Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Barua kwa Wakorintho

Mambo Makuu Katika Barua kwa Wakorintho

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Barua kwa Wakorintho

MTUME Paulo anahangaikia sana hali ya kiroho ya kutaniko la Korintho. Amesikia kwamba kuna migawanyiko kati ya ndugu huko. Upotovu wa maadili unaachiliwa. Pia, kutaniko limemwandikia Paulo ili kuomba mwongozo kuhusu mambo fulani. Hivyo, yapata mwaka wa 55 W.K., Paulo anapokuwa Efeso wakati wa safari yake ya tatu ya umishonari, anaandika barua yake ya kwanza kati ya barua zake mbili kwa Wakorintho.

Barua ya pili, ambayo inaelekea iliandikwa miezi michache tu baada ya barua ya kwanza, inaendeleza mawazo ya barua ya kwanza. Kwa kuwa hali za ndani na za nje za kutaniko la Korintho la karne ya kwanza zinalingana kwa njia nyingi na za nyakati zetu, ujumbe wa barua za Paulo kwa Wakorintho ni wa maana sana kwetu.—Ebr. 4:12.

‘KAENI MACHO, SIMAMENI IMARA, IWENI NA NGUVU’

(1 Kor. 1:1–16:24)

Paulo anahimiza hivi: “Nyote mseme kwa upatano.” (1 Kor. 1:10) ‘Hakuna msingi mwingine wowote kuliko Yesu Kristo,’ ambao juu yake sifa za Kikristo zinajengwa. (1 Kor. 3:11-13) Kuhusu mwasherati katika kutaniko, Paulo anasema hivi: “Ondoeni yule mtu mwovu kati yenu.” (1 Kor. 5:13) “Mwili si kwa ajili ya uasherati,” anasema, “bali kwa ajili ya Bwana.”—1 Kor. 6:13.

Ili kujibu “mambo ambayo [waliandika],” Paulo anatoa mashauri mazuri kuhusu ndoa na useja. (1 Kor. 7:1) Baada ya kueleza kuhusu ukichwa wa Kikristo, utaratibu kwenye mikutano ya Kikristo, na uhakikisho wa ufufuo, Paulo anatoa himizo hili: “Kaeni macho, simameni imara katika imani, endeleeni kuwa kama wanaume, iweni na nguvu.”—1 Kor. 16:13.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:21—Je, ni kweli kwamba Yehova anatumia “upumbavu” ili kuwaokoa waamini? Hapana, hafanyi hivyo. Hata hivyo, kwa kuwa “ulimwengu kupitia hekima yake haukuja kumjua Mungu,” njia anazotumia ili kuwaokoa watu zinaonekana kuwa upumbavu kwa ulimwengu.—Yoh. 17:25.

5:5—Ni nini maana ya maneno, “mkamkabidhi mtu [mwovu] kwa Shetani kwa ajili ya kuangamizwa kwa mwili, ili roho iokolewe”? Mtu anayezoea kutenda dhambi nzito bila kutubu anapotengwa na kutaniko, anakuwa tena sehemu ya ulimwengu mwovu wa Shetani. (1 Yoh. 5:19) Hivyo, inasemwa kuwa amekabidhiwa kwa Shetani. Kutengwa kwa mtu huyo kunaharibu au kunaondoa uvutano mbaya wa mtu huyo katika kutaniko na kunalinda roho au mtazamo wa kutaniko.—2 Tim. 4:22.

7:33, 34—Ni nini maana ya “mambo ya ulimwengu” ambayo mwanamume au mwanamke anayefunga ndoa anahangaikia? Paulo anazungumza kuhusu mambo ya maisha ya kila siku ambayo Wakristo waliofunga ndoa wanahitaji kuhangaikia. Mambo hayo yanatia ndani chakula, mavazi, na makao, lakini hayahusishi mambo mabaya ya ulimwengu ambayo Wakristo wanakataa.—1 Yoh. 2:15-17.

11:26—Ni kwa njia gani kifo cha Yesu kinapaswa kuadhimishwa “kila mara,” nacho kinapaswa kuadhimishwa “mpaka” wakati gani? Paulo hakuwa akisema kwamba kifo cha Yesu kingeadhimishwa mara nyingi. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “kila mara” linamaanisha “wakati wowote ambapo” au “kila wakati ambapo.” Hivyo, Paulo alikuwa akisema kwamba kila mara Wakristo watiwa-mafuta wanapokula mkate na kunywa divai ya Ukumbusho, mara moja kwa mwaka siku ya Nisani 14, ‘wanatangaza kifo cha Bwana.’ Wanafanya hivyo “mpaka atakapofika,” yaani, mpaka atakapowapokea mbinguni kupitia ufufuo.—1 The. 4:14-17.

13:13—Ni katika njia gani upendo ni mkuu kuliko imani na tumaini? Wakati “mambo yanayotumainiwa” yanapotimia na “tarajio lililohakikishwa” la mambo hayo linapotimizwa, imani na tumaini zinafikia mwisho wake. (Ebr. 11:1) Upendo ni mkuu kuliko imani na tumaini katika maana ya kwamba upendo unadumu milele.

15:29—Inamaanisha nini ‘kubatizwa kwa kusudi la kuwa wafu’? Paulo hakuwa akipendekeza kwamba watu walio hai wabatizwe kwa ajili ya wale waliokufa bila kubatizwa. Hapa Paulo anazungumza kuhusu kubatizwa kwa Wakristo watiwa-mafuta katika maisha yanayohusisha kushika utimilifu mpaka wanapokufa na kufufuliwa kwenye uhai wa roho.

Mambo Tunayojifunza:

1:26-31; 3:3-9; 4:7. Kujisifu katika Yehova kwa unyenyekevu, badala ya kujisifu wenyewe, kunadumisha umoja katika kutaniko.

2:3-5. Alipokuwa akihubiri huko Korintho, kituo cha elimu na falsafa ya Kigiriki, huenda Paulo alihangaikia ikiwa angeweza kuwashawishi wasikilizaji wake. Hata hivyo, hakuruhusu udhaifu wowote au woga ambao huenda alikuwa nao umzuie asitimize huduma aliyopewa na Mungu. Vivyo hivyo, hatupaswi kuruhusu hali zisizo za kawaida zituzuie tusitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu. Kama Paulo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatusaidia.

2:16. Kuwa na “akili ya Kristo” ni kujua njia yake ya kufikiri, kufikiri kama anavyofikiri, kuelewa kabisa utu wake, na kuiga kielelezo chake. (1 Pet. 2:21; 4:1) Ni jambo la maana kama nini kujifunza kwa uangalifu maisha na huduma ya Yesu!

3:10-15; 4:17. Tunapaswa kuchunguza na kuboresha uwezo wetu wa kufundisha na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Ikiwa hatufundishi vizuri, huenda wanafunzi wetu wakashindwa na majaribu ya imani, na huenda tukapata hasara kubwa hivi kwamba tutaokolewa “kama kupitia katika moto.”

6:18. ‘Kukimbia uasherati’ si kuepuka tu matendo ya por·neiʹa bali pia ponografia (picha au habari za ngono), uchafu wa kiadili, mawazo mapotovu, kuwachezea wengine kimapenzi—jambo lolote ambalo linaweza kuongoza kwenye uasherati.—Mt. 5:28; Yak. 3:17.

7:29. Wenzi wa ndoa wanapaswa kuwa waangalifu ili wasihangaikiane sana na hivyo kukosa kutanguliza mambo ya Ufalme.

10:8-11. Yehova alikasirika sana Waisraeli walipomnung’unikia Musa na Haruni. Ni jambo la hekima kuepuka kusitawisha zoea la kunung’unika.

16:2. Tutatoa michango ya pesa kwa ukawaida ili kuendeleza kazi ya Ufalme ikiwa tutafanya mipango mapema na kutoa michango hiyo.

‘ENDELEENI KUREKEBISHWA UPYA’

(2 Kor. 1:1–13:14)

Paulo anawaambia Wakorintho kwamba wanapaswa “kumsamehe kwa fadhili na kumfariji” mkosaji aliyetubu ambaye amekaripiwa. Ingawa barua yake ya kwanza iliwahuzunisha, Paulo anashangilia kwa sababu ‘walihuzunishwa kufikia kutubu.’—2 Kor. 2:6, 7; 7:8, 9.

‘Kama vile wanavyozidi katika kila jambo,’ Paulo anawatia moyo Wakorintho ‘kuzidi katika utoaji.’ Baada ya kuwajibu wapinzani, anatoa shauri la mwisho kwa wote: “Endeleeni kushangilia, kurekebishwa upya, kufarijiwa, kufikiri kwa upatano, kuishi kwa amani.”—2 Kor. 8:7; 13:11.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:15, 16—Sisi ni “harufu tamu ya Kristo” jinsi gani? Inakuwa hivyo kwa sababu tunashikamana na Biblia na tunahubiri ujumbe wake. Ingawa huenda ‘harufu hiyo nzuri’ ikawa yenye kuchukiza kwa watu wasio waadilifu, ni tamu kwa Yehova na watu wenye mioyo minyoofu.

5:16—Ni kwa njia gani Wakristo watiwa-mafuta ‘hawamjui mtu yeyote kulingana na mwili’? Hawawatazami watu kwa njia ya kimwili, yaani, kuonyesha upendeleo kwa sababu ya utajiri, rangi ya ngozi, au jamii au taifa la mtu. Jambo la maana kwao ni uhusiano wao wa kiroho pamoja na waamini wenzao.

11:1, 16; 12:11—Je, Paulo alikosa usawaziko kuelekea Wakorintho? Hapana. Hata hivyo, huenda watu wengine walifikiri kwamba alikuwa akijisifu na kukosa usawaziko kwa sababu ya yale aliyolazimika kusema ili kutetea utume wake.

12:1-4—Ni nani ‘aliyenyakuliwa kuingia katika paradiso’? Kwa kuwa Biblia haisemi kuhusu mtu mwingine ambaye alipata maono hayo na kwa vile Paulo alisema maneno hayo baada ya kutetea utume wake, inaelekea alikuwa akisimulia mambo aliyoyaona. Inaelekea mtume huyo alipata maono ya paradiso ya kiroho ambayo kutaniko la Kikristo linafurahia ‘wakati huu wa mwisho.’—Dan. 12:4.

Mambo Tunayojifunza:

3:5. Kanuni inayopatikana katika andiko hilo inaonyesha kwamba Yehova ndiye anayefanya Wakristo wastahili kwa ajili ya huduma kupitia Neno lake, roho yake takatifu, na sehemu ya kidunia ya tengenezo lake. (Yoh. 16:7; 2 Tim. 3:16, 17) Tunapaswa kujifunza kwa bidii Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia, kusali daima ili tupewe roho takatifu, na kuhudhuria na kushiriki kwa ukawaida katika mikutano ya Kikristo.—Zab. 1:1-3; Luka 11:10-13; Ebr. 10:24, 25.

4:16. Kwa kuwa Yehova anafanya upya ‘mtu tuliye kwa ndani siku baada ya siku,’ tunapaswa kutumia kwa ukawaida maandalizi ya Yehova, na kutoacha siku ipite bila kufikiria mambo ya kiroho.

4:17, 18. Kukumbuka kwamba “dhiki ni ya dakika na ni nyepesi” kunaweza kutusaidia kubaki waaminifu kwa Yehova wakati wa taabu.

5:1-5. Paulo anaonyesha kwa njia nzuri kama nini hisia za Wakristo watiwa-mafuta kuhusu tumaini lao la kimbingu!

10:13. Kwa kawaida, tunapaswa kuhubiri tu katika eneo ambalo kutaniko letu limegawiwa isipokuwa mipango fulani hususa ifanywe ya kusaidia mahali penye uhitaji mkubwa.

13:5. Ili ‘kujijaribu kama sisi tuko katika imani,’ tunapaswa kuhakikisha kwamba mwenendo wetu unapatana na mambo tunayojifunza katika Biblia. Ili ‘kuthibitisha jinsi sisi wenyewe tulivyo,’ tunapaswa kupima hali yetu ya kiroho, kutia ndani uwezo wa kutumia ‘nguvu zetu za ufahamu’ na wingi wa matendo yetu ya imani. (Ebr. 5:14; Yak. 1:22-25) Tukifuata mashauri mazuri ya Paulo, tunaweza kuendelea kutembea katika njia ya ile kweli.

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Ni nini maana ya maneno “kila mara mnapokula mkate huu na kunywa kikombe hiki”?—1 Kor. 11:26