Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ipinge “Roho ya Ulimwengu”

Ipinge “Roho ya Ulimwengu”

Ipinge “Roho ya Ulimwengu”

“Tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu.”—1 KOR. 2:12.

1, 2. (a) Kwa nini ndege walikuwa wakiwekwa katika migodi huko Uingereza? (b) Wakristo wanakabili hatari gani?

MWAKA wa 1911, wenye mamlaka nchini Uingereza walitunga sheria ili kuokoa uhai wa wachimbaji wa migodi ya makaa ya mawe. Kila mgodi ulipaswa kuwa na ndege wawili wanaoitwa kurumbiza. Kwa nini? Ikiwa moto ungetokea katika mgodi, waokoaji wangewapeleka ndege hao chini ya ardhi. Ndege hao wadogo wanaweza kutambua gesi zenye sumu, kama vile kaboni monoksidi. Ikiwa hewa ingechafuliwa na gesi hizo, ndege hao wangeweza kuonyesha dalili za kwamba wanateseka, na hata kuanguka. Onyo hilo la mapema lilikuwa la maana. Kaboni monoksidi ni gesi isiyo na rangi, isiyo na harufu, na inayoua kwa kuzuia chembe nyekundu za damu zisipitishe oksijeni ndani ya mwili. Ikiwa waokoaji hao hawangeonywa, wangezimia na kufa bila kutambua kwamba wanapumua hewa yenye sumu.

2 Katika maana ya kiroho, Wakristo wanakabili hali kama ile iliyowakabili wachimbaji hao wa migodi. Jinsi gani? Yesu alipowapa wanafunzi wake mgawo wa kuhubiri habari njema ulimwenguni pote, alijua kwamba anawatuma katika eneo hatari, ambalo linatawaliwa na Shetani na roho ya ulimwengu. (Mt. 10:16; 1 Yoh. 5:19) Yesu aliwahangaikia sana wanafunzi wake hivi kwamba usiku uliotangulia kifo chake, alisali hivi kwa Baba yake: “Ninakuomba, si kwamba uwatoe ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu.”—Yoh. 17:15.

3, 4. Yesu aliwapa wanafunzi wake onyo gani, na kwa nini tupendezwe nalo?

3 Yesu aliwaonya wafuasi wake kuhusu hatari ambayo ingesababisha wasinzie na kufa kiroho. Maneno yake yanatuhusu sana, kwa kuwa tunaishi wakati wa umalizio wa mfumo wa mambo. Aliwahimiza wanafunzi wake hivi: “Endeleeni kukesha . . . ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.” (Luka 21:34-36) Hata hivyo, inatia moyo kwamba Yesu aliahidi pia kuwa Baba yake angewapa roho takatifu ambayo ingewakumbusha mambo na kuwasaidia kuwa macho na imara.—Yoh. 14:26.

4 Namna gani sisi leo? Je, roho hiyo takatifu inaweza kutusaidia? Ikiwa ndivyo, ni lazima tufanye nini ili tuipokee? Roho ya ulimwengu ni nini, nayo inatenda kazi jinsi gani? Nasi tunaweza kufanya nini ili kupinga roho ya ulimwengu huu?—Soma 1 Wakorintho 2:12.

Roho Takatifu au Roho ya Ulimwengu?

5, 6. Roho takatifu inaweza kutusaidia jinsi gani, lakini ni lazima tufanye nini ili tuipokee?

5 Si watu wa karne ya kwanza tu waliopokea roho takatifu. Badala yake, inatumika sana hata leo, na roho ya Mungu inaweza kututia nguvu kufanya yaliyo sawa na kutuimarisha katika utumishi wake. (Rom. 12:11; Flp. 4:13) Pia inaweza kutusaidia kusitawisha sifa nzuri kama vile upendo, fadhili, na wema, ambazo ni sehemu ya “matunda ya roho.” (Gal. 5:22, 23) Hata hivyo, Yehova Mungu hawalazimishi watu wapokee roho yake takatifu ikiwa hawaitaki.

6 Hivyo basi, ni vizuri tujiulize, ‘Ninaweza kufanya nini ili niipokee roho takatifu?’ Biblia inaonyesha kwamba kuna mambo fulani tunayoweza kufanya. Hatua moja ya maana ni ile ya moja kwa moja, yaani, kumwomba Mungu akupe roho takatifu. (Soma Luka 11:13.) Hatua nyingine ni kujifunza na kutumia mashauri yaliyo katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (2 Tim. 3:16) Bila shaka, si kila mtu anayesoma tu Biblia ambaye anaipokea roho ya Mungu. Lakini Mkristo mnyoofu anapojifunza Neno la Mungu, anaweza kupata hisia na mtazamo unaopatana na Neno hilo lililoongozwa na roho. Pia ni jambo la maana tukubali kwamba Yehova amemweka Yesu kuwa mwakilishi Wake na kwamba Mungu amemtumia kutupa roho yake. (Kol. 2:6) Kwa hiyo, tunataka kupatanisha maisha yetu na kielelezo na mafundisho ya Yesu. (1 Pet. 2:21) Kadiri tunavyojitahidi kuwa kama Kristo, ndivyo tutakavyopokea zaidi roho takatifu.

7. Roho ya ulimwengu inawachochea watu jinsi gani?

7 Kinyume cha hilo, roho ya ulimwengu inawachochea watu kuwa na utu kama wa Shetani. (Soma Waefeso 2:1-3.) Roho ya ulimwengu inatenda kazi katika njia mbalimbali. Inawachochea watu kuasi kanuni za Mungu, nasi tunaona jambo hilo waziwazi kila mahali. Inachochea “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani.” (1 Yoh. 2:16) Inatokeza matendo ya mwili, kama vile uasherati, ibada ya sanamu, kuwasiliana na pepo, wivu, milipuko ya hasira, na ulevi. (Gal. 5:19-21) Na inawachochea watu kusema maneno ya uasi-imani ambayo yanachafua mambo matakatifu. (2 Tim. 2:14-18) Kwa hakika, kadiri mtu anavyojiruhusu aongozwe na roho ya ulimwengu, ndivyo anavyozidi kuwa kama Shetani.

8. Kila mmoja wetu anaweza kuchagua nini?

8 Hatuwezi kuepuka kabisa uvutano wote wa nje. Lazima kila mtu achague atakubali kuongozwa na nini maishani—roho takatifu au roho ya ulimwengu. Wale wanaotawaliwa sasa na roho ya ulimwengu wanaweza kuikataa na kuruhusu roho takatifu iongoze maisha yao. Kwa upande mwingine, wale ambao kwa muda fulani waliongozwa na roho takatifu wanaweza kunaswa na roho ya ulimwengu. (Flp. 3:18, 19) Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kuipinga roho ya ulimwengu.

Tambua Dalili Ambazo Zinakuonya Mapema

9-11. Ni dalili gani zinazotuonya kwamba huenda tunaongozwa na roho ya ulimwengu?

9 Wachimbaji wa migodi huko Uingereza waliotajwa mwanzoni, walitumia ndege ili kutambua mapema ikiwa kuna gesi zenye sumu. Ikiwa mchimbaji angeona ndege akianguka, alijua kwamba anahitaji kuchukua hatua ya haraka ili kuokoka. Vivyo hivyo, kwa upande wa kiroho, ni dalili gani zinazoweza kutuonya mapema kwamba tunaongozwa na roho ya ulimwengu?

10 Tulipoanza kujifunza kweli za Neno la Mungu na kujiweka wakfu kwa Yehova, huenda tulisoma Biblia kwa bidii. Labda tulisali kwa bidii mara nyingi. Na tulifurahia kuhudhuria mikutano ya kutaniko, tukiona kila mkutano kuwa wenye kuburudisha kiroho, kama ambavyo maji yanavyomburudisha mtu mwenye kiu. Mazoea hayo yalitusaidia kuikataa na kuendelea kuipinga roho ya ulimwengu.

11 Je, bado tunajitahidi kusoma Biblia kila siku? (Zab. 1:2) Je, tunasali mara nyingi na kwa moyo wote? Je, tunapenda mikutano ya kutaniko na kuhudhuria yote kila juma? (Zab. 84:10) Au, je, tumeacha mengine kati ya mazoea hayo mazuri? Bila shaka, huenda tuna shughuli nyingi zinazochukua wakati na nguvu zetu, na huenda ikawa vigumu kuendelea kuwa na ratiba nzuri ya kiroho. Lakini ikiwa tumeacha mazoea fulani mazuri ambayo tulikuwa nayo, je, inawezekana kwamba sasa tunaongozwa na roho ya ulimwengu? Je, tutajitahidi sana kusitawisha tena mazoea mazuri tuliyokuwa nayo?

‘Usilemewe Kamwe’

12. Yesu aliwaambia wanafunzi wake wafanye nini, na kwa nini?

12 Tunaweza kufanya jambo gani lingine ili kupinga roho ya ulimwengu? Yesu alipowahimiza wanafunzi wake ‘waendelee kukesha,’ alikuwa ametoka tu kuwaonya waziwazi kuhusu hatari fulani. Alisema hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego.”—Luka 21:34, 35.

13, 14. Ni vyema tujiulize maswali gani kuhusu kula na kunywa?

13 Fikiria onyo hilo. Je, Yesu alikuwa akiwakataza watu wasifurahie kula na kunywa? Hapana! Alijua maneno haya ya Sulemani: “Nimekuja kujua kwamba hakuna jambo lingine bora [kwa wana wa binadamu] kuliko mtu kufurahi na kufanya mema maishani mwake; na pia kwamba kila mtu ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.” (Mhu. 3:12, 13) Ndiyo, Yesu alijua kwamba roho ya ulimwengu inafanya watu washindwe kujizuia wanapokula na kunywa.

14 Ni kwa njia gani tunaweza kuwa na hakika kwamba sumu ya roho ya ulimwengu haijatupofusha tusione hatari za kula kupita kiasi au kunywa kupita kiasi? Huenda tukajiuliza: ‘Ninachukua hatua gani ninaposoma mashauri katika Biblia au katika vichapo vyetu kuhusu ulafi? Je, nina mwelekeo wa kupuuza mashauri hayo na kuona kwamba hayanihusu au ni makali mno, na labda kutoa visababu au visingizio vya kutetea mazoea yangu? * Ikiwa ninatumia kileo, nina maoni gani kuhusu mashauri juu ya kileo, kunywa kwa kiasi, na kuepuka “vipindi vya kulewa”? Je, ninapunguza uzito wa mashauri hayo, na kuona kwamba hayanihusu? Wengine wanaponishauri kuhusu mazoea yangu ya kunywa kileo, je, ninajitetea au kukasirika? Je, ninawatia moyo wengine wasichukue kwa uzito shauri hilo la Biblia?’ Ndiyo, mtazamo wa mtu unaonyesha ikiwa anaongozwa na roho ya ulimwengu.—Linganisha na Waroma 13:11-14.

Epuka Kusongwa na Mahangaiko

15. Yesu alionya kuhusu mwelekeo gani wa wanadamu?

15 Hatua nyingine ya maana katika kuipinga roho ya ulimwengu inahusu jinsi ya kushughulikia mahangaiko. Yesu alijua kwamba tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, tuna mwelekeo wa kuhangaikia mahitaji yetu ya kila siku. Kwa upendo, aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Acheni kuhangaika.” (Mt. 6:25) Hakuna ubaya kuhangaikia mambo ya maana, kama vile kumpendeza Mungu, kushughulikia madaraka ya Kikristo, na kuandalia familia zetu mambo ya msingi maishani. (1 Kor. 7:32-34) Kwa hiyo, tunaweza kujifunza nini kutokana na onyo la Yesu?

16. Roho ya ulimwengu inafanya watu wengi wawe katika hali gani?

16 Roho ya ulimwengu, ambayo inawachochea watu kuonyesha mali zao, inawaletea wengi mahangaiko yanayowaumiza. Watu hao wanaweza kutusadikisha kwamba pesa zinaleta usalama na kwamba thamani ya mtu inapimwa, kwa ubora na wingi wa mali zake, bali si kwa sifa zake za kiroho. Wale wanaopumbazwa na uwongo huo wanajitumikisha sana ili kupata utajiri na wanahangaikia daima jinsi watakavyopata vitu vipya zaidi, vikubwa zaidi, na vya kisasa zaidi. (Met. 18:11) Maoni hayo yaliyopotoka kuhusu vitu vya kimwili yanamfanya mtu awe na mahangaiko yanayomsonga na kuzuia ukuzi wake wa kiroho.—Soma Mathayo 13:18, 22.

17. Tunaweza kufanya nini ili tusisongwe na mahangaiko?

17 Tunaweza kuepuka kusongwa na mahangaiko ikiwa tutatii amri hii ya Yesu: “Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu].” Yesu anatuhakikishia kwamba tukifanya hivyo, tutaongezewa vitu ambavyo kwa kweli tunavihitaji. (Mt. 6:33) Tunaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba tunaamini ahadi hiyo? Njia moja ni kutafuta kwanza uadilifu wa Mungu—kufuata kanuni za Mungu kuhusu mambo ya pesa. Kwa mfano, tunakataa kusema uwongo kuhusu kodi tunayostahili kutozwa, au hata kusema uwongo “mdogo-mdogo” katika shughuli zetu za biashara. Tunafanya yote tunayoweza ili kutimiza mapatano yetu kuhusu pesa, na kuacha ‘neno letu Ndiyo limaanishe Ndiyo’ inapohusu kulipa madeni. (Mt. 5:37; Zab. 37:21) Huenda mtu asiwe tajiri anapoonyesha unyoofu katika njia hizo, lakini atapata kibali cha Mungu, dhamiri safi, na kuepuka sana mahangaiko.

18. Yesu alituwekea mfano gani bora, nasi tunapata faida gani tunapomwiga?

18 Kuutafuta kwanza Ufalme kunatia ndani kutanguliza mambo ya maana zaidi maishani. Fikiria mfano wa Yesu. Nyakati nyingine, alivalia vazi la hali ya juu. (Yoh. 19:23) Alifurahia chakula na divai akiwa na marafiki wazuri. (Mt. 11:18, 19) Lakini mali na burudani zilikuwa kama vikolezo katika maisha yake, bali si chakula chenyewe. Chakula cha Yesu kilikuwa kufanya mapenzi ya Yehova. (Yoh. 4:34-36) Maisha yanafurahisha sana tunapoiga mfano wa Yesu! Tunapata shangwe ya kuwasaidia watu waliokandamizwa wapate faraja kutokana na Maandiko. Tunapendwa na kutegemezwa na kutaniko. Na tunafanya moyo wa Yehova ushangilie. Tunapotanguliza mambo ya maana zaidi, hatuwi watumwa wa mali na raha. Badala yake, vitu hivyo vinakuwa watumwa kwetu, yaani, tunavitumia au vinatusaidia kumwabudu Yehova. Na kadiri tunavyojitahidi sana kuutegemeza Ufalme wa Mungu, ndivyo inavyokuwa vigumu zaidi kushindwa na roho ya ulimwengu.

Endelea “Kukaza Akili Juu ya Roho”

19-21. Tunaweza kufanya nini ili kuendelea “kukaza akili juu ya roho,” na kwa nini tunapaswa kufanya hivyo?

19 Mawazo yanatangulia matendo. Mara nyingi mambo ambayo kwa kawaida yanaonwa kuwa matendo yasiyo ya akili yanachochewa na mawazo ya kimwili. Hivyo, mtume Paulo anatukumbusha kwamba tunahitaji kulinda mawazo yetu. Aliandika hivi: “Wale wanaopatana na mwili hukaza akili zao juu ya mambo ya mwili, lakini wale wanaopatana na roho juu ya mambo ya roho.”—Rom. 8:5.

20 Tunaweza kufanya nini ili roho ya ulimwengu isiongoze mawazo yetu—na hivyo matendo yetu? Ni lazima tuchuje mambo ambayo yanaingia katika akili zetu na kujitahidi tuwezavyo kuzuia propaganda ya ulimwengu isiingie akilini. Kwa mfano, tunapochagua burudani, hatukubali akili zetu zichafuliwe na programu zinazotukuza maadili mapotovu au jeuri. Tunatambua kwamba roho ya Mungu iliyo takatifu, au safi, haiwezi kukaa katika akili chafu. (Zab. 11:5; 2 Kor. 6:15-18) Zaidi ya hayo, tunairuhusu roho ya Mungu iongoze akili zetu kwa kuwa na mazoea ya kujifunza Biblia, kusali, kutafakari, na kuhudhuria mikutano. Na tunafanya kazi pamoja na roho hiyo tunapofanya kwa ukawaida kazi ya Kikristo ya kuhubiri.

21 Bila shaka, ni lazima tuipinge roho ya ulimwengu na tamaa za mwili zinazochochewa nayo. Lakini tunapaswa kujitahidi sana kufanya hivyo kwa sababu, kama vile Paulo alivyosema, “kukaza akili juu ya mwili humaanisha kifo, bali kukaza akili juu ya roho humaanisha uzima na amani.”—Rom. 8:6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Ulafi ni mtazamo wa akili, na mlafi anakula kupita kiasi au kwa pupa. Kwa hiyo, ulafi hauonekani kupitia ukubwa wa mwili wa mtu, bali kupitia mtazamo wake kuhusu chakula. Mtu anaweza kuwa na unene wa kadiri au hata awe mwembamba lakini bado awe mlafi. Kwa upande mwingine, mtu anaweza kuwa mzito kupita kiasi kwa sababu ya ugonjwa au anaweza kurithi hali ya kuwa mnene kupita kiasi. Jambo kuu ni ikiwa mtu, hata awe mzito kadiri gani, anakula kwa pupa nyingi sana.—Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 2004.

Je, Unakumbuka?

• Ili tupate roho takatifu, tunapaswa kufanya nini?

• Roho ya ulimwengu inaweza kutuongoza katika njia gani?

• Tunaweza kufanya nini ili tuipinge roho ya ulimwengu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kabla ya kwenda kazini au shuleni salini ili mpate roho takatifu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ni lazima tutunze akili zetu zikiwa safi, kujiendesha kwa unyoofu katika shughuli za biashara, na kuwa na kiasi katika mazoea yetu