Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ongeza Ujuzi Sahihi Ukiwa na ‘Hamu ya Akili’

Ongeza Ujuzi Sahihi Ukiwa na ‘Hamu ya Akili’

Ongeza Ujuzi Sahihi Ukiwa na ‘Hamu ya Akili’

WATUMISHI wote wa Yehova wanajitahidi kukubaliwa naye. Kwa kuwa tunatamani atukubali, tunataka sana kuboresha imani yetu na kutoa utumishi mtakatifu kwa bidii. Hata hivyo, mtume Paulo anatuonyesha hatari fulani, ambayo iliwapata Wayahudi fulani wa siku zake: “Wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Rom. 10:2) Bila shaka, imani na ibada yetu kwa Yehova haipaswi kutegemea hisia tu. Tunahitaji ujuzi sahihi kumhusu Muumba wetu na kuhusu mapenzi yake.

Katika maandishi yake mengine, Paulo alionyesha kwamba kuna uhusiano kati ya mwenendo unaompendeza Mungu na hamu yetu ya kupata ujuzi. Alisali kwamba wafuasi wa Kristo ‘wajazwe ujuzi sahihi’ wa mapenzi ya Mungu ‘ili watembee kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili wanapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.’ (Kol. 1:9, 10) Kwa nini “ujuzi sahihi” ni wa maana sana? Na kwa nini tuongeze ujuzi huo?

Jinsi ya Kupata Imani

Ujuzi sahihi kumhusu Mungu na kuhusu mapenzi yake ambayo yanaonyeshwa katika Biblia ndio msingi wa imani yetu. Tusipokuwa na ujuzi huo wenye kutegemeka, imani yetu katika Yehova inaweza kuwa kama karatasi ambayo inapeperushwa hata na upepo mdogo. Paulo anatuhimiza tumtolee Mungu utumishi mtakatifu ‘pamoja na nguvu zetu za kufikiri’ na ‘kufanya upya akili zetu.’ (Rom. 12:1, 2) Kujifunza Biblia kwa ukawaida kunaweza kutusaidia kufanya hivyo.

Ewa, painia wa kawaida huko Poland, anakubali hivi: “Ikiwa singejifunza Neno la Mungu kwa ukawaida, singeongeza ujuzi sahihi kumhusu Yehova. Ningepoteza utambulisho wangu wa Kikristo, na imani yangu katika Mungu ingedhoofika—ningekufa kiroho.” Jambo kama hilo lisitupate kamwe! Fikiria mfano wa mtu aliyeongeza ujuzi sahihi kumhusu Yehova na hivyo kukubaliwa Naye.

“Jinsi Ninavyoipenda Sheria Yako!”

Wimbo wa kishairi ulio katika Zaburi ya 119 katika Biblia zetu unaonyesha jinsi mtungaji wa zaburi hiyo alivyohisi kuhusu sheria, vikumbusho, maagizo, amri, na maamuzi ya hukumu ya Yehova. Mtunga-zaburi huyo aliandika: “Nitazipenda sheria zako. . . . Ninavipenda vikumbusho vyako.” Aliandika hivi pia: “Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.”—Zab. 119:16, 24, 47, 48, 77, 97.

Maneno ‘kupenda’ na ‘kuhangaikia’ yanamaanisha kutafakari Neno la Mungu, na hasa, kufurahia kutafakari. Maneno hayo yanakazia jinsi mtunga-zaburi huyo alivyopenda kujifunza sheria ya Mungu. Mtunga-zaburi huyo hakupenda kujifunza kwa sababu ya kusukumwa tu na hisia. Badala yake, alitamani sana ‘kuihangaikia’ sheria, kufahamu maneno ya Yehova. Mtazamo wake unatuonyesha kwamba alitaka kumjua Mungu na mapenzi yake kwa usahihi iwezekanavyo.

Ni wazi kwamba mtunga-zaburi huyo alilipenda Neno la Mungu kwa moyo wote. Tunaweza kujiuliza: ‘Je, hata mimi ninalipenda kwa kadiri hiyo? Je, ninafurahia kusoma na kuchanganua sehemu fulani ya Biblia kila siku? Je, ninasoma Neno la Mungu kwa bidii na kusali kabla ya kuanza kusoma?’ Ikiwa tunaweza kujibu ndiyo kwa maswali hayo, basi inaelekea kwamba ‘tunaongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.’

Ewa anasema: “Ninaendelea kujitahidi kuboresha funzo langu la kibinafsi. Tangu nilipopata broshua ‘Ona Nchi Nzuri,’ ninaitumia karibu kila wakati ninapojifunza. Ninajitahidi zaidi kuchunguza kitabu Insight on the Scriptures (Étude perspicace des Écritures) na vichapo vingine.”

Pia, fikiria mfano wa Wojciech na Małgorzata, ambao wana madaraka mazito ya familia. Wanafanya nini ili wafaulu kujifunza Biblia? “Kila mmoja wetu anatenga wakati wa kujifunza Neno la Mungu kibinafsi. Kisha, wakati wa funzo letu la familia na katika mazungumzo, tunazungumzia mambo makuu tuliyofurahia au yale yaliyotutia moyo.” Kujifunza Biblia kwa undani kunawapa shangwe nyingi na kunawasaidia “kuongezeka katika ujuzi sahihi.”

Jifunze Ukiwa Tayari Kukubali Mambo Mapya

Tukiwa Wakristo, tunaamini kwamba mapenzi ya Mungu ni “kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Jambo hilo linakazia umuhimu wa kusoma Biblia na kujitahidi ‘kuielewa.’ (Mt. 15:10) Jambo moja linaloweza kutusaidia ni kujifunza tukiwa tayari kukubali mambo mapya. Huo ndio mtazamo ambao Waberoya wa kale walionyesha wakati Paulo alipowahubiria habari njema: “Walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.”—Mdo. 17:11.

Je, unaiga mfano wa Waberoya wa kuwa na hamu ya kujifunza na kuzuia akili zako zisitangetange unapojifunza Biblia? Mkristo anaweza kujitahidi kuwaiga Waberoya, hata ikiwa hakufurahia kujifunza zamani. Zaidi ya hilo, watu fulani wanaacha kusoma na kujifunza sana kadiri umri unavyosonga, lakini Mkristo hapaswi kufanya hivyo. Hata mtu awe na umri gani, anaweza kujitahidi kuzuia akili yake isitangetange. Na unaposoma, unaweza kuwa macho kuona habari ambazo ungependa kuwaeleza wengine. Kwa mfano, je, unaweza kumweleza mwenzi wako au rafiki yako Mkristo mambo ambayo umesoma au kujifunza? Ukifanya hivyo, mambo hayo yanaweza kukazwa katika akili na moyo wako, na wengine watatiwa moyo.

Unapojifunza, mwige Ezra, mtumishi wa kale wa Mungu ambaye “alikuwa ameutayarisha moyo wake kutafuta shauri katika sheria ya Yehova.” (Ezra 7:10) Unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Unaweza kuchagua mahali panapofaa pa kujifunzia. Kisha, keti chini na umwombe Yehova mwongozo wake na hekima. (Yak. 1:5) Jiulize hivi, ‘Ninatazamia kujifunza nini?’ Unapojifunza, uwe macho kuona mambo makuu. Unaweza kuyaandika au kutia alama sehemu ambazo unataka kukumbuka. Fikiria jinsi unavyoweza kutumia habari hizo unapohubiri, unapofanya maamuzi, au unapowatia moyo waamini wenzako. Unapokaribia kumaliza kujifunza, rudia kwa ufupi mambo uliyojifunza. Hilo litakusaidia kukumbuka mambo ambayo umejifunza.

Ewa anaeleza jinsi anavyofanya: “Ninaposoma Biblia, ninatumia marejeo ya pambizoni, Fahirisi, na Watchtower Library inayopatikana katika CD-ROM. Ninaandika mambo makuu ili niyatumie katika kazi yangu ya kuhubiri.”

Wengine wamefurahia kujifunza kwa miaka mingi mambo mazito ya kiroho. (Met. 2:1-5) Hata hivyo, wana madaraka mengi na si rahisi kwao kutenga wakati kwa ajili ya funzo la kibinafsi. Ikiwa uko katika hali kama hiyo, unaweza kufanya marekebisho gani katika ratiba yako?

Ninaweza Kupata Wakati Jinsi Gani?

Huenda ukakubali kwamba ni rahisi zaidi kutenga wakati ili kufanya mambo unayofurahia. Wengi wamegundua kwamba wakijiwekea mradi ambao wanaweza kufikia, kama vile kusoma Biblia nzima, wanafaulu kuwa na funzo la kibinafsi. Ni kweli kwamba, mtu anaweza kuona ni vigumu sana kusoma orodha ndefu za ukoo, maelezo ya ndani kuhusu hekalu la zamani, au unabii wenye mambo mengi ambayo hayaonekani kuwa yanahusiana na maisha ya leo. Jitahidi kuchukua hatua zitakazokusaidia kufikia mradi wako. Kwa mfano, kabla ya kuchunguza sehemu ya Biblia inayoonekana kuwa ngumu, unaweza kusoma historia ya sehemu hiyo au matumizi yake. Habari hizo zinaweza kupatikana katika kitabu “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa,” ambacho kinapatikana katika lugha karibu 50.

Inasisimua kutumia akili yako ili kuwazia mambo unayosoma katika Biblia. Hilo linaweza kukusaidia kuwazia wahusika na matukio yanayotajwa. Kutumia mapendekezo hayo machache kunaweza kufanya usomaji wako ukufurahishe na kukunufaisha zaidi. Hivyo, utakuwa na hamu kubwa zaidi ya kutenga wakati ili kujifunza. Itakuwa rahisi zaidi kuendelea na zoea lako la kusoma Biblia kila siku.

Ingawa mapendekezo hayo yanaweza kutusaidia kibinafsi, familia yenye shughuli nyingi inaweza kufanya nini? Kwa nini msiketi chini pamoja na kuzungumzia kwa uhuru faida za kuwa na funzo la familia? Huenda kupitia mazungumzo hayo mkapata maoni yatakayowasaidia, kama vile kupunguza muda wa kulala kwa dakika chache kila siku ili msome sehemu fulani ya Biblia. Au huenda kupitia mazungumzo hayo mkagundua kwamba mnahitaji kurekebisha ratiba ya familia. Kwa mfano, familia fulani zimeona inafaa kuzungumzia andiko la siku au kusoma sehemu fulani ya Biblia baada ya kula. Kabla ya yeyote kusimama ili kuondoa vyombo au kufanya shughuli nyingine, familia hizo zinatumia dakika 10 au 15 kuzungumzia Maandiko au kufanya usomaji wa Biblia ulioratibiwa. Mwanzoni, huenda hilo likaonekana kuwa jambo gumu, lakini baada ya muda familia itazoea na itafurahia sana.

Wojciech na Małgorzata wanaeleza kilichosaidia familia yao: “Zamani, wakati wetu ulikuwa ukiisha kwa mambo yasiyo na maana. Tuliamua kupunguza muda tunaotumia kutuma barua-pepe. Pia, tumepunguza muda tunaotumia kwa burudani na kutenga siku na wakati hususa ili kujifunza kwa undani.” Familia hiyo haijuti kwa sababu ya marekebisho hayo, na familia yako inaweza kuhisi hivyo pia.

Kuongezeka Katika Ujuzi Sahihi Kuna Faida!

Kujifunza Neno la Mungu kwa undani kunaweza kumsaidia mtu “kuzaa matunda katika kila kazi njema.” (Kol. 1:10) Ukifanya hivyo, maendeleo yako yatakuwa wazi kwa wote. Utakuwa mtu wa kiroho anayeelewa kweli za Biblia kwa undani. Badala ya kufanya maamuzi yanayopita kiasi kwa sababu ya kutojua mambo, utafanya maamuzi yenye usawaziko na utakuwa tayari zaidi kuwasaidia wengine. Zaidi ya yote, utamkaribia Yehova zaidi. Utafahamu sifa zake kwa undani zaidi, na hilo litaonekana wazi unapowaeleza wengine kuhusu sifa hizo.—1 Tim. 4:15; Yak. 4:8.

Hata uwe na umri gani au uwe na uzoefu kadiri gani, fanya yote uwezayo kuendelea kufurahia Neno la Mungu na kujifunza kwa undani ukiwa tayari kukubali mambo mapya. Uwe na hakika kwamba Yehova hatasahau jitihada zako. (Ebr. 6:10) Atakumwagia baraka zake tele.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

‘TUNAPOONGEZEKA KATIKA UJUZI SAHIHI’. . .

Tunaimarisha imani yetu katika Mungu na tunatembea kwa kumstahili Yehova.—Kol. 1:9, 10

Tunapata ufahamu, na tunaweza kutumia utambuzi kufanya maamuzi ya busara.—Zab. 119:99

Tunapata furaha nyingi zaidi katika kuwasaidia wengine kumkaribia Yehova.—Mt. 28:19, 20

[Picha katika ukurasa wa 14]

Ingawa si rahisi kupata mahali panapofaa pa kujifunzia, ni jambo linalofaa kufanya hivyo

[Picha katika ukurasa wa 15]

Familia fulani zinasoma sehemu fulani ya Biblia baada ya kula