Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tufuatilie Mambo Yanayofanya Kuwe na Amani”

“Tufuatilie Mambo Yanayofanya Kuwe na Amani”

“Tufuatilie Mambo Yanayofanya Kuwe na Amani”

BARABARA iliyowekwa lami hivi karibuni inaonekana kuwa imara na isiyoweza kuharibika. Hata hivyo, baada ya muda mipasuko na mashimo yanatokea. Barabara hiyo inahitaji kurekebishwa ili iwe salama na idumu.

Vivyo hivyo, mara kwa mara huenda uhusiano wetu pamoja na wengine ukaharibika au hata kuvunjika. Mtume Paulo alitambua kwamba Wakristo huko Roma walikuwa na maoni yaliyotofautiana. Aliwashauri Wakristo wenzake hivi: “Na tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.” (Rom. 14:13, 19) Kwa nini ni jambo la maana “tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani”? Tunaweza kufuatilia amani kwa ujasiri na kwa matokeo jinsi gani?

Kwa Nini Tufuatilie Amani?

Barabara isiporekebishwa, mipasuko midogo inaweza kupanuka na kuwa mashimo makubwa yaliyo hatari. Vivyo hivyo, kutotatua hali ya kutoelewana kunaweza kuwa hatari. Mtume Yohana aliandika: “Yeyote akisema: ‘Mimi nampenda Mungu,’ na bado anamchukia ndugu yake, yeye ni mwongo. Kwa maana yeye ambaye hampendi ndugu yake, ambaye amemwona, hawezi kuwa anampenda Mungu, ambaye hajamwona.” (1 Yoh. 4:20) Hali ya kutoelewana isipotatuliwa inaweza kumfanya Mkristo amchukie ndugu yake.

Yesu Kristo alionyesha kwamba ibada yetu haitakubaliwa na Yehova ikiwa hatutafanya amani pamoja na wengine. Yesu aliwaagiza hivi wanafunzi wake: “Basi, ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo ukumbuke kwamba ndugu yako ana jambo fulani juu yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, itoe zawadi yako.” (Mt. 5:23, 24) Ndiyo, sababu ya msingi inayotufanya tufuatilie amani ni kwamba tunataka kumpendeza Yehova Mungu. *

Hali fulani iliyokuwapo katika kutaniko la Filipi inaonyesha sababu nyingine ya kufuatilia amani. Inaelekea kwamba tatizo fulani lisilotajwa lililokuwa kati ya dada wawili Wakristo, Euodia na Sintike, lilitishia amani ya kutaniko lote. (Flp. 4:2, 3) Watu wasipotatua hali ya kutoelewana, hali hiyo inaweza kujulikana haraka na wengi. Tamaa ya kutaka kudumisha upendo na umoja wa kutaniko inatuchochea kufuatilia amani pamoja na waamini wenzetu.

Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani.” (Mt. 5:9) Kufuatilia amani kunaleta uradhi na shangwe. Zaidi ya hilo, amani inamwezesha mtu kuwa na afya nzuri, kwa kuwa “moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.” (Met. 14:30) Kwa upande mwingine, mtu anayefungia kinyongo anakabili hatari ya kuwa mgonjwa.

Ingawa Wakristo wengi wanakubali kwamba kufuatilia amani ni jambo la maana, huenda usijue jinsi ya kutatua hali ya kutoelewana. Acheni tuchunguze kanuni za Kimaandiko ambazo zinaweza kutuongoza.

Kuzungumza kwa Utulivu Kunaweza Kurudisha Amani

Mara nyingi, mipasuko midogo kwenye barabara inaweza kurekebishwa kwa kufunika sehemu iliyoharibika. Je, tunaweza kusamehe na kufunika makosa madogo ya ndugu zetu? Inaelekea tukifanya hivyo tutafaulu kutatua hali ya kutoelewana, kwa kuwa mtume Petro aliandika kwamba “upendo hufunika dhambi nyingi.”—1 Pet. 4:8.

Hata hivyo, nyakati nyingine tatizo linaonekana kuwa zito sana hivi kwamba hatuwezi tu kulifunika. Fikiria kile kilichotokea kwa Waisraeli muda mfupi tu baada ya wao kuingia katika Nchi ya Ahadi. Kabla ya “wana wa Rubeni na wana wa Gadi na nusu ya kabila la Manase” kuvuka ng’ambo ya Mto Yordani, walijenga “madhabahu kubwa yenye kuonekana wazi.” Makabila mengine ya Israeli yaliamini kwamba madhabahu hiyo ilitumiwa kwa ajili ya ibada ya sanamu na kwamba hawangeweza tu kupuuza jambo hilo. Walijitayarisha kupigana nao.—Yos. 22:9-12.

Huenda Waisraeli fulani walifikiri kwamba tayari kulikuwa na uthibitisho wa kutosha wa kosa na kwamba kuwashambulia kwa ghafula kungezuia watu wengi wasife. Hata hivyo, badala ya kutenda kwa haraka, makabila yaliyokuwa magharibi mwa Yordani yalituma wajumbe ili kuzungumzia tatizo hilo na ndugu zao. Yaliuliza hivi: “Mmefanya tendo gani hili la kukosa uaminifu juu ya Mungu wa Israeli kwa kugeuka nyuma msimfuate Yehova leo?” Kwa kweli, makabila ambayo yalijenga madhabahu hayo hayakutenda hivyo kwa sababu ya kukosa uaminifu. Lakini makabila hayo yangeshughulikia shtaka hilo jinsi gani? Je, yangewashambulia washtaki wao kwa maneno makali au kukataa kuzungumza nao? Makabila yaliyoshtakiwa yalijibu kwa upole, na yakaeleza waziwazi kwamba matendo yao yalichochewa na tamaa yao ya kumtumikia Yehova. Jibu lao la upole lilidumisha uhusiano wao mzuri pamoja na Mungu na liliokoa uhai. Kuzungumza kwa utulivu kulitatua tatizo hilo na kurudisha amani.—Yos. 22:13-34.

Kabla ya kuchukua hatua nzito, kwa hekima wale Waisraeli wengine walizungumzia tatizo lao pamoja na yale makabila ya Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase. Neno la Mungu linasema hivi: “Usiwe na haraka kuudhika katika roho yako, kwa maana kuudhika hukaa katika kifua cha wajinga.” (Mhu. 7:9) Njia ya Kimaandiko ya kutatua matatizo makubwa ya kutoelewana ni kuzungumza kwa utulivu na waziwazi. Je, tunaweza kutazamia kupata baraka za Yehova tukifungia kinyongo na kukataa kuzungumza na mtu ambaye tunahisi alitukosea?

Kwa upande mwingine, namna gani ikiwa Mkristo mwenzetu anatuambia kwamba tumemkosea, na labda hata anatushtaki kimakosa? Biblia inasema: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu.” (Met. 15:1) Makabila ya Israeli yaliyoshutumiwa yalieleza msimamo wao kwa upole na waziwazi, na kwa njia hiyo yakasuluhisha tatizo ambalo lilichochea hisia kali za ndugu zao. Tukiamua kuzungumza na ndugu yetu au akiamua kuzungumza nasi kuhusu tatizo fulani, tunapaswa kujiuliza, ‘Tutatumia maneno gani, kuzungumza kwa njia gani, na kuwa na mtazamo gani ili tufanye amani?’

Tumia Ulimi kwa Hekima

Yehova anaelewa kwamba tunahitaji kueleza mahangaiko yetu. Hata hivyo, tukishindwa kutatua hali ya kutoelewana, inaelekea tutashawishiwa kumweleza mtu mwingine jambo hilo. Tunapofungia kinyongo, ni rahisi kuwachambua-chambua wengine. Kuhusu matumizi mabaya ya ulimi, andiko la Methali 11:11 linasema hivi: “[Mji] hubomolewa kwa sababu ya kinywa cha waovu.” Vivyo hivyo, usemi usiozuiliwa kuhusu Mkristo mwenzetu unaweza kuvuruga amani ya kutaniko ambalo linalinganishwa na mji.

Hata hivyo, kufuatilia amani hakumaanishi kuepuka kabisa kuzungumza kuhusu ndugu na dada zetu. Mtume Paulo aliwashauri waamini wenzake: “Msiache kamwe maneno maovu yapite katika midomo yenu.” Lakini aliongeza hivi: “Semeni tu mambo mema ambayo watu wanahitaji kusikia, mambo yatakayowasaidia kwelikweli. . . . Iweni wenye fadhili kwa mmoja na mwingine, wenye huruma, na wenye kusameheana.” (Efe. 4:29-32, The New American Bible) Ikiwa ndugu ambaye aliumizwa na maneno au mwenendo wako anakufikia, je, haingekuwa rahisi kuomba msamaha na kufanya amani ikiwa hapo awali aliwaambia wengine mambo mema kukuhusu? Kwa hiyo, tukizoea kusema mambo yenye kujenga tunapozungumza kuhusu Wakristo wenzetu, itakuwa rahisi zaidi kurudisha amani tunapokosana na wengine.—Luka 6:31.

Mtumikie Mungu “Bega kwa Bega”

Tukiwa wanadamu wenye dhambi tuna mwelekeo wa kujitenga na wale ambao wametukosea. Lakini kutenda hivyo si jambo la hekima. (Met. 18:1) Tukiwa watu wenye umoja ambao wanaitwa kwa jina la Yehova, tumeazimia ‘kumtumikia bega kwa bega.’—Sef. 3:9.

Usemi au mwenendo wowote usiofaa wa watu wengine haupaswi kupunguza bidii yetu kwa ajili ya ibada safi. Siku chache tu kabla ya dhabihu ya Yesu kuchukua mahali pa matoleo kwenye hekalu na muda mfupi baada ya Yesu kuwashutumu vikali waandishi, aliona mjane maskini akitumbukiza “riziki yote aliyokuwa nayo” ndani ya sanduku la hazina la hekalu. Je, Yesu alijaribu kumzuia? Hapana. Badala yake, alimsifu kwa kuwa alitegemeza kwa ushikamanifu kutaniko la Yehova la wakati huo. (Luka 21:1-4) Matendo ya ukosefu wa uadilifu ya wengine hayakumzuia mjane huyo kutimiza wajibu wake wa kutegemeza ibada ya Yehova.

Ingawa huenda tukahisi kwamba ndugu au dada fulani Mkristo ametenda jambo lisilofaa, na hata kwa njia isiyo ya haki, tutafanya nini? Je, tutaruhusu hilo lituzuie tusimtumikie Yehova kwa nafsi yetu yote? Au je, tutatenda kwa ujasiri na kusuluhisha hali zozote za kutoelewana ili kudumisha amani yenye thamani ya kutaniko la Mungu leo?

Maandiko yanatushauri hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.” (Rom. 12:18) Na tuazimie kufanya hivyo ili tubaki kwenye barabara ya uzima.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kuhusu mashauri ya Yesu yaliyo kwenye Mathayo 18:15-17, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1999, (15/10/1999), ukurasa wa 17-22.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Euodia na Sintike walihitaji kufuatilia amani

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tutatumia maneno gani, kuzungumza kwa njia gani, na kuwa na mtazamo gani ili tudumishe amani?