Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wamishonari Ni Kama Nzige

Wamishonari Ni Kama Nzige

Kuhitimu kwa Darasa la 124 la Gileadi

Wamishonari Ni Kama Nzige

BAADA ya kila miezi sita, Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) inakuwa na programu ya kuhitimu na washiriki wote wa familia ya Betheli ya Marekani wanaalikwa kwenye programu hiyo. Machi 8, 2008, wageni kutoka katika nchi zaidi ya 30 walijiunga na familia ya Betheli kwa ajili ya kuhitimu kwa darasa la 124 la Shule ya Gileadi. Watu 6,411 waliohudhuria walifurahia siku hiyo ya pekee pamoja na wanafunzi.

Mwenyekiti wa programu, Stephen Lett wa Baraza Linaloongoza, alianza programu kwa hotuba yenye kichwa “Nendeni Pamoja na Nzige wa Mfano wa Yehova.” Andiko la Ufunuo 9:1-4 linalinganisha kikundi kidogo cha Wakristo watiwa-mafuta ambao walianza kutenda tena kiroho mwaka wa 1919 na kundi kubwa la nzige ambao walianza ghafula kutenda kwa bidii. Wanafunzi walikumbushwa kwamba wakiwa washiriki wa “kondoo wengine,” wamejiunga na kundi hilo kubwa la nzige wa mfano.—Yoh. 10:16.

Lon Schilling, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani, alifuata kwa hotuba yenye kichwa “Mkamilishane.” Hotuba hiyo ilitegemea mfano wa Akila na Prisila (au, Priska), wenzi wa ndoa Wakristo wa karne ya kwanza wanaotajwa katika Biblia. (Rom. 16:3, 4) Darasa hilo la Gileadi lilikuwa na wanafunzi 56, wote wakiwa wenzi wa ndoa. Walikumbushwa kwamba ili wafanikiwe wakiwa wamishonari, wanahitaji kudumisha kifungo cha ndoa chenye nguvu. Kila mara Biblia inapomtaja Akila, inamtaja pia mke wake, Prisila. Hivyo, mtume Paulo na washiriki wa kutaniko waliwaona kuwa wenzi wa ndoa wenye uhusiano wa karibu. Vivyo hivyo, wenzi wa ndoa wamishonari leo wanapaswa kufanya kazi pamoja, kuabudu pamoja, na kushughulikia pamoja matatizo ya pekee ya eneo la kigeni, na hivyo kukamilishana.—Mwa. 2:18.

Hotuba iliyofuata yenye kichwa “Onyesha Kwamba Unathamini Wema wa Yehova,” ilitolewa na Guy Pierce wa Baraza Linaloongoza. Ndugu Pierce alieleza kwamba kuwa mwema kunatia ndani mengi zaidi ya kutofanya mabaya. Mtu mwema anafanya mambo mema yanayowaletea wengine faida. Wema wa Yehova Mungu hauna kifani. (Zek. 9:16, 17) Wema na upendo wa Mungu unaweza kutusukuma tuwatendee wengine mema. Akiwapongeza wanafunzi, Ndugu Pierce alimalizia kwa kusema hivi: “Mmekuwa mkitenda mema. Tuna hakika kwamba mtaendelea kuonyesha kwamba mnathamini wema wa Mungu kwa kutenda mema katika migawo yoyote ambayo Yehova Mungu atawapa.”

Kisha, Michael Burnett, mmishonari wa zamani ambaye hivi majuzi alipewa mgawo wa kuwa mwalimu wa Gileadi, alitoa hotuba yenye kichwa “Ivae Kama Utepe wa Kipaji Katikati ya Macho Yako.” Kana kwamba walikuwa wamevaa “utepe wa kipaji” katikati ya macho yao, Waisraeli walipaswa kukumbuka jinsi Yehova alivyowakomboa kimuujiza kutoka Misri. (Kut. 13:16) Wanafunzi walihimizwa wakumbuke mambo mengi waliyofundishwa katika Shule ya Gileadi kana kwamba walikuwa wamevaa mafundisho hayo kama utepe wa kipaji katikati ya macho yao. Ndugu Burnett alikazia uhitaji wa kuwa mnyenyekevu na mwenye kiasi na kufuata kanuni za Biblia wanapotatua matatizo yoyote ya kutoelewana na wamishonari wenzao na watu wengine pia.—Mt. 5:23, 24.

Mark Noumair, mwalimu wa muda mrefu wa Gileadi, alitoa hotuba yenye kichwa “Ni Wimbo Gani Utakaoimbwa Juu Yako?” Zamani za kale, watu walikuwa na desturi ya kuimba nyimbo ili kusherehekea ushindi vitani. Wimbo mmoja kama huo, unafunua kwamba makabila ya Rubeni, Dani, na Asheri hayakutaka kujitolea sana, lakini kabila la Zabuloni linasifiwa kwa sababu ya roho yake ya kujidhabihu. (Amu. 5:16-18) Matendo ya kila Mkristo ni kama maneno ya wimbo, yatajulikana mwishowe. Mtu anayefanya kazi ya Mungu kwa bidii na kuvumilia kwa ushikamanifu huku akifuata mwongozo wa kitheokrasi atakuwa na sifa nzuri machoni pa Yehova, naye atakuwa mfano mzuri kwa ndugu zake. Washiriki wengine wa kutaniko wanaposikiliza wimbo wa mfano unaoandikwa na matendo yetu, wanachochewa kuiga mfano wetu mzuri.

Katika mazoezi hayo ya Gileadi, darasa hilo la 124 lilihubiri jumla ya saa 3,000 hivi. Katika hotuba yenye kichwa “Kufuata Mwongozo wa Roho Takatifu,” wanafunzi walimsimulia Sam Roberson wa Idara ya Shule za Kitheokrasi mambo fulani waliyoona katika utumishi wa shambani na kuigiza mengine. Baada ya masimulizi hayo yenye kutia moyo, wahitimu wa Gileadi wanaotumikia katika nchi mbalimbali walihojiwa na Patrick LaFranca wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani. Wanafunzi walithamini mashauri mazuri waliyopokea kutoka kwa ndugu hao.

Anthony Morris wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya mwisho yenye kichwa, “Kumbukeni, Vitu Vinavyoonekana Ni vya Muda.” Maandiko yanatutia moyo tukazie fikira baraka za wakati ujao kutoka kwa Yehova badala ya kukazia fikira dhiki yoyote ya muda ambayo huenda tukapata sasa. (2 Kor. 4:16-18) Leo, sote tunaona umaskini mkubwa sana, ukosefu wa haki, uonevu, magonjwa, na vifo. Huenda wamishonari wakakabiliana moja kwa moja na mambo kama hayo yenye kuhuzunisha. Lakini kukumbuka kwamba mambo hayo ni ya muda kutatusaidia kuendelea kuwa na usawaziko wa kiroho na kudumisha tumaini letu.

Ndugu Lett alitoa maelezo ya kumalizia programu huku wahitimu wote wakiwa jukwaani. Aliwatia moyo wasikate tamaa, kisha akasema: “Tunaweza kuvumilia majaribu yoyote na kubaki watimilifu ikiwa Yehova yuko upande wetu.” Aliwahimiza wamishonari hao wapya wawe kama nzige, na kuazimia kuendelea katika utumishi wa Yehova wakiwa wenye bidii, washikamanifu, na watiifu milele.

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi ambazo zimewakilishwa: 7

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 16

Idadi ya wanafunzi: 56

Wastani wa umri: 33.8

Wastani wa miaka katika kweli: 18.2

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13.8

[Picha katika ukurasa wa 31]

Darasa la 124 Lililohitimu la Shule ya Gileadi

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Nicholson, T.; Main, H.; Senge, Y.; Snape, L.; Vanegas, C.; Pou, L. (2) Santana, S.; Oh, K.; Lemaitre, C.; Williams, N.; Alexander, L. (3) Woods, B.; Stainton, L.; Huntley, E.; Alvarez, G.; Cruz, J.; Bennett, J. (4) Williamson, A.; González, N.; Zuroski, J.; Degandt, I.; May, J.; Diemmi, C.; Tavener, L. (5) Lemaitre, W.; Harris, A.; Wells, C.; Rodgers, S.; Durrant, M.; Senge, J. (6) Huntley, T.; Vanegas, A.; Pou, A.; Santana, M.; Bennett, V.; Tavener, D.; Oh, M. (7) Zuroski, M.; Rodgers, G.; Diemmi, D.; Nicholson, L.; Alvarez, C.; Snape, J. (8) Harris, M.; González, P.; Main, S.; Woods, S.; Stainton, B.; Williamson, D.; Durrant, J. (9) Cruz, P.; Degandt, B.; Williams, D.; Wells, S.; Alexander, D.; May, M.

[Picha katika ukurasa wa 32]

Shule ya Gileadi iko kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower