Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umefurahia kusoma matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

• Wakristo fulani wamepata matatizo gani mazito baada ya kufunga ndoa, nao wanapaswa kujitahidi kufanya nini?

Huenda Wakristo fulani wakagundua kwamba wako tofauti kabisa na mwenzi wao. Wakijua kwamba kutalikiana bila msingi wa kimaandiko si suluhisho linalokubalika, wanapaswa kujitahidi kabisa kulinda ndoa yao.—4/15, ukurasa wa 17.

• Mkristo aliye katika makao ya kuwatunzia wazee anaweza kukabili hali gani ngumu?

Huenda asijue kutaniko lililo katika eneo hilo. Huenda watu wengi katika makao hayo wana imani tofauti na huenda wakajaribu kumshirikisha katika mambo ya kidini. Watu wa jamaa yake ambao ni Wakristo na washiriki wa kutaniko la karibu wanapaswa kutambua matatizo hayo na wawategemeze na kuwatunza.—4/15, ukurasa wa 25-27.

• Ni hatua gani nne zinazoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa kusuluhisha matatizo?

Pangeni wakati wa kuzungumzia matatizo. (Mhu. 3:1, 7) Eleza maoni yako kwa unyoofu na kwa heshima. (Efe. 4:25) Sikiliza na uelewe hisia za mwenzi wako. (Mt. 7:12) Mkubaliane kuhusu suluhisho, na mshirikiane kupata suluhisho hilo. (Mhu. 4:9, 10)—5/1, ukurasa wa 10-12.

• Yesu alipotuhimiza tusali ili tusamehewe madeni yetu, alimaanisha madeni gani?

Tunapolinganisha Mathayo 6:12 na Luka 11:4 tunaona wazi kwamba Yesu hakumaanisha madeni ya kifedha. Alimaanisha dhambi. Tunahitaji kumwiga Mungu kwa kuwa tayari kusamehe.—5/15, ukurasa wa 9.

• Washiriki wa Baraza Linaloongoza wanatumika katika halmashauri gani mbalimbali?

Halmashauri ya Mratibu; Halmashauri ya Wafanyakazi; Halmashauri ya Utangazaji; Halmashauri ya Utumishi; Halmashauri ya Ufundishaji; Halmashauri ya Uandikaji.—5/15, ukurasawa 29.

• kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Gharika ya Noa ilienea duniani pote?

Yesu aliamini kwamba Gharika hiyo ilikuwapo na ilienea duniani pote. Maonyo ya Biblia yanategemea uhakika wa kuwapo kwa Gharika ulimwenguni pote.—6/1, ukurasa wa 8.

• Je, mwenendo ambao unaelezwa katika Waroma 1:24-32 unawahusu Wayahudi au watu wasio Wayahudi?

Ufafanuzi huo ungeweza kufaa vikundi vyote viwili, lakini mtume Paulo alikuwa hasa akizungumza kuhusu Waisraeli wa zamani ambao kwa karne nyingi walishindwa kufuata Sheria. Walijua amri za uadilifu za Mungu, hata hivyo hawakuishi kupatana na amri hizo.—6/15, ukurasa wa 29.

• Eneo la Tel Aradi liko wapi, na kwa nini ni muhimu?

Kilima hicho kilicho Israel kinaonyesha mahali palipokuwa na jiji la Aradi na kinapatikana upande wa magharibi wa Bahari ya Chumvi. Katika kilima hicho, wachimbuaji wamepata vigae vilivyotumiwa kama mabamba ya kuandikia. Vigae fulani vina majina yanayopatikana katika Biblia, na vinaonyesha kwamba jina la kibinafsi la Mungu lilitumiwa katika maandishi mengi yasiyo ya kidini.—7/1, ukurasa wa 23-24.

• kwa nini kuwa na matarajio yenye usawaziko kunaongeza shangwe yetu?

Tukijitahidi kufikia miradi ambayo hatuwezi kutimiza, tunajiletea mikazo isiyo ya lazima. Hata hivyo, hatupaswi kujihurumia sana na kutumia udhaifu wetu kuwa kisingizio cha kupunguza bidii yetu katika huduma ya Kikristo.—7/15, ukurasa wa 29.

• Ni mambo gani yanayoweza kuwazuia wazazi wasiwasiliane na vijana wao?

Mambo hayo yanaweza kutia ndani kijana kuwa mwenye haya, tamaa ya kujitegemea, na kutaka kuwa peke yake. Wazazi wanaweza kujaribu kuwasiliana na vijana wanapostarehe na kujitahidi kutambua hisia zinazochochea maneno ya kijana.—8/1, ukurasa wa 10-11.