Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Ni wa Kwanza Katika Kuonyesha Heshima?

Je, Wewe Ni wa Kwanza Katika Kuonyesha Heshima?

Je, Wewe Ni wa Kwanza Katika Kuonyesha Heshima?

“Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.”—ROM. 12:10.

1. Ni jambo gani ambalo halionekani tena katika sehemu nyingi za ulimwengu?

KATIKA sehemu fulani za ulimwengu, watoto wanawaheshimu watu wazima kwa kupiga magoti kwa heshima wanapokuwa pamoja nao. Wanapopiga magoti, watoto hao hawaonekani kuwa warefu kuliko wale wenye umri mkubwa zaidi. Katika jamii hizo, mtoto anayemgeuzia mtu mzima mgongo anaonwa kuwa hana adabu. Ingawa heshima inaonyeshwa kwa njia tofauti katika tamaduni mbalimbali, njia hizo za kuonyesha heshima zinatukumbusha Sheria ya Musa. Sheria hiyo ilitia ndani amri hii: “Unapaswa kusimama [ili kuonyesha heshima] mbele ya mtu mwenye mvi, nawe umwonyeshe ufikirio mtu mzee.” (Law. 19:32) Inasikitisha kwamba katika maeneo mengi watu hawaheshimiani tena. Kwa kweli, ukosefu wa heshima unaonekana kila mahali leo.

2. Neno la Mungu linatuambia tumheshimu nani?

2 Neno la Mungu linasema kwamba kuonyesha heshima ni jambo la maana sana. Linatuambia tumheshimu Yehova na Yesu. (Yoh. 5:23) Pia, tunaamuriwa tuwaonyeshe heshima watu wa familia yetu na waamini wenzetu na pia watu fulani nje ya kutaniko. (Rom. 12:10; Efe. 6:1, 2; 1 Pet. 2:17) Tunaonyesha katika njia gani mbalimbali kwamba tunamheshimu Yehova? Tunaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba tunawaheshimu sana ndugu na dada zetu Wakristo? Acheni tuchunguze maswali hayo na mengine yanayohusiana nayo.

Kumheshimu Yehova na Jina Lake

3. Taja njia moja kuu ya kumheshimu Yehova.

3 Njia moja kuu ya kumheshimu Yehova ni kuheshimu jina lake, kwa sababu sisi ni “watu kwa ajili ya jina lake.” (Mdo. 15:14) Kwa kweli, ni heshima kubwa kuitwa kwa jina la Mungu mweza-yote, Yehova. Nabii Mika alisema hivi: “Vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Mika 4:5) ‘Tunatembea katika jina la Yehova’ kwa kujitahidi kuishi kila siku katika njia ambayo inamletea Yehova sifa. Kama Paulo alivyowakumbusha Wakristo huko Roma, ikiwa hatuishi kulingana na habari njema tunayohubiri, jina la Mungu ‘litafanyiwa makufuru,’ litatukanwa.—Rom. 2:21-24.

4. Una maoni gani kuhusu pendeleo la kutoa ushahidi kumhusu Yehova?

4 Pia, tunamheshimu Yehova kwa kazi yetu ya kuhubiri. Zamani, Yehova aliwaalika washiriki wa taifa la Israeli wawe mashahidi wake, lakini walishindwa kutimiza wajibu wao. (Isa. 43:1-12) Mara nyingi walimwasi Yehova na “wakamtia uchungu Mtakatifu wa Israeli.” (Zab. 78:40, 41) Mwishowe, taifa hilo lilipoteza kabisa kibali cha Yehova. Hata hivyo, sisi leo tunashukuru kwamba tuna pendeleo la kutoa ushahidi kumhusu Yehova na tunatangaza jina lake. Tunafanya hivyo kwa sababu tunampenda na tunataka sana jina lake litakaswe. Kwa sababu tunajua ukweli kumhusu Baba yetu wa mbinguni na makusudi yake, hatuwezi kukosa kuhubiri. Tunahisi kama mtume Paulo alivyohisi aliposema hivi: “Nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sitangazi habari njema!”—1 Kor. 9:16.

5. Kuna uhusiano gani kati ya kumwamini Yehova na kumheshimu?

5 Mtunga-zaburi Daudi alisema hivi: “Wale wanaolijua jina lako watakutegemea, kwa maana hakika hutawaacha wale wanaokutafuta, Ee Yehova.” (Zab. 9:10) Ikiwa kweli tunamjua Yehova na tunaheshimu maana ya jina lake, tutamtegemea kama walivyofanya watumishi wake waaminifu wa zamani. Kumtegemea na kumwamini Yehova ni njia nyingine ya kuonyesha kwamba tunamheshimu. Ona jinsi Neno la Mungu linavyoonyesha kwamba kumtegemea Yehova kunahusiana na kumheshimu. Taifa la Israeli la kale lilipokosa kumtegemea Yehova, alimuuliza Musa hivi: “Watu hawa wataendelea kunitendea bila heshima mpaka wakati gani, nao watakosa kuniamini mpaka wakati gani ijapokuwa ishara zote ambazo nilifanya katikati yao?” (Hes. 14:11) Kwa upande mwingine, tunapomtegemea Yehova atulinde na kututegemeza hata wakati wa majaribu, tunaonyesha kwamba tunamheshimu.

6. Ni nini kinachotuchochea tumheshimu sana Yehova?

6 Yesu alionyesha kwamba ni lazima tumheshimu Yehova kutoka moyoni. Akizungumza na wale ambao hawakumwabudu Mungu kwa unyoofu, Yesu alimnukuu Yehova akisema: “Watu hawa huniheshimu kwa midomo yao, bali moyo wao umepelekwa mbali nami.” (Mt. 15:8) Kumheshimu Yehova kwa unyoofu kunachochewa na kumpenda kutoka moyoni. (1 Yoh. 5:3) Na tunakumbuka pia ahadi hii ya Yehova: “Wale wanaoniheshimu nitawaheshimu.”—1 Sam. 2:30.

Wale Wanaoongoza Wanawaheshimu Wengine

7. (a) Kwa nini ndugu wenye madaraka wanapaswa kuwaonyesha heshima wale walio chini ya usimamizi wao? (b) Paulo aliwaonyesha heshima waamini wenzake jinsi gani?

7 Mtume Paulo aliwahimiza waamini wenzake hivi: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Rom. 12:10) Ndugu wenye madaraka katika kutaniko wanapaswa kuwa mifano kwa ‘kuwa wa kwanza’ katika kuwaonyesha heshima wale walio chini ya usimamizi wao. Kuhusiana na hilo, wale walio na madaraka mazito wanapaswa kufuata mfano uliowekwa na Paulo. (Soma 1 Wathesalonike 2:7, 8.) Ndugu katika makutaniko ambayo Paulo alitembelea walijua kwamba hangeweza kamwe kuwaomba wafanye mambo ambayo yeye mwenyewe hangefanya. Paulo aliwaheshimu waamini wenzake, na wao pia wakamheshimu. Paulo aliposema: “Kwa hiyo, nawasihi ninyi, iweni waigaji wangu,” tunaweza kuwa na uhakika kwamba wengi walimwiga kwa kupenda kwa sababu ya mfano wake mzuri.—1 Kor. 4:16.

8. (a) Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake heshima katika njia gani moja muhimu? (b) Waangalizi wanaweza kufuata mfano wa Yesu jinsi gani leo?

8 Njia nyingine ambayo ndugu mwenye madaraka anawaonyesha heshima wale walio chini ya usimamizi wake ni kuwaambia kwa nini anawaomba wafanye jambo fulani au wafuate maagizo fulani. Kwa kufanya hivyo, anamwiga Yesu. Kwa mfano, Yesu alipowaambia wanafunzi wake wasali ili wafanyakazi zaidi watumwe katika mavuno, aliwaambia pia kwa nini walipaswa kufanya hivyo. Alisema hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Vivyo hivyo, alipowaambia wanafunzi wake ‘waendelee kukesha,’ aliwaambia pia kwa nini wanapaswa kufanya hivyo. Alisema: “Kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.” (Mt. 24:42) Mara nyingi, Yesu hakuwaambia wanafunzi wake yale tu ambayo walipaswa kufanya bali pia kwa nini walipaswa kuyafanya. Katika njia hiyo, aliwaonyesha heshima. Alikuwa mfano mzuri kama nini kwa waangalizi Wakristo!

Heshimu Kutaniko la Yehova na Mwongozo wa Kutaniko

9. Kuliheshimu kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote na wawakilishi wake kunaonyesha nini? Eleza.

9 Ili kumheshimu Yehova, tunahitaji pia kuheshimu kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote pamoja na wawakilishi wake. Tunapotii mashauri ya Kimaandiko kutoka kwa jamii ya mtumwa mwaminifu, tunaonyesha kwamba tunaheshimu mpango wa Yehova. Katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, mtume Yohana aliona uhitaji wa kuwakaripia vikali wale ambao hawakuwaheshimu wanaume waliowekwa rasmi. (Soma 3 Yohana 9-11.) Maneno ya Yohana yanaonyesha kwamba mbali na kutowaheshimu waangalizi mmoja-mmoja hawakuheshimu pia mafundisho na mwongozo wao. Hata hivyo, Wakristo wengi hawakuwa hivyo. Mitume walipokuwa wangali hai, ni wazi kwamba Wakristo wote kwa ujumla waliwaheshimu sana wale waliokuwa wakiongoza.—Flp. 2:12.

10, 11. Eleza ukitumia Maandiko kwa nini inafaa watu fulani wawe na mamlaka ya kadiri katika kutaniko la Kikristo.

10 Wengine wamedai kwamba kwa kuwa Yesu aliwaambia wanafunzi wake “ninyi nyote ni ndugu,” basi kutaniko la Kikristo halipaswi kuwa na watu wenye mamlaka. (Mt. 23:8) Hata hivyo, Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki yana mifano mingi ya wanaume ambao walipewa mamlaka na Mungu. Historia ya wazee wa ukoo, waamuzi, na wafalme wa kale Waebrania inathibitisha wazi kwamba Yehova anatoa mwongozo kupitia wawakilishi wa kibinadamu. Yehova aliwaadhibu watu walipokosa kuwaheshimu inavyofaa wale waliowekwa rasmi.—2 Fal. 1:2-17; 2:19, 23, 24.

11 Vivyo hivyo, Wakristo wa karne ya kwanza walitambua mamlaka ya mitume. (Mdo. 2:42) Kwa mfano, Paulo aliwapa ndugu zake mwongozo. (1 Kor. 16:1; 1 The. 4:2) Hata hivyo, yeye pia alikuwa tayari kujitiisha kwa wale waliokuwa na mamlaka juu yake. (Mdo. 15:22; Gal. 2:9, 10) Kwa kweli, Paulo alikuwa na maoni yanayofaa kuhusu mamlaka katika kutaniko la Kikristo.

12. Ni mambo gani mawili tunayojifunza kuhusu mamlaka kupitia mifano ya Kibiblia?

12 Tunajifunza mambo mawili. Kwanza, ni jambo linalopatana na Maandiko kwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kupitia Baraza lake Linaloongoza kuwakabidhi wanaume madaraka, na wanaume fulani wanawekwa rasmi ili kuwa na mamlaka juu ya wanaume wengine waliowekwa rasmi. (Mt. 24:45-47; 1 Pet. 5:1-3) Pili, sisi sote, kutia ndani wanaume waliowekwa rasmi, tunapaswa kuwaheshimu wale walio na mamlaka juu yetu. Basi, ni katika njia gani mbalimbali tunaweza kuwaheshimu wale walio na madaraka ya usimamizi katika kutaniko la ulimwenguni pote la Kikristo?

Kuwaheshimu Waangalizi Wanaosafiri

13. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunawaheshimu wawakilishi wa kutaniko la Kikristo leo?

13 Paulo alisema: “Tunawaomba ninyi, akina ndugu, mwatilie maanani wale wanaofanya kazi kwa bidii kati yenu na kuwasimamia ninyi katika Bwana na kuwaonya ninyi; na kuwafikiria kwa njia inayozidi ile ya kawaida katika upendo kwa sababu ya kazi yao. Iweni wenye kufanya amani mtu na mwenzake.” (1 The. 5:12, 13) Bila shaka, waangalizi wanaosafiri ni kati ya “wale wanaofanya kazi kwa bidii.” Kwa hiyo, acheni ‘tuwafikirie kwa njia inayozidi ile ya kawaida.’ Njia moja ya kufanya hivyo ni kufuata kwa moyo wote mashauri yao na mwongozo wao. Mwangalizi anapotupa mwongozo kutoka kwa jamii ya mtumwa mwaminifu, “hekima inayotoka juu” itatuchochea tuwe “tayari kutii.”—Yak. 3:17.

14. Kutaniko linaonyesha jinsi gani kwamba linawaheshimu kutoka moyoni waangalizi wanaosafiri, na kunakuwa na matokeo gani?

14 Namna gani ikiwa tunaagizwa tufanye mambo kwa njia tofauti na ile ambayo tumezoea? Nyakati nyingine, huenda kuonyesha heshima kukamaanisha kutopinga mwongozo kwa kusema hivi: “Hapa kwetu hatufanyi mambo hivyo” au, “Wazo hilo linaweza kufaa mahali pengine lakini si katika kutaniko letu.” Badala yake, tunajitahidi kufuata mwongozo. Kuendelea kukumbuka kwamba kutaniko ni la Yehova na kwamba Yesu ndiye Kichwa cha kutaniko kutatusaidia kufanya hivyo. Kutaniko linapopokea na kufuata kwa shangwe mwongozo wa mwangalizi anayesafiri, linathibitisha kwamba linamheshimu kutoka moyoni. Mtume Paulo aliwapongeza akina ndugu wa Korintho kwa sababu walitii kwa heshima mwongozo uliotolewa na Tito, mzee aliyewatembelea. (2 Kor. 7:13-16) Leo, tunaweza pia kuwa na uhakika kwamba tunapofuata kwa moyo wote mwongozo ambao unatoka kwa waangalizi wanaosafiri tunapata shangwe zaidi katika kazi yetu ya kuhubiri.—Soma 2 Wakorintho 13:11.

“Waheshimuni Watu wa Namna Zote”

15. Tunawaheshimu waamini wenzetu katika njia gani?

15 Paulo aliandika hivi: “Usimkemee kwa ukali mwanamume mzee. Badala yake, msihi kama baba, wanaume vijana kama ndugu, wanawake wazee kama mama, wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili. Waheshimu wajane ambao ni wajane kwelikweli.” (1 Tim. 5:1-3) Ndiyo, Neno la Mungu linatuhimiza tumheshimu kila mtu katika kutaniko la Kikristo. Namna gani basi ukikosa kuelewana na ndugu au dada yako kutanikoni? Je, hilo litakuzuia usimheshimu Mkristo mwenzako? Au je, unaweza kurekebisha mtazamo wako kwa kutambua sifa nzuri za kiroho za mtumishi huyo wa Mungu? Hasa wale ambao wana madaraka wanapaswa kuwaheshimu ndugu zao, yaani, hawapaswi kamwe “kupiga ubwana juu ya . . . kundi.” (1 Pet. 5:3) Kwa kweli, tuna nafasi nyingi za kuheshimiana katika kutaniko la Kikristo, ambalo linatambuliwa kwa upendo wa kutoka moyoni kati ya washiriki wake.—Soma Yohana 13:34, 35.

16, 17. (a) Kwa nini ni jambo la maana kuwaheshimu si wale tu ambao tunahubiria bali pia wapinzani wetu? (b) ‘Tunawaheshimu watu wa namna zote’ jinsi gani?

16 Bila shaka, hatuwaheshimu tu wale ambao ni washiriki wa kutaniko la Kikristo. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa siku zake: “Tukiwa na wakati unaofaa kwa ajili ya hilo, tuwatendee wote mema.” (Gal. 6:10) Ni kweli kwamba inaweza kuwa vigumu kufuata kanuni hiyo ikiwa mfanyakazi au mwanashule mwenzetu hatutendei kwa fadhili. Katika nyakati kama hizo, tunahitaji kukumbuka maneno haya: “Usijionyeshe umewaka hasira kwa sababu ya watenda-maovu.” (Zab. 37:1) Kutumia shauri hilo kutatusaidia kuwatendea kwa heshima hata wapinzani wetu. Vivyo hivyo, tunapokuwa katika kazi yetu ya kuhubiri, unyenyekevu unaweza kutusaidia kumjibu kila mtu kwa “tabia-pole na heshima kubwa.” (1 Pet. 3:15) Hata sura yetu na mavazi yetu yanaweza kuonyesha kwamba tunawaheshimu wale ambao tunawahubiria.

17 Kwa kweli, iwe tunashughulika na waamini wenzetu au watu walio nje ya kutaniko, na tujitahidi kufuata himizo hili: “Waheshimuni watu wa namna zote, upendeni ushirika mzima wa akina ndugu, mwogopeni Mungu, mheshimuni mfalme.”—1 Pet. 2:17.

Ungesema Nini?

Ni kwa njia gani unaweza kuonyesha heshima inayofaa kwa:

• Yehova?

• Wazee wa kutaniko na waangalizi wanaosafiri?

• Kila mshiriki wa kutaniko?

• Wale ambao unawahubiria?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wakristo wa karne ya kwanza waliheshimu usimamizi wa baraza linaloongoza

[Picha katika ukurasa wa 24]

Wazee katika kila nchi wanawaheshimu waangalizi wanaosafiri ambao wamewekwa rasmi na Baraza Linaloongoza