Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Mpinge Ibilisi’ Kama Yesu Alivyofanya

‘Mpinge Ibilisi’ Kama Yesu Alivyofanya

‘Mpinge Ibilisi’ Kama Yesu Alivyofanya

“Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”—YAK. 4:7.

1. Yesu alijua atapingwa na nani duniani, na matokeo yangekuwa nini?

YESU KRISTO alijua kwamba atapingwa na Ibilisi. Jambo hilo la hakika lilionyeshwa wazi na maneno ambayo Mungu alimwambia huyo kiumbe mwovu wa roho aliyeasi ambaye alizungumza kupitia nyoka: “Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamke [sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova] na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye [Yesu Kristo] atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.” (Mwa. 3:14, 15; Ufu. 12:9) Yesu alitiwa jeraha la muda tu kwenye kisigino kwa kuuawa akiwa duniani, kwa kuwa Yehova alimfufua kwenye utukufu wa kimbingu. Lakini nyoka atapondwa kichwa, yaani, Ibilisi atauawa bila tumaini la kuishi tena.—Soma Matendo 2:31, 32; Waebrania 2:14.

2. Kwa nini Yehova alikuwa na hakika kwamba Yesu angefanikiwa kumpinga Ibilisi?

2 Yehova alikuwa na uhakika kwamba Yesu angefanikiwa kutimiza mgawo wake na kumpinga Ibilisi hapa duniani. Kwa nini Yehova alikuwa na uhakika huo? Kwa sababu alimuumba Yesu mbinguni miaka mingi iliyopita, alikuwa amemchunguza, na alijua kwamba huyo “stadi wa kazi” na “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote” alikuwa mtiifu na mwaminifu. (Met. 8:22-31; Kol. 1:15) Kwa hivyo, wakati Yesu alipotumwa duniani, na Ibilisi akaruhusiwa kumjaribu mpaka kifo, Mungu alikuwa na hakika kwamba Mwana Wake mzaliwa-pekee angeshinda.—Yoh. 3:16.

Yehova Anawalinda Watumishi Wake

3. Ibilisi ana mtazamo gani kuelekea watumishi wa Yehova?

3 Yesu alimwita Ibilisi “mtawala wa ulimwengu huu” na akawaonya wanafunzi Wake kwamba watateswa kama yeye alivyoteswa. (Yoh. 12:31; 15:20) Ulimwengu, ambao unakaa katika nguvu za Shetani Ibilisi, unawachukia Wakristo wa kweli kwa sababu wanamtumikia Yehova na wanahubiri uadilifu. (Mt. 24:9; 1 Yoh. 5:19) Ibilisi anawalenga hasa mabaki ya watiwa-mafuta ambao mwishowe watatawala pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa mbinguni. Shetani pia anawalenga Mashahidi wengi wa Yehova ambao wana tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani. Neno la Mungu linatuonya hivi: “Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.”—1 Pet. 5:8.

4. Ni nini kinachothibitisha kwamba watu wa Mungu wamefanikiwa kumpinga Ibilisi nyakati zetu?

4 Tukiwa tengenezo ambalo linategemezwa na Yehova Mungu, tunafanikiwa kumpinga Ibilisi. Fikiria mambo haya ya hakika: Katika miaka 100 ambayo imepita, serikali fulani zilizoongozwa na madikteta wakatili zaidi katika historia zimejaribu kuwakomesha kabisa Mashahidi wa Yehova. Lakini hesabu ya Mashahidi inaendelea kuongezeka na sasa kuna Mashahidi karibu 7,000,000 katika makutaniko zaidi ya 100,000 ulimwenguni pote. Serikali za kidikteta zenye jeuri zilizowatesa watu wa Yehova ndizo ambazo zimekomeshwa kabisa!

5. Andiko la Isaya 54:17 limethibitika jinsi gani kuwa la kweli kuhusiana na watumishi wa Yehova?

5 Akizungumza na kutaniko la kale la Israeli kana kwamba ni “mwanamke” wake, Mungu aliahidi hivi: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu. Hilo ndilo fungu la urithi la watumishi wa Yehova, na uadilifu wao ni kutoka kwangu.” (Isa. 54:11, 17) Ahadi hiyo imethibitika kuwa ya kweli kabisa kuhusiana na watu wa Yehova duniani pote katika ‘siku hizi za mwisho.’ (2 Tim. 3:1-5, 13) Tunaendelea kumpinga Ibilisi, na hakuna silaha yoyote ambayo anajaribu kutumia kuwaangamiza watu wa Mungu itakayofanikiwa, kwa kuwa Yehova yuko upande wetu.—Zab. 118:6, 7.

6. Unabii wa Danieli unatuambia nini kuhusu utawala wa Ibilisi wakati ujao?

6 Katika mwisho unaokaribia haraka wa mfumo huu wote mwovu wa mambo, kila sehemu ya utawala wa Shetani itaondolewa kabisa. Nabii Danieli aliandika unabii huu kwa mwongozo wa roho ya Mungu: “Katika siku za wafalme hao [waliopo leo], Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [mbinguni] ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [zilizopo leo], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Dan. 2:44) Hilo litakapotukia, utawala wa Shetani na utawala wa wanadamu wasio wakamilifu utatoweka kabisa. Kila sehemu ya mfumo wa mambo wa Ibilisi itakuwa imeondolewa milele, na Ufalme wa Mungu utatawala dunia yote bila kupingwa.—Soma 2 Petro 3:7, 13.

7. Tunajua jinsi gani kwamba watumishi wa Yehova wakiwa mtu mmoja-mmoja wanaweza kufanikiwa kumpinga Ibilisi?

7 Hakuna shaka kwamba tengenezo la Yehova litalindwa na kusitawi kiroho. (Soma Zaburi 125:1, 2.) Namna gani sisi? Biblia inatuambia kwamba tunaweza kufanikiwa kumpinga Ibilisi, kama Yesu alivyofanya. Kwa kweli, unabii ambao Kristo alitoa kupitia mtume Yohana unaonyesha kwamba “umati mkubwa” wa watu wenye tumaini la kuishi duniani utaokoka mwisho wa mfumo huu hata ingawa wanapingwa na Shetani. Maandiko yanasema kwamba wanapaaza sauti hivi: “Wokovu unatoka kwa Mungu wetu, anayeketi juu ya kiti cha ufalme, na Mwana-Kondoo [Yesu Kristo].” (Ufu. 7:9-14) Biblia inasema kwamba watiwa-mafuta wanamshinda Shetani, na waandamani wao, “kondoo wengine,” wanafanikiwa kumpinga pia. (Yoh. 10:16; Ufu. 12:10, 11) Lakini wanapaswa kujitahidi sana na kusali kwa bidii ili ‘wakombolewe kutokana na yule mwovu.’—Mt. 6:13.

Mfano Bora Kabisa Katika Kumpinga Ibilisi

8. Ni jaribu gani la kwanza ambalo Ibilisi alitumia kumshawishi Yesu nyikani, na Kristo alimjibu namna gani?

8 Ibilisi alijaribu kuvunja utimilifu wa Yesu. Huko nyikani, Shetani alitumia majaribu mbalimbali kumshawishi Yesu asimtii Yehova. Hata hivyo, Yesu aliweka mfano bora kabisa katika kumpinga Shetani. Baada ya kufunga kwa siku 40, mchana na usiku, inaelekea kwamba Yesu alitamani sana kula. “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu,” akasema Shetani, “yaambie mawe haya yawe mikate.” Lakini Yesu alikataa kutumia nguvu alizopewa na Mungu ili kujifaidi. Badala yake, Yesu alisema: “Imeandikwa, ‘Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.’”—Mt. 4:1-4; Kum. 8:3.

9. Kwa nini ni lazima tupinge jitihada za Ibilisi za kujaribu kutushawishi akitumia tamaa zetu za asili za mwili?

9 Leo, Ibilisi anajaribu kuwashawishi watumishi wa Yehova akitumia tamaa za asili za mwili. Kwa hiyo, ni lazima tuazimie kupinga kabisa vishawishi vya kufanya ngono haramu ambavyo vimejaa katika ulimwengu huu uliopotoka. Neno la Mungu linasema hivi kwa mkazo: “Kwani! Je, hamjui kwamba watu wasio waadilifu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msipotoshwe. Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume wanaolala na wanaume . . . hawataurithi ufalme wa Mungu.” (1 Kor. 6:9, 10) Basi, ni wazi kwamba watu wanaoishi maisha mapotovu na kukataa kubadilika hawataruhusiwa kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu.

10. Kulingana na Mathayo 4:5, 6, Shetani alitumia kishawishi gani kingine kujaribu kuvunja utimilifu wa Yesu?

10 Maandiko yanasema hivi kuhusu kishawishi kingine ambacho Yesu alipata nyikani: “Ibilisi akamchukua, akaenda pamoja naye, na kuingia katika lile jiji takatifu, naye akamsimamisha juu ya mnara wa hekalu na kumwambia: ‘Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, jitupe chini; kwa maana imeandikwa, “Atawaagiza malaika zake kukuhusu wewe, nao watakuchukua mikononi mwao, ili usipate kamwe kuugonga mguu wako juu ya jiwe.”’” (Mt. 4:5, 6) Inaonekana kwamba alitaka kumchochea Yesu afanye tamasha ya ajabu ili kuthibitisha kwamba yeye ndiye Masihi. Hata hivyo, ukweli ni kwamba hilo lingekuwa tendo lisilofaa na la kujitutumua ambalo halingeungwa mkono na Mungu wala halingempendeza. Kwa mara nyingine tena, Yesu alishikilia utimilifu wake kwa Yehova na kumjibu Shetani kwa kunukuu andiko. Alisema hivi: “Tena imeandikwa, ‘Usimjaribu Yehova Mungu wako.’”—Mt. 4:7; Kum. 6:16.

11. Shetani anaweza kutushawishi jinsi gani, na matokeo yanaweza kuwa nini?

11 Huenda Shetani akatushawishi tujitafutie utukufu kwa njia mbalimbali. Anaweza kutushawishi tuige mitindo ya ulimwengu ya mavazi na mapambo au tujihusishe na burudani isiyofaa. Lakini tukipuuza mashauri ya Biblia na kuiga ulimwengu, je, tunaweza kutazamia malaika watulinde tusipatwe na madhara ya mwenendo wetu? Ingawa Mfalme Daudi alitubu dhambi alizofanya kuhusiana na Bath-sheba, hakulindwa asipatwe na madhara ya matendo yake. (2 Sam. 12:9-12) Tusimjaribu Yehova kwa njia zisizofaa, labda kwa kusitawisha urafiki na ulimwengu.—Soma Yakobo 4:4; 1 Yohana 2:15-17.

12. Ni kishawishi gani kinachotajwa katika Mathayo 4:8, 9, na Mwana wa Mungu alikabiliana nacho jinsi gani?

12 Ibilisi alimshawishi tena Yesu nyikani kwa kujaribu kumpa cheo cha kisiasa. Shetani alimwonyesha Yesu falme zote za ulimwengu na utukufu wa falme hizo, kisha akasema: “Nitakupa mambo yote haya ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” (Mt. 4:8, 9) Alitumia njia yenye hila kama nini kujaribu kupata ibada ambayo ilikuwa ya Yehova na kumshawishi Yesu amwasi Mungu! Alipotafakari kuhusu tamaa ya kuabudiwa, malaika huyo ambaye mwanzoni alikuwa mshikamanifu, aligeuka na kuwa Shetani Ibilisi ambaye ni mshawishi mwovu kupindukia, mwenye dhambi na tamaa. (Yak. 1:14, 15) Hata hivyo, Yesu alikuwa tofauti kabisa na Shetani kwa kuwa aliazimia kuendelea kuwa mwaminifu kwa Baba yake wa mbinguni. Yesu alisema hivi: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’” Kwa hiyo, Yesu alimpinga tena Ibilisi waziwazi na moja kwa moja. Mwana wa Mungu hakutaka kujiingiza katika sehemu yoyote ya ulimwengu wa Shetani naye hangemwabudu kamwe mwovu huyo!—Mt. 4:10; Kum. 6:13; 10:20.

‘Mpinge Ibilisi, Naye Atakukimbia’

13, 14. (a) Kwa kumwonyesha Yesu falme zote za ulimwengu, Ibilisi alitaka kumpa nini? (b) Shetani anatumia njia gani kujaribu kutupotosha?

13 Ibilisi alipomwonyesha Yesu falme zote za ulimwengu, alitaka kumpa mamlaka ambayo hakuna mwanadamu amewahi kuwa nayo. Shetani alitumaini kwamba Yesu angevutiwa na mambo aliyoona na kusadiki kwamba angekuwa kiongozi wa kisiasa mwenye nguvu zaidi duniani. Leo, Ibilisi hatupi falme, lakini anajaribu kuchafua mioyo yetu kwa mambo tunayoona, tunayosikia, na kufikiria.

14 Ibilisi anaongoza ulimwengu huu. Kwa hivyo, anaongoza vyombo vya habari vya ulimwengu. Basi haishangazi kwamba mambo ambayo watu wa ulimwengu wanatazama, wanasikiliza, na kusoma yamejaa maadili mapotovu na jeuri. Matangazo ya kibiashara ya ulimwengu huu yanatuchochea tuwe na tamaa ya kununua vitu vingi sana ambavyo hatuhitaji. Kupitia njia hizo, Ibilisi anatushawishi daima kwa vitu vya kimwili vinavyovutia macho, masikio, na akili zetu. Lakini tunapokataa kutazama, kusikiliza, na kusoma mambo ambayo hayapatani na Maandiko, ni kana kwamba tunasema: “Nenda zako, Shetani!” Tunapofanya hivyo tunamwiga Yesu kwa kukataa kwa uthabiti ulimwengu mchafu wa Shetani. Tunaonyesha pia kwamba sisi si sehemu ya ulimwengu wa Shetani kwa kujitambulisha kwa ujasiri kazini, shuleni, katika ujirani wetu, na kwa watu wetu wa ukoo kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova na wafuasi wa Kristo.—Soma Marko 8:38.

15. Kwa nini tunapaswa kuendelea kuwa macho ili tumpinge Shetani?

15 Baada ya kushindwa kwa mara ya tatu kumshawishi Yesu avunje utimilifu wake kwa Mungu, ‘Ibilisi alimwacha.’ (Mt. 4:11) Hata hivyo, Shetani hakukusudia kuacha kumjaribu Yesu, kwa kuwa tunaambiwa hivi: “Kwa hiyo Ibilisi, akiisha kumaliza majaribu yote [nyikani], akamwacha mpaka wakati mwingine unaofaa.” (Luka 4:13) Tunapofanikiwa kumpinga Ibilisi, tunapaswa kumshukuru Yehova. Lakini tunapaswa pia kumwomba Mungu aendelee kutusaidia, kwa kuwa Ibilisi atarudi kutushawishi wakati mwingine unaomfaa yeye, bali si lazima arudi wakati ambapo tunatarajia kushawishiwa. Hivyo, ni lazima tuwe macho kila wakati, na kuwa tayari kuvumilia tunapomtolea Yehova utumishi mtakatifu hata tukikabili majaribu gani.

16. Yehova anatupa uwezo gani wenye nguvu zaidi, na kwa nini tunapaswa kumwomba uwezo huo?

16 Ili tufaulu katika jitihada zetu za kumpinga Ibilisi, tunapaswa kusali ili tupokee uwezo wenye nguvu zaidi katika ulimwengu wote, yaani, roho takatifu ya Mungu. Itatusaidia kutimiza mambo ambayo hatuwezi kutimiza kwa uwezo wetu. Yesu aliwahakikishia wafuasi wake kwamba wanaweza kupata roho ya Mungu aliposema hivi: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa [wasio wakamilifu na hivyo] waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:13) Acheni tuendelee kumwomba Yehova atupe roho yake takatifu. Tukiazimia kumpinga Ibilisi huku tukitegemezwa na roho hiyo yenye nguvu nyingi zaidi, tutamshinda kabisa. Zaidi ya kusali kwa bidii na kwa ukawaida, tunahitaji kuvaa mavazi kamili ya silaha za kiroho kutoka kwa Mungu ili ‘tusimame imara kupinga hila za Ibilisi.’—Efe. 6:11-18.

17. Ni shangwe gani iliyomsaidia Yesu kumpinga Ibilisi?

17 Kuna jambo lingine lililomsaidia Yesu kumpinga Ibilisi, na linaweza kutusaidia pia. Biblia inasema hivi: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele [ya Yesu], yeye alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu, naye ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.” (Ebr. 12:2) Tunaweza kuwa na shangwe kama hiyo kwa kuunga mkono enzi kuu ya Yehova, kuliheshimu jina lake takatifu, na kukazia fikira zawadi ya uzima wa milele. Tutapata shangwe kubwa kama nini wakati Shetani atakapoharibiwa milele pamoja na kazi zake zote, kisha ‘wapole waimiliki dunia, na kupata furaha yao tele katika wingi wa amani’! (Zab. 37:11) Kwa hiyo, endelea kumpinga Ibilisi, kama Yesu alivyofanya.—Soma Yakobo 4:7, 8.

Ungesema Nini?

• Ni nini kinachothibitisha kwamba Yehova anawalinda watu wake?

• Ni mfano gani ambao Yesu aliweka katika kumpinga Shetani?

• Unaweza kumpinga Ibilisi katika njia gani mbalimbali?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Tukiwa marafiki wa ulimwengu tunakuwa maadui wa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 31]

Yesu alikataa falme zote za ulimwengu ambazo Shetani alitaka kumpa