Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhubiri Sokoni

Kuhubiri Sokoni

Kuhubiri Sokoni

MTUME Paulo alipokuwa katika jiji la Athene, alienda kila siku sokoni ili kuhubiri habari njema kumhusu Yesu. (Mdo. 17:17) Paulo alihubiri sokoni kwa sababu wakaaji wengi wa Athene walitumia wakati mwingi sana wakiwa sokoni.

Miaka 2,000 hivi baadaye, bado watu wa Yehova wanaeneza ujumbe wa Ufalme wa Mungu sokoni pia. Kwa nini? Kwa sababu watu wengi wanaweza kupatikana mahali hapo. Leo, huenda watu wengi wakanunua vitu madukani. Baada ya kuruhusiwa na msimamizi wa duka au mwenye duka mwenyewe, Mashahidi fulani wametumia meza au kibanda ili kuonyesha vichapo vinavyozungumzia Biblia.

Kwa mfano, katika duka moja kubwa huko New Jersey, Marekani, kulikuwa na maonyesho yenye kuvutia ya vichapo vinavyozungumza kuhusu “Jinsi ya Kudumisha Viwango vya Familia.” Kukawa na matokeo gani? Kwa siku moja tu, vitabu 153 katika lugha sita vilichukuliwa.

Mwanamke mmoja aliyekaribia kibanda cha vichapo alisikiliza kwa makini maelezo yaliyotolewa na Shahidi mmoja. Mwanamke huyo alikiri kwamba ni jambo la maana kumfikiria Mungu katika maisha yetu na pia katika familia yetu. Alipewa vichapo vifuatavyo: Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, na Siri ya Kupata Furaha ya Familia.

Wakati wa alasiri, mwanamume mmoja alipita karibu na kibanda hicho cha maonyesho ya vichapo alipokuwa akielekea kwenye duka lililokuwa karibu. Alivutiwa na kitabu Vijana Huuliza. Dada aliyekuwa ndani ya kibanda hicho alitambua kwamba mwanamume huyo alipendezwa na kitabu hicho. Dada huyo alimuuliza, “Je, kuna kitabu chochote kinachokuvutia?” Aliitikia kwa kutikisa kichwa na kuonyesha kitabu Vijana Huuliza. Dada huyo alimpa kitabu hicho, ambacho mtu huyo alikuwa tayari amekifikia. Alisema kwamba ana watoto watatu. Mazungumzo yalipokuwa yakiendelea, alisema kwamba anakuwa na mazungumzo na watoto wake mara moja kwa juma. Watoto wake wawili wakubwa ni matineja. Alipokuwa akiangalia kitabu hicho, alisema kwamba angekitumia kwa urahisi sana kuwa msingi wa mazungumzo yao ya familia. Mhubiri huyo alimwonyesha pia mwanamume huyo kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, na akamhakikishia kwamba yeye na mke wake wangepata mashauri fulani mazuri sana kuhusu kufanya maamuzi ya familia. Mwanamume huyo alishukuru kwa pendekezo hilo, akatoa mchango, na akakubali mtu fulani awatembelee nyumbani kwao.

Mashahidi hao walihisi jinsi gani kuhusu siku yao ya kuhubiri katika kibanda hicho? Dada mmoja alisema hivi: “Mimi binafsi nilifurahia njia hii ya kuhubiri. Lilikuwa jambo la pekee sana!” Dada mwingine alisema hivi: “Yehova anasema kwamba habari njema itahubiriwa mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia. Leo, habari njema imegusa mioyo ya watu wa lugha mbalimbali hapa Paramus, New Jersey. Ilifurahisha sana kuhubiri katika eneo hili la maduka. Kila mtu aliyeshiriki katika mahubiri haya alikuwa na furaha. Mwishoni mwa siku, hakuna yeyote kati yetu aliyetaka kuondoka.”

Je, unaweza kupanua njia zako za kuhubiri habari njema? Njia yetu ya msingi ni kwenda nyumba kwa nyumba. (Mdo. 20:20) Hata hivyo, je, ungependa kuhubiri sokoni au madukani?