Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Barua kwa Tito, kwa Filemoni, na kwa Waebrania

Mambo Makuu Katika Barua kwa Tito, kwa Filemoni, na kwa Waebrania

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Barua kwa Tito, kwa Filemoni, na kwa Waebrania

MTUME Paulo anatembelea kisiwa cha Krete muda mfupi baada ya kuachiliwa huru kutoka gerezani huko Roma mwaka wa 61 W.K., baada ya kumaliza kifungo chake cha kwanza. Anapoona hali ya kiroho ya makutaniko katika kisiwa hicho, anamwacha Tito huko ili ayatie nguvu. Baadaye, inaelekea akiwa Makedonia, Paulo anamwandikia Tito barua ya kumwongoza katika madaraka yake na ambayo inaonyesha kwamba mtume Paulo alimpa mamlaka ya kutimiza madaraka hayo.

Mapema kidogo, muda mfupi kabla ya kuachiliwa huru kutoka gerezani mwaka wa 61 W.K., Paulo alimwandikia barua Filemoni, ndugu Mkristo aliyeishi Kolosai. Alimwandikia barua ya kumsihi akiwa rafiki.

Karibu mwaka wa 61 W.K., Paulo aliwaandikia pia waamini Waebrania huko Yudea na kuonyesha kwa nini Ukristo ni bora kuliko mfumo wa Kiyahudi. Barua zote tatu zina mashauri ya maana sana kwetu.—Ebr. 4:12.

ENDELEA KUWA NA AFYA NZURI YA KIROHO

(Tito 1:1–3:15)

Baada ya kutoa mwongozo kuhusu ‘kuwekwa rasmi kwa wanaume wazee katika jiji baada ya jiji,’ Paulo anamshauri Tito ‘aendelee kuwakaripia kwa ukali [watu watundu], ili wawe na afya katika imani.’ Anayashauri makutaniko yote huko Krete ‘yakatae kabisa kutomwogopa Mungu na yaishi kwa utimamu wa akili.’—Tito 1:5, 10-13; 2:12.

Paulo anatoa mashauri zaidi ya kuwasaidia ndugu wa Krete waendelee kuwa na afya nzuri ya kiroho. Anamwagiza Tito ‘aepuke maswali ya upumbavu na mapigano juu ya Sheria.’—Tito 3:9.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:15—“Vitu vyote” vinaweza jinsi gani kuwa “safi kwa watu safi” na visivyo safi “kwa watu waliotiwa unajisi na wasio na imani”? Ili kupata jibu ni lazima tuelewe Paulo alimaanisha nini aliposema “vitu vyote.” Hakuwa akizungumza kuhusu vitu ambavyo vinashutumiwa moja kwa moja katika Neno la Mungu lililoandikwa, bali alikuwa akizungumza kuhusu mambo ambayo Maandiko yanawaruhusu watu wajifanyie maamuzi ya kibinafsi. Mtu ambaye anafikiri kupatana na viwango vya Mungu, anaona vitu hivyo kuwa safi. Yeye ni tofauti na mtu ambaye fikira zake zimepotoka na dhamiri yake imetiwa unajisi. *

3:5—Wakristo watiwa-mafuta ‘wanaokolewa jinsi gani kupitia kuoshwa’ na ‘kufanywa kuwa wapya kwa roho takatifu’? ‘Wanaokolewa kupitia kuoshwa’ katika maana ya kwamba Mungu amewaosha, au amewatakasa, kwa damu ya Yesu kwa msingi wa dhabihu ya fidia. ‘Wanafanywa kuwa wapya kwa roho takatifu’ kwa sababu wamekuwa “kiumbe kipya” wakiwa wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho.—2 Kor. 5:17.

Mambo Tunayojifunza:

1:10-13; 2:15. Ni lazima waangalizi Wakristo wawe jasiri wanaporekebisha makosa katika kutaniko.

2:3-5. Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, dada Wakristo wakomavu leo wanahitaji ‘kuwa wenye tabia ya kumhofu Mungu, si wachongezi, wala si watumwa wa divai nyingi sana, wawe walimu wa yaliyo mema.’ Wakifanya hivyo, watafaulu kuwafundisha faraghani “wanawake vijana” katika kutaniko.

3:8, 14. Kukaza ‘akili zetu juu ya kudumisha matendo yaliyo mazuri’ ni ‘jambo zuri na lenye faida’ kwa sababu linatusaidia kuzaa matunda katika utumishi wa Mungu na kujitenga na ulimwengu mwovu.

HIMIZA “KWA MSINGI WA UPENDO”

(Flm. 1-25)

Filemoni anapongezwa kwa sababu ya kielelezo chake kizuri katika kuonyesha ‘upendo na imani.’ Paulo amepata “shangwe nyingi na faraja” kwa sababu Filemoni amekuwa akiwaburudisha Wakristo wenzake.—Flm. 4, 5, 7.

Paulo anawawekea waangalizi wote mfano mzuri kwa kushughulikia tatizo la kibinafsi kumhusu Onesimo, kwa kutoa himizo “kwa msingi wa upendo” badala ya kutoa amri. Anamwambia Filemoni: “Ninakuandikia, nikitumaini kwamba utakubali, nikijua kwamba utafanya hata zaidi ya mambo ninayosema.”—Flm. 8, 9, 21.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

10, 11, 18—Onesimo ambaye zamani alikuwa ‘asiyefaa kitu’ alipata jinsi gani kuwa “mwenye faida sana”? Onesimo alikuwa mtumwa asiyetaka kufanya kazi ambaye alitoroka kutoka katika nyumba ya Filemoni huko Kolosai na kukimbilia Roma. Inaelekea kwamba Onesimo aliiba pia pesa za bwana wake ili agharimie safari hiyo ya kilomita 1,400. Kwa kweli, alikuwa asiyefaa kitu kwa Filemoni. Hata hivyo, akiwa Roma, Paulo alimsaidia Onesimo kuwa Mkristo. Sasa ndugu huyo wa kiroho, ambaye zamani alikuwa mtumwa ‘asiyefaa kitu’ akawa “mwenye faida sana.”

15, 16—Kwa nini Paulo hakumwomba Filemoni amwachilie huru Onesimo? Paulo alitaka kushikamana kabisa na kazi aliyopewa ya ‘kuhubiri ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yanayohusu Bwana Yesu Kristo.’ Kwa hiyo, aliamua kutojihusisha na masuala ya kijamii, kama vile masuala ya utumwa.—Mdo. 28:31.

Mambo Tunayojifunza:

2. Filemoni alikubali nyumba yake itumiwe kwa ajili ya mikutano ya Kikristo. Ni pendeleo mkutano wa utumishi wa shambani kufanyiwa katika nyumba yetu.—Rom. 16:5; Kol. 4:15.

4-7. Tunapaswa kuchukua hatua ya kuwapongeza waamini wenzetu ambao wanaweka mfano mzuri katika imani na upendo.

15, 16. Hatupaswi kuruhusu matukio mabaya katika maisha yetu yatufanye tuhangaike kupita kiasi. Matukio hayo yanaweza kutunufaisha, kama vile yalivyomnufaisha Onesimo.

21. Paulo alitazamia kwamba Filemoni angemsamehe Onesimo. Sisi pia tunatazamiwa tumsamehe ndugu ambaye huenda ametukosea.—Mt. 6:14.

‘SONGA MBELE KUELEKEA UKOMAVU’

(Ebr. 1:1–13:25)

Ili kuthibitisha kwamba imani katika dhabihu ya Yesu ni bora kuliko matendo ya Sheria, Paulo anakazia ubora wa Mwanzilishi wa Ukristo, ubora wa ukuhani wake, ubora wa dhabihu yake, na ubora wa agano jipya. (Ebr. 3:1-3; 7:1-3, 22; 8:6; 9:11-14, 25, 26) Bila shaka, ujuzi huo uliwasaidia Wakristo Waebrania kukabiliana na mateso ambayo walipata mikononi mwa Wayahudi wenzao. Paulo anawahimiza waamini wenzake Waebrania ‘wasonge mbele kuelekea ukomavu.’—Ebr. 6:1.

Imani ni ya maana kadiri gani katika Ukristo? Paulo anaandika hivi: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema.” Anawatia moyo Waebrania: “Acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu,” na kufanya hivyo kwa imani.—Ebr. 11:6; 12:1.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:14, 15—Kwa kuwa Shetani ana “uwezo wa kusababisha kifo,” je, inamaanisha kwamba anaweza kusababisha kifo cha mapema cha mtu yeyote yule? Hapana, haimaanishi hivyo. Hata hivyo, tangu Shetani alipoanza kutenda uovu huko Edeni, uwongo wake umesababisha kifo kwa sababu Adamu alitenda dhambi na kufanya wanadamu wote warithi dhambi na kifo. (Rom. 5:12) Kwa kuongezea, wale wanaofanya mapenzi ya Shetani duniani wamewatesa na hata kuwaua watumishi wa Mungu, kama walivyomuua Yesu. Lakini hilo halimaanishi kwamba Shetani ana nguvu za kumuua yeyote anayetaka. Ikiwa angekuwa na nguvu za kufanya hivyo, bila shaka angekuwa amewaua waabudu wote wa Yehova zamani za kale. Yehova anawalinda watu wake wakiwa kikundi naye hamruhusu Shetani kuwafagilia mbali. Hata Mungu akimruhusu Shetani awaue wengine wetu, tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu ataondoa kabisa madhara yoyote tunayopata.

4:9-11—‘Tunaingia katika pumziko’ la Mungu jinsi gani? Mwishoni mwa siku sita za uumbaji, Mungu alipumzika kutokana na kazi zake za uumbaji, akiwa na uhakika kwamba kusudi lake kuhusu dunia na wanadamu lingetimizwa. (Mwa. 1:28; 2:2, 3) ‘Tunaingia katika pumziko hilo’ kwa kuacha matendo ya kujifanya waadilifu na kukubali mpango wa Mungu wa kutuokoa. Tunapokuwa na imani katika Yehova na kumfuata Mwana wake kwa kumtii badala ya kufuatia mapendezi ya kichoyo, tunapata baraka zinazotuburudisha na kutupumzisha kila siku.—Mt. 11:28-30.

9:16—Ni nani “yule mwanadamu mwenye kufanya agano” wa agano jipya? Yehova ndiye Mwanzilishi wa agano jipya, na Yesu ndiye “yule mwanadamu mwenye kufanya agano.” Yesu ndiye Mpatanishi wa agano hilo, na kupitia kifo chake aliandaa dhabihu iliyohitajiwa kufanya agano hilo liwe halali.—Luka 22:20; Ebr. 9:15.

11:10, 13-16—Abrahamu alikuwa akingojea “jiji” gani? Halikuwa jiji halisi, lilikuwa la mfano. Abrahamu alikuwa akingojea “Yerusalemu la mbinguni,” ambalo linafanyizwa na Kristo Yesu na watawala wenzake 144,000. Wakiwa katika utukufu wao wa kimbingu, watawala hao wenzi wa Kristo wanaitwa “jiji takatifu, Yerusalemu Jipya.” (Ebr. 12:22; Ufu. 14:1; 21:2) Abrahamu alikuwa akitazamia kuishi chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.

12:2—Ni ‘shangwe gani iliyowekwa mbele ya Yesu’ ambayo ilimfanya ‘avumilie mti wa mateso’? Ni shangwe ya kuona mambo ambayo huduma yake ingetimiza, kutia ndani kutakasa jina la Yehova, kuitetea enzi kuu ya Mungu, na kuwakomboa wanadamu kutoka katika kifo. Yesu pia alitazamia thawabu ya kutawala akiwa Mfalme na kutumika akiwa Kuhani Mkuu kwa faida ya wanadamu.

13:20—Kwa nini agano jipya linasemwa kuwa ‘linadumu milele’? Kwa sababu tatu: (1) Hakuna agano lingine litakalochukua mahali pake, (2) matokeo ya agano hilo yanadumu, na (3) mpango wa agano jipya utaendelea kuwaletea faida “kondoo wengine” baada ya Har–Magedoni.—Yoh. 10:16.

Mambo Tunayojifunza:

5:14. Tunapaswa kujifunza kwa bidii Neno la Mungu, Biblia, na kutumia yale tunayojifunza. Hiyo ndiyo njia ya pekee ya ‘kuzoeza nguvu zetu za ufahamu kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’—1 Kor. 2:10.

6:17-19. Ikiwa tumaini letu litategemea kabisa ahadi za Mungu na kiapo chake, tumaini hilo litatuzuia tusikengeushwe kutoka katika njia ya kweli.

12:3, 4. Badala ya ‘kuchoka na kuzimia katika nafsi’ zetu kwa sababu ya majaribu madogo au upinzani ambao huenda tukakabili, tunapaswa kufanya maendeleo kufikia ukomavu na kuboresha uwezo wetu wa kuvumilia majaribu. Tunapaswa kuazimia kupinga “kufikia damu,” yaani, kufikia kifo.—Ebr. 10:36-39.

12:13-15. Hatupaswi kuruhusu ‘mzizi wenye sumu,’ au mtu yeyote kutanikoni anayelalamika kuhusu jinsi mambo yanavyofanywa, atuzuie ‘tusiifanyie miguu yetu mapito yaliyonyooka.’

12:26-28. ‘Vitu ambavyo havijafanywa’ kwa mikono ya Mungu vitatikiswa na kuondolewa kabisa, yaani, mfumo wote uliopo wa mambo, kutia ndani “mbingu” zenye uovu. Kisha, “vitu ambavyo havitikiswi” vitabaki, yaani, Ufalme na wale ambao wanauunga mkono. Ni jambo la maana sana kwamba tutangaze kwa bidii Ufalme na kuishi kupatana na kanuni zake!

13:7, 17. Tukikazia uangalifu himizo hilo la kunyenyekea na kuwatii waangalizi katika makutaniko, hilo litaonyesha kwamba tuko tayari kushirikiana nao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Ona Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15, 2007 (15/10/2007), ukurasa wa 26-27.