Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha “Kamba Yenye Nyuzi Tatu” Katika Ndoa

Dumisha “Kamba Yenye Nyuzi Tatu” Katika Ndoa

Dumisha “Kamba Yenye Nyuzi Tatu” Katika Ndoa

“Kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.”—MHU. 4:12.

1. Ni nani aliyemuunganisha mwanamume na mwanamke wa kwanza katika ndoa?

BAADA ya kuumba mimea na wanyama, Yehova Mungu alimuumba mwanadamu wa kwanza, Adamu. Baadaye, Mungu alimfanya Adamu alale usingizi mzito, naye Mungu alitumia ubavu mmoja wa Adamu kumfanyia msaidizi mkamilifu. Adamu alipomwona mwanamke, akasema: “Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu.” (Mwa. 1:27; 2:18, 21-23) Yehova alifurahishwa na kazi hiyo ya uumbaji, naye akamuunganisha mwanamume na mwanamke wa kwanza katika ndoa na kuwabariki.—Mwa. 1:28; 2:24.

2. Ni kwa njia gani Shetani alitokeza pengo kati ya Adamu na Hawa?

2 Inasikitisha kwamba baada ya muda mfupi tu mpango wa ndoa ulioanzishwa na Mungu ulishambuliwa. Jinsi gani? Roho fulani mwovu, ambaye baadaye aliitwa Shetani, alimdanganya Hawa ale kutokana na mti mmoja tu ambao wenzi hao wa ndoa walikuwa wamekatazwa. Muda mfupi baadaye, Adamu aliungana na mke wake kupinga haki ya Mungu ya kutawala na kukataa mwongozo wake mzuri. (Mwa. 3:1-7) Yehova alipowauliza wenzi hao wamefanya nini, ilionekana wazi kwamba tayari uhusiano wao ulikuwa na matatizo. Adamu alimlaumu mke wake, akisema: “Mwanamke uliyenipa awe pamoja nami, alinipa tunda kutoka katika ule mti nami nikala.”—Mwa. 3:11-13.

3. Wayahudi fulani walikuwa na maoni gani yasiyofaa?

3 Katika karne zote tangu wakati huo, Shetani ametumia mbinu mbalimbali za ujanja kusababisha mgawanyiko katika ndoa. Kwa mfano, nyakati nyingine amewatumia viongozi wa dini kuendeleza maoni fulani kuhusu ndoa ambayo hayapatani na maandiko. Viongozi fulani Wayahudi walipunguza uzito wa kanuni za Mungu kwa kuwaruhusu waume kuwataliki wake zao kwa sababu ndogo-ndogo kama vile kutia chumvi nyingi mno katika chakula. Lakini Yesu alisema: “Mtu yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine, ila kwa sababu ya uasherati, anafanya uzinzi.”—Mt. 19:9.

4. Mpango wa ndoa unashambuliwa jinsi gani leo?

4 Shetani angali anajitahidi sana kuvunja ndoa. Ndoa za watu wa jinsia moja, wanaume na wanawake wanaoishi pamoja bila kufunga ndoa, na talaka zinazofanywa kwa sababu ndogo-ndogo ni kati ya mambo yanayoonyesha kwamba anafanikiwa sana. (Soma Waebrania 13:4.) Tukiwa Wakristo, tunaweza kufanya nini ili tusiwe na maoni hayo yasiyofaa kuhusu ndoa? Acheni tuchunguze mambo fulani yanayofanya ndoa iwe yenye furaha na mafanikio.

Mhusishe Yehova Katika Ndoa Yako

5. Maneno “kamba yenye nyuzi tatu” yanamaanisha nini yanapotumiwa kuhusu ndoa?

5 Ili ndoa ifanikiwe, Yehova anapaswa kuhusishwa katika uhusiano huo. Neno lake linasema hivi: “Kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.” (Mhu. 4:12) Maneno “kamba yenye nyuzi tatu” ni ya mfano. Mfano huo unapotumiwa kuhusu ndoa, mume na mke ndio kamba mbili za kwanza, nao wamesokotwa pamoja na kamba ya katikati, ambayo ni Yehova Mungu. Wenzi wa ndoa wanapounganishwa pamoja na Mungu wanapata nguvu za kiroho za kushughulikia matatizo, na hiyo ndiyo siri ya kuwa na furaha nyingi katika ndoa.

6, 7. (a) Wakristo wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba Mungu yuko katika ndoa yao? (b) Dada mmoja anathamini mambo gani kumhusu mume wake?

6 Lakini wenzi wa ndoa wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba ndoa yao ni kama kamba hiyo yenye nyuzi tatu? Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zab. 40:8) Vivyo hivyo, kumpenda Mungu kunatuchochea kumtumikia kwa moyo kamili. Hivyo, wenzi wote wa ndoa wanapaswa kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kufurahia kufanya mapenzi yake. Wenzi wa ndoa pia wanapaswa kuwasaidia wenzi wao kumpenda Mungu zaidi.—Met. 27:17.

7 Ikiwa kweli sheria ya Mungu imo ndani yetu, tutaonyesha sifa kama vile imani, tumaini, na upendo, sifa ambazo zitatusaidia kuimarisha muungano wa ndoa. (1 Kor. 13:13) Mkristo anayeitwa Sandra, ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 50, anasema hivi: “Kile kinachonivutia zaidi kuhusu mume wangu ni mwongozo na mashauri ya kiroho anayotoa na upendo wake kwa Yehova, ambao ni wenye nguvu zaidi kuliko upendo wake kwangu.” Enyi waume, je, wake zenu wanaweza kusema hivyo kuwahusu?

8. Ni jambo gani linalohitajiwa ili kupokea “thawabu nzuri” katika ndoa?

8 Mkiwa wenzi wa ndoa, je, mnatanguliza maishani mwenu mambo ya kiroho na mambo yanayohusu Ufalme? Zaidi ya hilo, je, kweli unamwona mwenzi wako wa ndoa kuwa mfanyakazi mwenzako katika utumishi wa Yehova? (Mwa. 2:24) Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu.” (Mhu. 4:9) Kwa kweli, ni lazima mume na mke wajitahidi sana ili wapate “thawabu nzuri,” yaani, muungano wenye upendo na wa kudumu ambao una baraka za Mungu.

9. (a) Waume wana madaraka gani? (b) Kulingana na Wakolosai 3:19, mume anapaswa kumtendea mke wake jinsi gani?

9 Jambo moja linaloonyesha kwamba Mungu yuko katika ndoa ni jitihada ambayo mume na mke wanafanya ili kutimiza matakwa Yake. Waume wana daraka la msingi la kuwaandalia watu wa familia zao kimwili na kiroho. (1 Tim. 5:8) Pia wanahimizwa wajali mahitaji ya kihisia ya wake zao. Andiko la Wakolosai 3:19 linasema: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.” Msomi mmoja wa Biblia alieleza kwamba maneno ‘kukasirikia kwa uchungu’ yanatia ndani “kuwarushia maneno makali, au kuwapiga, na kutowaonyesha upendo, kutowajali, kutowaandalia mahitaji yao, kutowalinda, na kutowasaidia.” Ni wazi kwamba mwenendo kama huo haufai katika nyumba ya Kikristo. Mume anapoonyesha ukichwa wake kwa njia ya upendo, mke wake atachochewa hata zaidi kujitiisha kwake.

10. Wake Wakristo wanapaswa kuwa na mtazamo gani?

10 Ni lazima wake Wakristo wanaojitahidi kumweka Yehova katika ndoa yao watimize pia matakwa ya Mungu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko.” (Efe. 5:22, 23) Shetani alimdanganya Hawa na kueneza uwongo kwamba kutomtegemea Mungu kutaleta furaha ya kudumu. Roho hiyo ya kujitegemea inaonekana wazi katika ndoa nyingi leo. Hata hivyo, wake walio na maoni ya Mungu kuhusu ndoa hawachukii kujitiisha chini ya kichwa chao mwenye upendo. Wanakumbuka kwamba Yehova alimweka Hawa kuwa “kikamilisho” cha mume wake, na Mungu aliona daraka hilo kuwa lenye kuheshimika. (Mwa. 2:18) Mke Mkristo anayeunga mkono mpango huo kwa kupenda ni “taji” kwa mume wake.—Met. 12:4.

11. Ndugu mmoja alisema ni mambo gani ambayo yameisaidia ndoa yake?

11 Jambo lingine litakalowasaidia wenzi wa ndoa kumhusisha Mungu katika ndoa yao ni kujifunza Neno la Mungu pamoja. Gerald, ambaye amefurahia ndoa kwa miaka 55, anasema, “Jambo la maana zaidi linaloweza kufanya ndoa ifanikiwe ni kusoma na kujifunza Biblia pamoja.” Anaongeza hivi, “Kufanya mambo pamoja, hasa mambo ya kiroho, kunafanya wenzi wa ndoa wawe na uhusiano wa karibu kati yao na pamoja na Yehova.” Kujifunza Biblia pamoja kunasaidia familia kukumbuka waziwazi kanuni za Yehova, kuwa imara kiroho, na kufanya maendeleo zaidi.

12, 13. (a) Kwa nini ni jambo la maana sana kwa wenzi wa ndoa kusali pamoja? (b) Ni shughuli gani nyingine za kiroho zinazoimarisha ndoa?

12 Wenzi wa ndoa wenye furaha wanasali pamoja pia. Mume ‘anapomimina moyo wake’ kwa kutoa maombi yaliyo wazi kuhusu hali zao, muungano wa ndoa utaimarika. (Zab. 62:8) Kwa mfano, ni rahisi zaidi kutatua hali ya kutoelewana pamoja na mwenzi wako baada ya kusali pamoja na kumwomba Mweza-Yote mwongozo! (Mt. 6:14, 15) Kupatana na sala hiyo, inafaa kama nini kwa wenzi wote wawili kuazimia kusaidiana na ‘kuendelea kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.’ (Kol. 3:13) Kumbuka kwamba sala inaonyesha kuwa mtu anamtegemea Mungu. Mfalme Daudi alisema: “Macho ya wote yanakutazama yakiwa na tumaini.” (Zab. 145:15) Tunapomtazama Mungu tukiwa na tumaini tunaposali, mahangaiko yetu yanapungua kwa sababu ya kujua kwamba ‘anatujali.’—1 Pet. 5:7.

13 Njia nyingine kuu ya kumhusisha Yehova katika ndoa ni kuhudhuria mikutano ya kutaniko na kuhubiri pamoja. Kwenye mikutano, wenzi wa ndoa wanajifunza jinsi ya kushinda “hila” ambazo Shetani anatumia kugawanya familia. (Efe. 6:11) Na mume na mke ambao wanahubiri pamoja kwa ukawaida wanajifunza ‘kuwa imara, na thabiti.’—1 Kor. 15:58.

Matatizo Yanapotokea

14. Ni mambo gani yanayoweza kusababisha mikazo katika ndoa?

14 Ni kweli kwamba huenda mapendekezo hayo si mapya, lakini mbona usiyazungumzie waziwazi pamoja na mwenzi wako? Tambueni ikiwa kuna jambo mnalohitaji kufanyia maendeleo zaidi katika ndoa yenu. Hata hivyo, Biblia inakubali kwamba hata wale ambao wanamhusisha Mungu katika ndoa yao “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Kor. 7:28) Kwa sababu ya kutokamilika kwa wanadamu, uvutano mbaya wa ulimwengu huu usiotii sheria, na mitego ya Ibilisi, hata ndoa za watumishi waaminifu wa Mungu zinaweza kukabili mikazo mingi. (2 Kor. 2:11) Lakini Yehova anatuwezesha kukabiliana na mikazo hiyo. Ndiyo, inawezekana. Mwanamume mwaminifu Ayubu alipoteza mifugo yake, watumishi wake, na watoto wake. Hata hivyo, Biblia inasema: “Katika hayo yote Ayubu hakutenda dhambi, wala kumhesabia Mungu jambo lolote lisilofaa.”—Ayu. 1:13-22.

15. Mikazo inaweza kumfanya mtu atende jinsi gani, na wenzi wa ndoa wanaweza kushughulikia hali hizo jinsi gani?

15 Lakini, mke wa Ayubu, alimwambia Ayubu hivi: “Je, bado unashikilia sana utimilifu wako? Mlaani Mungu, ufe!” (Ayu. 2:9) Ndiyo, misiba au hali nyingine ngumu zinapotokea, mtu anaweza kutenda bila kufikiri kwa sababu ya kuumia kihisia. Yule mwanamume mwenye hekima alisema hivi: “Uonevu mtupu unaweza kumfanya mtu mwenye hekima atende kiwazimu.” (Mhu. 7:7) Mwenzi wako akikurushia maneno yenye kuumiza kwa sababu anakabili hali ngumu au “uonevu,” jitahidi kutulia. Kulipiza kisasi kunaweza kumfanya mmoja wenu au nyote wawili kusema mambo yanayoweza kufanya hali iwe mbaya zaidi. (Soma Zaburi 37:8.) Kwa hiyo, puuza “mazungumzo ya ovyoovyo” ambayo huenda yamesemwa kwa sababu ya kufadhaika au kuvunjika moyo.—Ayu. 6:3.

16. (a) Maneno ya Yesu kwenye Mathayo 7:1-5 yanahusu ndoa jinsi gani? (b) Kwa nini usawaziko ni wa maana sana katika ndoa?

16 Wenzi wa ndoa wanapaswa kuwa na matarajio yanayofaa. Mwenzi mmoja anaweza kuona kasoro za yule mwenzi mwingine na kufikiri, ‘Ninaweza kumbadili.’ Kwa upendo na subira, huenda ukamsaidia mwenzi wako kufanya maendeleo hatua kwa hatua. Hata hivyo, usisahau kwamba Yesu alimlinganisha mtu anayechambua-chambua makosa madogo ya mwenzake na mtu anayeona “unyasi” ulio katika jicho la ndugu yake lakini anakosa kuona “boriti” lililo katika jicho lake mwenyewe. Yesu alituhimiza hivi: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe.” (Soma Mathayo 7:1-5.) Hilo halimaanishi kwamba makosa mazito yanapaswa kupuuzwa. Robert, ambaye amefunga ndoa kwa karibu miaka 40, alisema: “Ili wenzi wa ndoa waseme mambo waziwazi na kuwa tayari kukubali maoni ya kweli huenda wakahitaji kubadili mtazamo wao.” Kwa hiyo, uwe mwenye usawaziko. Badala ya kuudhika kwa sababu mwenzi wako hana sifa fulani, jifunze kuthamini na kufurahia sifa nzuri alizo nazo sasa.Mhu. 9:9.

17, 18. Matatizo yanapoongezeka, tunaweza kupata wapi msaada?

17 Majaribu yanaweza kutokea hali zinapobadilika katika maisha. Wenzi wa ndoa wanaweza kukabili magumu fulani wanapopata watoto. Huenda mwenzi wa ndoa au mtoto akawa mgonjwa sana. Huenda wazazi waliozeeka wakahitaji kutunzwa kwa njia ya pekee. Watoto wanapokua, huenda wakahamia mbali sana kutoka nyumbani. Mabadiliko mengine yanaweza kutokea kwa sababu ya mapendeleo na madaraka mengine ya kiroho. Mabadiliko yote hayo yanaweza kusababisha mikazo na mahangaiko katika uhusiano wa ndoa.

18 Unaweza kufanya nini ikiwa umevunjika moyo kwa sababu ya mkazo ulio katika ndoa yako? (Met. 24:10) Usikate tamaa! Shetani anataka sana kumwona mmoja wa watumishi wa Mungu akiacha ibada safi. Anaweza kufurahi hata zaidi akiona wenzi wa ndoa wakifanya hivyo. Basi, fanya yote unayoweza kuhakikisha kwamba ndoa yako ni kama kamba yenye nyuzi tatu. Biblia ina masimulizi mengi ya watu walioendelea kuwa waaminifu hata walipopatwa na majaribu makali. Kwa mfano, pindi moja, Daudi alimimina moyo wake mbele za Yehova, akisema: “Unionyeshe kibali, Ee Mungu, kwa sababu mwanadamu anayeweza kufa . . . anaendelea kunikandamiza.” (Zab. 56:1) Je, umewahi kukandamizwa na “mwanadamu anayeweza kufa”? Hata ikiwa mkazo unaohisi unatokana na mtu wa mbali au mtu wa karibu, kumbuka jambo hili: Daudi alipata nguvu za kuvumilia, nawe unaweza kuvumilia pia. Daudi alisema hivi: “Nilimuuliza Yehova, naye akanijibu, naye akanikomboa kutoka katika mambo yote yenye kuniogopesha.”—Zab. 34:4.

Baraka Zaidi

19. Tunaweza kuepuka mashambulizi ya Shetani kwa njia gani?

19 Katika nyakati hizi za mwisho, wenzi wa ndoa wanahitaji ‘kuendelea kufarijiana na kujengana.’ (1 The. 5:11) Usisahau kuwa Shetani anaamini kwamba sisi ni washikamanifu kwa Yehova kwa sababu ya ubinafsi. Atatumia njia yoyote ile, kutia ndani kuivunja ndoa, ili tuache kuwa watimilifu kwa Mungu. Ili kuepuka mashambulizi ya Shetani, tunahitaji kumtegemea Yehova kabisa. (Met. 3:5, 6) Paulo aliandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—Flp. 4:13.

20. Ni baraka gani zinazotokana na kumhusisha Mungu katika ndoa?

20 Kuna baraka nyingi zinazotokana na kumhusisha Mungu katika ndoa. Joel na mke wake, ambao wamekuwa katika ndoa kwa miaka 51, wamejionea jambo hilo. Joel anasema: “Ninamshukuru Yehova daima kwa kunipa mke na furaha katika uhusiano wetu. Mke wangu ni mwenzi bora sana.” Siri yao ni nini? “Sikuzote tumejitahidi kuonyeshana fadhili, subira, na upendo.” Hakuna mmoja wetu atakayefanya hivyo kikamilifu katika mfumo huu wa mambo. Hata hivyo, acheni tujitahidi kutumia kanuni za Biblia na kumhusisha Yehova katika ndoa yetu. Tukifanya hivyo, ndoa yetu itakuwa kama “kamba yenye nyuzi tatu [ambayo] haiwezi kukatika upesi.”—Mhu. 4:12.

Je, Unakumbuka?

• Ni nini maana ya kumhusisha Yehova katika ndoa?

• Wenzi wa ndoa wanapaswa kufanya nini matatizo yanapotokea?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba Mungu yuko katika ndoa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kusali pamoja kunawasaidia wenzi wa ndoa kukabiliana na hali ngumu