Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jibu la Yehova kwa Sala ya Kutoka Moyoni

Jibu la Yehova kwa Sala ya Kutoka Moyoni

Jibu la Yehova kwa Sala ya Kutoka Moyoni

“Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”—ZAB. 83:18.

1, 2. Watu wengi wameguswa moyo na jambo gani, na tunaweza kujiuliza maswali gani?

MIAKA fulani iliyopita, mwanamke mmoja alifadhaishwa sana na msiba uliotukia katika ujirani wake. Kwa kuwa alizaliwa katika familia ya Kikatoliki, aliomba kasisi wa eneo lao amsaidie, lakini kasisi huyo alikataa hata kuzungumza naye. Kwa hiyo, akasali hivi kwa Mungu: “Sijui wewe ni nani . . . , lakini ninajua upo. Tafadhali niruhusu nikujue!” Muda mfupi baadaye, Mashahidi wa Yehova walimtembelea, wakamfariji, na kumpa ujuzi ambao alikuwa akitafuta. Kati ya mambo mengine, walimfundisha kwamba Mungu ana jina, anaitwa Yehova. Aliguswa moyo sana alipojifunza jambo hilo. Alisema hivi: “Kwa kweli, huyo ndiye Mungu niliyetamani kumjua tangu nilipokuwa mtoto!”

2 Watu wengi wameguswa moyo sana baada ya kujifunza jina la Mungu. Wengi wao waliliona jina la Yehova kwa mara ya kwanza waliposoma Zaburi 83:18 katika Biblia. Katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, andiko hilo linasema hivi: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Hata hivyo, je, umewahi kujiuliza kwa nini Zaburi ya 83 iliandikwa? Ni matukio gani yatakayomlazimisha kila mtu atambue kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli? Zaburi hiyo ina ujumbe gani kwetu leo? Tutachunguza maswali hayo katika habari hii. *

Njama ya Kuwaangamiza Watu wa Yehova

3, 4. Zaburi ya 83 iliandikwa na nani, na inazungumza kuhusu tishio gani?

3 Kulingana na maneno ya utangulizi, Zaburi ya 83 ni “muziki wa Asafu.” Inaelekea mtungaji wa zaburi hiyo alikuwa mzao wa Mlawi aliyeitwa Asafu, mwanamuziki maarufu wakati wa utawala wa Mfalme Daudi. Katika zaburi hiyo, mtunga-zaburi anamsihi Yehova achukue hatua ya kuitetea enzi Yake kuu na kulifanya jina Lake lijulikane. Inaonekana zaburi hiyo ilitungwa muda fulani baada ya kifo cha Sulemani. Kwa nini? Kwa sababu wakati wa utawala wa Daudi na Sulemani, mfalme wa Tiro alikuwa na uhusiano mzuri na Israeli. Kufikia wakati Zaburi ya 83 ilipoandikwa, wakaaji wa Tiro walikuwa maadui wa Israeli nao walikuwa wameungana na maadui wa taifa hilo.

4 Mtunga-zaburi huyo anataja majina ya mataifa kumi ambayo yalikuwa yakipanga njama ya kuwaangamiza watu wa Mungu. Maadui wote hao walikuwa katika maeneo yaliyokuwa kandokando ya Israeli na yanaorodheshwa ifuatavyo: “Mahema ya Edomu na Waishmaeli, Moabu na Wahagri, Gebali na Amoni na Amaleki, Ufilisti pamoja na wakaaji wa Tiro. Pia, Ashuru imejiunga nao.” (Zab. 83:6-8) Zaburi hiyo inazungumza kuhusu tukio gani la kihistoria? Watu fulani wanasema kwamba zaburi hiyo inazungumza kuhusu kushambuliwa kwa Israeli na majeshi ya muungano ya Amoni, Moabu, na wakaaji wa Mlima Seiri katika siku za Yehoshafati. (2 Nya. 20:1-26) Wengine wanaamini kwamba inazungumza kuhusu uadui ambao taifa la Israeli lilionyeshwa na majirani wake katika historia yake yote.

5. Wakristo wanapata faida gani leo kutokana na Zaburi ya 83?

5 Kwa vyovyote vile, ni wazi kwamba Yehova Mungu aliongoza kwa roho yake kuandikwa kwa zaburi hiyo wakati ambapo taifa lake lilikuwa hatarini. Pia, zaburi hiyo inawatia moyo watumishi wa Mungu leo, ambao katika muda wote wa historia wameshambuliwa tena na tena na maadui ambao wameazimia kuwaangamiza. Na kwa kweli zaburi hiyo itatutia nguvu hivi karibuni wakati Gogu wa Magogu atakapokusanya majeshi yake katika jaribio la mwisho la kuwaangamiza wote wanaomwabudu Mungu katika roho na kweli.—Soma Ezekieli 38:2, 8, 9, 16.

Hangaiko Kuu Zaidi la Mtunga-Zaburi

6, 7. (a) Mtunga-zaburi anasali kuhusu nini katika maneno ya utangulizi ya Zaburi ya 83? (b) Ni nini lililokuwa hangaiko kuu zaidi la mtunga-zaburi?

6 Msikilize mtunga-zaburi anapoeleza hisia zake katika sala: “Ee Mungu, usinyamaze; usikae bila kusema, wala kukaa kimya, Ee Mungu. Kwa maana, tazama! adui zako wanafanya fujo; na wale wanaokuchukia vikali wameinua kichwa chao. Wanaendeleza kwa ujanja mazungumzo ya siri juu ya watu wako . . . Kwa maana kwa moyo wameshauriana kwa umoja; naam, wakafanya agano dhidi yako.”—Zab. 83:1-3, 5.

7 Ni nini lililokuwa hangaiko kuu zaidi la mtunga-zaburi? Ni wazi kwamba huenda alikuwa anahofia sana usalama wake mwenyewe na wa familia yake. Hata hivyo, katika sala yake alikazia sana suto iliyoletwa juu ya jina la Yehova na kutishwa kwa taifa ambalo liliitwa kwa jina la Yehova. Sote na tudumishe maoni kama hayo yenye usawaziko tunapovumilia siku ngumu za mwisho za ulimwengu huu wa kale.—Soma Mathayo 6:9, 10.

8. Kwa nini mataifa yalipanga njama ya kuwaangamiza Waisraeli?

8 Mtunga-zaburi ananukuu maadui wa Israeli wakisema: “Njooni, tuwafutilie mbali wasiwe taifa, ili jina la Israeli lisikumbukwe tena.” (Zab. 83:4) Mataifa hayo yaliwachukia kama nini watu waliochaguliwa wa Mungu! Lakini kulikuwa na sababu nyingine iliyofanya mataifa hayo yapange njama yao. Yalitamani sana nchi ya Israeli na yalijigamba hivi: “Na tumiliki makao ya Mungu.” (Zab. 83:12) Je, jambo kama hilo limetukia leo? Ndiyo!

“Makao Yako Matakatifu”

9, 10. (a) Nyakati za kale, ni nchi gani iliyokuwa makao matakatifu ya Mungu? (b) Mabaki ya watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wanafurahia baraka gani leo?

9 Nyakati za kale, Nchi ya Ahadi iliitwa makao matakatifu ya Mungu. Kumbuka wimbo wa ushindi ambao Waisraeli waliimba baada ya kukombolewa kutoka Misri: “Wewe katika fadhili zako zenye upendo umewaongoza watu ambao umewakomboa; wewe katika nguvu zako hakika utawaongoza mpaka kwenye makao yako matakatifu.” (Kut. 15:13) Baadaye, ‘makao hayo matakatifu’ yalitia ndani hekalu pamoja na makuhani wake na jiji kuu, Yerusalemu, pamoja na wafalme wa ukoo wa Daudi walioketi juu ya kiti cha ufalme cha Yehova. (1 Nya. 29:23) Ndiyo sababu Yesu aliliita Yerusalemu “jiji la yule Mfalme mkuu.”—Mt. 5:35.

10 Namna gani leo? Katika mwaka wa 33 W.K., taifa jipya, “Israeli wa Mungu,” lilizaliwa. (Gal. 6:16) Taifa hilo la ndugu watiwa-mafuta wa Yesu Kristo, lilitimiza kazi ambayo Waisraeli wa asili walishindwa kutimiza, yaani, kuwa mashahidi kwa ajili ya jina la Mungu. (Isa. 43:10; 1 Pet. 2:9) Yehova aliwapa ndugu hao watiwa-mafuta wa Yesu ahadi ileile ambayo aliwapa Waisraeli wa kale: “Nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.” (2 Kor. 6:16; Law. 26:12) Mnamo 1919, Yehova aliwaingiza mabaki wa “Israeli wa Mungu” katika hali yenye upendeleo, na wakati huo, wakamiliki “nchi,” yaani, makao ya kiroho ya utendaji ambamo wamefurahia paradiso ya kiroho. (Isa. 66:8) Tangu miaka ya 1930, mamilioni ya “kondoo wengine” wamejiunga nao. (Yoh. 10:16) Furaha na ufanisi wa kiroho wa Wakristo hao wa siku hizi unathibitisha wazi kwamba Yehova ana haki ya kutawala. (Soma Zaburi 91:1, 2.) Hilo linamkasirisha Shetani kama nini!

11. Kusudi kuu la maadui wa Mungu ni nini?

11 Kwa muda wote wa mwisho, Shetani amewachochea wale wanaofanya mapenzi yake duniani kuwapinga mabaki ya watiwa-mafuta na waandamani wao, kondoo wengine. Upinzani kama huo ulitukia Ulaya Magharibi chini ya utawala wa Nazi na Ulaya Mashariki chini ya serikali ya Kikomunisti ya Muungamo wa Sovieti. Hilo lilitukia pia katika nchi nyingine nyingi, na litatukia tena, hasa wakati wa shambulio la mwisho la Gogu wa Magogu. Katika shambulio hilo, huenda wapinzani wakanyakua kwa pupa mali za watu wa Yehova, kama vile maadui wamewahi kufanya wakati uliopita. Hata hivyo, sikuzote shabaha kuu ya Shetani imekuwa kutuangamiza sisi sote ili jina letu ambalo tumepewa na Mungu lisikumbukwe tena kamwe. Yehova atafanya nini kuhusu uasi huo kuelekea enzi yake kuu? Tuchunguze tena maneno ya mtunga-zaburi.

Matukio ya Kale Yaliyoonyesha Kwamba Yehova Angeshinda

12-14. Mtunga-zaburi anaandika kuhusu pindi gani mbili za ushindi mkubwa karibu na jiji la Megido?

12 Ona jinsi mtunga-zaburi alivyokuwa na imani yenye nguvu kwamba Yehova anaweza kuzuia mipango ya mataifa adui. Katika zaburi hiyo, anataja pindi mbili ambazo Waisraeli waliwashinda maadui wao karibu na jiji la kale la Megido, ambalo lilikuwa juu ya bonde tambarare lililoitwa pia Megido. Wakati wa kiangazi, njia kavu ya Mto Kishoni inaweza kuonekana ikiwa imepinda-pinda katika bonde lote tambarare. Baada ya mvua kubwa za majira ya baridi kali, maji ya mto huo yanafurika katika bonde hilo. Huenda ndiyo sababu mto huo unaitwa pia “maji ya Megido.”—Amu. 4:13; 5:19.

13 Karibu kilomita 15 ng’ambo ya bonde hilo kutoka Megido kuna kilima cha More ambapo katika siku za Mwamuzi Gideoni, majeshi ya muungano ya Wamidiani, Waamaleki, na watu wa Mashariki yalikusanyika kwa ajili ya vita. (Amu. 7:1, 12) Kikosi kidogo cha Gideoni mwishowe kilikuwa na wanaume 300, lakini kwa msaada wa Yehova, kilishinda jeshi kubwa la maadui. Jinsi gani? Kwa kufuata mwongozo wa Mungu, wanaume hao waliizingira kambi ya maadui usiku wakiwa na mitungi ambayo ilifunika mienge iliyowaka. Gideoni alipotoa ishara, wanaume wake waliivunja mitungi hiyo na kwa ghafula mienge iliyofichwa ikaonekana. Wakati huohuo, walipiga baragumu zao na kupaaza sauti: “Upanga wa Yehova na wa Gideoni!” Maadui walivurugika, wakaanza kuuana; na wale waliookoka wakakimbilia ng’ambo ya Mto Yordani. Wakati huohuo, Waisraeli wengine walijiunga nao ili kuwakimbiza maadui. Kwa ujumla, askari-jeshi maadui 120,000 waliuawa.—Amu. 7:19-25; 8:10.

14 Mlima Tabori uko kilomita 6 hivi kutoka kwenye kilima cha More, ng’ambo ya bonde kutoka Megido. Mapema, hapo ndipo Mwamuzi Baraka alipokusanya askari-jeshi 10,000 wa Israeli ili wapambane na jeshi la Yabini, mfalme Mkanaani wa Hasori, ambalo liliongozwa na Sisera, mkuu wa jeshi. Jeshi hilo la Kanaani lilikuwa na magari ya vita 900 yenye miundu ya chuma iliyozunguka pamoja na magurudumu. Askari-jeshi Waisraeli wenye silaha chache walipokusanyika kwenye Mlima Tabori, jeshi la Sisera liliwafuata bondeni. Kisha, “Yehova akaanza kumvuruga Sisera na magari yake yote ya vita na kambi yote.” Inaelekea kwamba mvua kubwa ilinyesha ghafula na kufanya magari hayo yaanze kuzama ndani ya matope kwa sababu ya kufurika kwa Mto Kishoni. Waisraeli waliangamiza jeshi hilo lote.—Amu. 4:13-16; 5:19-21.

15. (a) Mtunga-zaburi anasali Yehova achukue hatua gani? (b) Jina la vita vya mwisho vya Mungu linatukumbusha nini?

15 Mtunga-zaburi anamsihi Yehova achukue hatua kama hiyo juu ya mataifa yanayowatisha Waisraeli wa siku zake. Anasali hivi: “Uwatendee kama Midiani, kama Sisera, kama Yabini kwenye bonde la mto la Kishoni. Waliangamizwa huko En-dori; wakawa mbolea kwa ajili ya udongo.” (Zab. 83:9, 10) Inaeleweka kwa nini vita vya mwisho vya Mungu juu ya ulimwengu wa Shetani vinaitwa Har–Magedoni (linalomaanisha “Mlima wa Megido”). Jina hilo linatukumbusha vita vya kukata maneno vilivyopiganwa karibu na Megido. Ushindi wa Yehova katika vita hivyo vya kale unatuhakikishia ushindi wake kwenye vita vya Har–Magedoni.—Ufu. 16:13-16.

Kusali Ili Enzi Kuu ya Yehova Itetewe

16. Nyuso za wapinzani ‘zimejaa aibu’ jinsi gani leo?

16 Katika kipindi chote cha ‘siku hizi za mwisho,’ Yehova amezuia jitihada zote za kuwaangamiza watu wake. (2 Tim. 3:1) Kwa sababu hiyo, wapinzani wameaibishwa. Zaburi 83:16 ilionyesha hilo mapema iliposema hivi: “Ujaze nyuso zao aibu, ili watu wapate kulitafuta jina lako, Ee Yehova.” Katika nchi mbalimbali, wapinzani wameshindwa kabisa katika jitihada zao za kuwanyamazisha Mashahidi wa Yehova. Katika nchi hizo, uthabiti na uvumilivu wa waabudu wa Mungu wa pekee wa kweli umekuwa ushahidi kwa watu wenye mioyo minyoofu, na wengi wao ‘wamelitafuta jina la Yehova.’ Katika nchi fulani ambako Mashahidi wa Yehova waliteswa vikali wakati mmoja, sasa kuna makumi ya maelfu, hata mamia ya maelfu, ya watu wanaomsifu Yehova kwa furaha. Ni ushindi kama nini kwa Yehova na aibu kwa wapinzani wake!—Soma Yeremia 1:19.

17. Ni hali gani ngumu ambayo wanadamu wanakabili, na ni maneno gani ambayo tutakumbuka hivi karibuni?

17 Tunajua wazi kwamba wapinzani wataendelea kututesa. Nasi tunaendelea kuwahubiria habari njema hata wapinzani. (Mt. 24:14, 21) Hata hivyo, nafasi inayotolewa sasa kwa wapinzani hao kutubu na kupata wokovu itakwisha hivi karibuni. Kutakaswa kwa jina la Yehova ndilo jambo la maana zaidi hata kuliko wokovu wa wanadamu. (Soma Ezekieli 38:23.) Mataifa yote duniani yanapoungana duniani pote ili kujaribu kuwaangamiza watu wa Mungu kama ilivyotabiriwa, tutakumbuka maneno yafuatayo ya sala ya mtunga-zaburi: “Na waone aibu na kusumbuka nyakati zote, nao wafedheheshwe na kuangamia.”—Zab. 83:17.

18, 19. (a) Wapinzani washupavu wa enzi kuu ya Yehova watapatwa na nini hivi karibuni? (b) Kutetewa kwa mara ya mwisho kwa enzi kuu ya Yehova ambako kunakaribia kunakuchochea ufanye nini?

18 Wapinzani ambao wameazimia kuipinga enzi kuu ya Yehova watapatwa na mwisho wenye kufedhehesha. Neno la Mungu linafunua kwamba wale “wasiotii habari njema,” ambao wataangamizwa kwenye Har–Magedoni, watapata adhabu ya “uharibifu wa milele.” (2 The. 1:7-9) Kuharibiwa kwao na kuokolewa kwa wale ambao wanamwabudu Yehova katika kweli kutathibitisha kwa njia yenye kusadikisha kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli. Katika ulimwengu mpya, ushindi huo mkubwa hautasahauliwa. Wale watakaofufuliwa katika “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu” watajulishwa kuhusu tendo hilo kuu la Yehova. (Mdo. 24:15) Katika ulimwengu mpya, wataona uthibitisho wenye kusadikisha kwamba kuishi chini ya enzi kuu ya Yehova ni jambo la hekima. Na wapole kati yao watasadiki haraka kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli.

19 Ni wakati ujao mzuri kama nini ambao Baba yetu wa mbinguni amewatayarishia waabudu wake waaminifu! Je, huchochewi kusali ili Yehova ajibu hivi karibuni kwa mara ya mwisho sala hii ya mtunga-zaburi: “[Maadui wako] waone aibu na kusumbuka nyakati zote, nao wafedheheshwe na kuangamia; ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote”?—Zab. 83:17, 18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Kabla ya kuchunguza habari hii, utafaidika ukisoma Zaburi ya 83 ili ufahamiane na mambo yaliyomo.

Je, Unaweza Kueleza?

• Waisraeli walikuwa wakikabili hali gani Zaburi ya 83 ilipoandikwa?

• Ni nini lililokuwa hangaiko kuu la mwandikaji wa Zaburi ya 83?

• Ni nani walio shabaha ya uadui wa Shetani leo?

• Yehova atajibu mwishowe sala iliyo katika Zaburi 83:18 jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Ramani katika ukurasa wa 15]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Vita vilivyopiganwa karibu na jiji la kale la Megido vina uhusiano gani na wakati wetu ujao?

Mto Kishoni

Haroshethi

Ml. Karmeli

Bonde la Yezreeli

Megido

Taanaki

Ml. Gilboa

Kisima cha Harodi

More

En-dori

Ml. Tabori

Bahari ya Galilaya

Mto Yordani

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ni nini kilichomchochea mtunga-zaburi mmoja aandike sala ya kutoka moyoni?