Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unazungumza Ile “Lugha Safi” kwa Ufasaha?

Je, Unazungumza Ile “Lugha Safi” kwa Ufasaha?

Je, Unazungumza Ile “Lugha Safi” kwa Ufasaha?

‘Nitabadilisha lugha ya vikundi vya watu na kuwapa lugha safi, ili wote waliitie jina la Yehova.’—SEF. 3:9.

1. Yehova ametupa zawadi gani nzuri ajabu?

ZAWADI ya lugha haikutokana na wanadamu, bali ilitoka kwa Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu. (Kut. 4:11, 12) Yehova hakumpa mwanadamu wa kwanza, Adamu, uwezo wa kuongea tu bali pia alimpa uwezo wa kutunga na kujifunza maneno mapya. (Mwa. 2:19, 20, 23) Hiyo ni zawadi nzuri ajabu! Imewawezesha wanadamu kuwasiliana na Baba yao wa mbinguni na kulisifu jina lake tukufu.

2. Kwa nini wanadamu hawazungumzi tena lugha moja tu?

2 Katika karne 17 za kwanza tangu mwanadamu alipoumbwa, wanadamu wote walizungumza lugha moja tu, nao walikuwa na “maneno ya namna moja.” (Mwa. 11:1) Kisha, uasi ukatokea katika siku za Nimrodi. Kinyume na maagizo ya Yehova, wanadamu wasio watiifu walikusanyika mahali ambapo baadaye paliitwa Babeli wakiwa wameazimia kubaki katika eneo moja. Walianza kujenga mnara mkubwa sana, na kusudi lao halikuwa kumtukuza Yehova, bali ‘kujifanyia jina maarufu.’ Kwa hiyo, Yehova akavuruga lugha ya asili ya waasi hao na kuwafanya wazungumze lugha mbalimbali. Hivyo, wakatawanywa juu ya uso wote wa dunia.—Soma Mwanzo 11:4-8.

3. Ni nini kilichotokea wakati Yehova alipovuruga usemi wa waasi huko Babeli?

3 Leo, maelfu ya lugha zinazungumzwa ulimwenguni, na hata watu fulani wanasema kwamba lugha zaidi ya 6,800 zinazungumzwa. Kila moja ya lugha hizo ina njia yake ya kupanga mawazo. Hivyo basi, inaonekana kwamba wakati Yehova Mungu alipovuruga usemi wa waasi hao, alifutilia mbali kumbukumbu zozote walizokuwa nazo za ile lugha moja waliyoizungumza kwanza. Zaidi ya kuingiza maneno mapya katika akili zao, alibadili pia njia zao za kufikiri na kutokeza njia mpya za kupanga maneno. Haishangazi kwamba baadaye mahali ambapo mnara huo ulijengwa paliitwa Mvurugo, au “Babeli”! (Mwa. 11:9) Ni Biblia tu inayoeleza kwa njia ya kuridhisha mwanzo wa lugha mbalimbali zilizopo leo.

Lugha Safi na Mpya

4. Yehova alitabiri jambo gani ambalo lingetukia katika siku zetu?

4 Ingawa masimulizi ya Biblia kuhusu jinsi Mungu alivyoingilia kati mambo huko Babeli yanasisimua, jambo fulani lenye kupendeza na la maana hata zaidi limetokea katika siku zetu. Kupitia nabii wake Sefania, Yehova alitabiri hivi: “Ndipo nitakapobadilisha lugha ya vikundi vya watu na kuwapa lugha safi, ili wote waliitie jina la Yehova, wamtumikie bega kwa bega.” (Sef. 3:9) ‘Lugha hiyo safi’ ni nini, nasi tunaweza kufanya nini ili tuizungumze kwa ufasaha?

5. Lugha safi ni nini, na ni matokeo gani ambayo yametokana na badiliko hilo la lugha?

5 Lugha safi ni kweli kumhusu Yehova Mungu na makusudi yake ambayo yanapatikana katika Neno lake, Biblia. “Lugha” hiyo inatia ndani kuelewa kwa usahihi kweli kuhusu Ufalme wa Mungu na jinsi utakavyolitakasa jina la Yehova, kuitetea enzi yake kuu, na kuwaletea wanadamu waaminifu baraka za milele. Ni matokeo gani yanayotokana na badiliko hilo la lugha? Tunaambiwa kwamba watu ‘wataliitia jina la Yehova’ na ‘kumtumikia bega kwa bega.’ Tofauti na mambo yaliyotukia Babeli, badiliko hilo kuelekea lugha safi limeleta sifa kwa jina la Yehova na umoja kati ya watu wake.

Kujifunza Ile Lugha Safi

6, 7. (a) Ni mambo gani yanayohusika katika kujifunza lugha mpya, na mambo hayo yanahusika jinsi gani katika kujifunza ile lugha safi? (b) Tutazungumzia nini sasa?

6 Mtu anapoanza kujifunza lugha nyingine, anahitaji kufanya mengi zaidi ya kukumbuka tu maneno mapya. Kujifunza lugha mpya kunatia ndani kujifunza kufikiri kwa njia tofauti. Njia za kueleza habari na mambo ya kuchekesha zinaweza kuwa tofauti katika lugha nyingine. Ili mtu atamke maneno ya lugha mpya, anapaswa kutumia viungo vya usemi, kama vile ulimi, kwa njia tofauti na ile aliyoizoea. Ndivyo ilivyo tunapoanza kujifunza ile lugha safi ya kweli ya Biblia. Mengi zaidi yanahitajiwa kuliko kujifunza tu mafundisho machache ya msingi ya Biblia. Ili tuijue vizuri lugha hiyo mpya tunahitaji kurekebisha njia yetu ya kufikiri na kufanya upya akili zetu.—Soma Waroma 12:2; Waefeso 4:23.

7 Ni nini kitakachotusaidia kuielewa lugha safi na kuizungumza kwa ufasaha? Kama ilivyo na kujifunza lugha yoyote, kuna mbinu fulani za msingi zinazoweza kutusaidia kuzungumza lugha ya kweli ya Biblia kwa ufasaha. Acheni tuchunguze hatua fulani za msingi ambazo watu wanatumia wanapojifunza lugha nyingine na tuone jinsi hatua hizo zinavyoweza kutusaidia kujifunza lugha hiyo mpya ya mfano.

Kuzungumza Ile Lugha Safi kwa Ufasaha

8, 9. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunataka kujifunza ile lugha safi, na kwa nini hilo ni jambo la maana sana?

8 Sikiliza kwa uangalifu. Mwanzoni, lugha mpya inaweza kusikika kuwa ngeni kabisa kwa mtu ambaye hajapata kuisikia. (Isa. 33:19) Lakini anapoendelea kujifunza kukazia fikira mambo anayosikia, ataanza kuelewa maneno fulani-fulani na njia za kuzungumza. Vivyo hivyo, tunahimizwa hivi: “Ni lazima kwetu kuyakazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo tuliyosikia, ili tusipeperushwe kamwe.” (Ebr. 2:1) Yesu aliwahimiza tena na tena wafuasi wake hivi: “Yule aliye na masikio na asikilize.” (Mt. 11:15; 13:43; Marko 4:23; Luka 14:35) Ndiyo, tunahitaji ‘kusikiliza na kuelewa maana’ ya mambo tunayosikia ili tufanye maendeleo katika kuielewa lugha safi.—Mt. 15:10; Marko 7:14.

9 Ili kusikiliza, tunahitaji kukaza fikira, na kuna faida za kufanya hivyo. (Luka 8:18) Tunapokuwa kwenye mikutano ya Kikristo, je, tunakazia fikira mambo yanayosemwa, au fikira zetu zinatangatanga? Ni jambo la maana tufanye yote tunayoweza kukazia fikira mambo yanayozungumziwa. Tusipofanya hivyo, tunaweza kuwa wazito katika kusikia.—Ebr. 5:11.

10, 11. (a) Zaidi ya kusikiliza kwa uangalifu, tunapaswa kufanya nini? (b) Ni jambo gani lingine linalohusika katika kuzungumza ile lugha safi?

10 Iga wasemaji wenye ufasaha. Zaidi ya kusikiliza kwa uangalifu, watu wanaojifunza lugha mpya wanatiwa moyo pia wajaribu kuiga matamshi ya wasemaji wenye ufasaha na njia yao ya kuzungumza. Hilo linawasaidia watu hao kuepuka matamshi yasiyofaa ambayo huenda baadaye yakawazuia wasizungumze kwa njia inayoeleweka. Vivyo hivyo, tunapaswa kujifunza kutoka kwa wale walio na “ufundi wa kufundisha” lugha hiyo mpya. (2 Tim. 4:2) Omba msaada. Uwe tayari kukubali kurekebishwa unapokosea.—Soma Waebrania 12:5, 6, 11.

11 Kuzungumza ile lugha safi hakuhusishi tu kuamini kweli na kuwafundisha wengine kweli hiyo bali pia kujiendesha kupatana na sheria na kanuni za Mungu. Kuwaiga wengine kutatusaidia kufanya hivyo. Hilo linatia ndani kuiga imani na bidii yao. Pia inatia ndani kuiga jinsi Yesu alivyojiendesha katika maisha yake yote. (1 Kor. 11:1; Ebr. 12:2; 13:7) Tukiendelea kufanya hivyo, tutachangia umoja kati ya watu wa Mungu, na ni kana kwamba tutakuwa tukitamka maneno kwa njia ileile.—1 Kor. 4:16, 17.

12. Kukumbuka mambo kunahusika jinsi gani katika kujifunza lugha mpya?

12 Jitahidi kukumbuka mambo. Watu wanaojifunza lugha nyingine wanahitaji kukumbuka mambo mengi mapya. Hiyo inatia ndani kukumbuka maneno na misemo mipya. Kwa Wakristo, kujitahidi kukumbuka mambo kunaweza kuwa msaada mkubwa katika kuijua vizuri ile lugha safi. Bila shaka, tunapaswa kujitahidi kukumbuka majina ya vitabu vya Biblia kama vinavyofuatana. Wengine wamejiwekea mradi wa kukumbuka maneno ya maandiko fulani ya Biblia au mahali ambapo maandiko fulani yanapatikana. Wengine wameona faida za kujitahidi kukumbuka maneno ya nyimbo za Ufalme, majina ya makabila ya Israeli na ya wale mitume 12, na sifa ambazo ni sehemu ya matunda ya roho. Katika nyakati za zamani, Waisraeli wengi walizijua zaburi neno kwa neno. Katika nyakati za sasa, mvulana mmoja alijifunza mistari zaidi ya 80 ya Biblia neno kwa neno kufikia wakati ambapo alikuwa na umri wa miaka sita tu. Mbona tusitumie vizuri uwezo huo wenye thamani wa kukumbuka mambo?

13. Kwa nini ni jambo la maana sana kurudia-rudia mambo?

13 Kurudia-rudia kunasaidia kumbukumbu, na vikumbusho vinavyotolewa tena na tena ni vya maana katika elimu yetu ya Kikristo. Mtume Petro alisema hivi: “Sikuzote nitakuwa na mwelekeo wa kuwakumbusha ninyi kuhusu mambo haya, ijapokuwa mnayajua hayo na mmewekwa imara katika kweli iliyo ndani yenu.” (2 Pet. 1:12) Kwa nini tunahitaji vikumbusho? Kwa sababu vinatusaidia kuelewa mambo kwa undani zaidi, kupanua maoni yetu, na kuimarisha azimio letu la kubaki tukiwa imara kiroho. (Zab. 119:129) Kurudia-rudia viwango na kanuni za Mungu kunatusaidia kujichunguza na kutuzuia tusiwe ‘wasikiaji wasahaulifu.’ (Yak. 1:22-25) Tusipoendelea kujikumbusha ile kweli, mambo mengine yatapotosha mioyo yetu na huenda tukashindwa kuzungumza ile lugha safi kwa ufasaha.

14. Ni nini kitakachotusaidia tunapojifunza ile lugha safi?

14 Soma kwa sauti. (Ufu. 1:3) Wanafunzi fulani wanajaribu kujifunza lugha mpya kimyakimya wakiwa peke yao. Lakini hawapati matokeo mazuri. Tunapojifunza ile lugha safi, huenda nyakati nyingine tukahitaji kusoma “kwa sauti ya chini” ili tuweze kukaza fikira. (Soma Zaburi 1:1, 2.) Kufanya hivyo kunakazia kikiki akilini mwetu habari ambazo tunasoma. Katika Kiebrania, maneno ‘kusoma kwa sauti ya chini’ yanahusiana sana na kutafakari. Kama vile chakula kinavyohitaji kusagwa ili kitufaidi kabisa, tunahitaji kutafakari ili tuelewe waziwazi mambo tunayosoma. Je, tunatenga wakati wa kutosha ili kutafakari mambo tunayojifunza? Baada ya kusoma Biblia, tunapaswa kufikiria kwa uzito mambo ambayo tumesoma.

15. Ni kwa njia gani tunaweza kujifunza “kanuni” za ile lugha safi?

15 Chunguza kanuni za lugha. Baada ya muda inafaa kujifunza kanuni za lugha hiyo mpya na njia ya kupanga maneno, yaani, sarufi. Hilo linatuwezesha kuelewa muundo wa lugha hiyo, na kutuwezesha kuizungumza vizuri. Kama vile lugha ilivyo na kielelezo cha maneno au njia ya kupanga maneno, ile lugha safi ya kweli ya Biblia ina “kielelezo cha maneno yenye afya.” (2 Tim. 1:13) Tunapaswa kuiga “kielelezo” hicho.

16. Ni mwelekeo gani ambao tunahitaji kuushinda, nasi tunaweza kuushinda namna gani?

16 Endelea kufanya maendeleo. Huenda mtu akajifunza lugha kiasi cha kuweza kuitumia katika mazungumzo ya kawaida, lakini anaweza kuacha kufanya maendeleo. Wale wanaozungumza ile lugha safi wanaweza pia kuwa na tatizo kama hilo. (Soma Waebrania 5:11-14.) Ni nini kinachoweza kutusaidia kuushinda mwelekeo huo? Uwe tayari kuendelea kujifunza maneno zaidi ya lugha hiyo. “Kwa kuwa sasa tumeliacha fundisho la msingi juu ya Kristo, na tusonge mbele kuelekea ukomavu, tusiweke msingi tena, yaani, kutubu matendo yaliyokufa, na imani kwa Mungu, fundisho juu ya mabatizo na kuwekewa mikono, kufufuliwa kwa wafu na hukumu ya milele.”—Ebr. 6:1, 2.

17. Kwa nini ni jambo la maana kujifunza kwa ukawaida? Toa mfano.

17 Uwe na wakati hususa wa kujifunza. Kujifunza kwa ukawaida kwa muda mfupi ni afadhali kuliko kujifunza mara kwa mara kwa muda mrefu. Jifunze wakati ambapo uko chonjo na wakati ambapo akili yako haitangitangi kwa urahisi. Kujifunza lugha mpya ni kama kupasua njia katika msitu. Kadiri njia hiyo inavyotumiwa, ndivyo safari inavyokuwa rahisi zaidi. Njia hiyo isipotumiwa, muda si muda itafunikwa na majani. Kwa hiyo, kuendelea kujifunza kwa ukawaida ni jambo la maana sana! (Dan. 6:16, 20) Kwa msaada wa sala, ‘endelea kukaa macho daima’ unapozungumza ile lugha safi ya kweli ya Biblia.—Efe. 6:18.

18. Kwa nini tuzungumze ile lugha safi katika kila nafasi tunayopata?

18 Zungumza! Zungumza! Zungumza! Huenda watu fulani wanaojifunza lugha mpya wakasita kuizungumza kwa sababu wanaona aibu au wanaogopa kwamba watakosea. Hilo litawazuia wasifanye maendeleo. Mwanafunzi anapojifunza lugha mpya ni jambo la maana sana kufanya mazoezi. Kadiri mwanafunzi huyo anavyozungumza lugha hiyo mpya, ndivyo atakavyoizoea na kuitumia kwa urahisi zaidi. Vivyo hivyo, tunahitaji kuzungumza ile lugha safi nyakati zote. “Kwa moyo mtu huonyesha imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.” (Rom. 10:10) Tulifanya “tangazo la hadharani” wakati tulipobatizwa, lakini pia tunafanya tangazo hilo tunapozungumza kumhusu Yehova katika kila nafasi tunayopata, kutia ndani wakati tunaposhiriki katika huduma. (Mt. 28:19, 20; Ebr. 13:15) Mikutano yetu ya Kikristo inatuwezesha pia kuzungumza ile lugha safi waziwazi na kwa njia inayoeleweka.—Soma Waebrania 10:23-25.

Itumie Ile Lugha Safi kwa Umoja Kumsifu Yehova

19, 20. (a) Ni jambo gani la kustaajabisha ambalo Mashahidi wa Yehova wanatimiza leo? (b) Umeazimia kufanya nini?

19 Hebu wazia jinsi ilivyosisimua kuwa Yerusalemu asubuhi ya Jumapili, Sivani 6, mwaka wa 33 W.K.! Mapema asubuhi hiyo, kabla tu ya saa tatu, watu waliokusanyika katika chumba fulani cha juu ‘walianza kusema kimuujiza katika lugha tofauti.’ (Mdo. 2:4) Leo, watumishi wa Mungu hawapewi tena zawadi ya kusema katika lugha. (1 Kor. 13:8) Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wanatangaza habari njema ya Ufalme katika lugha zaidi ya 430.

20 Tunashukuru sana kwamba hata iwe tunazungumza lugha gani, sote tunazungumza kwa umoja ile lugha safi ya kweli ya Biblia! Ni kana kwamba hali iliyotukia Babeli imerekebishwa. Ni kana kwamba watu wa Yehova wanazungumza lugha moja wanapolisifu jina lake. (1 Kor. 1:10) Na tuazimie kuendelea kutumikia “bega kwa bega” pamoja na ndugu na dada zetu duniani pote tunapozidi kujifunza kuzungumza lugha hiyo moja kwa ufasaha zaidi, na hivyo kumletea utukufu Baba yetu wa mbinguni, Yehova.—Soma Zaburi 150:1-6.

Ungesema Nini?

• Lugha safi ni nini?

• Kuzungumza ile lugha safi kunatia ndani nini?

• Ni mambo gani yatakayotusaidia kuzungumza ile lugha safi kwa ufasaha?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

Unaweza Kuzungumza Lugha Safi kwa Ufasaha Zaidi kwa

◆ kusikiliza kwa uangalifu.

Luka 8:18; Ebr. 2:1

kuiga wasemaji wenye ufasaha.

1 Kor. 11:1; Ebr. 13:7

kujitahidi kukumbuka mambo na kuyarudia-rudia.

Yak. 1:22-25; 2 Pet. 1:12

kusoma kwa sauti.

Zab. 1:1, 2; Ufu. 1:3

kuchunguza “kanuni za lugha.”

2 Tim. 1:13

kuendelea kufanya maendeleo.

Ebr. 5:11-14; 6:1, 2

kuwa na wakati hususa wa kujifunza.

Dan. 6:16, 20; Efe. 6:18

kuizungumza.

Rom. 10:10; Ebr. 10:23-25

[Picha katika ukurasa wa 24]

Watu wa Yehova wanazungumza ile lugha safi kwa umoja