Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utatoa Nini Ili Uendelee Kuishi?

Utatoa Nini Ili Uendelee Kuishi?

Utatoa Nini Ili Uendelee Kuishi?

“Mtu atatoa nini ili aipate nafsi yake?”—MT. 16:26.

1. Kwa nini Yesu alikataa kemeo la Petro?

MTUME Petro alishangazwa sana na mambo aliyoyasikia. Kiongozi wake mpendwa, Yesu Kristo, alikuwa akisema “waziwazi” kwamba karibuni angeteswa na kuuawa! Inaelekea Petro, akiwa na nia nzuri, alimkemea Yesu hivi: “Jitendee kwa fadhili, Bwana; wewe hutapatwa hata kidogo na jambo hili.” Yesu alimgeuzia Petro mgongo na kuwatazama wanafunzi wengine. Inaelekea wao pia walikuwa na maoni hayo yasiyofaa. Kisha, akamwambia Petro: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu wewe unafikiri, si fikira za Mungu, bali za wanadamu.”—Marko 8:32, 33; Mt. 16:21-23.

2. Yesu alisema mwanafunzi wa kweli anatazamiwa afanye nini?

2 Huenda maneno ya Yesu yaliyofuata yalimsaidia Petro kuona kwa nini Yesu alimjibu kwa ukali. Yesu ‘aliuita umati pamoja na wanafunzi wake’ na kuwaambia: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote. Kwa maana yeyote yule anayetaka kuiokoa nafsi yake ataipoteza; lakini yeyote yule anayeipoteza nafsi yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ataiokoa.” (Marko 8:34, 35) Hapa Yesu alitumia neno “nafsi” kumaanisha “uhai.” Kwa wazi, si kwamba alikuwa tu karibu kudhabihu uhai wake bali pia alitazamia kwamba wale ambao walimfuata wangekuwa tayari kudhabihu uhai wao katika utumishi wa Mungu. Ikiwa wangefanya hivyo, wangepata thawabu kubwa.—Soma Mathayo 16:27.

3. (a) Yesu aliwauliza wasikilizaji wake maswali gani? (b) Huenda swali la pili la Yesu liliwakumbusha wasikilizaji wake nini?

3 Wakati huohuo, Yesu aliuliza maswali mawili yenye kuchochea fikira: “Mtu anapata faida gani ikiwa ataupata ulimwengu wote na kuipoteza nafsi yake?” na, “Kwa kweli, mtu anaweza kutoa nini ili aipate nafsi yake?” (Marko 8:36, 37) Watu wanaweza kujibu kwa urahisi sana swali la kwanza. Hakuna faida kwa mtu kuupata ulimwengu wote na kuupoteza uhai wake, au nafsi yake. Mali ni ya maana ikiwa tu mtu yuko hai ili aifurahie. Swali la pili la Yesu: “Kwa kweli, mtu anaweza kutoa nini ili aipate nafsi yake?” huenda liliwakumbusha wasikilizaji wake dai la Shetani katika siku za Ayubu: “Kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.” (Ayu. 2:4) Kwa watu fulani ambao hawamwabudu Yehova, huenda maneno ya Shetani yakaonekana kuwa ya kweli. Watu wengi wanaweza kufanya chochote kile, hata kuvunja kanuni yoyote ile, ili tu wabaki hai. Hata hivyo, Wakristo wana maoni tofauti.

4. Kwa nini maswali ya Yesu yana maana zaidi kwa Wakristo?

4 Tunajua kwamba Yesu hakuja duniani ili kutupa afya, utajiri, na maisha marefu katika ulimwengu huu. Alikuja ili kutupa nafasi ya kuishi milele katika ulimwengu mpya, na tunathamini sana tumaini la kupata uzima wa milele. (Yoh. 3:16) Kwa Mkristo, swali la kwanza la Yesu linamaanisha hivi, “Mtu anapata faida gani akiupata ulimwengu wote na kupoteza tumaini lake la uzima wa milele?” Jibu ni kwamba hakuna faida hata kidogo. (1 Yoh. 2:15-17) Ili kutusaidia kujibu swali la pili la Yesu, tunaweza kujiuliza, ‘Niko tayari kujidhabihu kwa kadiri gani sasa ili kuwa na uhakika wa kupata uzima katika ulimwengu mpya?’ Jibu letu kwa swali hilo, yaani, jinsi tunavyoishi, linafunua ikiwa tumaini hilo ni thabiti kabisa katika mioyo yetu.—Linganisha Yohana 12:25.

5. Tunaweza kupata zawadi ya uzima wa milele jinsi gani?

5 Kwa wazi, Yesu hakuwa akisema kwamba tunaweza kupata uzima wa milele kwa uwezo wetu. Uhai, hata uhai wetu ambao ni mfupi sana katika mfumo huu wa mambo, ni zawadi. Hatuwezi kununua uhai au kufanya jambo lolote ili kustahili kuupata. Njia moja tu ya kupata zawadi ya uzima wa milele ni ‘kuweka imani yetu katika Kristo Yesu’ na Yehova, ambaye ni “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Gal. 2:16; Ebr. 11:6) Hata hivyo, ni lazima imani ionyeshwe kwa matendo, kwa kuwa “imani bila matendo imekufa.” (Yak. 2:26) Hivyo, tunapotafakari zaidi swali la Yesu, tunapaswa kufikiria kwa uzito ni mambo mengi kadiri gani ambayo tuko tayari kujinyima katika mfumo huu wa mambo na yale ambayo tuko tayari kufanya katika utumishi wa Yehova ili kuonyesha kwamba kwa kweli imani yetu ina matendo.

“Kristo Hakujipendeza Mwenyewe”

6. Yesu alitanguliza nini?

6 Badala ya kukazia macho mambo ambayo angepata katika ulimwengu wa siku zake, Yesu alikazia fikira mambo ya maana na akakataa vishawishi vya kupata vitu vya kimwili ili kuwa na maisha yenye starehe. Aliishi maisha ya kujidhabihu na alimtii Mungu. Badala ya kujipendeza mwenyewe, alisema hivi: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza [Mungu].” (Yoh. 8:29) Yesu alijidhabihu kadiri gani ili kumpendeza Mungu?

7, 8. (a) Yesu alijidhabihu jinsi gani, naye alipewa thawabu gani? (b) Tunapaswa kujiuliza swali gani?

7 Pindi moja, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.’ (Mt. 20:28) Mapema, Yesu alipoanza kuwaonya wafuasi wake kwamba alikuwa anakaribia “kutoa nafsi yake,” Petro alimsihi ajitendee kwa fadhili. Hata hivyo, Yesu hakuyumbayumba. Alitoa nafsi yake kwa kupenda, yaani, uhai wake mkamilifu wa kibinadamu, kwa ajili ya wanadamu. Kwa sababu ya kujitoa bila ubinafsi, maisha ya Yesu ya wakati ujao yalikuwa salama. Alifufuliwa na ‘kuinuliwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu.’ (Mdo. 2:32, 33) Hivyo, akawa mfano mzuri sana kwetu.

8 Mtume Paulo aliwashauri Wakristo huko Roma ‘wasiwe wakijipendeza’ wenyewe naye akawakumbusha kwamba “hata Kristo hakujipendeza mwenyewe.” (Rom. 15:1-3) Hivyo basi, ni kwa kadiri gani tutafuata shauri hilo la mtume Paulo na kumwiga Kristo kwa kujidhabihu?

Yehova Anataka Tujitoe Kabisa

9. Mkristo anafanya nini anapojiweka wakfu kwa Mungu?

9 Katika Israeli la kale, Sheria ya Musa ilisema kwamba watumwa Waebrania walipaswa kuwekwa huru katika mwaka wa saba wa utumwa au katika mwaka wa Yubile. Hata hivyo, wangeweza kufanya uamuzi tofauti. Ikiwa mtumwa alimpenda bwana wake, angeweza kuamua kubaki akiwa mtumwa katika nyumba hiyo maisha yake yote. (Soma Kumbukumbu la Torati 15:12, 16, 17.) Tunafanya uamuzi kama huo tunapojiweka wakfu kwa Mungu. Tunakubali kufanya mapenzi ya Mungu bila kulazimishwa na hatufuati mielekeo yetu. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunampenda sana Yehova na kwamba tunataka kumtumikia kwa umilele wote.

10. Sisi ni mali ya Mungu katika njia gani, na hilo linapaswa kuwa na uvutano gani juu ya mawazo na matendo yetu?

10 Ikiwa kwa sasa unajifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, unahubiri habari njema, na unahudhuria mikutano ya Kikristo, unastahili pongezi. Tunatumaini kwamba hivi karibuni utachochewa kujiweka wakfu kwa Yehova na kuuliza swali ambalo Mwethiopia alimuuliza Filipo: “Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” (Mdo. 8:35, 36) Kisha, uhusiano wako pamoja na Mungu utakuwa kama wa wale Wakristo ambao Paulo aliwaandikia hivi: “Ninyi si mali yenu wenyewe, kwa maana mlinunuliwa kwa bei.” (1 Kor. 6:19, 20) Iwe tunatumaini kuishi mbinguni au duniani, ikiwa tumejiweka wakfu kwa Yehova, basi yeye ndiye Mmiliki wetu. Hivyo, ni jambo la maana kama nini kuzuia tamaa zetu za kichoyo na ‘kuacha kuwa watumwa wa wanadamu’! (1 Kor. 7:23) Ni pendeleo kama nini kuwa mtumishi mshikamanifu ambaye anatumiwa na Yehova kama Anavyotaka!

11. Wakristo wanahimizwa watoe dhabihu gani, na hilo linamaanisha nini hasa, kama inavyoonyeshwa na dhabihu zilizotolewa chini ya Sheria ya Musa?

11 Paulo aliwahimiza hivi waamini wenzake: “Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.” (Rom. 12:1) Huenda maneno hayo yaliwakumbusha Wakristo Wayahudi kuhusu dhabihu ambazo walitoa katika ibada kabla ya kuwa wafuasi wa Yesu. Walijua kwamba chini ya Sheria ya Musa, wanyama waliotolewa kwenye madhabahu ya Yehova walipaswa kuwa wanyama bora zaidi. Dhabihu yoyote ya hali ya chini haikukubaliwa. (Mal. 1:8, 13) Ndivyo ilivyo pia tunapotoa miili yetu kuwa “dhabihu iliyo hai.” Tunampa Yehova kile kilicho bora zaidi, na si kile kinachobaki baada ya sisi kutosheleza tamaa zetu. Tunapojiweka wakfu kwa Mungu, tunampa bila masharti “nafsi” zetu au uhai wetu, kutia ndani nguvu zetu, mali, na uwezo wetu. (Kol. 3:23) Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

Tumia Wakati Wako kwa Hekima

12, 13. Taja njia moja ya kumpa Yehova kilicho bora zaidi.

12 Njia moja ya kumpa Yehova kilicho bora zaidi ni kutumia wakati wetu kwa hekima. (Soma Waefeso 5:15, 16.) Ili tufanye hivyo, tunahitaji sifa ya kujizuia. Uvutano wa ulimwengu pamoja na kutokamilika tulikorithi kunatuchochea tutumie wakati wetu wote kujifurahisha au kwa mapendezi yetu. Ni kweli kwamba “kuna wakati uliowekwa wa kila kitu,” kutia ndani wakati wa kuburudika na wa kufanya kazi ili kutimiza wajibu wetu wa Kikristo. (Mhu. 3:1) Hata hivyo, Mkristo aliyejiweka wakfu anahitaji kuwa mwenye usawaziko na kutumia wakati wake kwa hekima.

13 Paulo alipotembelea Athene, aliona kwamba “Waathene wote na wageni waliokuwa wakikaa huko kwa muda hawakuwa wakitumia wakati wao wa starehe wakifanya chochote ila kuambiana jambo au kusikiliza jambo jipya.” (Mdo. 17:21) Leo, watu wengi pia wanapoteza wakati wao. Vitu vya kisasa vinavyokengeusha fikira vinatia ndani televisheni, kucheza michezo ya video, na kuchunguza Intaneti. Leo kuna vitu vingi ambavyo vinaweza kutukengeusha fikira na kutupotezea wakati. Tukivifuatilia sana, huenda tukapuuza mahitaji yetu ya kiroho. Huenda hata tukaanza kuamini kwamba tuna shughuli nyingi sana hivi kwamba hatuwezi kutimiza “mambo yaliyo ya maana zaidi,” mambo yanayohusiana na utumishi wa Yehova.—Flp. 1:9, 10.

14. Tunapaswa kufikiria kwa uzito maswali gani?

14 Kwa hiyo, ukiwa mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu, jiulize hivi, ‘Je, ratiba yangu ya kila siku inatia ndani wakati wa kusoma Biblia, kutafakari, na kusali?’ (Zab. 77:12; 119:97; 1 The. 5:17) ‘Je, ninatenga wakati wa kutayarisha mikutano ya Kikristo? Je, ninawatia wengine moyo kwa kutoa maelezo kwenye mikutano?’ (Zab. 122:1; Ebr. 2:12) Neno la Mungu linasema kwamba Paulo na Barnaba walitumia “muda mrefu wakisema kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova.” (Mdo. 14:3) Je, unaweza kurekebisha hali zako ili utumie wakati zaidi, hata “muda mrefu,” katika kazi ya kuhubiri, pengine ukitumikia ukiwa painia?—Soma Waebrania 13:15.

15. Wazee wanatumia wakati wao kwa hekima jinsi gani?

15 Mtume Paulo na Barnaba walipotembelea kutaniko la Kikristo huko Antiokia, ‘walitumia muda usio mdogo wakiwa pamoja na wanafunzi’ ili kuwatia moyo. (Mdo. 14:28) Vivyo hivyo leo, wazee wenye upendo wanatumia muda mwingi ili kuwatia wengine nguvu. Zaidi ya kuhubiri, wazee wanalichunga kundi kwa bidii, wanatafuta kondoo waliopotea, wanawasaidia wagonjwa, na kushughulikia madaraka mengine mengi katika kutaniko. Ikiwa wewe ni ndugu aliyebatizwa, je, hali zako zinakuruhusu kufikia mapendeleo hayo ya utumishi?

16. Ni katika njia gani mbalimbali tunaweza ‘kuwatendea wote mema, wale ambao katika imani ni jamaa zetu’?

16 Wengi wamepata shangwe kwa kuwasaidia waliopata hasara kwa sababu ya misiba ya asili au ile iliyosababishwa na wanadamu. Kwa mfano, dada mmoja mwenye umri wa miaka 65 hivi ambaye anatumika Betheli alikuwa akisafiri kilomita nyingi ili kutoa misaada. Kwa nini alitumia siku zake za likizo kwa njia hiyo? Anasema hivi: “Ingawa sikuwa na ustadi wa pekee, lilikuwa pendeleo kutimiza mgawo wowote ule. Nilitiwa moyo sana kuona imani yenye nguvu ya ndugu na dada zangu ambao walipoteza vitu vingi vya kimwili.” Zaidi ya hayo, maelfu ulimwenguni pote wanasaidia kujenga Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko. Tunaposhiriki katika utendaji huo mbalimbali, ‘tunawatendea wote mema’ bila uchoyo “wale ambao katika imani ni jamaa zetu.”—Gal. 6:10.

“Mimi Nipo Pamoja Nanyi Siku Zote”

17. Wewe binafsi ungetoa nini ili upate uzima wa milele?

17 Hivi karibuni, jamii ya wanadamu iliyotengwa na Mungu itaharibiwa. Hatujui ni wakati gani hasa ambapo hilo litatukia. Hata hivyo, tunachojua ni kwamba “wakati uliobaki umepungua” na kwamba “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.” (Soma 1 Wakorintho 7:29-31.) Hilo linaongeza uzito kwa swali hili la Yesu: “Kwa kweli, mtu anaweza kutoa nini ili aipate nafsi yake?” Bila shaka, tutajinyima jambo lolote lile ambalo Yehova anatuomba ili tuweze kupata “uzima ulio wa kweli.” (1 Tim. 6:19) Kwa kweli, ni lazima tutii himizo la Yesu la ‘kuendelea kumfuata’ na “kuutafuta kwanza ufalme.”—Mt. 6:31-33; 24:13.

18. Tunaweza kuwa na uhakika gani, na kwa nini?

18 Ni kweli kwamba si rahisi kumfuata Yesu sikuzote, na kulingana na onyo la Yesu, wengine wamepoteza uhai wao katika mfumo huu wa mambo kwa sababu hiyo. Hata hivyo, kama Yesu, tunaepuka kishawishi cha ‘kujitendea kwa fadhili.’ Tunaamini ahadi hii aliyowapa wafuasi wake watiwa-mafuta wa karne ya kwanza: “Mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Hivyo basi, acheni tutumie kadiri iwezekanavyo wakati na uwezo wetu katika utumishi mtakatifu. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha tuna uhakika kwamba Yehova atatulinda ili tupite dhiki kuu au atatufufua katika ulimwengu mpya. (Ebr. 6:10) Hivyo, tutakuwa tumeonyesha kwamba tunathamini sana zawadi ya uzima.

Ungesema Nini?

• Yesu alionyesha jinsi gani kwamba alikuwa tayari kabisa kumtumikia Mungu na wanadamu?

• Kwa nini tunapaswa kujikana wenyewe, na tunafanya hivyo jinsi gani?

• Katika Israeli la kale, ni dhabihu za aina gani zilizokubaliwa na Yehova, na hilo linatufunza nini leo?

• Tunaweza kutumia wakati wetu kwa hekima katika njia gani mbalimbali?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yesu alifanya sikuzote mambo yaliyompendeza Mungu

[Picha katika ukurasa wa 28]

Waisraeli wenye uthamini waliitegemeza kabisa ibada ya kweli

[Picha katika ukurasa wa 29]

Tunampendeza Mungu kwa kutumia wakati wetu kwa hekima