Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Huduma ya Nyumba kwa Nyumba Ni ya Maana Sasa?

Kwa Nini Huduma ya Nyumba kwa Nyumba Ni ya Maana Sasa?

Kwa Nini Huduma ya Nyumba kwa Nyumba Ni ya Maana Sasa?

“Kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.”—MDO. 5:42.

1, 2. (a) Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa sababu wanatumia njia gani ya kuhubiri? (b) Tutazungumzia nini katika habari hii?

JAMBO hili linatukia katika mataifa mengi sana duniani. Watu wawili waliovalia vizuri wanakaribia nyumba fulani ili kumpa mwenye nyumba ujumbe mfupi wa Biblia kuhusu Ufalme wa Mungu. Akipendezwa na ujumbe huo, watu hao wanaweza kumwachia vichapo vinavyozungumzia Biblia na kumweleza kuhusu mpango wa kujifunza Biblia nyumbani bila malipo. Kisha wanaenda kwenye nyumba inayofuata. Ikiwa unashiriki katika kazi hiyo, inaelekea kwamba mara nyingi watu wanatambua kwamba wewe ni Shahidi wa Yehova hata kabla hujaanza kuzungumza. Ndiyo, inajulikana kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wanaohubiri nyumba kwa nyumba.

2 Tunatumia njia mbalimbali kutimiza agizo la Yesu la kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Tunahubiri sokoni, barabarani, na katika maeneo mengine ya watu wote. (Mdo. 17:17) Tunawahubiria wengi kupitia simu na barua. Tunawaeleza kweli za Biblia watu ambao tunakutana nao katika shughuli zetu za kila siku. Hata tuna kituo rasmi cha Intaneti, ambacho kinawawezesha watu kupata habari za Biblia katika lugha zaidi ya 300. * Njia hizo zote zina matokeo mazuri. Lakini, katika sehemu nyingi, njia yetu kuu ya kueneza habari njema ni kuhubiri nyumba kwa nyumba. Ni nini msingi wa njia hiyo ya kuhubiri? Kwa nini watu wa Mungu katika nyakati za sasa walianza kuitumia sana njia hiyo? Na kwa nini ni ya maana sasa?

Njia Ambayo Mitume Walitumia

3. Yesu aliwapa mitume wake maagizo gani kuhusu kuhubiri, na hilo linaonyesha nini kuhusu jinsi ambavyo wangehubiri?

3 Njia ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ina msingi wa Kimaandiko. Yesu alipowatuma mitume kuhubiri, aliwaagiza hivi: “Katika jiji lolote lile au kijiji chochote kile mtakapoingia, tafuteni ni nani humo anayestahili.” Wangetumia njia gani kuwatafuta wale wanaostahili? Yesu aliwaambia waende kwenye nyumba za watu, aliposema hivi: “Mnapoingia ndani ya nyumba, wapeni salamu watu wa nyumba hiyo; na ikiwa nyumba hiyo inastahili, acheni amani mnayoitakia ikae juu yake.” Je, wangeenda kwenye nyumba hizo bila kualikwa mapema? Ona maneno ya Yesu yanayofuata: “Popote pale ambapo mtu hawakaribishi au hasikilizi maneno yenu, mnapoondoka katika nyumba hiyo au jiji hilo yakung’uteni mavumbi kutoka miguuni penu.” (Mt. 10:11-14) Maagizo hayo yanaonyesha wazi kwamba mitume ‘walipopita katika eneo hilo kutoka kijiji mpaka kijiji, wakitangaza habari njema,’ walipaswa kuwatembelea watu katika nyumba zao bila kualikwa mapema.—Luka 9:6.

4. Ni wapi katika Biblia ambapo huduma ya nyumba kwa nyumba inatajwa waziwazi?

4 Biblia inataja waziwazi kwamba mitume walihubiri nyumba kwa nyumba. Kwa mfano, andiko la Matendo 5:42 linasema hivi kuwahusu: “Kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.” Miaka 20 hivi baadaye, mtume Paulo aliwakumbusha hivi wanaume wazee wa kutaniko la Efeso: “Sikuepuka kuwaambia ninyi lolote kati ya mambo yenye faida wala kuwafundisha ninyi hadharani na nyumba kwa nyumba.” Je, Paulo aliwatembelea wazee hao kabla hawajawa waamini? Inaonekana alifanya hivyo, kwa kuwa kati ya mambo mengi aliyowafundisha, aliwafundisha pia “juu ya toba kwa Mungu na imani katika Bwana wetu Yesu.” (Mdo. 20:20, 21) Kitabu kimoja (Word Pictures in the New Testament cha Robertson) kinasema hivi kuhusu andiko la Matendo 20:20: “Ni jambo la pekee kuona kwamba mhubiri huyu mkubwa zaidi alihubiri nyumba kwa nyumba.”

Jeshi la Nzige Leo

5. Unabii wa Yoeli unasema nini kuhusu kazi ya kuhubiri?

5 Ushahidi uliotolewa katika karne ya kwanza ulionyesha kimbele kazi kubwa zaidi ambayo ingefanywa katika siku zetu. Nabii Yoeli alilinganisha kazi ya kuhubiri ya Wakristo watiwa-mafuta na uharibifu unaosababishwa na wadudu, kutia ndani nzige. (Yoe. 1:4) Nzige hao wanaosonga kama jeshi, wanashinda vizuizi, wanaingia ndani ya nyumba, na kuharibu kila kitu wanachokuta njiani. (Soma Yoeli 2:2, 7-9.) Hilo linaonyesha waziwazi jinsi ambavyo watu wa Mungu leo wangetimiza kazi ya kutoa ushahidi kwa uvumilivu na kwa ukamili! Huduma ya nyumba kwa nyumba ndiyo njia kuu ambayo Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao wa “kondoo wengine” wanatumia ili kutimiza unabii huo. (Yoh. 10:16) Sisi, Mashahidi wa Yehova, tulianza namna gani kutumia njia hiyo ya kuhubiri iliyotumiwa na mitume?

6. Katika mwaka wa 1922, ni himizo gani ambalo lilitolewa kuhusu kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba, lakini wengine waliitikia jinsi gani?

6 Tangu mwaka wa 1919, imekaziwa kwamba kila Mkristo ana wajibu wa kushiriki katika kazi ya kutoa ushahidi. Kwa mfano, habari yenye kichwa “Utumishi Ni wa Lazima” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1922, iliwakumbusha Wakristo watiwa-mafuta kwamba ni jambo la maana “kuwa na bidii katika kuwapelekea watu vichapo na kuzungumza nao kwenye nyumba zao, na kutoa ushahidi kwamba ufalme wa mbinguni uko karibu.” Habari zaidi zilitolewa katika kichapo Bulletin (sasa ni Huduma Yetu ya Ufalme). Hata hivyo, mwanzoni ni watu wachache waliohubiri nyumba kwa nyumba. Wengine walisita kufanya hivyo. Walitoa sababu mbalimbali, lakini tatizo kuu lilikuwa kwamba wengine wao waliona kuwa kuhubiri nyumba kwa nyumba ni kujishushia heshima. Utumishi wa shambani ulipozidi kukaziwa, wengi wao waliacha hatua kwa hatua kushirikiana na tengenezo la Yehova.

7. Katika miaka ya 1950, ni uhitaji gani ulioonekana wazi?

7 Katika makumi ya miaka yaliyofuata, wengi zaidi walianza kuhubiri. Hata hivyo, ikawa wazi zaidi kwamba mazoezi zaidi ya kibinafsi yalihitajiwa katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Kwa mfano, fikiria hali ilivyokuwa katika nchi ya Marekani. Mwanzoni mwa miaka ya 1950, asilimia 28 ya Mashahidi katika nchi hiyo walihubiri tu kwa kugawa trakti au kusimama barabarani wakiwa na magazeti. Zaidi ya asilimia 40 hawakuwa wa kawaida katika kazi ya kuhubiri, kwa sababu miezi ilipita bila wao kuhubiri hata kidogo. Ni jambo gani ambalo lingefanywa ili kuwasaidia Wakristo wote waliojiweka wakfu wahubiri nyumba kwa nyumba?

8, 9. Ni programu gani ya mazoezi iliyoanzishwa mwaka wa 1953, nayo imekuwa na matokeo gani?

8 Katika kusanyiko la kimataifa lililofanywa huko New York City mwaka wa 1953, huduma ya nyumba kwa nyumba ilikaziwa sana. Ndugu Nathan H. Knorr alitangaza kwamba kazi kuu ya waangalizi wote Wakristo ni kumsaidia kila Shahidi awe mhudumu wa kawaida katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Alisema hivi: ‘Kila mtu anapaswa kuwa na uwezo wa kuhubiri habari njema nyumba kwa nyumba.’ Programu ya ulimwenguni pote ya mazoezi ilianzishwa ili kutimiza kusudi hilo. Wale ambao hawakuwa wameanza kuhubiri nyumba kwa nyumba walizoezwa kuwahubiria watu kwenye nyumba zao, kuwasadikisha kwa kutumia Biblia, na kujibu maswali yao.

9 Programu hiyo ya mazoezi ilikuwa na matokeo mazuri ajabu. Katika kipindi cha miaka kumi tu, hesabu ya wahubiri ulimwenguni pote iliongezeka kwa asilimia 100, hesabu ya ziara za kurudia kwa asilimia 126, na mafunzo ya Biblia kwa asilimia 150. Leo, karibu wahubiri wa Ufalme milioni saba wanahubiri habari njema ulimwenguni pote. Ongezeko hilo kubwa ni jambo moja linalothibitisha kwamba Yehova amebariki jitihada za watu wake katika huduma ya nyumba kwa nyumba.—Isa. 60:22.

Kuwatia Watu Alama kwa Ajili ya Wokovu

10, 11. (a) Ezekieli alipata maono gani ambayo yameandikwa katika Ezekieli sura ya 9? (b) Maono hayo yanatimia kwa njia gani leo?

10 Maono fulani ambayo nabii Ezekieli alipata yanaonyesha jinsi ambavyo huduma ya nyumba kwa nyumba ni ya maana. Katika maono hayo, Ezekieli anaona wanaume sita wakiwa wamebeba silaha mikononi mwao na mwanamume wa saba ambaye amevaa kitani huku akiwa na kidau cha wino kiunoni. Mwanamume huyo wa saba anaambiwa ‘apite katikati ya jiji’ na ‘kutia alama kwenye mapaji ya uso ya watu wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanywa katikati yake.’ Baada ya kazi hiyo ya kutia alama, wale wanaume sita wenye silaha za kuua wanaagizwa wawaangamize watu wote ambao hawana alama.—Soma Ezekieli 9:1-6.

11 Tunajua kwamba katika utimizo wa unabii huo, yule mwanamume “aliyevaa kitani” anawakilisha mabaki ya Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho. Kupitia kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, jamii ya watiwa-mafuta inawatia alama ya mfano wale wanaokuwa sehemu ya “kondoo wengine” wa Kristo. (Yoh. 10:16) Alama hiyo ni nini? Ni uthibitisho, ambao ni kana kwamba uko kwenye mapaji yao yasiyofunikwa, unaoonyesha kwamba kondoo hao ni wanafunzi wa Yesu Kristo waliojiweka wakfu na kubatizwa na kwamba wamevaa utu mpya ulio kama wa Kristo. (Efe. 4:20-24) Watu hao walio kama kondoo wanakuwa kundi moja pamoja na Wakristo watiwa-mafuta na wanawasaidia katika kazi yao ya maana ya kuwatia wengine alama.—Ufu. 22:17.

12. Maono ya Ezekieli kuhusu kutia alama kwenye mapaji ya uso yanakazia jinsi gani umuhimu wa jitihada zetu za kuendelea kuwatafuta watu walio kama kondoo?

12 Maono ya Ezekieli yanakazia sababu moja inayoonyesha kwa nini jitihada zetu za kuendelea kuwatafuta watu “wanaougua na kulia” ni za haraka sana. Uhai wa watu uko hatarini. Hivi karibuni, majeshi ya mbinguni ya kutekeleza hukumu ya Yehova, ambayo yanawakilishwa na wale wanaume sita wenye silaha, yatawaharibu wale ambao hawana ile alama ya mfano. Kuhusiana na hukumu hiyo inayokuja, mtume Paulo aliandika kwamba Bwana Yesu, akiwa na “malaika zake wenye nguvu,” ataleta “kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” (2 The. 1:7, 8) Ona kwamba watu watahukumiwa kulingana na jinsi wanavyoitikia habari njema. Kwa hiyo, ujumbe wa Mungu unapaswa kuendelea kutangazwa kwa bidii mpaka mwisho. (Ufu. 14:6, 7) Hivyo, watumishi wote wa Yehova waliojiweka wakfu wana wajibu mzito sana.—Soma Ezekieli 3:17-19.

13. (a) Mtume Paulo aliona kwamba ana wajibu gani, na kwa nini? (b) Unaona una wajibu gani kuelekea watu wa eneo lenu?

13 Mtume Paulo aliona kwamba yeye binafsi ana wajibu wa kuwahubiria wengine habari njema. Aliandika hivi: “Nina deni kwa Wagiriki na kwa Wabaribari pia, kwa wenye hekima na kwa wasio na akili pia: kwa hiyo nina hamu ya kuitangaza habari njema kwenu pia mlio huko Roma.” (Rom. 1:14, 15) Ili kuonyesha kwamba alithamini rehema alizoonyeshwa, Paulo aliona ni lazima ajaribu kuwasaidia wengine wafaidike kutokana na fadhili zisizostahiliwa za Mungu kama yeye pia alivyokuwa amefaidika. (1 Tim. 1:12-16) Ni kana kwamba alikuwa na deni kwa kila mtu aliyekutana naye, deni ambalo angeweza kulipa ikiwa tu angemhubiria mtu huyo habari njema. Je, wewe pia unaona kwamba una deni kwa watu wa eneo lenu?—Soma Matendo 20:26, 27.

14. Tuna sababu gani kuu ya kuhubiri hadharani na nyumba kwa nyumba?

14 Ingawa kuokoa uhai wa wanadamu ni jambo la maana sana, kuna sababu kubwa zaidi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Katika unabii ulioandikwa kwenye Malaki 1:11, Yehova anatangaza hivi: “Tangu kuchomoza kwa jua mpaka kutua kwake jina langu litakuwa kuu kati ya mataifa, na . . . toleo litafanywa kwa jina langu, pia zawadi safi; kwa kuwa jina langu litakuwa kuu kati ya mataifa.” Katika utimizo wa unabii huo, watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu wanalisifu jina lake hadharani katika dunia yote wanapoendelea kutimiza huduma yao kwa unyenyekevu. (Zab. 109:30; Mt. 24:14) Kumtolea Yehova “dhabihu ya sifa” ndiyo sababu yetu kuu ya kuhubiri hadharani na nyumba kwa nyumba.—Ebr. 13:15.

Matukio ya Maana Sana Yako Mbele Yetu

15. (a) Waisraeli waliongeza utendaji wao jinsi gani walipokuwa wakipiga mwendo kuzunguka Yeriko siku ya saba? (b) Hilo linaonyesha nini kuhusu kazi ya kuhubiri?

15 Ni mambo gani kuhusiana na kazi ya kuhubiri ambayo yangali mbele yetu? Masimulizi ya kitabu cha Yoshua kuhusu kuzingirwa kwa Yeriko yanaonyesha mambo tunayoweza kutazamia. Kumbuka kwamba kabla tu ya Mungu kuharibu Yeriko, Waisraeli waliagizwa wapige mwendo kuzunguka jiji hilo mara moja kila siku kwa siku sita. Hata hivyo, katika siku ya saba, walipaswa kuongeza utendaji wao. Yehova alimwambia Yoshua: “Mpige mwendo kuzunguka jiji mara saba, nao makuhani wazipige pembe. Na itatukia kwamba watakapopiga pembe ya kondoo-dume, . . . watu wote watapaaza kelele kubwa za vita; na ukuta wa jiji utaanguka chini.” (Yos. 6:2-5) Vivyo hivyo, inawezekana kwamba kazi yetu ya kuhubiri itaongezeka. Hakuna shaka kwamba kufikia wakati wa uharibifu wa mfumo huu wa mambo, tutakuwa tumeona ushahidi mkubwa zaidi ukitolewa kuhusu jina la Mungu na Ufalme wake katika historia yote ya ulimwengu huu.

16, 17. (a) Ni jambo gani litakalotimizwa kabla ya “dhiki kuu” kwisha? (b) Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

16 Siku moja, ujumbe ambao tunatangaza utakuwa kama “kelele kubwa za vita.” Katika kitabu cha Ufunuo, ujumbe mkali wa hukumu unafananishwa na “mvua kubwa ya mawe iliyo na kila jiwe lenye uzito wa karibu talanta moja.” * Na andiko la Ufunuo 16:21 linasema: “Pigo lake lilikuwa kubwa isivyo kawaida.” Kwa sasa hatujui huduma ya nyumba kwa nyumba itatimiza nini katika kutangaza ujumbe huo mbalimbali wa mwisho wa hukumu. Lakini tunaweza kuwa na hakika kwamba kabla ya “dhiki kuu” kwisha, jina la Yehova litakuwa limejulishwa kwa mapana na marefu kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya wanadamu.—Ufu. 7:14; Eze. 38:23.

17 Tunapongojea matukio hayo ya maana sana, acheni tuendelee kutangaza habari njema ya Ufalme kwa bidii. Tunapotimiza mgawo huo, ni magumu gani tunayopata katika huduma ya nyumba kwa nyumba, nasi tunaweza kuyashinda kwa njia gani? Maswali hayo yatazungumziwa katika habari inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Anwani ya kituo chetu cha Intaneti ni www.watchtower.org.

^ fu. 16 Ikiwa talanta inayotajwa hapa ni ile ya Wagiriki, basi kila jiwe la mvua lina uzito wa kilo 20 hivi.

Ungesema Nini?

• Kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ina msingi gani wa Kimaandiko?

• Huduma ya nyumba kwa nyumba ilikaziwa jinsi gani katika nyakati za sasa?

• Kwa nini watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu wana wajibu wa kuhubiri?

• Ni matukio gani ya maana sana yaliyo mbele yetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 4]

Kama mtume Paulo, je, unaona kwamba una wajibu wa kuwahubiria wengine?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Ndugu Knorr, mwaka wa 1953