Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Yehova Ni Nguvu Zangu”

“Yehova Ni Nguvu Zangu”

“Yehova Ni Nguvu Zangu”

Limesimuliwa na Joan Coville

Nilizaliwa mnamo Julai (Mwezi wa 7) 1925 huko Huddersfield, Uingereza. Nilikuwa mtoto wa pekee na afya yangu ilikuwa mbaya sana. Kwa kawaida, baba yangu alisema hivi: “Ukipigwa tu na upepo, unakuwa mgonjwa.” Kwa kweli, nilikuwa mgonjwa-mgonjwa!

NILIPOKUWA mtoto, viongozi wa kidini walisali sana ili kuwe na amani, lakini vita vya pili vya ulimwengu vilipoanza, walisali ili taifa lao lipate ushindi. Hilo lilinishangaza sana na nilijiuliza maswali mengi. Wakati huohuo, nilitembelewa na Annie Ratcliffe, na ni yeye tu aliyekuwa Shahidi wa Yehova katika eneo letu.

Nilivyojifunza Kweli

Annie alituachia kitabu Salvation (Wokovu), naye akamwalika Mama yangu kwa ajili ya mazungumzo ya Biblia katika nyumba yake. * Mama aliniomba niende naye. Bado ninakumbuka mazungumzo hayo ya kwanza. Yalihusu dhabihu ya fidia, na nilishangaa kwamba mazungumzo hayo hayakuchosha hata kidogo. Maswali mengi niliyokuwa nayo yalijibiwa wakati huo. Juma lililofuata, tulienda huko tena kwa ajili ya mazungumzo hayo. Wakati huo, unabii wa Yesu kuhusu ishara ya siku za mwisho ulifafanuliwa. Tulipoangalia hali mbaya za ulimwengu, mimi na Mama tulitambua mara moja kwamba tulikuwa tumepata kweli. Siku hiyohiyo, tulialikwa kwenye Jumba la Ufalme.

Katika Jumba la Ufalme, nilikutana na mapainia fulani vijana, kutia ndani Joyce Barber (sasa anaitwa Ellis), ambaye bado anatumika katika Betheli ya London pamoja na mume wake, Peter. Nilifikiria kwamba kila mtu alikuwa painia. Kwa hiyo, bila kukawia nilianza kuhubiri saa 60 kila mwezi, hata ingawa bado nilikuwa nikienda shuleni.

Miezi mitano baadaye, mnamo Februari 11, 1940 (11/2/1940), mimi na Mama tulibatizwa huko Bradford kwenye kusanyiko la eneo (ambalo sasa linaitwa kusanyiko la mzunguko). Baba hakupinga imani yetu mpya, lakini hakupata kamwe kuwa Shahidi. Wakati tulipobatizwa, kazi ya kuhubiri barabarani ilianzishwa. Nilihubiri barabarani nikiwa nimebeba mabango na mkoba wa magazeti. Jumamosi moja (Siku ya Posho), nilipewa mgawo wa kuhubiri nikiwa nimesimama katika eneo lenye shughuli nyingi sana za kibiashara. Bado niliwaogopa watu, na ni kana kwamba wanashule wenzangu wote walipitia mahali nilipokuwa nimesimama!

Mwaka wa 1940, kutaniko letu (wakati huo kutaniko liliitwa kampuni) lilihitaji kugawanywa. Kutaniko letu lilipogawanywa, marafiki wangu wengi walijiunga na kutaniko jipya. Nilimlalamikia mtumishi wa kampuni (sasa anaitwa mwangalizi-msimamizi) kuhusu jambo hilo. Akasema hivi: “Ikiwa unataka marafiki vijana, nenda uwatafute shambani.” Na hivyo ndivyo nilivyofanya! Muda si muda, nilikutana na Elsie Noble. Alikubali kweli, akawa rafiki yangu kwa muda mrefu sana.

Utumishi wa Painia na Baraka Zake

Baada ya kukamilisha masomo, nilimfanyia kazi mtaalamu mmoja wa hesabu za pesa. Hata hivyo, nilipoona shangwe ambayo watumishi wa wakati wote walikuwa nayo, nilitamani sana kumtumikia Yehova nikiwa painia. Katika Mei (Mwezi wa 5) 1945, nilipata shangwe ya kuanza kutumika nikiwa painia wa pekee. Siku yangu ya kwanza ya upainia, mvua kubwa ilinyesha siku nzima. Hata hivyo, nilifurahia sana kuhubiri hivi kwamba sikujali mvua. Kwa kweli, afya yangu iliboreka kwa sababu nilifanya mazoezi kwa ukawaida nilipokuwa nikiendesha baiskeli yangu kila siku katika huduma. Ingawa mimi ni mwembamba na sijawahi kuzidi kilo 42, sijalazimika kukatiza utumishi wangu wa upainia kwa sababu ya ugonjwa. Kwa miaka mingi, nimemwona ‘Yehova akiwa nguvu zangu’ kwa njia halisi.—Zab. 28:7.

Nilitumwa nikiwa painia wa pekee katika miji ambayo haikuwa na Mashahidi ili nianzishe makutaniko mapya. Kwanza nilitumika kwa miaka mitatu nchini Uingereza kisha kwa miaka mitatu nchini Ireland. Nilipokuwa nikifanya upainia huko Lisburn, Ireland, nilijifunza na mtu fulani ambaye alikuwa msaidizi wa kasisi katika kanisa la Kiprotestanti. Alipoendelea kujifunza ukweli kuhusu mafundisho ya msingi ya Biblia, aliwafundisha washiriki wa kanisa lake mambo aliyokuwa akijifunza. Wengine wao walilalamika kwa wakuu wa kanisa hilo, na bila shaka aliagizwa aeleze kwa nini alikuwa akifundisha mambo hayo. Alisema kwamba ana wajibu wa Kikristo wa kuwaambia washiriki wa kundi lake kwamba alikuwa amewafundisha mambo mengi ya uwongo. Ingawa familia yake ilimpinga vikali, alijiweka wakfu kwa Yehova naye akamtumikia kwa uaminifu mpaka alipokufa.

Katika mgawo wangu wa pili wa upainia huko Larne, Ireland, nilihubiri peke yangu kwa majuma sita, kwa kuwa painia mwenzangu alikuwa amehudhuria Kusanyiko la Ongezeko la Kitheokrasi huko New York, mwaka wa 1950. Huo ulikuwa wakati mgumu kwangu. Nilitamani sana kuhudhuria kusanyiko hilo. Hata hivyo, katika majuma hayo, nilipata mambo mengi yenye kutia moyo katika utumishi wa shambani. Nilikutana na mwanamume fulani mzee ambaye alichukua kitabu chetu kimoja miaka zaidi ya 20 mapema. Kwa miaka mingi, alikisoma mara nyingi sana hivi kwamba alikumbuka karibu kila jambo. Alikubali kweli pamoja na mwana wake na binti yake.

Kuzoezwa Katika Shule ya Gileadi

Mwaka wa 1951, nilialikwa pamoja na mapainia wengine kumi kutoka Uingereza kwenye darasa la 17 la Shule ya Gileadi huko South Lansing, New York. Nilifurahia sana mafundisho ya Biblia ambayo tulipata katika miezi hiyo! Wakati huo, akina dada hawakuandikishwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika makutaniko, lakini katika Gileadi sisi akina dada tulipata migawo ya kutoa hotuba za wanafunzi na ripoti. Tuliogopa sana! Nilipokuwa nikitoa hotuba yangu ya kwanza, mkono wangu ulitetemeka sana nikiwa nimeshika maandishi. Ndugu Maxwell Friend aliyekuwa mwalimu akasema hivi kwa ucheshi: “Ni kweli kwamba ulitetemeka mwanzoni kama wasemaji wote wenye uzoefu, hata hivyo, uliendelea kutetemeka mpaka mwisho.” Wakati wa shule, sote tuliboresha uwezo wetu wa kutoa hotuba darasani. Punde si punde, mazoezi yetu yalimalizika, na tulipohitimu tulitumwa katika nchi mbalimbali. Nilitumwa Thailand!

“Nchi ya Tabasamu”

Astrid Anderson alipopewa mgawo wa kuwa mmishonari mwenzangu nchini Thailand nilimwona kuwa zawadi kutoka kwa Yehova. Tulisafiri muda wa majuma saba kwa meli ya mizigo ili kufika huko. Tulipofika katika mji mkuu, Bangkok, tuliona masoko mengi yenye hekaheka nyingi na mifereji ambayo inatumiwa kama njia ya usafiri. Mwaka wa 1952, hesabu ya wahubiri wa Ufalme nchini Thailand haikuzidi 150.

Tulipoona Mnara wa Mlinzi wa lugha ya Kithai kwa mara ya kwanza, tulijiuliza hivi: ‘Tutaweza kweli kuzungumza lugha hiyo?’ Tatizo kubwa hasa lilikuwa kutumia matamshi yanayofaa. Kwa mfano, neno khaù likitamkwa kwa sauti ya juu linamaanisha “mchele,” lakini neno hilohilo likitamkwa kwa sauti nzito ya chini linamaanisha “habari.” Kwa hiyo, tulipokuwa katika utumishi wa shambani, mwanzoni hatukujua kwamba tulikuwa tukiwaambia watu, “Ninakuletea mchele mzuri” badala ya “Ninakuletea habari njema”! Lakini pole kwa pole tulijifunza lugha hiyo ingawa tulikosea mara nyingi na kucheka.

Watu wa Thailand ni wenye urafiki sana. Kwa hiyo, nchi ya Thailand inaitwa Nchi ya Tabasamu. Mgawo wetu wa kwanza ulikuwa katika jiji la Khorat (ambao sasa unaitwa Nakhon Ratchasima), ambako tulitumikia kwa miaka miwili. Baadaye, tulitumwa katika mji wa Chiang Mai. Wathai wengi ni Wabudha na hawaifahamu Biblia. Huko Khorat, nilijifunza na msimamizi wa posta. Tulizungumza naye kuhusu mzee wa ukoo Abrahamu. Mtu huyo alitikisa kichwa kwa furaha kwa sababu alikuwa amewahi kusikia jina Abrahamu. Hata hivyo, muda si muda niligundua kwamba hakuelewa ni Abrahamu gani tuliyekuwa tunamzungumzia. Msimamizi huyo wa posta alifikiri tunazungumzia Abraham Lincoln, rais wa zamani wa Marekani!

Tulifurahia kuwafundisha Biblia watu wa Thailand wenye mioyo minyoofu, nao wakatufundisha jinsi ya kuishi maisha rahisi kwa furaha. Jambo hilo lilitusaidia sana, kwa kuwa katika makao yetu ya kwanza ya wamishonari huko Khorat, hatukuwa na umeme wala maji. Katika migawo kama hiyo, ‘tulijifunza siri ya jinsi ya kuwa na wingi na pia jinsi ya kupatwa na uhitaji.’ Kama mtume Paulo, tulijifunza maana ya ‘kuwa na nguvu kupitia yeye anayetupa nguvu.’—Flp. 4:12, 13.

Mwenzi Mpya na Mgawo Mpya

Katika mwaka wa 1945, nilitembelea London. Katika safari hiyo, nilitembelea Jumba la Makumbusho la Uingereza pamoja na mapainia wengine na Wanabetheli. Mmoja wao alikuwa Allan Coville, ambaye muda mfupi baadaye alihudhuria darasa la 11 la Gileadi. Alitumwa nchini Ufaransa na Ubelgiji. * Baadaye, nilipokuwa bado mmishonari nchini Thailand, aliniomba tufunge ndoa, nami nikakubali.

Tulifunga ndoa huko Brussels, Ubelgiji mnamo Julai 9, 1955. Nilitamani sana kwenda kustarehe huko Paris baada ya arusi, kwa hiyo Allan alipanga tuhudhurie kusanyiko huko juma lililofuata. Hata hivyo, tulipofika tu, Allan aliombwa asaidie katika kutafsiri hotuba kwenye kusanyiko hilo. Kila siku, aliondoka asubuhi na tulirudi mahali pa kulala usiku sana. Hivyo, baada ya arusi tulienda Paris kustarehe, lakini mara nyingi nilimwona Allan kwa mbali tu, akiwa jukwaani! Hata hivyo, nilifurahi kumwona mume wangu akiwatumikia ndugu na dada zake, na sikuwa na shaka yoyote kwamba tukimtanguliza Yehova katika ndoa yetu, tutapata furaha ya kweli.

Ndoa pia ilinifanya nihamie kwenye eneo jipya la kuhubiri huko Ubelgiji. Sikujua mengi kuhusu Ubelgiji isipokuwa tu kwamba vita vingi vilipiganwa huko, lakini muda si muda niligundua kwamba Wabelgiji wengi wanapenda amani. Kwa sababu ya mgawo huo, nililazimika pia kujifunza Kifaransa, lugha inayozungumzwa katika sehemu ya kusini ya nchi hiyo.

Mwaka wa 1955 kulikuwa na wahubiri 4,500 hivi nchini Ubelgiji. Kwa miaka karibu 50, mimi na Allan tulitumika Betheli na katika kazi ya kusafiri. Katika miaka miwili na nusu ya kwanza, tulisafiri kwa baiskeli, tulipanda na kushuka milima, kukiwa na jua na kukiwa na mvua. Katika miaka hiyo yote, tulilala katika nyumba zaidi ya 2,000 za Mashahidi wenzetu! Mara nyingi nilikutana na ndugu na dada ambao walikuwa dhaifu kimwili lakini walimtumikia Yehova kwa nguvu zao zote. Mfano wao ulinitia moyo kutoacha utumishi wangu. Mwishoni mwa juma la ziara kutanikoni, sikuzote tulihisi tumejengwa. (Rom. 1:11, 12) Allan alikuwa rafiki wa kweli. Maneno ya Mhubiri 4:9, 10 ni ya kweli kabisa: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, . . . kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake”!

Baraka za Kutumika kwa ‘Nguvu za Yehova’

Kwa miaka mingi, mimi na Allan tumefurahia kuwasaidia watu wengi wamtumikie Yehova. Kwa mfano, katika mwaka wa 1983 tulitembelea kutaniko la Kifaransa huko Antwerp, ambako tulikaa na familia ambayo ilikuwa inaishi na Benjamin Bandiwila, ndugu kijana kutoka Zaire (sasa ni Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo). Benjamin alikuwa amehamia Ubelgiji kupata elimu ya juu. Alituambia hivi: “Ninawaonea wivu kwa sababu mmejitolea kabisa kumtumikia Yehova.” Allan akamjibu: “Unasema unatuonea wivu; lakini unafuatia elimu ya kilimwengu. Je, huoni kwamba hufanyi yale unayosema?” Maneno hayo ya waziwazi yalimfanya Benjamin afikirie maisha yake. Baadaye aliporudi Zaire, alianza kufanya upainia, na sasa yeye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi.

Mwaka wa 1999, nilifanyiwa upasuaji wa kuondoa kidonda katika njia ya koo yangu. Tangu wakati huo, nimekuwa na uzito wa kilo 30 tu. Mimi kwa kweli ni ‘chombo dhaifu sana cha udongo.’ Hata hivyo, ninashukuru kwa sababu Yehova amenipa “nguvu zinazopita zile za kawaida.” Baada ya upasuaji, Yehova aliniwezesha kuambatana tena na Allan katika kazi ya kusafiri. (2 Kor. 4:7) Kisha, mnamo Machi 2004, Allan alikufa akiwa amelala. Ninamkosa sana, lakini ninafarijika kujua kwamba yuko katika kumbukumbu ya Yehova.

Sasa nina umri wa miaka 83, na nimekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 63. Ningali ninahubiri kwa bidii, ninaongoza funzo la Biblia la nyumbani na kutumia nafasi ninazopata kila siku kutangaza kusudi zuri sana la Yehova. Nyakati nyingine, ninajiuliza hivi, ‘Ningeishi maisha ya aina gani kama singeanza kufanya upainia mwaka wa 1945?’ Wakati huo, ningetoa kisingizio kwamba siwezi kufanya upainia kwa sababu ya matatizo ya afya. Hata hivyo, ninafurahi sana kwamba nilianza upainia nikiwa kijana! Nimekuwa na pendeleo la kujionea mwenyewe kwamba tukimtanguliza Yehova anakuwa nguvu zetu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kitabu Salvation kilichapishwa mwaka wa 1939. Sasa hakichapishwi tena.

^ fu. 22 Simulizi la maisha la Ndugu Coville lilichapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Machi 15, 1961 (15/3/1961).

[Picha katika ukurasa wa 18]

Nikiwa na mmishonari mwenzangu, Astrid Anderson (upande wa kulia)

[Picha katika ukurasa wa 18]

Nikiwa na mume wangu katika kazi ya kusafiri, mwaka wa 1956

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa na Allan mwaka wa 2000