Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hatukuogopa—Yehova Alikuwa Pamoja Nasi

Hatukuogopa—Yehova Alikuwa Pamoja Nasi

Hatukuogopa—Yehova Alikuwa Pamoja Nasi

Limesimuliwa na Egyptia Petridou

Mwaka wa 1972, Mashahidi katika maeneo yote ya Saiprasi walikusanyika huko Nicosia kusikiliza hotuba ya pekee iliyotolewa na Nathan H. Knorr, ambaye kwa miaka mingi aliongoza kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova. Alinitambua mara moja, na hata kabla sijajitambulisha, aliniuliza: “Je, una habari zozote kutoka Misri?” Nilikuwa nimekutana na Ndugu Knorr miaka 20 mapema katika mji wa nyumbani, Aleksandria, Misri.

NILIZALIWA huko Aleksandria Januari 23, 1914 (23/1/1914). Mimi ndiye niliyekuwa mkubwa katika familia yenye watoto wanne. Tulilelewa karibu sana na bahari. Wakati huo, Aleksandria lilikuwa jiji maridadi la kimataifa, maarufu kwa majengo na historia yake. Kwa kuwa Wazungu waliishi pamoja na Waarabu, tukiwa watoto tulijifunza kuzungumza Kiarabu, Kifaransa, Kiingereza, Kiitaliano, na Kigiriki, lugha ya familia yetu.

Baada ya kuhitimu shule, nilipata kazi katika nyumba moja ya mitindo ya Kifaransa, ambako nilifurahia sana kukata vitambaa na kushona nguo maridadi kwa ajili ya wanawake matajiri. Pia, nilipenda sana mambo ya dini na kusoma Biblia, hata ingawa sikuelewa mambo mengi niliyosoma.

Karibu na wakati huo—katikati ya miaka ya 1930—nilikutana na kijana mmoja, mzaliwa wa Saiprasi. Theodotos Petrides alikuwa mpiganaji hodari wa mieleka, lakini alijifunza pia kutengeneza vitu vitamu-vitamu na alipata kazi katika duka moja maarufu la kuoka mikate. Theodotos alinipenda—mwanamke mdogo mwenye nywele nyeusi. Mara nyingi, akiwa chini ya dirisha langu, aliniimbia nyimbo za mapenzi za Kigiriki. Tulifunga ndoa Juni 30, 1940 (30/6/1940). Hizo zilikuwa siku zenye furaha. Mama yangu aliishi katika chumba cha juu na sisi chumba cha chini. John, mtoto wetu wa kwanza, alizaliwa mwaka wa 1941.

Kujifunza Kweli za Biblia

Kwa muda fulani, Theodotos alikuwa na mashaka kuhusu dini yetu, naye alikuwa akiuliza maswali kuhusu Biblia. Bila mimi kujua, Mashahidi wa Yehova walianza kujifunza Biblia pamoja naye. Siku moja, nilipokuwa nyumbani pamoja na mtoto wetu mchanga, mwanamke mmoja alipiga hodi na kunipa kadi yenye ujumbe wa Biblia. Ili kuonyesha heshima, nilitua kidogo halafu nikaisoma. Kisha, akanipa vichapo fulani vya Biblia. Vilifanana kabisa na vitabu ambavyo Theodotos alikuwa ameleta nyumbani.

“Ndiyo, nina vitabu hivi,” nilisema. “Tafadhali ingieni ndani.” Bila kukawia, nilimuuliza Shahidi huyo, Eleni Nicolaou, maswali mengi. Kwa subira, alitumia Biblia kunijibu. Nilifurahia jambo hilo. Kwa ghafula, nikaanza kuelewa ujumbe wa Biblia. Tulipotua kidogo wakati wa mazungumzo yetu, Eleni alitambua picha ya mume wangu. “Ninamjua mwanamume huyu!” akasema. Sasa nilijua jambo ambalo Theodotos alikuwa akifanya, na nilishangaa. Kumbe Theo alikuwa akienda kuhudhuria mikutano ya Kikristo akiwa peke yake—bila hata kunijulisha! Theodotos aliporudi nyumbani siku hiyo, nilimwambia: “Juma hili nitaenda pamoja nawe mahali ulipoenda Jumapili iliyopita (Siku ya Yenga)!”

Kwenye mkutano wa kwanza niliohudhuria, kikundi cha watu karibu kumi walikuwa wakizungumzia kitabu cha Biblia cha Mika. Nilielewa kila jambo! Tangu hapo na kuendelea, kila Ijumaa (Siku ya 5) jioni George na Katerini Petraki walitutembelea ili kutufundisha Biblia. Baba yangu na wengi wa ndugu na dada zangu hawakutaka tujifunze Biblia pamoja na Mashahidi, lakini dada yangu mdogo hakupinga, ingawa hakuwahi kuwa Shahidi. Hata hivyo, mama alikubali kweli ya Biblia. Katika mwaka wa 1942, Mama, Theodotos, na mimi tulibatizwa katika bahari huko Aleksandria ili kuonyesha kwamba tumejiweka wakfu kwa Yehova.

Maisha Yetu Yanavurugika

Mwaka wa 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilianza, na punde si punde vikaenea. Kufikia miaka ya mapema ya 1940, Jemadari Mjerumani Erwin Rommel na vikosi vyake vyenye vifaru walikuwa wamekaribia El Alamein, na jiji la Aleksandria lilikuwa limejaa wanajeshi wa Uingereza. Tulikusanya vyakula vingi vilivyokaushwa. Kisha, Theodotos aliombwa asimamie duka jipya la kutengeneza vitu vitamu-vitamu huko Port Taufiq, karibu na Suez, hivyo tukahamia huko. Mashahidi wawili wanaozungumza Kigiriki walianza kututafuta. Ingawa hawakujua tulipoishi, walihubiri nyumba kwa nyumba mpaka walipotupata.

Tukiwa Port Taufiq, tulijifunza Biblia pamoja na Stavros na Giula Kypraios na watoto wao, Totos na Georgia, nao wakawa marafiki wetu wa karibu. Stavros alifurahia sana kujifunza Biblia hivi kwamba wakati wa funzo alirudisha nyuma saa zote zilizokuwa nyumbani mwake kwa muda wa saa moja ili tukose gari-moshi la mwisho la kurudi nyumbani na hivyo kulazimika kukaa kwa muda mrefu zaidi. Mazungumzo yetu yaliendelea mpaka usiku sana.

Tuliishi Port Taufiq kwa miezi 18, na baada ya hapo tulirudi Aleksandria mama yangu alipokuwa mgonjwa. Alikufa mwaka wa 1947, akiwa mwaminifu kwa Yehova. Kwa mara nyingine tena, tuliona jinsi Yehova alivyotutia moyo kupitia ushirika wenye kujenga wa marafiki Wakristo wakomavu. Pia, tuliwakaribisha wamishonari ambao walikuwa wakienda katika migawo yao ya kigeni wakati meli zao zilipotia nanga kwa muda huko Aleksandria.

Shangwe na Matatizo

Katika mwaka wa 1952, nilimzaa James, mwana wetu wa pili. Tukiwa wazazi, tulitambua umuhimu wa kuwalea wana wetu katika mazingira ya kiroho, hivyo tulikubali nyumba yetu itumiwe kwa ajili ya mipango ya kawaida ya funzo la Biblia na mara nyingi tulikaribisha wahudumu wa wakati wote. Hivyo, mwana wetu mkubwa, John, alisitawisha upendo kwa ajili ya kweli ya Biblia, na alipokuwa angali tineja, alianza upainia. Wakati huohuo, alienda shuleni usiku ili akamilishe elimu yake ya kilimwengu.

Muda mfupi baadaye, Theodotos alipatwa na ugonjwa mbaya wa moyo na alishauriwa aache kazi aliyokuwa akifanya. Mwana wetu James alikuwa na umri wa miaka minne tu. Tungefanya nini? Je, Yehova hakuahidi: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe”? (Isa. 41:10) Fikiria mshangao na shangwe tuliyopata tulipoalikwa mwaka wa 1956 kutumikia tukiwa mapainia huko Ismailia, karibu na Mfereji wa Suez! Miaka iliyofuata ilikuwa yenye misukosuko huko Misri, na ndugu zetu Wakristo walihitaji kutiwa moyo.

Mwaka wa 1960 tulilazimika kuondoka Misri, huku kila mmoja wetu akiwa tu na sanduku moja. Tulihamia Saiprasi, kisiwa cha nyumbani cha mume wangu. Wakati huo, Theodotos alikuwa mgonjwa sana na hangeweza kufanya kazi. Hata hivyo, ndugu mmoja Mkristo mwenye fadhili na mke wake walitupa mahali pa kuishi katika nyumba yao. Jambo la kusikitisha ni kwamba, miaka miwili baadaye mume wangu alikufa, na niliachwa peke yangu pamoja na kijana wetu James. John, ambaye alikuja pia kuishi Saiprasi, alikuwa ameoa na alihitaji kuitunza familia yake.

Tunatunzwa Katika Nyakati Ngumu

Baadaye, Stavros na Dora Kairis walitupa mahali pa kuishi katika nyumba yao. Nilipiga magoti na kumshukuru Yehova kwa kushughulikia tena mahitaji yetu. (Zab. 145:16) Stavros na Dora walipoamua kuuza nyumba yao na kujenga nyingine mpya ikiwa na Jumba la Ufalme kwenye orofa ya chini, walituonyesha fadhili kwa kujenga jengo dogo lenye vyumba viwili kwa ajili yangu na James.

Mwishowe, James akaoa, naye akatumika pamoja na mke wake wakiwa mapainia mpaka mtoto wao wa kwanza kati ya watoto wao wanne alipozaliwa. Mwaka wa 1974, miaka miwili baada ya ziara isiyosahaulika ya Ndugu Knorr, kulikuwa na msukosuko wa kisiasa huko Saiprasi. * Watu wengi, kutia ndani Mashahidi, waliacha nyumba zao na kukimbilia mahali pengine. Mwana wangu John alikuwa kati yao. Alihamia Kanada pamoja na mke wake na watoto wao watatu. Ingawa watu wengi walikuwa wakiondoka, tulifurahia kuona hesabu ya wahubiri wa Ufalme ikiongezeka huko Saiprasi.

Nilipoanza kupokea malipo ya uzeeni, niliweza kushiriki kikamili zaidi katika kazi ya kuhubiri. Lakini miaka michache iliyopita, nilipatwa na ugonjwa wa kiharusi nikaenda kuishi pamoja na mwana wangu James na familia yake. Baadaye, afya yangu ilipokuwa mbaya zaidi, nililazwa hospitalini kwa majuma fulani kisha nikapelekwa katika makao ya kuwatunzia wazee. Ingawa bado nina maumivu, ninawahubiria wafanyakazi wa makao hayo, wagonjwa, na wageni. Pia, ninatumia saa nyingi kujifunza kibinafsi na, kwa msaada wa ndugu zangu wa kiroho, ninahudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko la karibu.

Faraja Katika Miaka Yangu ya Uzee

Ninafarijika ninaposikia kuhusu wale ambao mimi na Theodotos tuliwasaidia. Wengi wa watoto na wajukuu wao wako katika utumishi wa wakati wote, wengine wanatumikia Australia, Kanada, Ugiriki, Uingereza, na Uswisi. Leo, mwana wangu John na mke wake wanaishi Kanada pamoja na mwana wao. Binti yao mkubwa na mume wake ni mapainia. Binti yao mdogo, Linda, na mume wake, Joshua Snape, walialikwa kuhudhuria darasa la 124 la Shule ya Gileadi.

Mwana wangu James na mke wake sasa wanaishi Ujerumani. Wawili kati ya wana wao wanatumika Betheli—mmoja huko Athens, Ugiriki, na mwingine huko Selters, Ujerumani. Mwana wao mdogo, binti yao, na mume wake ni mapainia nchini Ujerumani.

Tutakuwa na habari nyingi kama nini za kuwaeleza mama yangu na mpendwa wangu Theodotos watakapofufuliwa! Watasisimuka kuona urithi mzuri ambao waliiachia familia yao. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Ona Amkeni! la Kiingereza la Oktoba 22, 1974 (22/10/1974), ukurasa wa 12-15 au la Kifaransa la Februari 8, 1975 (8/2/1975), ukurasa wa 12-15.

^ fu. 26 Habari hii ilipokuwa ikitayarishwa ili ichapishwe, Dada Petridou alikufa akiwa na umri wa miaka 93.

[Blabu katika ukurasa wa 24]

Kwa mara nyingine tena, tuliona jinsi Yehova alivyotutia moyo kupitia ushirika wenye kujenga wa marafiki Wakristo wakomavu

[Ramani katika ukurasa wa 24]

 

SAIPRASI

NICOSIA

BAHARI YA MEDITERANIA

MISRI

CAIRO

El Alamein

Aleksandria

Ismailia

Suez

Port Taufiq

Mfereji wa Suez

[Hisani]

Based on NASA/Visible Earth imagery

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na Theodotos mwaka wa 1938

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mwana wangu James na mke wake

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mwana wangu John na mke wake