Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwige Yesu—Mwabudu Mungu kwa Njia Inayokubalika

Mwige Yesu—Mwabudu Mungu kwa Njia Inayokubalika

Mwige Yesu—Mwabudu Mungu kwa Njia Inayokubalika

Kwa upendo, Mungu anawaalika watu “kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha” ili wamwabudu. (Ufu. 7:9, 10; 15:3, 4) Wale wanaokubali mwaliko huo wanaweza “kuuona uzuri wa Yehova.” (Zab. 27:4; 90:17) Kama mtunga-zaburi, wanapaaza sauti zao kumsifu Mungu, wakisema: “Tuabudu na kuinama; na tupige magoti mbele za Yehova Mtengenezaji wetu.”—Zab. 95:6.

Ibada Inayothaminiwa Sana

Akiwa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, Yesu alikuwa na nafasi nzuri ya kujifunza fikira, kanuni, na viwango vya Baba yake. Hivyo, Yesu angeweza kuwaonyesha wengine kwa uhakika njia ya ibada ya kweli. Alisema hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.”—Yoh. 1:14; 14:6.

Yesu aliweka mfano mkamilifu wa kujitiisha kwa unyenyekevu kwa Baba yake. Alisema hivi: “Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” Kisha akaongeza: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.” (Yoh. 8:28, 29) Yesu alimpendeza Baba yake katika njia gani?

Kwanza, Yesu alijitoa kikamili kwa Baba yake, na hiyo ndiyo maana hasa ya kumwabudu Mungu. Yesu alionyesha kwamba alishikamana na Baba yake kwa kumtii, kwa kufanya mapenzi Yake, hata ingawa hilo lilimaanisha kuteseka sana. (Flp. 2:7, 8) Sehemu ya maana sana ya ibada ya Yesu ilikuwa kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kufanya wanafunzi, hivi kwamba waamini na wasio waamini walimwita Mwalimu. (Mt. 22:23, 24; Yoh. 3:2) Zaidi ya hayo, Yesu alitumia wakati na nguvu zake kuwasaidia wengine. Roho yake ya kujidhabihu ilifanya awe na wakati mchache sana wa kujishughulikia, lakini alifurahi kuwahudumia wengine. (Mt. 14:13, 14; 20:28) Ingawa alikuwa mwenye shughuli nyingi, sikuzote Yesu alitenga wakati wa kuzungumza na Baba yake wa mbinguni katika sala. (Luka 6:12) Ibada ya Yesu ilikuwa yenye thamani kwa Mungu kama nini!

Jitihada za Kumpendeza Vema Mungu

Yehova aliona mwenendo wa Mwana wake naye akamkubali. (Mt. 17:5) Hata hivyo, Shetani Ibilisi, aliona pia maisha ya uaminifu ya Yesu. Hivyo, Yesu akawa shabaha ya pekee ya Shetani. Kwa nini? Kwa sababu kufikia wakati huo hakuna mwanadamu aliyekuwa amedumisha utii mkamilifu kwa Mungu, yaani, kumwabudu kikamili. Na Ibilisi alitaka kumzuia Yesu asimtolee Yehova ibada ambayo anastahili kabisa.—Ufu. 4:11.

Katika jitihada zake za kumpotosha Yesu, Shetani alimtolea Yesu zawadi yenye kushawishi. Alimpeleka Yesu kwenye “mlima mrefu isivyo kawaida, na kumwonyesha falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.” Kisha akamwambia: “Nitakupa mambo yote haya ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” Yesu alifanya nini? Alisema hivi: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’” (Mt. 4:8-10) Ndiyo, Yesu alitambua kwamba kumwangukia Shetani kungekuwa ni kuabudu sanamu hata ikiwa tendo hilo lingeonekana kuwa lenye faida kadiri gani. Alikataa kufanya hata tendo moja la ibada kwa mtu mwingine yeyote isipokuwa Yehova.

Kwa upande wetu, huenda Shetani asitutolee falme zote za ulimwengu na utukufu wazo ili tumwabudu. Lakini bado anajaribu kupotosha ibada ambayo Wakristo wa kweli wanamtolea Mungu. Ibilisi anataka tuabudu mtu mwingine au kitu kingine.—2 Kor. 4:4.

Kristo Yesu alibaki mwaminifu mpaka kifo. Kwa kudumisha utimilifu wake kwa Mungu, Yesu alimtukuza Yehova katika njia ambayo hakuna mwanadamu mwingine alikuwa amewahi kufanya. Leo, tukiwa Wakristo wa kweli, tunajitahidi kuiga uaminifu wa Yesu kwa kutanguliza ibada yetu kwa Muumba kabla ya jambo lingine lolote. Kwa kweli, uhusiano mzuri pamoja na Mungu ndicho kitu chenye thamani zaidi tulicho nacho.

Baraka Zinazotokana na Kuabudu kwa Njia Inayokubalika

Kuunga mkono “namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi” kwa maoni ya Mungu kunaleta baraka nyingi. (Yak. 1:27) Kwa mfano, tunaishi katika wakati ambao watu wengi zaidi ni wenye “kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai,” na “wasiopenda wema.” (2 Tim. 3:1-5) Hata hivyo, katika nyumba ya Mungu, tuna pendeleo la kushirikiana na watu safi, watu wazuri, ambao wanajitahidi kuishi kulingana na viwango vya Mungu vya ibada. Hilo ni jambo lenye kuburudisha kama nini!

Kwa kubaki bila unajisi kutokana na ulimwengu huu, tunabarikiwa zaidi kwa kuwa na dhamiri safi. Tunataka kuendelea kuwa na dhamiri safi kwa kukubali kanuni za uadilifu za Mungu na kutii sheria za Kaisari ambazo hazipingani na sheria za Mungu.—Marko 12:17; Mdo. 5:27-29.

Kumwabudu Mungu kwa nafsi yote kunaleta baraka za aina nyingine. Tunapokazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu badala ya mambo yetu wenyewe, maisha yetu yanakuwa na kusudi na yenye kuridhisha. Badala ya kusema: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa,” tuna tumaini lenye kutegemeka la uzima wa milele katika paradiso duniani.—1 Kor. 15:32.

Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha kwamba wale ambao wanadumisha msimamo mzuri mbele za Yehova ‘watatoka katika ile dhiki kuu.’ Simulizi hilo linasema kwamba “Yule anayeketi juu ya kiti cha ufalme atatandaza hema lake juu yao.” (Ufu. 7:13-15) Huyo anayeketi kwenye kiti cha ufalme si mwingine ila Yehova Mungu, yule aliye Mtukufu zaidi katika ulimwengu wote. Fikiria shangwe ambayo utakuwa nayo atakapokualika uwe mgeni katika hema lake na kukulinda ili usipatwe na madhara yoyote! Na kwa kadiri fulani, hata sasa tunaweza kufurahia ulinzi na utunzaji wake.

Zaidi ya hayo, wote ambao wanamwabudu Mungu kwa njia inayokubalika wanasemwa kuwa wanaongozwa kwenye “chemchemi za maji ya uzima.” Chemchemi hizo zenye kuburudisha zinawakilisha maandalizi yote ambayo Yehova anafanya ili tupate uzima wa milele. Ndiyo, kupitia fidia ya Kristo, “Mungu atafuta kila chozi katika macho yao.” (Ufu. 7:17) Wanadamu watainuliwa kwenye ukamilifu, na hilo litaleta shangwe kubwa kwa wale wanaotazamia kuishi milele duniani. Hata sasa, waabudu wenye furaha wa Mungu wanapiga vigelegele kwa shangwe, huku wakimwonyesha Yehova uthamini wao wa kutoka moyoni na kumwabudu pamoja na wale walio mbinguni ambao wanaimba hivi: “Matendo yako ni makuu na ya ajabu, Yehova Mungu, Mweza-Yote. Njia zako ni za uadilifu na za kweli, Mfalme wa umilele. Ni nani ambaye kwa kweli hatakuogopa wewe, Yehova, na kulitukuza jina lako, kwa sababu wewe peke yako ni mshikamanifu? Kwa maana mataifa yote yatakuja na kuabudu mbele zako, kwa sababu amri zako za uadilifu zimefunuliwa.”—Ufu. 15:3, 4.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Shetani anatuahidi nini ili tumpe ibada yetu?