Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Macho ya Yehova Yanayong’aa’ Yanawachunguza Wote

‘Macho ya Yehova Yanayong’aa’ Yanawachunguza Wote

‘Macho ya Yehova Yanayong’aa’ Yanawachunguza Wote

“Macho [ya Yehova] yanayong’aa yanawachunguza wana wa binadamu.”—ZAB. 11:4.

1. Tunavutiwa na watu wa aina gani?

UNA maoni gani kuhusu watu wanaopendezwa nawe kikweli? Unapowaomba wakueleze waziwazi maoni yao kuhusu jambo fulani, wanafanya hivyo bila kukuficha lolote. Unapohitaji msaada, wako tayari kukusaidia. Unapohitaji shauri, wanakushauri kwa upendo. (Zab. 141:5; Gal. 6:1) Bila shaka, unavutiwa na watu kama hao! Yehova na Mwana wake wanapendezwa nawe kikweli. Wanapendezwa nawe kuliko mwanadamu mwingine yeyote, na hawafanyi hivyo kwa sababu ya ubinafsi hata kidogo; wanataka kukusaidia ‘ushike imara uzima ulio wa kweli.’—1 Tim. 6:19; Ufu. 3:19.

2. Yehova anapendezwa na watumishi wake kadiri gani?

2 Mtunga-zaburi Daudi alieleza jinsi Yehova anavyopendezwa sana nasi aliposema hivi: “Macho [ya Yehova] yanaangalia, macho yake yanayong’aa yanawachunguza wana wa binadamu.” (Zab. 11:4) Ndiyo, Mungu hatuangalii tu, bali pia anatuchunguza. Pia, Daudi aliandika hivi: “Umeuchunguza moyo wangu, umefanya ukaguzi wakati wa usiku . . . Utagundua kwamba sijapanga hila.” (Zab. 17:3) Bila shaka, Daudi alijua kwamba Yehova anapendezwa sana naye. Alijua kwamba Yehova angeumia na kuchukizwa ikiwa angesitawisha mawazo ya dhambi au kuwa na moyo wenye hila. Je, Yehova ni halisi kwako kama alivyokuwa kwa Daudi?

Yehova Anaona Moyo

3. Yehova anaonyesha jinsi gani kwamba anaelewa hali yetu ya kutokamilika?

3 Yehova anapendezwa hasa na jinsi tulivyo kwa ndani, yaani, jinsi moyo wetu ulivyo. (Zab. 19:14; 26:2) Kwa upendo, yeye hakazii fikira makosa madogo-madogo. Kwa mfano, Sara, mke wa Abrahamu, alipokosa kumwambia malaika ukweli, inaonekana kwamba malaika huyo alitambua kuwa Sara aliogopa na kuaibika, kwa hiyo akamkaripia Sara kwa upole tu. (Mwa. 18:12-15) Ayubu alipotangaza “nafsi yake mwenyewe kuwa adilifu badala ya Mungu,” Yehova hakumnyima baraka, kwa kuwa alijua kwamba Ayubu alikuwa ameteswa sana na Shetani. (Ayu. 32:2; 42:12) Vivyo hivyo, Yehova hakukasirika wakati yule mjane wa Sarefathi alipomwambia nabii Eliya waziwazi mambo yaliyokuwa moyoni mwake. Mungu alielewa kwamba mjane huyo alikuwa na huzuni nyingi baada ya mwana wake wa pekee kufa.—1 Fal. 17:8-24.

4, 5. Yehova alionyesha fadhili kwa njia gani aliposhughulika na Abimeleki?

4 Kwa sababu Yehova anauchunguza moyo, anawajali hata watu ambao si waamini. Fikiria jinsi alivyoshughulika na Abimeleki, mfalme wa jiji la Ufilisti la Gerari. Kwa kuwa Abimeleki hakutambua kwamba Abrahamu na Sara ni wenzi wa ndoa, alimchukua Sara ili awe mke wake. Hata hivyo, kabla ya Abimeleki kulala naye, Yehova alimwambia hivi katika ndoto: “Mimi pia nimejua kwamba katika unyoofu wa moyo wako umefanya hili, nami pia nilikuwa nikikuzuia usinitendee dhambi. Ndiyo sababu mimi sikukuruhusu umguse. Lakini sasa mrudishe mke wa huyo mwanamume, kwa maana yeye ni nabii, naye atakuombea dua. Kwa hiyo uendelee kuishi.”—Mwa. 20:1-7.

5 Kwa hakika, Yehova angemtendea kwa ukali Abimeleki, aliyeabudu miungu ya uwongo. Lakini Mungu aliona kwamba katika kisa hicho, Abimeleki alikuwa ametenda kwa unyoofu. Kwa fadhili, Yehova alitambua jambo hilo, naye akamwambia mfalme huyo jinsi anavyoweza kupata msamaha na ‘kuendelea kuishi.’ Je, hungependa kumwabudu Mungu wa aina hiyo?

6. Yesu alimwiga Baba yake kwa njia gani?

6 Yesu alimwiga Baba yake kikamilifu. Alikazia fikira sifa nzuri za wanafunzi wake na alikuwa tayari kuwasamehe makosa yao. (Marko 10:35-45; 14:66-72; Luka 22:31, 32; Yoh. 15:15) Mtazamo wa Yesu ulipatana na maneno yake kwenye Yohana 3:17: “Mungu alimtuma Mwana wake ulimwenguni, si ili auhukumu ulimwengu, bali ili ulimwengu uokolewe kupitia kwake.” Ndiyo, Yehova na Yesu wanatupenda sana na wanatupenda sikuzote. Tunajua wanatupenda kwa sababu wanataka tupate uzima. (Ayu. 14:15) Upendo huo unatusaidia kuelewa kwa nini Yehova anatuchunguza, maoni yake kutuhusu, na hatua anazochukua baada ya kutuchunguza.—Soma 1 Yohana 4:8, 19.

Kuchunguzwa kwa Upendo

7. Yehova anatuchunguza akiwa na nia gani?

7 Basi, ni vibaya kama nini kufikiri kwamba Yehova ni kama polisi anayetutazama akiwa mbinguni ili atukamate tunapofanya dhambi! Shetani ndiye anayetushuku na kutushtaki. (Ufu. 12:10) Hata wakati ambapo watu hawana nia mbaya, Shetani anadai kwamba wana nia mbaya! (Ayu. 1:9-11; 2:4, 5) Mtunga-zaburi aliandika hivi kumhusu Mungu: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zab. 130:3) Jibu la swali hilo ni, Hakuna hata mmoja! (Mhu. 7:20) Hata hivyo, Yehova anatuchunguza kwa rehema na fadhili kama mzazi anayejali ambaye anataka kuwalinda watoto wake wapendwa wasiumie. Mara nyingi anatuonyesha udhaifu wetu ili tuepuke kujiumiza.—Zab. 103:10-14; Mt. 26:41.

8. Ni kwa njia gani Yehova anawafundisha na kuwatia nidhamu watumishi wake?

8 Upendo wa Mungu unaonekana kupitia mafundisho na nidhamu anayotoa katika Maandiko na chakula cha kiroho kinachoandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45; Ebr. 12:5, 6) Pia, Yehova anatusaidia kupitia kutaniko la Kikristo na “zawadi katika wanadamu.” (Efe. 4:8) Zaidi ya hayo, Yehova anatutazama ili aone jinsi tunavyotumia mazoezi anayotupa kwa upendo, naye anatafuta njia za kutusaidia hata zaidi. Andiko la Zaburi 32:8 linasema hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” Basi, ni jambo la maana kama nini tumsikilize Yehova sikuzote! Tunapaswa kuendelea kuwa wanyenyekevu mbele zake, na kutambua kwamba yeye ni Mwalimu na Baba yetu mwenye upendo.—Soma Mathayo 18:4.

9. Tunapaswa kuepuka sifa gani mbaya, na kwa nini?

9 Kwa upande mwingine, tusiwe wagumu kamwe kwa sababu ya kiburi, kukosa imani, au “nguvu za udanganyifu za dhambi.” (Ebr. 3:13; Yak. 4:6) Mara nyingi, sifa hizo mbaya zinaanza wakati mtu anapositawisha mawazo au tamaa zisizofaa. Anaweza hata kufikia hatua ya kukataa mashauri ya Biblia yanayomhusu. Anaweza hata kuendelea kuwa na mtazamo mbaya au kujiingiza sana katika mwenendo mbaya hivi kwamba anakuwa adui wa Mungu—jambo lenye kuogopesha kama nini! (Met. 1:22-31) Fikiria mfano wa Kaini, mzaliwa wa kwanza wa Adamu na Hawa.

Yehova Anaona Mambo Yote na Anachukua Hatua Inayofaa

10. Kwa nini Yehova alikataa toleo la Kaini, na Kaini alifanya nini?

10 Kaini na Abeli walipomtolea Yehova toleo, hakupendezwa tu na zawadi yao bali alipendezwa pia na nia yao. Hivyo, Mungu alikubali toleo la Abeli, lililotolewa kwa imani, lakini akakataa toleo la Kaini, ambalo kwa njia fulani halikutolewa kwa imani. (Mwa. 4:4, 5; Ebr. 11:4) Badala ya kujifunza kupitia tukio hilo na kubadili mtazamo wake, Kaini alimkasirikia sana ndugu yake.—Mwa. 4:6.

11. Kaini alionyesha jinsi gani kwamba ana moyo wenye hila, na tunajifunza nini?

11 Yehova aliona kwamba mtazamo wa Kaini ulikuwa hatari, naye akazungumza na Kaini kwa upendo na kumwambia kwamba akitenda mema, atainuliwa. Inasikitisha kwamba Kaini alipuuza shauri la Muumba wake na kumuua ndugu yake. Moyo mbaya wa Kaini ulionekana pia alipojibu kwa dharau swali hili la Mungu: “Yuko wapi Abeli ndugu yako?” Kaini akapayuka hivi: “Sijui. Kwani mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?” (Mwa. 4:7-9) Moyo unaweza kuwa wenye hila kama nini—hata unaweza kumfanya mtu adharau shauri linalotoka kwa Mungu mwenyewe! (Yer. 17:9) Hivyo basi, acheni tujifunze kupitia masimulizi hayo na kukataa haraka mawazo na tamaa zisizofaa. (Soma Yakobo 1:14, 15.) Tukishauriwa kupitia Biblia, acheni tuthamini mashauri hayo na kuona kwamba tumeyapokea kwa sababu Yehova anatupenda.

Hakuna Dhambi ya Siri

12. Yehova anatenda jinsi gani anapomchukulia hatua mtenda-dhambi?

12 Huenda wengine wakafikiri kwamba ikiwa hakuna mtu yeyote anayewaona wakitenda mabaya, basi hawataadhibiwa. (Zab. 19:12) Kwa kweli, hakuna dhambi ya siri. “Vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Ebr. 4:13) Yehova ni Mwamuzi anayechunguza nia zetu za ndani kabisa, naye anatenda kwa haki kamilifu anapomchukulia hatua mtenda-dhambi. Yeye ni “Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli.” Hata hivyo, “hatakosa kuadhibu” wale wasiotubu ‘wanapozoea kutenda dhambi kimakusudi’ au kuonyesha mtazamo wa udanganyifu, wa kupanga hila. (Kut. 34:6, 7; Ebr. 10:26) Jambo hilo lilionekana Yehova aliposhughulika na Akani, na Anania na Safira.

13. Huenda mawazo mabaya yalimchochea jinsi gani Akani atende mabaya?

13 Akani alivunja waziwazi amri ya Mungu wakati alipochukua nyara kutoka katika jiji la Yeriko na kuzificha ndani ya hema lake, na inaelekea aliungwa mkono na familia yake. Dhambi yake ilipofichuliwa, Akani alionyesha kwamba alitambua uzito wa jambo alilotenda, kwa sababu alisema hivi: “Nimemtendea dhambi Yehova.” (Yos. 7:20) Akani alikuwa amesitawisha moyo mbaya kama Kaini. Pupa hasa ndiyo iliyomchochea Akani awe mdanganyifu. Kwa kuwa nyara zilizotoka Yeriko zilikuwa za Yehova, ni kana kwamba Akani alimwibia Mungu, na jambo hilo lilifanya auawe pamoja na familia yake.—Yos. 7:25.

14, 15. Kwa nini Anania na Safira walistahili hukumu ya Mungu, nasi tunajifunza nini?

14 Anania na mke wake, Safira, walikuwa washiriki wa kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza huko Yerusalemu. Baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., hazina fulani ilianzishwa ili kushughulikia mahitaji ya kimwili ya waamini wapya kutoka nchi za mbali ambao walibaki Yerusalemu. Hazina hiyo ilitegemezwa kwa michango iliyotolewa kwa kupenda. Anania aliuza shamba, naye akatoa kiasi fulani cha pesa alizopata ziwe mchango kwa hazina hiyo. Hata hivyo, Anania alidai kwa unafiki kwamba ametoa pesa zote, na mke wake alijua vizuri kabisa jambo hilo. Inaonekana wenzi hao wa ndoa walitaka kuonwa kuwa watu wa pekee katika kutaniko. Lakini walitenda kwa udanganyifu. Yehova alimfunulia kimuujiza mtume Petro udanganyifu huo, kisha Petro akamuuliza Anania kwa nini amedanganya. Papo hapo, Anania akaanguka chini, naye akafa. Muda mfupi baadaye, Safira pia akafa.—Mdo. 5:1-11.

15 Anania na Safira hawakufanya dhambi kwa sababu ya udhaifu wa muda mfupi. Walipanga hila na kusema uwongo ili kuwadanganya mitume. Na jambo baya hata zaidi ni kwamba ‘walimdanganya Mungu na roho takatifu.’ Hatua ambayo Yehova alichukua inaonyesha wazi kabisa kwamba yuko tayari kulilinda kutaniko lisiwe na wanafiki. Kwelikweli, “ni jambo lenye kuogopesha kuanguka mikononi mwa Mungu aliye hai”!—Ebr. 10:31.

Endelea Kuwa Mtimilifu Nyakati Zote

16. (a) Shetani anajitahidi jinsi gani kuwachafua watu wa Mungu? (b) Ibilisi anatumia njia gani kuwachafua watu katika eneo lenu?

16 Shetani anajitahidi juu chini kutuchafua na kutuzuia tusikubaliwe na Yehova. (Ufu. 12:12, 17) Nia mbovu za Ibilisi zinaonekana wazi katika ulimwengu, ambao umezama katika uasherati na jeuri. Sasa ponografia (picha au habari za ngono) inaweza kupatikana kwa urahisi kupitia kompyuta au vyombo vingine vya elektroniki. Tusikubali kamwe kushindwa na mashambulizi ya Shetani. Badala yake, acheni tuseme kama mtunga-zaburi Daudi, aliyeandika hivi: “Nitatenda kwa busara katika njia isiyo na kosa. . . . Nitatembea katika utimilifu wa moyo wangu ndani ya nyumba yangu.”—Zab. 101:2.

17. (a) Kwa nini mwishowe Yehova anafichua dhambi zilizofichwa? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

17 Leo, Yehova hafunui kimuujiza dhambi nzito na mwenendo wa udanganyifu kama alivyofanya nyakati nyingine zamani. Lakini bado anaona mambo yote, na kwa wakati wake na kwa njia yake anafichua mambo yaliyofichwa. Paulo alisema hivi: “Dhambi za watu wengine huwa wazi mbele ya watu wote, zikiongoza moja kwa moja kwenye hukumu, lakini kwa habari ya watu wengine pia dhambi zao huwa wazi baadaye.” (1 Tim. 5:24) Upendo hasa ndio unaomfanya Yehova afichue matendo mabaya. Analipenda kutaniko na anataka kulilinda likiwa safi. Pia, anawaonyesha rehema wale waliotenda dhambi na ambao sasa wametubu kikweli. (Met. 28:13) Basi, acheni tujitahidi kuendelea kuwa na moyo kamili mbele za Mungu na kukataa mambo yote yanayoweza kutuchafua.

Endelea Kuwa na Moyo Kamili

18. Mfalme Daudi alitaka mwana wake awe na maoni gani kumhusu Mungu?

18 Mfalme Daudi alimwambia hivi Sulemani, mwana wake: “Mjue Mungu wa baba yako, umtumikie kwa moyo kamili na kwa nafsi yenye shangwe; kwa maana Yehova anaichunguza mioyo yote, naye anatambua kila mwelekeo wa fikira.” (1 Nya. 28:9) Daudi alitaka mwana wake afanye mengi zaidi kuliko kumwamini tu Mungu. Alitaka Sulemani athamini jinsi ambavyo Yehova anapendezwa sana na watumishi Wake. Je, unamthamini Yehova kwa njia hiyo?

19, 20. Kulingana na Zaburi 19:7-11, ni nini kilichomsaidia Daudi amkaribie Mungu, nasi tunaweza kumwiga Daudi jinsi gani?

19 Yehova anajua kwamba watu wenye mwelekeo unaofaa watavutwa kwake na kwamba ujuzi kuhusu sifa zake zenye kuvutia utachochea mioyo yao. Hivyo, Yehova anataka tumjue na kufahamu utu wake wenye kuvutia. Ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo? Ni kujifunza Neno lake na kuona baraka zake maishani mwetu.—Met. 10:22; Yoh. 14:9.

20 Je, unasoma Neno la Mungu kila siku ukiwa na mtazamo unaofaa na kusali ili uweze kutumia mambo unayojifunza? Je, unaona faida za kuishi kulingana na kanuni za Biblia? (Soma Zaburi 19:7-11.) Ikiwa ndivyo, imani na upendo wako kumwelekea Yehova utazidi kukua. Naye Yehova atakukaribia na kutembea pamoja nawe akiushika mkono wako. (Isa. 42:6; Yak. 4:8) Ndiyo, Yehova atakuthibitishia kwamba anakupenda kwa kukubariki na kukulinda kiroho unapotembea katika barabara yenye nafasi ndogo inayoenda kwenye uzima.—Zab. 91:1, 2; Mt. 7:13, 14.

Ungesema Nini?

• Kwa nini Yehova anatuchunguza?

• Ni nini kilichofanya watu fulani wawe maadui wa Mungu?

• Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunamwona Yehova kuwa halisi?

• Tunaweza kufanya nini ili kuendelea kuwa na moyo kamili mbele za Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 4]

Yehova anatutazama jinsi gani kama mzazi anayejali?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Tunapata onyo gani katika kisa cha Anania?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kumtumikia Yehova kwa moyo kamili?