Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Hatawaacha Washikamanifu Wake

Yehova Hatawaacha Washikamanifu Wake

Yehova Hatawaacha Washikamanifu Wake

“[Yehova] hatawaacha washikamanifu wake. Hakika watalindwa mpaka wakati usio na kipimo.”—ZAB. 37:28.

1, 2. (a) Ni mambo gani yaliyojaribu ushikamanifu wa watumishi wa Mungu katika karne ya kumi K.W.K.? (b) Yehova aliwalinda washikamanifu wake katika hali gani tatu?

NI KARNE ya kumi K.W.K. na ni wakati wa kufanya uamuzi. Vita vya wenyewe kwa wenyewe vimeepukwa chupuchupu wakati makabila ya kaskazini ya Israeli yenye msukosuko yanapopewa uhuru wa kadiri fulani. Yeroboamu, mfalme wao aliyewekwa rasmi hivi karibuni tu, anaimarisha haraka mamlaka yake kwa kuanzisha dini mpya ya taifa. Anataka raia wake wamtii kikamili. Watumishi waaminifu wa Yehova watafanya nini? Je, watabaki washikamanifu kwa Mungu wanayemwabudu? Maelfu wanafanya hivyo, na Yehova anawalinda wanapodumisha utimilifu wao.—1 Fal. 12:1-33; 2 Nya. 11:13, 14.

2 Leo pia ushikamanifu wa watumishi wa Mungu unajaribiwa. Biblia inaonya hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” Je, tunaweza kufanikiwa ‘kuchukua msimamo kumpinga yeye, tukiwa imara katika imani’? (1 Pet. 5:8, 9) Acheni tuchunguze mambo fulani yaliyotukia Mfalme Yeroboamu alipowekwa rasmi mwaka wa 997 K.W.K. na kuona yale tunayoweza kujifunza. Katika nyakati hizo ngumu, watumishi waaminifu wa Yehova walikuwa wakikandamizwa. Walikabiliana pia na uvutano mbalimbali wa uasi-imani walipokuwa wakitimiza migawo migumu. Katika kila moja ya hali hizo, Yehova hakuwaacha washikamanifu wake, naye hatawaacha leo.—Zab. 37:28.

Wanapokandamizwa

3. Kwa nini utawala wa Mfalme Daudi haukuwakandamiza watu?

3 Acheni kwanza tuchunguze ni katika hali gani Yeroboamu alikuja kuwa mfalme. Andiko la Methali 29:2 linasema hivi: “Mtu yeyote mwovu anapotawala, watu huugua.” Chini ya utawala wa Mfalme Daudi wa Israeli la kale, watu hawakuugua. Daudi hakuwa mkamilifu, lakini alikuwa mshikamanifu kwa Mungu na alimtegemea. Utawala wa Daudi haukuwakandamiza watu. Yehova alifanya agano pamoja na Daudi, na kumwambia: “Nyumba yako na ufalme wako hakika zitakuwa imara mpaka wakati usio na kipimo mbele yako; nacho kiti chako cha ufalme kitafanywa imara mpaka wakati usio na kipimo.”—2 Sam. 7:16.

4. Baraka ambazo watu walifurahia wakati wa utawala wa Sulemani zilitegemea nini?

4 Mwanzoni, utawala wa Sulemani, mwana wa Daudi, ulikuwa wenye amani na ufanisi sana hivi kwamba ulifananisha vizuri Utawala ujao wa Miaka Elfu wa Kristo Yesu. (Zab. 72:1, 17) Wakati huo, hakuna hata kabila moja kati ya makabila 12 ya Israeli ambalo lilikuwa na sababu ya kuasi. Hata hivyo, baraka ambazo Sulemani na raia wake walifurahia zilikuwa na masharti. Yehova alimwambia Sulemani hivi: “Ukitembea katika sheria zangu na kutenda maamuzi yangu ya hukumu na kushika amri zangu zote kwa kutembea ndani yake, mimi pia hakika nitakutimizia neno nililomwambia Daudi baba yako; nami hakika nitakaa katikati ya wana wa Israeli, wala sitawaacha watu wangu Israeli.”—1 Fal. 6:11-13.

5, 6. Kulikuwa na matokeo gani Sulemani alipoacha kuwa mshikamanifu kwa Mungu?

5 Alipozeeka, Sulemani aliacha kuwa mwaminifu kwa Yehova naye akaanza kushiriki katika ibada ya uwongo. (1 Fal. 11:4-6) Hatua kwa hatua, Sulemani aliacha kutii sheria za Yehova na akawakandamiza sana watu. Aliwakandamiza watu sana hivi kwamba baada ya kifo chake, watu waliendelea kulalamika kumhusu kwa mwana na mrithi wake, Rehoboamu, na kumwomba awapunguzie nira nzito. (1 Fal. 12:4) Yehova alihisi jinsi gani Sulemani alipoacha kuwa mwaminifu?

6 Biblia inatuambia hivi: “Yehova akamkasirikia Sulemani, kwa sababu moyo wake ulikuwa umegeuka ukamwacha . . . Mungu wa Israeli, yeye aliyemtokea mara mbili.” Yehova akamwambia Sulemani: “Kwa sababu . . . hukushika agano langu na sheria zangu nilizokuamuru, hakika nitaurarua ufalme kutoka kwako, nami nitampa mtumishi wako.”—1 Fal. 11:9-11.

7. Ingawa Sulemani alikataliwa, Yehova aliwajali jinsi gani washikamanifu Wake?

7 Kisha, Yehova akamtuma nabii Ahiya amtie mafuta mkombozi. Mkombozi huyo alikuwa Yeroboamu, mwanamume mwenye uwezo aliyefanya kazi katika serikali ya Sulemani. Ingawa Yehova alibaki mshikamanifu kwa agano la Ufalme alilofanya na Daudi, Alikubali serikali ya makabila 12 igawanyike. Yeroboamu angepewa makabila kumi; na mawili yangebaki katika familia ya ukoo wa Daudi, ambayo sasa iliwakilishwa na Mfalme Rehoboamu. (1 Fal. 11:29-37; 12:16, 17, 21) Yehova alimwambia Yeroboamu hivi: “Itatukia kwamba, ukitii yote ambayo nitakuamuru, nawe utembee katika njia zangu na kwa kweli ufanye yaliyo sawa machoni pangu kwa kushika sheria zangu na amri zangu, kama Daudi mtumishi wangu alivyofanya, mimi pia nitakuwa pamoja nawe, nami nitakujengea nyumba yenye kudumu, kama nilivyomjengea Daudi, nami nitakupa Israeli.” (1 Fal. 11:38) Yehova alichukua hatua ili kuwasaidia watu wake naye akatayarisha njia ili kuwatoa katika ukandamizaji huo.

8. Ni majaribu gani yanayowapata watu wa Mungu leo?

8 Leo ukandamizaji na ukosefu wa haki umeenea. Andiko la Mhubiri 8:9 linasema hivi: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” Huenda biashara zenye pupa na utawala wenye ufisadi ukafanya hali za kiuchumi ziwe ngumu. Mara nyingi viongozi katika serikali, biashara, na dini ni mifano mibaya kiadili. Kwa hiyo, kama Loti aliyekuwa mwadilifu, washikamanifu wa Mungu leo ‘wanataabishwa sana na kule kujitia mno katika mwenendo mpotovu kwa watu wanaokaidi sheria.’ (2 Pet. 2:7) Zaidi ya hayo, ingawa tunajitahidi sana kuishi kulingana na viwango vya Mungu bila kuwasumbua watu wengine, mara nyingi tunakuwa shabaha ya mateso kutoka kwa watawala wenye kiburi.—2 Tim. 3:1-5, 12.

9. (a) Tayari Yehova amefanya nini ili kuwakomboa watu wake? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote Yesu atakuwa mshikamanifu kwa Mungu?

9 Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kuhusu ukweli huu wa msingi: Yehova hatawaacha washikamanifu wake! Hebu fikiria hatua ambazo tayari amechukua ili kuwaondoa watawala wa ulimwengu waliopotoka. Ufalme wa Kimasihi wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo Yesu tayari umesimamishwa. Yesu Kristo amekuwa akitawala mbinguni kwa karibu miaka mia moja sasa. Hivi karibuni atawaletea kitulizo kamili wale wanaoliogopa jina la Mungu. (Soma Ufunuo 11:15-18.) Tayari Yesu amejithibitisha mwenyewe kuwa mshikamanifu kwa Mungu mpaka kifo. Hatawakatisha tamaa raia wake, kama Sulemani alivyofanya.—Ebr. 7:26; 1 Pet. 2:6.

10. (a) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini Ufalme wa Mungu? (b) Tunapokabili majaribu, tunaweza kuwa na uhakika gani?

10 Ufalme wa Mungu ni serikali halisi ambayo itakomesha ukandamizaji wote. Tunamtii Yehova Mungu na Ufalme wake. Tukiwa na uhakika kabisa katika Ufalme, tunauchukia kabisa ulimwengu usiomwogopa Mungu na tunafuatilia kwa bidii kazi njema. (Tito 2:12-14) Tunajitahidi kubaki bila doa kutokana na ulimwengu huu. (2 Pet. 3:14) Hata tukikabili majaribu gani sasa, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatulinda tusipatwe na madhara ya kiroho. (Soma Zaburi 97:10.) Zaidi ya hayo, Zaburi 116:15 inatuhakikishia hivi: “Ni chenye thamani machoni pa Yehova kifo cha washikamanifu wake.” Watumishi wa Yehova ni wenye thamani sana machoni pake hivi kwamba hataruhusu kamwe waangamie wakiwa kikundi.

Wanapokabili Uvutano Mbalimbali wa Uasi-Imani

11. Yeroboamu aliacha jinsi gani kuwa mshikamanifu?

11 Utawala wa Mfalme Yeroboamu ungewaletea watu wa Mungu kitulizo fulani. Badala yake, matendo yake yalijaribu hata zaidi ushikamanifu wao kwa Mungu. Kwa kuwa hakuridhika na heshima na pendeleo alilokuwa tayari amepewa, Yeroboamu alianza kutafuta njia za kuimarisha cheo chake. Alifikiri hivi: “Watu hawa wakiendelea kwenda kutoa dhabihu katika nyumba ya Yehova huko Yerusalemu, moyo wa watu hawa pia utarudi kwa bwana wao, Rehoboamu mfalme wa Yuda; nao hakika wataniua na kurudi kwa Rehoboamu mfalme wa Yuda.” Hivyo, Yeroboamu akaanzisha dini mpya iliyotegemea ndama wawili wa dhahabu. “Kisha akaweka mmoja kule Betheli, na mwingine akamweka kule Dani. Na jambo hilo likaja kusababisha dhambi, na watu wakaanza kwenda mpaka kule Dani mbele ya yule aliyekuwa huko. Naye akaanza kujenga nyumba ya mahali pa juu na kuweka makuhani kutoka kwa watu wa kawaida, ambao hawakuwa wa wana wa Lawi.” Yeroboamu hata akaanzisha siku yake mwenyewe ya “sherehe kwa ajili ya wana wa Israeli,” naye akaanza “kutoa matoleo juu ya madhabahu ili kufukiza moshi wa dhabihu.”—1 Fal. 12:26-33.

12. Washikamanifu wa Mungu katika ufalme wa kaskazini walifanya nini Yeroboamu alipoanzisha ibada ya ndama huko Israeli?

12 Sasa washikamanifu wa Mungu katika ufalme wa kaskazini wangefanya nini? Walawi waliokuwa wakiishi katika majiji waliyopewa katika eneo la ufalme wa kaskazini walichukua hatua mara moja kama walivyofanya mababu wao waaminifu. (Kut. 32:26-28; Hes. 35:6-8; Kum. 33:8, 9) Waliacha urithi wao wote, wakahamishia familia zao kusini huko Yuda, ambako wangeendelea kumwabudu Yehova bila vipingamizi. (2 Nya. 11:13, 14) Waisraeli wengine ambao walikuwa wakiishi kwa muda huko Yuda waliamua kubaki Yuda badala ya kurudi nyumbani. (2 Nya. 10:17) Yehova alihakikisha kwamba njia ya kurudia ibada ya kweli iliachwa wazi ili katika vizazi vya baadaye wengine kutoka katika ufalme wa kaskazini waweze kuacha ibada ya ndama na kurudi Yuda.—2 Nya. 15:9-15.

13. Katika nyakati za kisasa, watu wa Mungu wamejaribiwa jinsi gani na uvutano wa waasi-imani?

13 Waasi-imani na uvutano wao ni hatari kwa watu wa Mungu leo. Watawala fulani wamejaribu kuanzisha dini yao ya taifa na kuwasukuma raia wao waikubali. Makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo na watu wengine wenye kimbelembele wamejaribu kujinyakulia ukuhani wa kiroho. Hata hivyo, Wakristo wa kweli tu ndio walio na watiwa-mafuta wa kweli, wanaofanyiza “ukuhani wa kifalme.”—1 Pet. 2:9; Ufu. 14:1-5.

14. Tunapaswa kuchukua hatua gani kuelekea mawazo ya waasi-imani?

14 Kama Walawi waaminifu wa karne ya kumi K.W.K., washikamanifu wa Mungu leo hawadanganywi na mawazo ya waasi-imani. Watiwa-mafuta na washiriki wenzao Wakristo wanaepuka na kukataa kabisa mawazo ya waasi-imani. (Soma Waroma 16:17.) Ingawa tunajitiisha kwa kupenda kwa mamlaka za serikali katika mambo ya kimwili na hatuungi mkono upande wowote katika mizozo ya ulimwengu, tunashikamana na Ufalme wa Mungu. (Yoh. 18:36; Rom. 13:1-8) Tunakataa madai ya uwongo ya wale wanaodai kumtumikia Mungu lakini wanamvunjia heshima kwa mwenendo wao.—Tito 1:16.

15. Kwa nini “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anastahili ushikamanifu wetu?

15 Fikiria pia ukweli wa kwamba Yehova amefungua njia ili watu wenye mioyo minyoofu watoke, kwa njia ya mfano, katika ulimwengu mwovu, na kuingia katika paradiso ya kiroho ambayo ametokeza. (2 Kor. 12:1-4) Tukiwa na mioyo iliyojaa shukrani, tunabaki karibu na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa.” Kristo amemweka rasmi mtumwa huyo “juu ya mali zake zote.” (Mt. 24:45-47) Kwa hiyo, hata ikiwa sisi binafsi hatuelewi kikamili msimamo fulani wa jamii ya mtumwa, hiyo si sababu ya kukataa jamii hiyo au kurudi tena katika ulimwengu wa Shetani. Badala yake, ushikamanifu utatuchochea kutenda kwa unyenyekevu na kumngojea Yehova afunue mambo waziwazi.

Wanapotimiza Migawo Ambayo Wamepewa na Mungu

16. Nabii fulani kutoka Yuda alipewa mgawo gani?

16 Yehova alimhukumu Yeroboamu kwa sababu ya uasi-imani. Yehova alimtuma nabii fulani kutoka Yuda aende kaskazini mpaka Betheli ili amwone Yeroboamu alipokuwa akifukiza moshi wa dhabihu kwenye madhabahu. Nabii huyo alipaswa kumpa Yeroboamu ujumbe wa hukumu wenye kushtua. Bila shaka, huo ulikuwa mgawo mgumu.—1 Fal. 13:1-3.

17. Yehova alimlinda mjumbe wake jinsi gani?

17 Yeroboamu alikasirika sana aliposikia hukumu ya Yehova. Akamnyooshea mkono mwakilishi wa Mungu na kuwapaazia sauti wanaume waliokuwa karibu, akisema: “Mkamateni!” Lakini papo hapo, kabla mtu yeyote hajatenda, ‘mkono aliomnyooshea ukapooza, naye hakuweza kuurudisha nyuma kwake. Na ile madhabahu ikapasuka hivi kwamba majivu yenye mafuta yakamwagika kutoka katika madhabahu.’ Yeroboamu alilazimika kumwomba nabii huyo autulize uso wa Yehova na kusali ili mkono huo uliopooza uponywe. Nabii huyo alifanya hivyo, na mkono ukapona. Hivyo, Yehova alimlinda mjumbe wake asipatwe na madhara.—1 Fal. 13:4-6.

18. Yehova anatulinda jinsi gani tunapomtolea utumishi mtakatifu bila woga?

18 Tunaposhiriki kwa ushikamanifu katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi, nyakati nyingine tunakutana na watu wenye ubaridi, au hata wakali. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Lakini hatupaswi kamwe kuruhusu woga wa kupingwa na watu upunguze bidii yetu katika huduma. Kama yule nabii asiyetajwa jina katika siku za Yeroboamu, tuna “pendeleo la kumtolea [Yehova] utumishi mtakatifu bila woga kwa ushikamanifu.” * (Luka 1:74, 75) Ingawa leo hatutazamii tulindwe kimuujiza, bado Yehova anatulinda na kututegemeza tukiwa Mashahidi wake kupitia roho yake takatifu na malaika. (Soma Yohana 14:15-17; Ufunuo 14:6.) Mungu hatawaacha kamwe wale wanaoendelea kusema neno lake bila woga.—Flp. 1:14, 28.

Yehova Atawalinda Washikamanifu Wake

19, 20. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hatatuacha kamwe? (b) Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika habari inayofuata?

19 Yehova ni Mungu wetu mshikamanifu. (Ufu. 15:4; 16:5) Yeye ni “mshikamanifu katika kazi zake zote.” (Zab. 145:17) Na Biblia inatuhakikishia hivi: “Atailinda njia ya washikamanifu wake.” (Met. 2:8) Washikamanifu wa Mungu wanapokabili majaribu au mawazo ya uasi-imani au wanapotimiza mgawo mgumu, wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawaongoza na kuwategemeza.

20 Jambo ambalo kila mmoja wetu anapaswa kufikiria sasa ni hili: Ni nini kitakachonisaidia kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova hata ninapopatwa na majaribu au vishawishi vya aina yoyote? Yaani, ninaweza kuuimarisha jinsi gani ushikamanifu wangu kwa Mungu?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Makala inayofuata itaonyesha ikiwa nabii huyo aliendelea kumtii Yehova na yale yaliyompata baadaye.

Ungesema Nini?

• Ni kwa njia gani Yehova ameonyesha kwamba hawaachi washikamanifu wake wanapokandamizwa?

• Tunapaswa kutenda jinsi gani kuelekea waasi-imani na mawazo yao?

• Yehova anawalinda jinsi gani washikamanifu wake wanaposhiriki katika huduma ya Kikristo?

[Maswali ya Funzo]

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 5]

 

UFALME WA KASKAZINI (Yeroboamu)

Dani

SHEKEMU

Betheli

UFALME WA KUSINI (Rehoboamu)

YERUSALEMU

[Picha]

Yehova hakuwaacha washikamanifu wake wakati Yeroboamu alipoanzisha ibada ya ndama

[Picha katika ukurasa wa 3]

Baraka ambazo Sulemani na raia wake walifurahia zilikuwa na masharti