Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Mungu Ndiye Anayeikuza’!

‘Mungu Ndiye Anayeikuza’!

‘Mungu Ndiye Anayeikuza’!

“Yeye anayepanda si kitu wala yeye anayetia maji, bali Mungu anayeikuza.”—1 KOR. 3:7.

1. Sisi ni “wafanyakazi wenzi wa Mungu” kwa njia gani?

“WAFANYAKAZI wenzi wa Mungu.” Hivyo ndivyo mtume Paulo alivyosema kuhusu kazi ya pekee ambayo sote tunaweza kufanya. (Soma 1 Wakorintho 3:5-9.) Paulo alikuwa akizungumzia kazi ya kufanya wanafunzi. Alilinganisha kazi hiyo na kazi ya kupanda mbegu na kuzitia maji. Tunahitaji msaada wa Yehova ili tufanikiwe katika kazi hiyo ya maana. Paulo anatukumbusha kwamba ‘Mungu ndiye anayeikuza.’

2. Kwa nini ukweli wa kwamba ‘Mungu ndiye anayeikuza’ unatusaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu huduma yetu?

2 Ukweli huo wenye kunyenyekeza unatusaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu huduma yetu. Huenda tukahubiri na kufundisha kwa bidii sana, lakini mwishowe Yehova ndiye anayestahili kusifiwa mwanafunzi mpya anapokua kiroho. Kwa nini? Kwa sababu hata tukijitahidi kadiri gani, hakuna yeyote kati yetu anayeweza kuelewa kikamili jinsi mtu anavyokua kiroho, na bila shaka hatuna uwezo wa kuongoza ukuzi huo. Mfalme Sulemani alieleza kwa usahihi jambo hilo alipoandika hivi: “Hujui kazi ya Mungu wa kweli, anayefanya mambo yote.”—Mhu. 11:5.

3. Kazi ya kupanda mbegu halisi inalingana namna gani na kazi ya kufanya wanafunzi?

3 Je, kazi yetu inafadhaisha kwa sababu hatuwezi kuelewa ukuzi wa kiroho? Hapana. Badala yake, hilo linafanya kazi yetu iwe yenye kusisimua na kupendeza. Mfalme Sulemani alisema hivi: “Asubuhi panda mbegu zako na mpaka jioni usiache mkono wako upumzike; kwa maana hujui ni wapi hii itafanikiwa, hapa au pale, au ikiwa zote mbili zitakuwa njema.” (Mhu. 11:6) Kwa kweli, tunapopanda mbegu halisi, hatujui kama itachipuka au mahali itakapochipukia. Kuna mambo mengi kuhusu ukuzi ambayo hatuwezi kuyaongoza. Ndivyo ilivyo na kazi ya kufanya wanafunzi. Yesu alikazia uhakika huo katika mifano miwili ambayo iliandikwa kwa ajili yetu katika sura ya 4 ya Injili ya Marko. Acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mifano hiyo miwili.

Udongo wa Aina Mbalimbali

4, 5. Eleza kwa ufupi mfano wa Yesu wa mpandaji anayetawanya mbegu.

4 Katika Marko 4:1-9, Yesu anaeleza kuhusu mpandaji ambaye anapanda au kutawanya mbegu ambazo zinaanguka katika sehemu mbalimbali: “Sikilizeni. Tazama! Mpandaji alienda kupanda. Naye alipokuwa akipanda, mbegu fulani zikaanguka kando ya barabara, na ndege wakaja wakazila. Na mbegu nyingine zikaanguka mahali penye miamba ambapo, bila shaka, hapakuwa na udongo mwingi, nazo zikachipuka mara moja kwa sababu ya kutokuwa na udongo wenye kina. Lakini jua lilipochomoza, zikaungua, na kwa sababu hazikuwa na mzizi zikanyauka. Na mbegu nyingine zikaanguka katikati ya miiba, na ile miiba ikamea na kuzisonga, nazo hazikuzaa tunda lolote. Lakini nyingine zikaanguka kwenye udongo mzuri, nazo zikamea na kuongezeka, zikaanza kuzaa matunda, nazo zilikuwa zikizaa matunda 30, na 60 na 100.”

5 Katika nyakati za Biblia, kwa kawaida mbegu zilipandwa kwa kutawanywa. Mpandaji alibeba mbegu katika upindo wa nguo yake au katika chombo fulani na kuzitawanya kwa kuzirusha kutoka upande mmoja hadi mwingine. Kwa hivyo, katika mfano huo, mpandaji hapandi mbegu kimakusudi kwenye udongo wa aina mbalimbali. Badala yake, mbegu anazotawanya zinaanguka sehemu tofauti-tofauti.

6. Yesu alieleza jinsi gani mfano wa mpandaji?

6 Hatuhitaji kukisia maana ya mfano huo. Yesu alieleza maana yake katika andiko la Marko 4:14-20: “Mpandaji hulipanda neno. Basi, hawa ndio wale walio kando ya barabara ambapo lile neno limepandwa, lakini mara tu baada ya kulisikia Shetani huja na kuliondoa neno lililopandwa ndani yao. Vivyo hivyo hawa ndio wale waliopandwa mahali penye miamba: mara tu baada ya kulisikia neno, wanalipokea kwa shangwe. Lakini hawana mzizi ndani yao wenyewe, bali wao huendelea kuwako kwa wakati fulani; kisha mara tu dhiki au mateso yanapotokea kwa sababu ya lile neno, wao hukwazika. Bado kuna wengine wanaopandwa katikati ya miiba; hawa ndio ambao wamelisikia neno, lakini mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu za utajiri na tamaa za mambo yale mengine hupenya na kulisonga neno, nalo hukosa kuzaa matunda. Mwishowe, wale waliopandwa kwenye udongo mzuri ndio wale wanaolisikiliza neno na kulipokea vizuri na kuzaa matunda mara 30 na 60 na 100.”

7. Mbegu na udongo wa aina mbalimbali unawakilisha nini?

7 Ona kwamba Yesu hasemi kwamba mbegu zinazopandwa ni za aina mbalimbali. Badala yake, anazungumzia mbegu ya aina moja ambayo inaanguka kwenye udongo wa aina mbalimbali, na kila moja inakuwa na matokeo tofauti. Udongo wa kwanza ni mgumu au umeshindiliwa; wa pili hauna kina; wa tatu umejaa miiba; na wa nne ni udongo mzuri na unatokeza mazao mengi. (Luka 8:8) Mbegu ni nini? Ni ujumbe wa Ufalme ulio katika Neno la Mungu. (Mt. 13:19) Udongo wa aina mbalimbali unawakilisha nini? Watu wenye mioyo yenye hali tofauti-tofauti.—Soma Luka 8:12, 15.

8. (a) Mpandaji anawakilisha nani? (b) Kwa nini watu wanaohubiriwa kuhusu Ufalme wanaitikia kwa njia mbalimbali?

8 Mpandaji anawakilisha nani? Anawakilisha wafanyakazi wenzi wa Mungu, ambao wanatangaza habari njema ya Ufalme. Wanapanda na kutia maji kama Paulo na Apolo walivyofanya. Lakini hata ingawa wanafanya kazi kwa bidii, matokeo wanayopata yanatofautiana. Kwa nini? Kwa sababu ya hali tofauti-tofauti za mioyo ya wale wanaosikiliza ujumbe huo. Katika mfano huo, mpandaji hawezi kamwe kuamua matokeo. Hilo linawafariji kama nini hasa ndugu na dada waaminifu ambao wamehubiri kwa miaka mingi, wengine wao kwa makumi ya miaka, bila kupata matokeo mengi mazuri! * Kwa nini?

9. Mtume Paulo na Yesu walikazia ukweli gani wenye kufariji?

9 Uaminifu wa mpandaji haupimwi kwa matokeo ya kazi yake. Paulo alikazia jambo hilo aliposema hivi: “Kila mtu atapokea thawabu yake mwenyewe kulingana na kazi yake mwenyewe.” (1 Kor. 3:8) Anapokea thawabu kulingana na kazi, si kulingana na matokeo ya kazi hiyo. Vivyo hivyo, Yesu alikazia jambo hilo wanafunzi wake waliporudi kutoka katika safari ya kuhubiri. Walishangilia sana kwa sababu roho waovu walitiishwa kwao kwa jina la Yesu. Hata ingawa habari hizo zilikuwa zenye kusisimua sana, Yesu aliwaambia hivi: “Msishangilie juu ya hili, kwamba roho wanatiishwa kwenu, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.” (Luka 10:17-20) Hata mahali ambapo huenda mpandaji haoni ongezeko kubwa kwa sababu ya kazi yake, haimaanishi kwamba hajajitahidi sana au si mwaminifu kama wengine. Kwa kadiri kubwa, matokeo yanategemea hali ya moyo wa msikilizaji. Lakini mwishowe, Mungu ndiye anayeikuza!

Daraka la Wale Wanaosikiliza Neno

10. Ni nini kinachoamua ikiwa mtu anayelisikia neno yuko kama udongo mzuri au mbaya?

10 Namna gani wale wanaosikiliza neno? Je, imeamuliwa kimbele jinsi watakavyoitikia? Hapana. Ni juu yao kuchagua ikiwa watakuwa kama udongo mzuri au mbaya. Kwa kweli, hali ya moyo wa mtu inaweza kubadilika na kuwa nzuri au mbaya. (Rom. 6:17) Katika mfano wake, Yesu alisema kwamba “mara tu baada ya [wengine] kulisikia” lile neno, Shetani huja na kuliondoa. Lakini si lazima iwe hivyo. Katika Yakobo 4:7, Wakristo wanatiwa moyo ‘wampinge Ibilisi,’ kisha atawakimbia. Yesu alisema kwamba wengine wanalipokea neno kwa shangwe mwanzoni lakini baada ya muda wanakwazwa kwa sababu hawana “mzizi ndani yao wenyewe.” Lakini watumishi wa Mungu wanahimizwa ‘watie mizizi na kuimarishwa juu ya ule msingi’ ili waweze kufahamu akilini “upana na urefu na kimo na kina, na kuujua upendo wa Kristo ambao unazidi ujuzi.”—Efe. 3:17-19; Kol. 2:6, 7.

11. Mtu anaweza kufanya nini ili mahangaiko na utajiri usilisonge lile neno?

11 Yesu alisema kwamba wengine wanaolisikia neno wanaruhusu “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu za utajiri” zipenye na kulisonga neno. (1 Tim. 6:9, 10) Wanaweza kuepuka jinsi gani hali hiyo? Mtume Paulo anajibu hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana yeye amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’”—Ebr. 13:5.

12. Kwa nini wale ambao ni kama udongo mzuri wanazaa matunda kwa viwango tofauti-tofauti?

12 Mwishowe, Yesu anasema kwamba wale wanaopandwa kwenye udongo mzuri ‘wanazaa matunda 30 na 60 na 100.’ Hata ingawa watu fulani wanaolikubali neno wana hali nzuri ya moyo na wanazaa matunda, mambo ambayo wanatimiza wanapotangaza habari njema yanatofautiana kulingana na hali zao. Kwa mfano, uzee au ugonjwa wenye kudhoofisha unaweza kuwazuia wengine wasifanye mengi katika kazi ya kuhubiri. (Linganisha Marko 12:43, 44.) Vivyo hivyo, huenda mpandaji asiweze kubadili hali hizo, lakini anashangilia anapoona kwamba Yehova ameikuza.—Soma Zaburi 126:5, 6.

Mpandaji Anayelala Usingizi

13, 14. (a) Eleza kwa ufupi mfano wa Yesu wa mtu anayetawanya mbegu. (b) Mpandaji anawakilisha nani, na mbegu ni nini?

13 Katika Marko 4:26-29, tunapata mfano mwingine kuhusu mpandaji: “Katika njia hii ufalme wa Mungu ni kama vile mtu anapotupa mbegu kwenye udongo, naye hulala usingizi usiku na huamka mchana, na ile mbegu huota na hukua na kuwa ndefu, naye hajui ni jinsi gani hasa. Udongo wenyewe hutokeza matunda hatua kwa hatua, kwanza jani, kisha suke, mwishowe nafaka iliyo kamili katika suke. Lakini mara tu matunda yanaporuhusu, yeye huutia mundu, kwa sababu wakati wa mavuno umefika.”

14 Mpandaji huyu ni nani? Watu fulani wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wanaamini kwamba mpandaji huyo ni Yesu mwenyewe. Lakini je, kweli Yesu anaweza kulala usingizi asijue jinsi mbegu inavyokua? Bila shaka, Yesu anajua jinsi mbegu hiyo inavyokua! Kwa hivyo, mpandaji huyu, kama yule aliyetajwa mwanzoni, anawakilisha mtangazaji mmoja-mmoja wa Ufalme, yaani, wale ambao wanapanda mbegu ya Ufalme kwa kuhubiri kwa bidii. Mbegu ambayo inatupwa kwenye udongo ni neno ambalo wanahubiri. *

15, 16. Katika mfano wa mpandaji, Yesu alikazia ukweli gani kuhusu ukuzi halisi na ukuzi wa kiroho?

15 Yesu anasema kwamba mpandaji “hulala usingizi usiku na huamka mchana.” Hilo halimaanishi kwamba mpandaji anapuuza kazi yake. Linaonyesha tu utaratibu wa kawaida wa maisha ambao unafuatwa na watu wengi. Maneno yanayotumiwa katika mstari huo yanaonyesha utaratibu wenye kuendelea wa kufanya kazi mchana na kulala usingizi usiku kwa muda fulani. Yesu alieleza kile kilichotukia wakati huo. Alisema hivi: “Ile mbegu huota na hukua na kuwa ndefu.” Kisha Yesu anaongeza hivi: “Naye hajui ni jinsi gani hasa.” Anakazia uhakika wa kwamba ukuzi unatokea “wenyewe.” *

16 Yesu alikuwa akikazia jambo gani? Ona kwamba anakazia ukuzi na jinsi ambavyo unatukia hatua kwa hatua. “Udongo wenyewe hutokeza matunda hatua kwa hatua, kwanza jani, kisha suke, mwishowe nafaka iliyo kamili katika suke.” (Marko 4:28) Ukuzi huo unatukia hatua kwa hatua. Hauwezi kulazimishwa au kuharakishwa. Ndivyo ilivyo na ukuzi wa kiroho. Unatukia hatua kwa hatua kadiri Yehova anavyoruhusu kweli ikue ndani ya moyo wa mtu ambaye ana mwelekeo unaofaa.—Mdo. 13:48; Ebr. 6:1.

17. Ni nani wanaoshangilia wakati mbegu ya kweli inapozaa matunda?

17 Mpandaji anashiriki jinsi gani katika mavuno “mara tu matunda yanaporuhusu”? Yehova anapofanya kweli ya Ufalme ikue katika mioyo ya wanafunzi wapya, mwishowe upendo wao kwa Mungu unawachochea kujiweka wakfu kwake. Wanaonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa kubatizwa katika maji. Ndugu wanaozidi kufanya maendeleo na kuwa wakomavu wanastahili hatua kwa hatua kupata mapendeleo zaidi katika kutaniko. Matunda ya Ufalme yanavunwa na yule aliyepanda mbegu na vilevile watangazaji wengine wa Ufalme ambao huenda hawakuhusika moja kwa moja katika kupanda mbegu ambayo ilizaa mwanafunzi huyo. (Soma Yohana 4:36-38.) Kwa kweli, ‘mpandaji na mvunaji wanashangilia pamoja.’

Mambo Tunayojifunza Leo

18, 19. (a) Mazungumzo haya kuhusu mifano ya Yesu yamekutia moyo jinsi gani? (b) Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

18 Tumejifunza nini katika mazungumzo yetu kuhusu mifano miwili iliyo katika Marko sura ya 4? Tunaona waziwazi kwamba tuna kazi ya kufanya, yaani, kazi ya kupanda. Hatupaswi kamwe kuruhusu visingizio, matatizo, na magumu ambayo huenda tukapata yatuzuie tusifanye kazi hiyo. (Mhu. 11:4) Hata hivyo, tunatambua pia kwamba tuna pendeleo zuri ajabu la kuhesabiwa kuwa wafanyakazi wenzi wa Mungu. Yehova ndiye anayetokeza ukuzi wa kiroho, na kubariki jitihada zetu na jitihada za wale wanaopokea ujumbe wetu. Tunatambua kwamba hatuwezi kumlazimisha mtu yeyote afanye maendeleo ya kiroho. Kwa hivyo, hatuhitaji kuvunjika moyo au kushuka moyo ikiwa watu hawafanyi maendeleo ya haraka au hawakui kiroho. Inafariji kama nini kujua kwamba mafanikio yetu yanapimwa na uaminifu wetu kwa Yehova na kwa pendeleo ambalo ametupa la kuhubiri “habari njema ya ufalme . . . kuwa ushahidi kwa mataifa yote.”—Mt. 24:14.

19 Yesu alitufundisha nini kingine kuhusu ukuzi wa wanafunzi wapya na kazi ya Ufalme? Jibu la swali hilo linapatikana katika mifano mingine iliyoandikwa katika masimulizi ya Injili. Tutachanganua mifano michache katika habari inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kwa mfano, fikiria huduma ya Ndugu Georg Fjölnir Lindal huko Iceland iliyosimuliwa katika Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2005, ukurasa wa 210-211, na mambo yaliyoonwa ya watumishi waaminifu ambao walivumilia huko Ireland kwa miaka mingi bila kupata matokeo ya haraka, kama yanavyosimuliwa katika Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1988, ukurasa wa 82-99, Kiingereza.

^ fu. 14 Zamani gazeti hili lilieleza kwamba mbegu inawakilisha sifa mbalimbali za watu ambazo zinahitaji kukua na kukomaa, ikitegemea hali za mazingira. Hata hivyo, tunapaswa kutilia maanani kwamba katika mfano wa Yesu mbegu haibadiliki na kuwa mbegu mbaya au tunda ambalo limeoza. Inakua tu na kukomaa.—Ona Mnara wa Mlinzi, Desemba 1, 1980 (1/12/1980), ukurasa wa 14-16 au Juni 15, 1980 (15/6/1980), (Kiingereza) ukurasa wa 17-19 au Septemba 15, 1980 (15/9/1980), (Kifaransa) ukurasa wa 17-19.

^ fu. 15 Neno kama hilo linatumiwa pia katika andiko la Matendo 12:10, ambalo linasema kwamba lango la chuma lilifunguka “lenyewe.”

Je, Unakumbuka?

• Kazi ya kupanda mbegu halisi na kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme zinalingana jinsi gani?

• Yehova anapima jinsi gani uaminifu wa mhubiri wa Ufalme?

• Yesu alikazia ulinganifu gani kati ya ukuzi halisi na ukuzi wa kiroho?

• ‘Mpandaji na mvunaji wanashangilia pamoja’ jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kwa nini Yesu alilinganisha mhubiri wa Ufalme wa Mungu na mpandaji wa mbegu?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wale walio kama udongo mzuri wanashiriki kwa moyo wote katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme kulingana na hali zao

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mungu ndiye anayeendelea kuikuza