Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe na Matarajio Yenye Usawaziko, na Uwe Mwenye Shangwe

Uwe na Matarajio Yenye Usawaziko, na Uwe Mwenye Shangwe

Uwe na Matarajio Yenye Usawaziko, na Uwe Mwenye Shangwe

“NILISHINDWA tena!” Ni mara ngapi umesema jambo kama hilo kwa sababu ulishindwa kutimiza yale uliyopanga kufanya? Mama Mkristo anaweza kusema hivyo kwa sababu anahisi amelemewa sana na kazi ya kumtunza mtoto wake mchanga na anafadhaika kwa sababu hawezi kukazia uangalifu mambo ya kiroho. Huenda Mkristo mwingine akahisi amepungukiwa kwa sababu ya jinsi alivyolelewa na kufikiri kwamba hatimizi mengi katika kutaniko. Shahidi aliyezeeka anaweza kuhisi kwamba ametupwa kwa sababu hawezi kushiriki kikamili katika utendaji mbalimbali wa Kikristo ambao alipenda sana alipokuwa na nguvu. “Nyakati nyingine ninalia ninaposikiliza hotuba ambayo inawatia watu moyo wafanye utumishi wa upainia,” anasema Christiane, ambaye hali yake ya familia inamzuia asitimize mengi katika utumishi wa Yehova kama anavyotaka.

Tunaweza kufanya nini tunapohisi hivyo? Wakristo fulani wamefanya nini ili kuwa na maoni yanayofaa kuhusu hali zao? Kuna faida gani za kuwa na matarajio yenye usawaziko?

Uwe Mwenye Usawaziko

Mtume Paulo anatuambia jinsi tunavyoweza kudumisha shangwe yetu anaposema hivi: “Shangilieni sikuzote katika Bwana. Mara nyingine tena nitasema, Shangilieni! Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Flp. 4:4, 5) Ili kupata shangwe na uradhi tunapomtumikia Mungu, tunahitaji kuwa na matarajio yenye usawaziko ikitegemea uwezo na hali zetu. Tukijitahidi kufikia miradi ambayo hatuwezi kutimiza, tunajiletea mikazo isiyo ya lazima. Kwa upande mwingine, tunapaswa kuwa waangalifu tusijihurumie sana, huku tukitumia udhaifu wetu kuwa kisingizio cha kupunguza bidii yetu isivyo lazima katika huduma ya Kikristo.

Haidhuru hali zetu, Yehova anataka tumpe kilicho bora zaidi, yaani, tumtumikie kwa nafsi yetu yote na kwa moyo wetu wote. (Kol. 3:23, 24) Ikiwa hatumpi Yehova kilicho bora zaidi, hatutakuwa tukiishi kulingana na wakfu wetu. (Rom. 12:1) Zaidi ya hayo, tutakosa uradhi, shangwe ya kweli, na baraka nyingine nyingi za kumtumikia Mungu kwa nafsi yote.—Met. 10:22.

Neno linalotafsiriwa “usawaziko” katika Biblia linadokeza wazo la kuwa mwenye kujali. Kihalisi, linamaanisha kukubali maoni ya wengine. (Yak. 3:17) Pia, neno hilo linamaanisha kutoshikilia maoni kupita kiasi. Hivyo basi, ikiwa tuna usawaziko, tutakuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu hali zetu. Je, ni vigumu kufanya hivyo? Kwa watu fulani ni vigumu, hata ingawa wanaweza kuwajali wengine. Kwa mfano, ikiwa rafiki wa karibu anaonekana amechoka kwa sababu ya kufanya mambo mengi kupita kiasi, je, hatungejaribu kumsaidia aone kwamba ni jambo la hekima kufanya marekebisho fulani katika maisha yake? Vivyo hivyo, tunahitaji kujifunza kutambua mambo yanayoonyesha kwamba tunafanya mengi kupita uwezo wetu.—Met. 11:17.

Inaweza kuwa vigumu zaidi kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu uwezo wetu ikiwa tulilelewa na wazazi wenye kudai mengi sana. Walipokuwa watoto, watu fulani walijilazimisha kufanya mambo mengi zaidi au kufanya vizuri zaidi ili wapendwe na wazazi wao. Ikiwa tulifanya hivyo, huenda tukawa na maoni yasiyofaa kuhusu maoni ya Yehova kutuelekea. Yehova anatupenda kwa sababu tunamtumikia kwa moyo wetu wote. Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba Yehova “analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zab. 103:14) Anajua uwezo wetu na anatupenda tunapomtumikia kwa bidii hata ingawa uwezo wetu una mipaka. Tukikumbuka kwamba Mungu wetu si bwana mkubwa mkali, hilo litatusaidia kuwa na matarajio yenye kiasi, huku tukitambua mipaka ya uwezo wetu.—Mika 6:8.

Hata hivyo, wengine wanaona ni vigumu kuwa na usawaziko. Ikiwa unaona hivyo, kwa nini usimwombe Mkristo mwenye uzoefu ambaye anakujua vizuri akusaidie? (Met. 27:9) Kwa mfano, je, unataka kutumika ukiwa painia wa kawaida? Huo ni mradi mzuri sana! Je, unashindwa kuufikia? Labda unahitaji msaada ili kurahisisha maisha yako. Au unaweza kuzungumza na rafiki Mkristo ambaye unamwamini ili akusaidie kuona ikiwa madaraka yako mengi ya kifamilia yanakuruhusu uwe painia wa kawaida kwa sasa. Anaweza kukusaidia uone ikiwa unaweza kutimiza mambo mengine au marekebisho unayoweza kufanya ili utimize mengi zaidi. Pia, mume ana nafasi nzuri ya kumsaidia mke wake kutimiza mambo kulingana na uwezo wake. Kwa mfano, anaweza kupendekeza kwamba mke wake apumzike kabla ya kuanza mwezi mpya wenye shughuli nyingi. Huenda hilo likamtia nguvu na kumzuia asipoteze shangwe yake katika huduma.

Jiwekee Miradi Unayoweza Kutimiza

Umri mkubwa au afya mbaya inaweza kutuzuia tusitimize mengi katika utumishi wa Yehova. Ikiwa wewe ni mzazi, labda unaweza kufikiri kwamba hufaidiki sana na funzo lako la kibinafsi au mikutano ya Kikristo kwa sababu unatumia nguvu na wakati wako mwingi kuwatunza watoto wako. Hata hivyo, je, inawezekana kwamba kukazia fikira udhaifu wako kunakuzuia nyakati nyingine usitambue mambo ambayo bado unaweza kutimiza?

Maelfu ya miaka iliyopita, Mlawi mmoja alieleza tamaa ambayo hangetosheleza. Alikuwa na pendeleo la kutumika majuma mawili kila mwaka kwenye hekalu. Hata hivyo, alieleza jinsi alivyotamani sana kukaa daima karibu na madhabahu. (Zab. 84:1-3) Ni nini kilichomsaidia mwanamume huyo mwaminifu kuridhika? Aliona kwamba ni pendeleo la pekee kuwa katika nyua za hekalu hata kwa siku moja tu. (Zab. 84:4, 5, 10) Vivyo hivyo, badala ya kufikiria sana udhaifu wetu, tunapaswa kujaribu kutambua na kuthamini mambo ambayo tunaweza kutimiza.

Fikiria mfano wa Nerlande, dada Mkristo huko Kanada ambaye anatumia kiti cha magurudumu. Alihisi kwamba hawezi kutimiza mengi sana katika huduma. Hata hivyo, alibadili mtazamo wake kwa kufanya eneo la maduka liwe eneo lake la kuhubiri. Anasema hivi: “Ninaketi katika kiti changu cha magurudumu karibu na kiti kirefu cha mbao katika eneo la maduka. Ninafurahia kuwahubiria watu wanaokuja kuketi ili kupumzika kwa muda.” Kushiriki katika sehemu hiyo muhimu ya huduma kunampa Nerlande uradhi mwingi.

Fanya Marekebisho Ikihitajiwa

Huenda chombo cha tanga kikaenda kwa mwendo wa kasi sana huku upepo ukizisukuma tanga zake. Hata hivyo, kunapokuwa na dhoruba kali, baharia aliye kwenye usukani analazimika kurekebisha tanga zake. Hana uwezo wa kuzuia dhoruba, lakini kwa kufanya marekebisho hayo, huenda akafaulu kukielekeza chombo chake. Vivyo hivyo, mara nyingi hatuna uwezo wa kubadili hali zilizo kama dhoruba tunazokabiliana nazo maishani. Lakini tunaweza kufaulu kuelekeza maisha yetu kwa kadiri tunavyoweza tukifanya marekebisho kuhusu jinsi tunavyotumia uwezo wetu wa kimwili, kiakili, na kihisia. Kufikiria hali zetu mpya kutatusaidia kuendelea kuwa na uradhi na shangwe katika kumtumikia Mungu.—Met. 11:2.

Fikiria mifano hii. Ikiwa hatuna nguvu nyingi, huenda ikafaa kuepuka kufanya kazi zenye kuchosha sana mapema asubuhi ili tuwe na nguvu za kuhudhuria mkutano wa Kikristo jioni. Hilo litatuwezesha kufaidika kikamili na ushirika wa Wakristo wenzetu. Au ikiwa mama hawezi kwenda katika huduma ya nyumba kwa nyumba kwa sababu mtoto wake ni mgonjwa, huenda akaona inafaa kumwalika dada Mkristo nyumbani kwake pamoja na wanafunzi wa Biblia ili ashiriki pamoja naye katika mazungumzo mtoto wake anapolala.

Namna gani ikiwa hali zako hazikuruhusu kujifunza mapema kila jambo ambalo litazungumziwa kwenye mikutano ya kutaniko? Unaweza kuchagua habari ambazo unaweza kutayarisha na kufanya hivyo vizuri iwezekanavyo. Kwa kurekebisha miradi ambayo tunataka kuifikia hivi karibuni, tunaweza kuendelea kuwa watendaji na wenye furaha.

Huenda tukahitaji kuazimia na kujitahidi sana ili kufanya marekebisho kuhusu miradi yetu. Serge na Agnès, wenzi wa ndoa wanaoishi Ufaransa, walihitaji kubadili kabisa mipango yao. “Tulipojua kwamba Agnès ana mimba, ndoto yetu ya kuwa wamishonari ilitoweka,” anasema Serge. Sasa akiwa baba ya wasichana wawili wenye furaha, Serge anaeleza jinsi yeye na mke wake walivyojiwekea mradi mwingine. Anasema: “Kwa kuwa hatungeweza kutumikia katika nchi ya kigeni, tuliamua kuwa ‘wamishonari’ katika nchi yetu wenyewe. Tulijiunga na kikundi cha lugha ya kigeni.” Je, walifaidika kwa kujiwekea mradi huo mpya? Serge anasema: “Tunaona tunathaminiwa sana katika kutaniko.”

Odile, dada Mkristo huko Ufaransa ambaye ana umri wa miaka zaidi ya 70 na aliye na ugonjwa fulani ambao umedhoofisha magoti yake (osteoarthritis), hawezi kusimama kwa muda mrefu. Alivunjika moyo kwa sababu matatizo yake ya kimwili yalimzuia asishiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Hata hivyo, hakukata tamaa. Alifanya marekebisho katika utendaji wake kwa kuhubiri kwa simu. Anasema: “Sikujua kwamba kuhubiri kwa njia hiyo ni rahisi na kunafurahisha sana!” Kutumia njia hiyo ya kuhubiri kulimpa tena nguvu za kuhubiri.

Kuwa na Matarajio Yenye Usawaziko Kunaleta Baraka

Kusitawisha maoni yenye usawaziko kuhusu yale tunayoweza kutimiza kutatuzuia tusifadhaike. Tunapojiwekea miradi yenye usawaziko, tunahisi kwamba tumetimiza jambo fulani hata ingawa hatuwezi kutimiza mengi. Hivyo, tunafurahia mambo ambayo tunatimiza, hata ikiwa ni machache.—Gal. 6:4.

Tunapoendelea kuwa na matarajio yenye usawaziko, tutawajali zaidi Wakristo wenzetu. Tunapotambua kwamba uwezo wao una mipaka, sikuzote tutathamini yale ambayo wanatutendea. Kwa kuthamini msaada wowote ule, tunachangia roho ya ushirikiano na maelewano. (1 Pet. 3:8) Kumbuka kwamba, akiwa Baba mwenye upendo, Yehova hatazamii tufanye mambo yanayopita uwezo wetu. Na tunapokuwa na matarajio yenye usawaziko na kujiwekea miradi ambayo tunaweza kuifikia, tutapata uradhi na shangwe zaidi katika utendaji wetu wa kiroho.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Ili kupata shangwe na uradhi tunapomtumikia Mungu, tunahitaji kuwa na matarajio yenye usawaziko ikitegemea uwezo na hali zetu

[Picha katika ukurasa wa 30]

Nerlande anapata shangwe kwa kufanya yale anayoweza katika huduma

[Picha katika ukurasa wa 31]

Jifunze “kurekebisha tanga”

[Hisani]

© Wave Royalty Free/age fotostock

[Picha katika ukurasa wa 32]

Serge na Agnès walifaidika kwa kujiwekea miradi mipya