Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anawatunza kwa Upendo Watumishi Wake Waliozeeka

Yehova Anawatunza kwa Upendo Watumishi Wake Waliozeeka

Yehova Anawatunza kwa Upendo Watumishi Wake Waliozeeka

“Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—EBR. 6:10.

1, 2. (a) Huenda ukakumbuka nini unapomwona mtu mwenye nywele nyeupe? (b) Yehova ana maoni gani kuelekea Wakristo waliozeeka?

UNAPOONA watu waliozeeka ambao wana nywele nyeupe au mvi katika kutaniko, je, unakumbuka simulizi fulani katika kitabu cha Biblia cha Danieli? Katika maono aliyompa Danieli, Yehova Mungu alijionyesha akiwa na nywele nyeupe. Danieli aliandika hivi: “Nikaendelea kutazama mpaka viti vya ufalme vikawekwa na Mzee wa Siku akaketi. Mavazi yake yalikuwa meupe kama theluji, na nywele za kichwa chake zilikuwa kama sufu safi.”—Dan. 7:9.

2 Kwa kawaida, sufu safi ina rangi nyeupe inayong’aa. Hivyo, nywele nyeupe na jina la cheo “Mzee wa Siku” vinaonyesha kwamba Mungu ameishi kwa miaka mingi sana naye ana hekima nyingi na hivyo tunapaswa kumheshimu sana. Hivyo basi, yule Mzee wa Siku, Yehova, ana maoni gani kuelekea wanaume na wanawake waaminifu waliozeeka? Neno la Mungu linasema kwamba “kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.” (Met. 16:31) Ndiyo, Mkristo mwaminifu akiwa na nywele nyeupe au mvi, anaonekana amekomaa na hivyo anampendeza Mungu. Je, unawaona ndugu na dada zako waliozeeka kama Yehova anavyowaona?

Kwa Nini Wanathaminiwa Sana?

3. Kwa nini tunawathamini sana waabudu wenzetu waliozeeka?

3 Watumishi hao wapendwa wa Mungu wenye umri mkubwa wanatia ndani washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, waangalizi wanaosafiri waliotumikia zamani na wale wanaotumikia sasa, mapainia wenye bidii, na wahubiri wa Ufalme ambao wamekomaa—ndugu na dada ambao wanatumikia kwa uaminifu katika makutaniko yetu. Huenda unajua wahubiri fulani ambao wamehubiri habari njema kwa bidii kwa makumi ya miaka na ambao wamewachochea vijana na kuwasaidia kubadili maisha yao kwa kuwawekea mifano mizuri. Waamini wengine wenzetu waliozeeka wamebeba madaraka mazito na wamevumilia mateso kwa ajili ya habari njema. Yehova na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” wanathamini sana mambo yote ambayo wahubiri hao walifanya zamani na mambo ambayo wanaendelea kufanya sasa katika kazi ya Ufalme.—Mt. 24:45.

4. Kwa nini tunapaswa kuwaheshimu Wakristo waliozeeka na kusali kwa ajili yao?

4 Wahubiri hao waaminifu waliozeeka wanastahili kupongezwa na kuheshimiwa na watumishi wengine wa Yehova Mungu. Kwa kweli, Sheria ya Mungu kupitia Musa inaonyesha kwamba kuna uhusiano kati ya kumwogopa Yehova na kuwaheshimu na kuwajali waliozeeka. (Law. 19:32) Tunapaswa kusali kwa ukawaida kwa ajili ya waaminifu hao na kumshukuru Mungu kwa kazi yao ya jasho yenye upendo. Mtume Paulo alisali kwa ajili ya wafanyakazi wenzake, wachanga na waliozeeka.—Soma 1 Wathesalonike 1:2, 3.

5. Tunaweza kufaidika jinsi gani kwa kushirikiana na waabudu wa Yehova waliozeeka?

5 Zaidi ya hayo, washiriki wote wa kutaniko wanaweza kufaidika kwa kushirikiana na Wakristo waliozeeka. Waabudu waaminifu wa Yehova waliozeeka wamepata ujuzi wenye thamani sana kupitia mambo waliyojifunza na waliyojionea. Wamejifunza kuonyesha subira na huruma, nao wanafurahi sana na kuridhika wanapofundisha vizazi vinavyofuata mambo waliyojifunza. (Zab. 71:18) Enyi vijana, iweni na hekima na mteke ujuzi kutoka katika vyanzo hivyo vya ujuzi kama mnavyoteka maji kutoka katika kisima kirefu.—Met. 20:5.

6. Unaweza kuwaonyesha kwa njia gani kwamba unawathamini kikweli waliozeeka?

6 Je, unawaambia waliozeeka kwamba unawathamini kama Yehova anavyowathamini? Njia moja ya kufanya hivyo ni kuwaambia jinsi unavyowapenda sana kwa sababu ya uaminifu wao na jinsi unavyothamini maoni yao. Zaidi ya hayo, ukitumia yale unayojifunza kutoka kwao, unaonyesha kwamba unawaheshimu kutoka moyoni. Wakristo wengi wenye umri mkubwa wanaweza kukumbuka mashauri yenye hekima waliyopokea kutoka kwa Wakristo waaminifu waliozeeka na jinsi ambavyo wamefaidika katika maisha yao yote kwa kufuata mashauri hayo. *

Waonyeshe Upendo Mwororo kwa Matendo

7. Yehova anawapa nani daraka la msingi la kuwatunza waliozeeka?

7 Mungu anawapa washiriki wa familia za watu waliozeeka daraka la msingi la kuwatunza. (Soma 1 Timotheo 5:4, 8.) Yehova anafurahi wakati familia zinapotimiza wajibu wao kuelekea watu waliozeeka wa jamaa yao na hivyo kuonyesha kwamba wanawajali watu hao kama yeye anavyowajali. Mungu anategemeza familia hizo na kuzibariki kwa sababu ya jitihada zao na dhabihu zao zote. *

8. Kwa nini makutaniko yanapaswa kuwahangaikia Wakristo waliozeeka?

8 Vivyo hivyo, Yehova anafurahi wakati makutaniko yanapowasaidia Wakristo waaminifu waliozeeka ambao wana uhitaji lakini hawana washiriki wa familia ambao ni waamini au walio tayari kuwatunza. (1 Tim. 5:3, 5, 9, 10) Kwa kufanya hivyo, washiriki wa kutaniko wanaonyesha kwamba wana ‘hisia-mwenzi, upendo wa kindugu, na huruma nyororo,’ kuelekea waliozeeka. (1 Pet. 3:8) Paulo anatoa mfano unaoonyesha jinsi kutaniko linavyopaswa kuwahangaikia washiriki wake waliozeeka anaposema kwamba kiungo kimoja cha mwili kikiumia, “viungo vingine vyote huumia pamoja nacho.” (1 Kor. 12:26) Tunapochukua hatua zinazofaa kuwasaidia waliozeeka kwa kuchochewa na huruma, tunaonyesha kwamba tunafuata kanuni ya shauri hili la Paulo: “Endeleeni kubebeana mizigo mizito, na hivyo kuitimiza sheria ya Kristo.”—Gal. 6:2.

9. Mtu aliyezeeka anaweza kubeba mizigo gani mizito?

9 Wakristo waliozeeka wanabeba mizigo gani mizito? Wengi wao wanachoka haraka. Huenda wakashindwa kufanya hata mambo ya kawaida, kama vile, kwenda kumwona daktari, kushughulikia barua, kulipia huduma mbalimbali, kusafisha nyumba, na kupika chakula. Kwa kuwa mara nyingi mtu anapozeeka anapoteza hamu ya kula chakula na kunywa maji, huenda wakafikiri kwamba hawahitaji kula au kunywa maji ingawa wanayahitaji sana. Wanaweza pia kupoteza hamu ya chakula cha kiroho. Kwa sababu ya macho na masikio kuzeeka, kusoma na kusikiliza programu za mambo ya kiroho, na pia kujitayarisha ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo kunaweza kuchosha. Basi, wengine wanaweza kuwasaidia kwa njia gani Wakristo hao waliozeeka?

Jinsi Unavyoweza Kusaidia

10. Wazee wa kutaniko wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba waliozeeka wanasaidiwa inavyofaa?

10 Katika makutaniko mengi, waliozeeka wanatunzwa kwa njia nzuri sana. Ndugu na dada wenye upendo wanawasaidia kununua vitu, kupika, na kufanya usafi. Wanawasaidia kujifunza, kujitayarisha kwa ajili ya mikutano, na kuwa wa kawaida katika huduma. Mashahidi vijana wanaenda pamoja nao kwenye mikutano na katika huduma na pia wanawasaidia kusafiri. Ikiwa waliozeeka hawawezi kutoka nyumbani, mipango inafanywa ili wasikilize mikutano kupitia simu, au mikutano inarekodiwa kwenye kanda ili wasikilize. Inapowezekana, wazee wa kutaniko wanahakikisha kwamba mipango inayofaa inafanywa ili kuwasaidia washiriki waliozeeka katika kutaniko. *

11. Simulia jinsi familia moja ilivyomsaidia ndugu mmoja aliyezeeka.

11 Mkristo mmoja-mmoja pia anaweza kuwakaribisha na kuwaonyesha ukarimu. Baada ya mke wa ndugu mmoja aliyezeeka kufa, ndugu huyo hangeweza tena kulipa kodi ya nyumba bila malipo ya uzeeni ya mke wake. Yeye na mke wake walikuwa wameifundisha familia moja Biblia, yaani, baba, mama, na binti zao wawili vijana. Familia hiyo ilikuwa na nyumba kubwa, na hivyo ikampa ndugu huyo vyumba viwili ili aishi humo. Kwa miaka 15, walikula pamoja, walikuwa na pindi za furaha, na walimwonyesha upendo wa kindugu. Binti zao vijana walifaidika sana na imani na uzoefu wake wa miaka mingi, naye alifaidika sana na ushirika wao wenye kufurahisha. Ndugu huyo aliyezeeka aliishi nao mpaka alipokufa akiwa na umri wa miaka 89. Familia hiyo bado inamshukuru Mungu kwa sababu ya baraka nyingi walizopata kwa kushirikiana na ndugu huyo. ‘Hawajapoteza thawabu yao’ kwa sababu ya kumsaidia mwanafunzi mwenzao wa Yesu Kristo.—Mt. 10:42. *

12. Unaweza kufanya nini ili kuwaonyesha upendo mwororo ndugu na dada waliozeeka?

12 Huenda usiweze kumsaidia ndugu au dada aliyezeeka kama familia hiyo ilivyofanya, lakini unaweza kuwasaidia waliozeeka kufika kwenye mikutano na kushiriki katika huduma ya shambani. Unaweza pia kuwaalika nyumbani kwako na kwenda nao katika tafrija. Unaweza kuwatembelea, hasa wanapokuwa wagonjwa au wanaposhindwa kutembea. Zaidi ya hayo, unaweza na unapaswa sikuzote kuwatendea kama watu wazima waliokomaa. Maadamu wanaweza kutumia uwezo wao wa kufikiri, Wakristo waliozeeka wanapaswa kushirikishwa katika kufanya maamuzi yote ambayo yanawahusu. Hata wale ambao wamepoteza uwezo wao wa kufikiri wanatambua ikiwa wanatendewa kwa heshima.

Yehova Hatasahau Kazi Yako

13. Kwa nini ni jambo la maana kujali hisia za Wakristo waliozeeka?

13 Ni jambo la maana sana kujali hisia za waliozeeka. Ni kawaida kwa waliozeeka kuhuzunika sana wanaposhindwa kufanya mambo yote waliyofanya walipokuwa vijana au wenye afya nzuri zaidi. Kwa mfano, dada mmoja aliyemtumikia Yehova kwa bidii kwa miaka 50 hivi na ambaye alikuwa painia wa kawaida, alishikwa na ugonjwa uliomdhoofisha hivi kwamba alihudhuria mikutano kwa shida sana. Alipolinganisha huduma yake ya wakati uliopita na hali yake ya sasa, alianza kulia. Aliinamisha kichwa chake na kusema hivi kwa machozi, “Ninahisi sifai hata kidogo.”

14. Zaburi zinaweza kuwatia moyo jinsi gani watumishi wa Yehova waliozeeka?

14 Ikiwa umezeeka, je, umewahi kuwa na hisia hizo zenye kuumiza? Au kuna nyakati ambazo unahisi kwamba huenda Yehova amekuacha? Huenda mtunga-zaburi alikuwa na hisia kama hizo katika miaka yake ya uzeeni, kwa kuwa alimsihi Yehova hivi: “Usinitupe wakati wa uzee; wakati tu nguvu zangu zinapungua, usiniache. . . . Mpaka wakati wa uzee na wa kuwa na kichwa chenye mvi, Ee Mungu, usiniache.” (Zab. 71:9, 18) Bila shaka, Yehova hangemwacha mtungaji wa zaburi hiyo, naye Hatakuacha. Katika zaburi nyingine, Daudi alieleza uhakika aliokuwa nao katika utegemezo wa Mungu. (Soma Zaburi 68:19.) Uwe na hakika kwamba ikiwa wewe ni Mkristo mwaminifu aliyezeeka, Yehova yupo pamoja nawe naye ataendelea kukutegemeza siku baada ya siku.

15. Ni nini kinachoweza kuwasaidia waliozeeka wawe na maoni yanayofaa?

15 Yehova hawezi kamwe kusahau mambo yote ambayo ninyi Mashahidi wake ambao mmezeeka mlifanya na yale mnayofanya sasa kwa utukufu wa Mungu. Biblia inasema hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” (Ebr. 6:10) Kwa hiyo, msiwe kamwe na maoni yasiyofaa, na kufikiri kimakosa kwamba Yehova hawahitaji tena eti kwa sababu mmezeeka. Mjitahidi kuwa na maoni yanayofaa badala ya maoni yasiyofaa yenye kuvunja moyo. Shangilieni kwa sababu ya baraka zenu na tumaini lenu la wakati ujao! Tuna “wakati ujao na tumaini”—bora zaidi—na Muumba wetu ndiye anayetuhakikishia mambo hayo. (Yer. 29:11, 12; Mdo. 17:31; 1 Tim. 6:19) Tafakari kuhusu tumaini lako, jitahidi sana kubaki ukiwa kijana katika moyo na akili, na usifikiri kamwe kwamba kutaniko halikuthamini! *

16. Kwa nini ndugu mmoja aliyezeeka alitaka kuacha kutumikia akiwa mzee, lakini baraza la wazee lilimtia moyo jinsi gani?

16 Mfikirie Johan, ambaye ana umri wa miaka 80 na anamtunza daima mke wake, Sannie, ambaye ni mgonjwa asiyejiweza. * Akina dada wanapanga zamu za kumtunza Sannie ili Johan ahudhurie mikutano na kwenda kuhubiri. Hata hivyo, hivi karibuni, Johan alikuwa amevunjika moyo sana hivi kwamba aliona hapaswi kuendelea kutumikia akiwa mzee wa kutaniko. Aliuliza hivi huku machozi yakiwa yamejaa machoni: “Kuna haja gani ya kuendelea kuwa mzee? Sifanyi tena kazi yoyote ya maana katika kutaniko.” Wazee wenzake walimhakikishia kwamba uzoefu wake na hekima yake inahitajiwa sana. Walimtia moyo aendelee kutumikia akiwa mzee, hata ikiwa hafanyi mengi sana. Johan alitiwa moyo sana, naye anaendelea kutumikia akiwa mzee kwa faida ya kutaniko.

Yehova Anajali Kabisa

17. Biblia inawahakikishia nini Wakristo waliozeeka?

17 Maandiko yanasema waziwazi kwamba waliozeeka wanaweza kuendelea kusitawi kiroho hata ingawa wanakabili matatizo ya kuzeeka. Mtunga-zaburi alitangaza hivi: “Wale ambao wamepandwa katika nyumba ya Yehova . . . bado wataendelea kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi, wataendelea kuwa wanono na wabichi.” (Zab. 92:13, 14) Mtume Paulo, ambaye huenda alikuwa na tatizo fulani la kimwili, ‘hakufa moyo, hata ingawa mtu aliye kwa nje alikuwa anachakaa.’—Soma 2 Wakorintho 4:16-18.

18. Kwa nini waamini wenzetu waliozeeka na wale wanaowatunza wanahitaji kusaidiwa na wengine?

18 Mifano mingi leo inathibitisha kwamba Wakristo waliozeeka wanaweza ‘kuendelea kusitawi.’ Lakini matatizo ya magonjwa na uzee yanaweza kuwalemea sana hata wale ambao wanasaidiwa na kutunzwa na washiriki wa familia wenye bidii. Wale wanaowatunza wanaweza pia kuchoka. Kutaniko lina pendeleo na daraka la kuonyesha upendo kwa matendo kwa kuwasaidia wale waliozeeka na wale wanaowatunza. (Gal. 6:10) Tunapowasaidia tunaonyesha kwamba hatuwaambii watu hao waende ‘wajipashe moto na kula vizuri’ bila kuwasaidia kwa njia inayofaa.—Yak. 2:15-17.

19. Kwa nini Wakristo waaminifu waliozeeka wanaweza kutazamia wakati ujao kwa uhakika?

19 Mkristo anapozeeka utendaji wake unaweza kubadilika, lakini upendo wa Yehova kwa watumishi wake washikamanifu waliozeeka hauwezi kupungua. Badala yake, Wakristo hao wote waaminifu ni wenye thamani sana machoni pake, naye hatawaacha kamwe. (Zab. 37:28; Isa. 46:4) Yehova atawategemeza na kuwaongoza katika miaka yote ya uzeeni.—Zab. 48:14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona habari yenye kichwa “Waliozeeka Ni Baraka kwa Vijana,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 2007 (1/6/2007).

^ fu. 7 Ona ukurasa wa 3-10 wa toleo la Amkeni! la Februari 8, 1994 (8/2/1994).

^ fu. 10 Katika nchi fulani, huenda hilo likatia ndani kuwasaidia waliozeeka kupata msaada wa serikali. Ona habari yenye kichwa “Mungu Anawajali Waliozeeka,” katika toleo la Juni 1, 2006 (1/6/2006), la Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 11 Ona habari yenye kichwa “Yehova Hutujali Sikuzote,” katika toleo la Septemba 1, 2003 (1/9/2003), la Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 15 Ona habari yenye kichwa “Utukufu wa Kichwa Chenye Mvi,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1993 (15/3/1993).

^ fu. 16 Majina yamebadilishwa.

Ungesema Nini?

• Kwa nini unawathamini sana Wakristo waaminifu waliozeeka?

• Tunaweza kuwaonyesha jinsi gani upendo mwororo waabudu wenzetu waliozeeka?

• Ni nini kinachoweza kuwasaidia watumishi waliozeeka wa Yehova wawe na maoni yanayofaa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Washiriki wa kutaniko wanawathamini sana waliozeeka