu.”—Yoh. 10:28.

Ungetoa Jibu Gani?

• Yesu alitoa onyo gani kwa viongozi wa kidini?

• Mamilioni ya watu wanakabili hatari gani leo?

• Ni lazima tukimbie ibada gani za sanamu ambazo hazitambuliki waziwazi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Unafikiria nini unaposikia neno “kimbia”?