Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unataka Kuwa Mtu wa Aina Gani?

Unataka Kuwa Mtu wa Aina Gani?

Unataka Kuwa Mtu wa Aina Gani?

MKUU wa polisi katika mji mmoja huko Filipino alimuuliza painia mmoja, “Ulifanya nini ili mtu huyo abadili mwenendo wake?” Akionyesha rundo la karatasi kwenye meza yake, aliongeza hivi: “Je, unajua kwamba karatasi hizi zote ni rekodi za wakati uliopita za kesi zake? Umetuondolea tatizo kubwa sana katika mji huu.” Mwanamume huyo alikuwa mlevi na mwenye ugomvi, naye alisababisha fujo kila mara. Ni nini kilichomchochea kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yake? Ni ujumbe wa Neno la Mungu, Biblia ulioongozwa na roho.

Watu wengi wamelichukua kwa uzito shauri la mtume Paulo la ‘kuuondolea mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wao wa kwanza na kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu.’ (Efe. 4:22-24) Iwe mabadiliko ambayo tunahitaji kufanya ni makubwa au madogo, ni lazima mtu anayekubali Ukristo avae utu mpya.

Hata hivyo, kufanya mabadiliko na maendeleo kufikia kubatizwa, ni mwanzo tu. Tunapojitoa kubatizwa katika maji, tunakuwa kama kipande cha mbao ambacho kimechongwa katika umbo fulani. Umbo hilo linaonekana wazi, lakini ni lazima kipande hicho cha mbao kifanyiwe kazi zaidi. Bado mchongaji anahitaji kuongeza madoido fulani ili kukifanya kipendeze. Wakati wa ubatizo, tuna sifa za msingi zinazohitajiwa ili kuwa mtumishi wa Mungu. Hata hivyo, utu wetu mpya bado uko kwenye hatua ya kwanza. Tunapaswa kuendelea kuuboresha kwa kufanya marekebisho.

Hata Paulo aliona umuhimu wa kufanya marekebisho. Alikiri hivi: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.” (Rom. 7:21) Bila shaka, Paulo alijua yeye ni mtu wa aina gani na alijua alitaka kuwa mtu wa aina gani. Namna gani sisi? Sisi pia tunahitaji kujiuliza: ‘Ni mambo gani yaliyo pamoja nami? Mimi ni mtu wa aina gani? Na ninataka kuwa mtu wa aina gani?’

Ni Mambo Gani ‘Yaliyo Pamoja Nami’?

Tunaporekebisha nyumba iliyozeeka, haitoshi tu kuipaka rangi nje ikiwa imeoza ndani. Kupuuza sehemu mbovu za nyumba hiyo kutatokeza tu matatizo baadaye. Vivyo hivyo, kujionyesha kwa nje kuwa mwadilifu hakutoshi. Tunapaswa kujichunguza jinsi tulivyo kikweli na kutambua matatizo ambayo yanahitaji kutatuliwa. Tusipofanya hivyo, tabia za utu wa zamani zitatokea tena. Hivyo, ni lazima tujichunguze. (2 Kor. 13:5) Tunahitaji kutambua tabia zisizopendeza na kuzirekebisha. Yehova ametuandalia msaada wa kufanya hivyo.

Paulo aliandika hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Ebr. 4:12) Ujumbe wa Neno la Mungu lililoandikwa, Biblia, unaweza kubadili sana maisha yetu. Unachoma kabisa ndani yetu, ni kana kwamba unafikia urojorojo ulio katika sehemu za ndani za mifupa. Unafunua fikira na nia zetu, ukionyesha jinsi tulivyo kwa ndani kwa kulinganisha na jinsi tunavyoonekana kwa nje au jinsi tunavyofikiri tuko. Neno la Mungu linatusaidia sana kutambua matatizo yetu!

Tunaporekebisha nyumba iliyozeeka, huenda isitoshe tu kubadili vitu vilivyoharibika. Kujua kisababishi cha kasoro hizo kunatusaidia kuchukua hatua ili kuzuia matatizo yaleyale yasitokee tena. Vivyo hivyo, badala ya kutambua tu tabia zetu zisizopendeza, tunapaswa pia kujua ni nini kinachozisababisha ili tuweze kupambana na udhaifu wetu. Kuna mambo mengi yanayohusika katika kujenga utu wetu. Mambo hayo yanatia ndani hali yetu ya kijamii na ya kiuchumi, mazingira yetu, utamaduni wetu, wazazi wetu, marafiki wetu, na malezi yetu ya kidini. Hata vipindi vya televisheni na sinema tunazotazama, na pia aina nyingine za burudani, zina uvutano juu ya utu wetu. Kutambua vitu ambavyo vina uvutano mbaya juu ya utu wetu kunatusaidia sana kuepuka uvutano huo.

Baada ya kujichunguza, huenda tukawa na mwelekeo wa kusema, ‘Hivyo ndivyo nilivyo.’ Hayo ni maoni yasiyofaa. Akizungumza na washiriki wa kutaniko la Korintho ambao zamani walikuwa waasherati, walawiti, walevi, na kadhalika, Paulo alisema hivi: “Bado wengine wenu mlikuwa hivyo. Lakini mmeoshwa mkawa safi . . . kwa roho ya Mungu wetu.” (1 Kor. 6:9-11) Kwa msaada wa roho takatifu ya Yehova, sisi pia tunaweza kufaulu kufanya mabadiliko tunayohitaji.

Fikiria kisa cha mwanamume anayeitwa Marcos, * anayeishi Filipino. Akizungumza kuhusu malezi yake, Marcos alisema: “Sikuzote wazazi wangu walibishana. Ndiyo sababu niliasi nilipokuwa na umri wa miaka 19.” Marcos alijihusisha sana na kucheza kamari na wizi, naye alifanya hivyo akitumia bunduki. Yeye na wengine walipanga njama ya kuteka ndege nyara, lakini mpango huo haukufaulu. Marcos aliendelea na tabia zake mbaya hata baada ya kuoa. Mwishowe, alipoteza kila kitu alichokuwa nacho kwa kucheza kamari. Muda mfupi baadaye, Marcos alijiunga na mke wake kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kwanza, aliona kwamba hastahili kuwa Shahidi. Hata hivyo, kufuata mambo aliyokuwa akijifunza na kuhudhuria mikutano kulimsaidia Marcos kuacha njia zake mbaya. Kwa sasa yeye ni Mkristo aliyebatizwa ambaye anawafundisha wengine kwa ukawaida jinsi wanavyoweza pia kufanya mabadiliko.

Unataka Kuwa Mtu wa Aina Gani?

Ni mabadiliko gani ambayo huenda tukahitaji kufanya ili kuboresha sifa zetu za Kikristo? Paulo anawashauri Wakristo hivi: “Yaondoleeni mbali mambo haya yote kutoka kwenu, ghadhabu, hasira, ubaya, matukano, na maneno machafu kutoka kinywani mwenu. Msiwe mkiambiana uwongo. Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake.” Mtume huyo anaendelea kusema: “Mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba.”—Kol. 3:8-10.

Hivyo, kusudi letu kuu, ni kuvua kabisa utu wetu wa zamani na kuvaa utu mpya. Tunahitaji kusitawisha sifa gani ili kutimiza kusudi hilo? Paulo anasema: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Kol. 3:12-14) Kujitahidi kusitawisha sifa hizo kutatufanya ‘tupendwe na Yehova na vilevile na wanadamu.’ (1 Sam. 2:26) Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha kwa njia ya pekee sifa hizo za kimungu. Tukijifunza na kuiga mfano wake, tunaweza kuwa kama Kristo kwa kuwa “waigaji wa Mungu.”—Efe. 5:1, 2.

Njia nyingine ya kutambua mabadiliko ambayo huenda tukahitaji kufanya ni kujifunza sifa za watu wanaotajwa katika Biblia, kuchunguza mambo yaliyowafanya wavutie na pia kasoro zao. Kwa mfano, fikiria kisa cha Yosefu, mwana wa Yakobo. Ingawa alitendewa isivyo haki, Yosefu alidumisha mtazamo unaofaa na sifa nzuri za moyoni. (Mwa. 45:1-15) Kwa upande mwingine, Absalomu, mwana wa Mfalme Daudi, alijifanya kuwa mtu mwenye kuwajali sana watu na alisifiwa kwa sababu ya sura yake nzuri. Hata hivyo, ukweli ni kwamba alikuwa msaliti na muuaji. (2 Sam. 13:28, 29; 14:25; 15:1-12) Kwa kweli, sura nzuri na kujifanya kuwa mwema hakumfanyi mtu awe mwenye kuvutia.

Tunaweza Kufaulu

Ili tufanye maendeleo na kuwa wenye kupendeza machoni pa Mungu, tunahitaji kuchunguza jinsi tulivyo kwa ndani. (1 Pet. 3:3, 4) Ili kufanya mabadiliko katika utu wetu tunahitaji kutambua sifa zetu mbaya na mambo yanayosababisha au kuchangia sifa hizo, kisha tusitawishe sifa za kimungu. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tukijitahidi kuboresha utu wetu tutafaulu.

Ndiyo, kwa msaada wa Yehova tunaweza kufanya mabadiliko yanayohitajiwa. Kama mtunga-zaburi, tunaweza kusali hivi: “Uumbe moyo safi ndani yangu, Ee Mungu, na kuweka ndani yangu roho mpya, iliyo imara.” (Zab. 51:10) Tunaweza kuomba roho ya Mungu ifanye kazi ndani yetu ili ichochee tamaa yetu ya kupatanisha kikamilifu maisha yetu na mapenzi yake. Kwa kweli, tunaweza kufaulu kuwa wenye kuvutia zaidi machoni pa Yehova!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Si jina lake halisi.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Je, inatosha kupaka rangi sehemu ya nje tu ya nyumba hii iliyoharibiwa na dhoruba?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Je, utu wako umekuwa kama wa Kristo?